Serikali imeanza kupanua mtambo wa maji wa Ruvu Juu
ili kuongeza uzalishaji maji kutoka lita
milioni 82 hadi milioni 196 kwa siku, imeelezwa.
Pia
imeelezwa kuwa ukosefu wa malighafi, umesababisha matengenezo ya mtambo huo uliopo Mlandizi Wilaya ya Kibaha,
kuchelewa.
Hayo yalisemwa na Waziri wa Maji,
Profesa Jumanne Maghembe wakati akitoa ufafanuzi kuhusu matatizo ya uzalishaji
wa maji katika mtambo huo, kutokana na Mbunge wa Ubungo, John Mnyika kuomba
mwongozo bungeni.
Mnyika alitaka Serikali itoe kauli,
kueleza matatizo yanayoukabili mtambo wa kuzalisha na kutibu maji kwa ajili ya
Jiji la Dar es Salaam na katika Mkoa wa Pwani.
Profesa
Maghembe alisema kuwa gharama za mradi wa upanuzi wa mtambo huo ni dola za
Marekani milioni 39.7, ambapo mkandarasi
ameshaanza kazi Februari mwaka huu na atakamilisha Agosti 14, mwakani.
Alisema
uwezo wa mtambo huo ni kuzalisha maji lita milioni 82 kwa siku na unaendeshwa
kwa kutumia seti tatu za pampu katika shughuli za uzalishaji maji.
Alisema
kwa nyakati tofauti, matengenezo yamechukua muda mrefu, kutokana na kutokupatikana kwa wakati malighafi zinazohitajika.
Alisema
wizara katika kukabiliana na matukio hayo, imechukua hatua za kuchonga vipuri
na vifaa vya pampu katika karakana zilizopo nchini kwa kutumia wataalam wa
jeshi, kuagiza vipuri nje ya nchi na kutoa matangazo kwa wananchi kuhusu
upungufu wa maji pale uzalishaji unaopungua au kusimama.
Aliongeza
kuwa pamoja na kuchukua hatua za dharura, vifaa na vipuri vya ziada vimeagizwa
kutoka nje ya nchi na vingine kuchongwa katika karakana za ndani na kuvihifadhi
kwa ajili ya dharura.
Pia,
alisema mpaka sasa zipo seti mbili za pampu kwa ajili ya dharura. Aidha, Mtambo wa maji Mtoni unafanyiwa ukarabati na Mamlaka
ya Majisafi na Majitaka Dar es Salaam (DAWASA), wameagiza pampu mbili mpya kwa
ajili ya kuchotea maji ghafi.
"Pampu
hizi zitawasili Agosti mwaka huu. Mkandarasi amekamilisha tathmini ya ukarabati
unaohitajika ili mtambo ufanye kazi vizuri katika kipindi chote cha mpito cha
miezi 18 wakati mtambo mpya unajengwa," alisema.
Aidha, alisema Serikali inaendelea
kudhibiti wizi mkubwa wa maji, unaofanyika katika Jiji la Dar es Salaam katika
maeneo ya Kinondoni, Mwananyamala, Kigogo, Mabibo, Magomeni, Tegeta, Kiluvya,
Kibamba, Mbezi na Kimara.
Alisema jumla ya watuhumiwa wa wizi wa
maji 162, wamekamatwa na kufikishwa mahakamani hadi sasa.
Watuhumiwa 23 walipatikana na hatia
ambapo 19 waliamriwa kulipa faini ya kati ya Sh 200,000 na Sh 2,316,400 na
watuhumiwa wanne walifungwa.
Aliongeza kuwa kumekuwa na matukio
mengi na ya kufululiza ya kuathiri uzalishaji wa maji katika mtambo wa
kusafishia maji wa Ruvu Juu.
Matatizo hayo yanahusu kuharibika kwa
pampu, umeme kukatika mara kwa mara na kupasuka kwa mabomba.
Alisema
Wizara imeunda Kamati maalumu, ambayo imeanza kufanya tathmini ya kina, kujua
chanzo cha matukio hayo.
Alisema
kamati hiyo itafanya uchunguzi, kubaini kama matatizo hayo yanatokana na mifumo
ya kiufundi, kiuendeshaji au makosa ya kibinadamu.
Kamati
inatarajiwa kutoa taarifa yake katika kipindi cha mwezi mmoja na hatua
zitaendelea kuchukuliwa ili kuhakikisha mtambo unarudi katika hali yake ya
kawaida.
No comments:
Post a Comment