Mtoto mwenye umri wa
miaka minne aliyefungiwa ndani ya boksi kwa zaidi na miaka mitatu mkoani
Morogoro, amehamishiwa katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) kwa ajili ya
uchunguzi na tiba zaidi huku wataalamu wakikuna vichwa namna ya kumrudishia
afya yake.
Imeelezwa jopo la
madaktari bingwa wa magonjwa mbalimbali ya binadamu wakiwemo wataalamu wa
saikolojia, wanahitajika kwa ajili ya kumwezesha mtoto huyo mwenye ulemavu kuwa
katika hali ya kawaida.
Aidha, pamoja na uhitaji
wa jopo la wataalamu hao, mtoto huyo ambaye amelazwa katika wadi ya watoto,
atahamishiwa katika wadi maalumu ya watoto wenye utapiamlo awe karibu na
uangalizi wa lishe baada ya kubainika ana udhaifu mkubwa wa lishe.
Wakizungumza na mwandishi
jana jijini Dar es Salaam kwa nyakati tofauti hospitalini hapo, Daktari Bingwa
wa Watoto wa MNH, Dk Mwajuma Ahmada alisema mtoto huyo hajazidiwa
kuumwa.
Alisema walimpokea juzi
usiku na hatua za awali zilizofanywa ni pamoja na kuchukua baadhi ya
vipimo kwa ajili ya uchunguzi.
“Mtoto aliletwa hapa jana
(juzi) usiku, baadhi ya vipimo vimechukuliwa, vingine atafanyiwa leo
(jana) ikiwa ni pamoja na kumfanyia huduma ya kum scan (kumwingiza kwenye
mashine maalumu) mwili mzima ili tufahamu tatizo na tiba sahihi,” alisema
Dk Ahmada.
Alisema huduma ya tiba
kwa mtoto huyo siyo ya daktari bingwa mmoja bali inahitaji jopo la wataalamu
wakiwemo wa mifupa, saikolojia, viungo na magonjwa mbalimbali ya binadamu
kumsaidia mtoto huyo.
“Kwa sasa hatuwezi
kusema lolote kubwa kuhusu mtoto huyo ndio kwanza kafika na ndiyo tuko
kwenye hatua ya awali ya kuchukua vipimo, na leo atafanyiwa huduma ya kumulikwa
mwili mzima ili tujue tunaanzia wapi”, alisema Dk Ahmada.
Alisema pamoja na
kusubiri majibu ya vipimo, hatua wanayochukua ni ya kumhamishia kwenye wadi ya
watoto wenye utapiamlo, ili kutibu maradhi hayo ambayo ndio yameonekana awali,
kwani mtoto amekosa lishe na virutubisho muhimu vya awali.
Alifafanua, katika hatua
hiyo ya awali, mtoto huyo atakuwa akipewa maziwa ya lishe na kuendelea na tiba
ya dawa za kuua vijasumu kutokana na kusumbuliwa na vichomi.
Akizungumzia kwa ufupi
ikiwa mtoto huyo anaweza kurejea katika hali ya kawaida kwa viungo kunyooka na
kutembea, Dk Ahmada alisema pamoja na kusubiri majibu ya vipimo, lakini
pia tiba ya mtoto inategemea zaidi historia ya mtoto mwenyewe.
“Tiba ya huyu mtoto
inategemea pia historia halisi ya mtoto husika, sasa hapa pana ugumu kwa
kuwa mlezi wake wa sasa haifahamu historia vizuri ya mtoto, tunahitaji
kuifahamu historia yake, mtoto alizaliwaje, hii ina maana kuwa je alizaliwa
akiwa hana ulemavu wowote? Au ukuaji wake ulikuaje, sasa hatujapata mtu wa
kutupa taarifa sahihi za mtoto”, alisema Dk Ahmada.
Alisema kitaalamu,
mazingira ya kuishi tu ndani ya boksi bado hayatoi picha sahihi ya athari
za sasa za mtoto huyo alizopata, na kwamba zipo sababu za kufahamu
historia hasa ya undani ya mtoto huyo iweze kutoa dira kwa wataalamu wa
tiba hospitalini hapo.
Alisema pamoja na kwamba
mtoto huyo atapatiwa tiba, lakini bado athari zitabaki za ukuaji wake.
Alifafanua kwamba kwa hali ya sasa, kimo chake na kutotembea haviendani
na umri wake.
Aliongeza, baada ya
vipimo kutokana na tatizo kujulikana watafahamu wapi pa kuanzia na hilo
litafanywa kwa ushirikiano wa jopo hilo la wataalamu na kwamba anaamini tiba
sahihi itarejesha afya ya mtoto huyo.
Kwa upande wake, Ofisa
Muuguzi Mwandamizi wa Wadi B ya watoto hospitalini hapo, Clara Nahum, alisema
hali ya mtoto siyo mbaya ila ana utapiamlo uliokithiri.
Muuguzi huyo alisema,
hali ya mtoto inaonesha alikosa huduma muhimu ikiwemo virutubisho muhimu
vilivyohitajika wakati wa makuzi ya awali.
“Amekosa mahitaji muhimu
yakiwemo madini na hata madini ya mwanga, hivi sasa tunamtibu vichomi na bado
anaendelea kuchukuliwa vipimo na majibu yakitoka madaktari watajua wapi pa
kuanzia, ila tunamhamishia wodi ya watoto wenye utapiamlo “, alisema Nahum.
Alisema katika wadi hiyo
kuna wataalamu wa lishe ambao wanafahamu watoto wenye maradhi hayo jinsi ya
kuwatibu kwa kutumia vyakula lishe vinavyotolewa kulingana na hali ya mtoto
ilivyo.
Kwa upande wake, mlezi wa
mtoto huyo , Josephina Joel akizungumza na gazeti hili wadini hapo alisema
mtoto anaendelea vizuri ingawa juzi alikuwa na homa. Hata hivyo alisema
imeshuka, na kwamba kadri siku zinavyosonga, anaona uchangamfu wa mtoto.
“Tulifika hapa juzi
usiku, tulitoka Morogoro na gari ya wagonjwa saa 11, jioni tukafika hapa saa
tatu usiku tukapokewa na mtoto akafanyiwa baadhi ya vipimo ndipo tukaletwa
wodini saa saba usiku, nilikuwa nimechoka nikalala, mtoto akawa ananiamsha,
mama usilale amka tucheze, ila baadaye naye akalala”, alisema Josephina.
Alisema mtoto bado ana
woga wa mwanga kwani usiku ili alale anataka taa izimwe na wakati mwingine bado
anaogopa watu na kukataa wasimbebe na kuongeza akiwa anambeba mara nyingine
hulalamika anaumia viungo.
Mwandishi wa habari hizi,
alizungumza na mtoto huyo katika mahojiano mafupi:
Mwandishi: Unaitwa nani
mtoto mzuri?
Mtoto : Akataja jina lake
Mwandishi :Utakula nini?
Mtoto:Chipsi (viazi vya
kukaanga)
Mwandishi:Njoo nikubebe
Mtoto:Sitaki naumia.
Akizungumza na mwandishi
wa habari hizi jana mjini Morogoro, Mganga Mkuu Mfawidhi wa Mkoa Morogoro,
Rita Lyamuya alisema mtoto huyo amepelekwa Muhimbili kwa ajili uchunguzi
zaidi hasa kwa upande wa mifupa.
Alisema kwa kuwa juzi
kulikuwa na wagonjwa wengine ambao walipewa rufaa ya kwenda hospitalini hapo,
uongozi uliona ni vyema pia mtoto huyo aingizwe kwenye msafara huo badala
ya kusubiri jana kama ilivyokuwa imepangwa.
“Hatukuona haja ya
kusubiri mpaka asubuhi wakati gari tayari limepatikana kuna wagonjwa ambao
wamepangiwa kwenda huko,” alisema
Ofisa Ustawi wa Jamii wa
Mkoa wa Morogoro, Oswin Ngungamtitu alisema juzi walipofika hospitalini mkoani
humo kwa ajili ya kumjulia hali mtoto huyo na kukuta wauguzi wakimhangaikia
huku akiwa analia, iliwafanya washituke na kudhani kuwa amezidiwa.
Mtoto huyo alikuwa
akiishi na wanandoa Mariamu Said (38) na mumewe Mtonga Omar (30) ambao juzi
walifikishwa mahakamani na kusomewa mashitaka ya kula njama na kutenda ukatili
kwa mtoto huyo. Pia baba yake mzazi, Rashid Mvungi (47) mkazi wa Lukobe
alifikishwa mahakamani na kusomewa mashitaka hayo.
No comments:
Post a Comment