PROFESA TIBAIJUKA ATAJA VIKWAZO VYA UPANGAJI MIJI



Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Profesa Anna Tibaijuka amesema  zoezi  la upangaji miji, haliwezi kufanikiwa, iwapo wanaohusika hukimbilia mahakamani huku  kesi zikichukua muda mrefu kutolewa maamuzi.
Profesa Tibaijuka alisema hayo mwishoni mwa wiki jijini Dar es Salaam, wakati akizungumza na watumishi wa wizara hiyo kwa lengo la kuwapatia nyenzo za kujiboresha katika utendaji.
Kuhusu mipango miji, alisema mchakato wa mahakama umekuwa ukiwakwamisha, jambo ambalo husababisha utekelezaji wa mikakati yake ya upangaji miji kuchukua muda mrefu.
“Sio kwamba tunaogopa wala kukosa nguvu katika kutekeleza zoezi la upangaji miji na hata bomoabomoa...ni suala la kisheria ambapo wamenifunga kasi, kwani kila anayehusika anakimbilia mahakamani,” alisema Profesa Tibaijuka.
Alitolea mfano maeneo ya fukwe kuwa walioko huko, wamekwenda mahakamani,  ambapo kwa hali hiyo kazi ya upangaji miji haiwezi kufanikiwa, kwani hata mahakama pia hazina kasi na wakati mwingine kuweza kusubiria hadi awamu nyingine ya uongozi.
Kuhusu  migogoro ya wafugaji na wakulima, alisema serikali ina mpango wa kurejesha baadhi ya ranchi zake kwa wafugaji ili kuacha kutangatanga katika kutafuta malisho yaliyo bora kwa mifugo.
Wakati huo huo, Rais Jakaya Kikwete amemteua Zakhia Meghji kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) huku Profesa Tibaijuka akiteua wajumbe saba wa Bodi hiyo katika uteuzi ulioanza April mosi.
Aliwataja wajumbe hao kuwa ni Charles Mafuru, Bedason Shallanda, Irene Isaka, Subira Mchumo, Patrick Rutabanzibwa, Diotrephes Mmari na Samson Kassala.
Aidha Profesa Tibaijuka amemteua Profesa Bavo Nyichomba kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Wakala wa Taifa wa Utafiti wa Nyumba na Vifaa vya Ujenzi (NHBRA) na wajumbe watano Bodi hiyo ni Dk. Yususu Fundi, Moshi Zebedia, Dk. Nicolas Nyange, Hilda Gion na Pius Tesha.

No comments: