MNYIKA ATAKA BAJETI YA WIZARA YA MAJI ISISOMWE LEO



Mbunge wa Ubungo, John Mnyika ameshauri bajeti ya Wizara ya Maji isisomwe leo bungeni,  badala yake irudishwe kwenye kamati ya bajeti  waifumue kwa kuiongezea fedha.  
Katika mkutano na waandishi wa habari jana mjini hapa,  Mnyika alisema bajeti  ya mwaka unaomalizika haikutekelezwa  kwani asilimia 27 ya fedha zilizopangwa, ndizo zimetolewa.  
Mnyika ambaye ni Kaimu Kiongozi wa Upinzani Bungeni, alisema  amebaini hayo kupitia randama za wizara hiyo zilizowasilishwa juzi bungeni.
Alisema leo  anamwandikia  Waziri wa wizara hiyo, Profesa Jumanne Maghembe kumshauri asisome bajeti hiyo na wakati huo huo Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni inakaa kikao kujadili namna ya kuzuia bajeti hiyo isisomwe.
Alisema mradi wa Programu ya Vijiji 10 kila halmashauri pamoja na Mpango Maalumu wa Maji wa Jiji la Dar es Salaam haijatekelezwa, licha ya serikali katika bajeti iliyopita kuahidi kuitekeleza katika bajeti hii.  
“Tulipewa matumaini  katika Bunge la Bejeti lililopita kwamba bajeti  ya Wizara ya Maji imeongezwa. ..tulipewa matumaini hewa   kwamba bajeti imeongezwa mpaka bilioni 312.1 sawa na nyongeza ya asilimia 123 ikilinganishwa na bajeti  ambayo ilitangulia ya Sh bilioni 140.1,” alisema Mnyika.
Hata hivyo Mnyika alisema randama iliyotolewa bungeni juzi, inasema kulingana na changamoto ya upatikanaji wa fedha, upande wa fedha za ndani kiasi kilichotolewa ni Sh bilioni 86 pekee sawa na asilimia 27.6 ambazo kati ya hizo, Sh bilioni 44.8 zimepelekwa kwa maji vijijini.
Alisema mradi wa maji wa vijiji 10 kila halmashauri umetengewa Sh bilioni 34 pekee. Alisema kiwango cha fedha kilichotolewa kwa mradi huo hakifiki hata theluthi moja ya kiasi kilichotengwa ikizingatiwa mwaka wa fedha unaisha Juni 31. 
Alisema sehemu kubwa ya miradi vijijini haijakamilika hadi leo. “Tunajadili vipi bajeti mpya wakati ambapo bajeti iliyotangulia utekelezaji ni finyu,” alihoji.  
Natoa mwito kwa wananchi, na wabunge wengine kuunga mkono kuhakikisha bajeti ya wizara ya maji haijadiliwi kesho. Alisema kama Waziri Maghembe atapuuza kutosoma bajeti, atalazimika kumtaka ajiuzulu na Waziri Mkuu ndiye afanye kazi ya kuondoa hoja kuipeleka kwenye kamati ya bajeti.  
Alipoulizwa  ni nini yeye pamoja na upinzani watafanya iwapo bajeti hiyo itasomwa, Mnyika alisema kwa sasa hawezi kueleza serikali watakachofanya. “Tutachukua hatua za ziada isisomwe…nitashauriana na wabunge wengine wa Ukawa bungeni kushauriana ni nini cha kuwafanya ili kuwe na uwajibikaji wa pamoja,” alisema Mnyika.
Kuhusu ni hatua gani serikali ingeweza kufanya  baada ya fedha za wafadhili kutotolewa mapema, Mnyika alisema, alisema fedha za wafadhili hazipaswi kuwa kisingizio kwa kuwa kipaumbele kingewekwa kwa kutenga asilimia 100 ya fedha za ndani.
Mnyika alisema suala si Waziri wa Maji, isipokuwa anayo orodha ya mawaziri wanaokwamisha mipango hiyo ya maji ambayo ikifika wakati, atawataja wote.

No comments: