Kiu ya Malawi ya kupata Rais wa nchi
hiyo baada ya Uchaguzi Mkuu uliofanyika Mei 20, mwaka huu, huenda ikashindwa
kukatika miongoni mwa raia wa nchi hiyo baada ya Rais anayemaliza muda wake, Dk
Joyce Banda kutangaza kusitisha shughuli zote za uchaguzi huo.
Banda aliyeiongoza nchi hiyo kwa miaka
miwili kuanzia Aprili 7, mwaka 2012, alikuwa miongoni mwa wagombea wanne wa
nafasi ya urais. Banda maarufu kama JB, aliingia kwenye uchaguzi kwa tiketi ya
chama chake cha People’s (PP).
Mgombea mwingine ni Mhadhiri wa zamani
wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Profesa Peter Mutharika wa chama cha
Democratic (DPP).
Mbali ya kufundisha Chuo Kikuu cha Dar
es Salaam mwishoni mwa miaka ya 1970, Mutharika (65) amefundisha pia katika
vyuo vikuu vya Haile Selassie
(Ethiopia), Rutgers (Marekani), Makerere (Uganda) na Washington (Marekani). Pia ni Mhadhiri
anayefundisha kwa muda katika Shule ya Uchumi ya London, Uingereza.
Wagombea wengine ni Mchungaji Dk
Lazarus Chakwera (59) wa chama kikongwe
cha Malawi Congress (MCP) na Atupele Muluzi wa chama cha United Democratic
Front (UDF).
Hata hivyo, baada ya siku mbili za
kusubiri matokeo, huku taarifa zikisambaa kwa kasi kwamba Rais huyo anaelekea
kushindwa uchaguzi, jana aliibuka na kuamuru kusitishwa mara moja kwa shughuli
ya kuhesabu kura na kutangaza matokeo ya uchaguzi huo mkuu wa nchi hiyo.
Akizungumza katika Ikulu yake jijini
Lilongwe jana, Banda mwenye umri wa miaka 64, ameamuru Tume ya Taifa ya
Uchaguzi ya Malawi (MEC ) kusitisha shughuli hiyo na kutangaza kuwa uchaguzi wa
Rais, Wabunge na Madiwani, utarudiwa ndani ya siku 90 kuanzia jana.
“Baada ya kujiridhisha kuwa kumekuwa na
ukiukwaji mkubwa wa taratibu katika Uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani,
kwa maslahi ya wananchi wa Malawi, shughuli zote za uchaguzi zinasitishwa.
“Mimi, Dk Joyce Banda, Rais wa Malawi
kwa mamlaka ya kikatiba niliyopewa kupitia Kifungu 88 (2) cha Katiba, natangaza
kusitisha taratibu zote za uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani, ikiwa pamoja
na kuhesabu kura na kutangaza matokeo yake.
“Hivyo, natangaza uchaguzi mpya wa
Rais, Wabunge na Madiwani utafanyika ndani ya siku 90 kuanzia leo (jana Mei
24),” imeeleza sehemu ya taarifa ya Rais Banda kwa vyombo vya umma jana.
Aidha, alikwenda mbali zaidi na kusema
yeye binafsi, hatakuwa miongoni mwa wagombea urais katika uchaguzi huo wa
marudio.
Katika maelezo yake, alisema ameamua
kuchukua uamuzi huo, kwa kile alichokiita ni kuvurugika kwa mtiririko mzima wa
shughuli za upigaji kura, kuhesabu na hata namna ya kusimamia utoaji wa matokeo
yake. Kwa ujumla, ameuita ulikuwa uchaguzi uliojaa `mchezo mchafu’.
Kutokana na amri ya Rais huyo wa nne wa
Malawi, Mwenyekiti wa MEC, Jaji Mackson
Mbendera alisema anawasiliana na Mwanasheria Mkuu wa Serikali ili kuona kama
utekelezaji wa amri hiyo ya Rais Banda, hautavunja Sheria ya Nchi.
Awali kabla ya amri hiyo, MEC ilianza
kutangaza matokeo ambayo yalionesha
Profesa Mutharika, mwanazuoni aliyebobea katika masuala ya sheria,
alikuwa akiongoza.
Mutharika pia ni mwanasiasa mzoefu na
mashuhuri, aliyeshika nyadhifa za uwaziri katika wizara mbalimbali, zikiwamo
Wizara ya Sheria, Wizara ya Mambo ya Nje na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia, nafasi
aliyoishika hadi anaingia katika uchaguzi mkuu hivi karibuni.
Katika matokeo ya awali ya MEC,
yaliyobeba asilimia 30 ya kura zote zilizohesabiwa na kupokelewa katika ofisi
kuu za tume hiyo, yalionesha Mutharika, mdogo wa
aliyekuwa Rais wa tatu wa Malawi, Bingu
wa Mutharika, alikuwa anaongoza kwa kupata 683,621 akifuatiwa na Banda kura
372,101.
Mgombea wa MCP, Mchungaji Chakwera
alikuwa na kura 289,145 huku Muluzi akiwa na kura 269,250. Muluzi ni mtoto wa
Rais wa Pili wa Malawi, Bakili Muluzi na ndiye mgombea kijana zaidi akiwa na
umri wa miaka 35. Kabla ya kujitosa kwenye urais, alikuwa Waziri wa Uchumi,
Mipango na Maendeleo katika Serikali ya Rais Banda.
Akizungumza na wanahabari juzi usiku,
Jaji Mbendera alisema Tume yake kwa pamoja na wawakilishi wa vyama vya siasa,
wamethibitisha matokeo hayo.
Jaji Mbendera alisema Tume yake,
imegundua kuwa kulikuwa na udanganyifu katika baadhi ya maeneo, ambapo wamekuta
idadi ya kura zilizopigwa ni zaidi ya watu walioandikishwa kupiga kura. Alisema
wamezuia matokeo hayo hadi watakapopata ufumbuzi na ukweli wa taarifa hiyo.
Wakati matokeo hayo yanaanza
kutangazwa, Mahakama nchini humo imezuia uamuzi wa Bodi ya Wakurugenzi wa
Shirika la Utangazaji la Malawi (MBC) kumlazimisha Mkurugenzi Mkuu, Dk Benson
Tembo kwenda likizo ya lazima na haraka.
Uamuzi huo umetokana na baadhi ya
wanasheria kutoka Tume ya wanasheria wa Malawi, kuweka zuio mahakamani kupinga
uamuzi wa bodi ya shirika hilo.
Juzi asubuhi, Dk Tembo alipewa barua ya
kumtaka aende likizo ya lazima, akidaiwa kushindwa kufuata maelekezo ya serikali,
ambayo ni pamoja na vyombo vya shirika hilo ikiwemo televisheni na redio za
taifa, kuendelea kutoa matokeo ya uchaguzi, ambayo hayajathibitishwa na MEC.
Inadaiwa MBC pia ilishindwa kurusha
moja kwa moja matangazo ya mkutano wa Rais Banda na wanahabari mjini Lilongwe,
uliofanyika Alhamisi iliyopita, ambapo Dk Banda alikuwa akitoa maelekezo kwa
MEC kuanza kuhesabu kura kwa kutumia mikono na kuzuia kutoa matokeo, kutokana
na udanganyifu uliojitokeza.
Rais alisema kuwa uchaguzi huo
umekumbwa na visa vingi, ikiwemo wizi wa kura na udukuzi kupitia mitambo ya
kujumlisha kura
Wakati hayo yakitokea, Mutharika
anayeonekana kujiamini, aliwataka wafuasi wake na wananchi wa Malawi, kuwa
watulivu wakati taratibu nyingine zikisubiriwa kufuatwa.
No comments:
Post a Comment