MNYIKA AMSHITAKI MWENYEKITI MTENDAJI WA UDA BUNGENI



Mbunge wa Ubungo, John Mnyika amemshitaki Mwenyekiti Mtendaji wa Simon Group inayoendesha Kampuni ya Usafiri Dar es Salaam (UDA), Robert Kisena kwa Spika wa Bunge, Anne Makinda, kutokana na kudai wabunge wa Dar
es Salaam wamehongwa.        
Katika mkutano wake na waandishi wa habari mwishoni mwa wiki, Kisena alidai kushangazwa na upotoshwaji unaofanywa na Mnyika juu ya uhalali wa umiliki wa hisa za shirika hilo.
Kisena alikwenda mbali zaidi na kudai mbunge huyo anatumiwa na mfanyabiashara mmoja aliyedai kuwa tangu 2001 amekuwa akiendesha kampeni chafu ya kuichafua Simon Group Limited.
Lakini jana bungeni, Mnyika akitumia Kanuni za Bunge,  alisema Kisena amekiuka kanuni hizo kwa kuwatuhumu wabunge kuwa wamehongwa, ilhali Serikali ndiyo iliyoweka bayana umiliki wa Uda.
Kwa mujibu wa Mnyika, wiki iliyopita katika kujibu swali la Mbunge wa Kawe, Halima Mdee (Chadema), Serikali ilisema hisa za Uda zinamilikiwa kwa asilimia 100, tofauti na madai ya Kisena aliyedai wanamiliki asilimia 76 na zilizobaki zinamilikiwa na Serikali.
Katika jibu lake kwa swali hilo, Naibu Waziri wa Fedha, Adam Malima, alisema Serikali inamiliki asilimia 100 katika Uda kwa maana asilimia 51 zinamilikiwa na Halmashauri ya Jiji na asilimia 49 za Msajili wa Hazina.
Aidha, Malima alikiri kuwapo kwa utata kuhusu kwa mazingira ya uuzwaji wa shirika hilo kutoka pande zote mbili za umiliki yaani Halmashauri ya Jiji na Serikali.
Mnyika alisema Kisena ameingilia uhuru wa majadiliano bungeni ambao kwa mujibu wa Kanuni na Sheria za nchi, kwamba hautahojiwa nje ya Bunge, hivyo akataka apelekwe katika Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kinga,  Haki na Madaraka ya Bunge.
“Kwa hiyo, Mheshimiwa Spika, nataka suala hilo lifikishwe mbele ya Kamati ya Kinga, Hadhi na Madaraka ya Bunge kwani amekiuka haki ya majadiliano bungeni,” alisema Mnyika.
Katika hoja yake, Mnyika alirejea habari zilizoandikwa na gazeti hili na la Uhuru, katika matoleo yao ya juzi.
Kutokana na hilo, Spika Makinda ameigiza Kamati ya Kinga, Hadhi na Madaraka ya Bunge, ilifanyie kazi na kumpelekea majibu kwake kwa hatua za utekelezaji.
Aidha, Makinda alikataa mwongozo uliokuwa    ukiomba kuhusu madai ya kuwapo kwa vyeti feki vya taaluma vikiwahusisha wabunge na mawaziri kutokana na kitabu kimoja kilichoandikwa nchini.

No comments: