PLAN YAWEZESHA VIJANA 700 KUJIAJIRI KILOMBERO



Vijana 700 wa Wilaya ya Kilombero mkoani Morogoro, wamenufaika na mafunzo  ya ufundi wa stadi za awali za ajira za kuwawezesha kujiajiri wenyewe na kuondokana kuwategemea wazazi wao na  kuwaokoa katika wimbi la kukaa vijiweni.
Vijana hao wamenufaika na mafunzo hayo  chini ya  ufadhili  wa Shirika la Plan International kwa kushirikiana na Serikali ya Canada kupitia Shirika lake la Maendeleo (CIDA).
Mpango huo wa kuwawezesha vijana ni wa miaka minne , ulianza mwaka 2011 na kutarajiwa kumalizika mwakani.
Meneja Miradi wa Plan Tawi la Ifakara, Emmanuel Mmbaga , alisema hayo jana wakati akimkaribisha  Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya hiyo,  Azimina Mbilinyi,  kwenye mahafali ya tatu ya wahitimu  150 wa  mafunzo ya ufundi wa stadi za awali za ajira  kutoka vijiji kadhaa vya  Tarafa ya Mang’ula, wilayani humo.
Kwa mujibu wa Meneja miradi huyo, Shirika la Plan International  limeona umuhimu wa kuanzisha mpango huo hasa baada ya kuona changamoto mbalimbali zinazowakabili vijana hapa Tanzania hususani  tatizo la ajira.
Hata hivyo alisema mpango huo umezingatia usawa kwa asilimia 50 zilizo sawa kwa vijana wa kiume na wa kike ambapo mafunzo hayo ni ya miezi minne katika fani ya udereva wa magari, upishi, udereva wa magari madogo na pikipiki.
Kwa upande wake Mkurugenzi  Mtendaji wa Halmashauri hiyo, katika hotuba yake iliyosomwa na  Ofisa Elimu wa Sekondari wa wilaya hiyo, Jackson Mpankuly, aliwataka wazazi  na jamii kuona umuhimu wa kuchangia mpango huo.
Alisema kuchangia kwao katika mpango huo, kutawahakikishia vijana nchini kutimiza malengo yao ya kujitengenezea maisha na pia kuchangia  namna ya kukabiliwa na tatizo la ajira kwa vijana.
Katika mradi huo wa mafunzo, Plan imeelekeza nguvu zake kwa vijana wa kata za Mang’ula, Mwaya, Kisawasawa, Mchombe na Mngeta, hususani kwa vijana wanaoishi katika mazingira magumu.

No comments: