Rais Jakaya Kikwete, amewaagiza wakuu wa
mikoa kupunguza vifo vya watoto na akina mama vinavyotokana na uzazi katika
mikoa yao, huku akiwahadharisha kwamba atafuatilia kwa karibu utendaji wao
kuona namna wanavyoshughughulikia tatizo hilo.
Alionya
kuwa hatakuwa na huruma na Mkuu wa Mkoa, atakayeshindwa kuweka mikakati
ya kupunguza tatizo hilo katika mkoa wake, na akawataka waachane na kisingizio
cha ufinyu wa bajeti ambacho kimekuwa kichaka cha viongozi wasiowajibika.
Akizundua
mpango mkakati wa kuongeza kasi ya kupunguza vifo vitokanavyo na uzazi na
vya watoto wachanga na wale wa chini ya miaka mitano, Rais Kikwete alisema
kuanzia sasa jambo la kwanza atakalofuatilia katika utendaji wa wakuu wa mikoa,
ni namna wanavyoshiriki kupunguza vifo vya watoto na akina mama katika maeneo
yao.
"Mimi
sio kiongozi wa kusikiliza na kuamini ninayoambiwa, hili linanigusa kwa karibu…
nawaambia nitafuatilia utendaji wenu kwa karibu, lengo nataka vifo vya watoto
wachanga na wale wa chini ya miaka mitano pamoja mama wajawazito
vinapungua," alisema Rais Kikwete.
Rais
Kikwete alisema wakuu wa mikoa, wamekuwa hawafuatilii masuala ya afya hadi
litokee tatizo la dharura la kipindupindu, wakati vifo vya watoto na akina mama
wanaokufa kwa uzazi vinaongezeka hata kuliko wanaokufa kwa kipindupindu.
Aliwataka
suala hilo iwe ajenda ya kisiasa katika ngazi zote za Serikali na akawaagiza
wakuu hao wa mikoa, wanaporejea mikoani kwao wakasambaze maagizo hayo katika
ngazi za chini yao, ili utekelezaji uanze mara moja.
"Wakuu
wa mikoa, wakuu wa wilaya wanafikiri suala hili ni la waganga wakuu na
watumishi wa afya, hata hawaulizi hali zikoje mikoani kwao, sasa lichukulieni
hili kuwa la dharura...nikija huko jambo la kwanza kuuliza na kufuatilia ni
suala hili," alisema Rais Kikwete.
Aliwataka
wakuu hao wa mikoa kuweka mikakati ya kupunguza tatizo hilo na yeye akaahidi
kuwa atalifuatilia binafsi utendaji wa kila Mkuu wa Mkoa, kupitia kadi maalum
za kutolea taarifa za vifo vya watoto wachanga, watoto wa chini ya miaka mitano
na akina mama wanaokufa kwa matatizo ya uzazi.
Alisema
baadhi ya vifo vya watoto na wajawazito vinatokea kwa sababu ya uzembe wa
watumishi wa afya, na akaeleza kuwa suala hilo linawezekana iwapo tu viongozi
watatimiza wajibu wao kwa kufuatilia kwa karibu.
"Kipimo
cha uwajibikaji wenu, itakuwa kupitia kadi hii," alisema Rais Kikwete na
kuahidi kuwa atahitaji kupokea taarifa ya kila mkoa kila baada ya miezi minne,
kuona namna wakuu wa mikoa na watendaji wao wanavyoshughulika na tatizo hilo.
Rais
Kikwete alisema sekta ya afya kwa sasa haiko katika mpango wa matokeo makubwa
sasa, ameagiza kitengo cha Rais cha kufuatilia utekelezaji wa Mfumo wa Matokeo
Makubwa Sasa (BRN), waiweke sekta hiyo kwenye mpango huo.
Rais
pia alitoa mwito kwa wajawazito, kuhakikisha wanapata chakula bora chenye
lishe, ili kuongeza usalama wakati wanapoenda kujifungua. Alisema pia
familia zinatakiwa kuzingatia uzazi wa mpango, ili kuwalea watoto na kuwapa mahitaji
yao ya msingi.
Awali
akitoa tamko la wakuu wa mikoa, ambalo waliazimia juzi baada ya kufanyiwa
semina, Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dk Christin Ishengoma, alisema wameazimia
kila mkoa uandae mpango mkakati wa kupunguza tatizo hilo ambao unatekelezeka na
uwe shirikishi.
Alisema
kuanzia sasa kila mkoa utawatambua wajawazito wote walioko katika maeneo yao na
watoto wa chini ya miaka mitano, ili kuwafuatilia kwa karibu na kuwapatia
huduma za msingi zinazotakiwa.
Akitoa
hali halisi ya vifo vya watoto na wajawazito wanaokufa kwa uzazi, Dk Neema
Rusibamanyika, alisema akina mama 7,900 wanakufa kila mwaka kwa matatizo ya
uzazi na vichanga 40,000 katika kila vizazi 100,000 pia hufariki.
Sababu
za vifo vya watoto, alisema ni kuugua nimonia, magonjwa ya kuharisha na
Malaria, wakati vifo vya wajawazito husababishwa na ukosefu wa vifaa tiba,
upungugu wa watumishi, miundombinu mibovu na ucheleweshaji wa huduma.
Takwimu
hizo zinaonesha kuwa asilimia 51 ya wajawazito ndio wanaojifungulia
hospitalini, wakati asilimia 49 hujifungulia kwa wakunga wa jadi.
Hali
hiyo ni chini ya Malengo ya Millenia, yanataka ifikapo mwaka 2015 asilimia 80
ya wajawazito wawe wanajifungulia hospitalini.
No comments:
Post a Comment