Aliyekuwa Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la
Umeme Tanzania (Tanesco), William Mhando, amepandishwa kizimbani katika
Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, akikabiliwa na mashitaka ya kutumia vibaya
madaraka kwa kutoa zabuni ya usambazaji wa vifaa kwa kampuni inayomilikiwa na
mkewe.
Mbali na Mhando, washitakiwa wengine katika
kesi hiyo ni mkewe Eva Mhando, ambaye ni Mkurugenzi wa Kampuni ya Santa Clara
Supplies. Wengine ni Wahasibu Wafawidhi wa Tanesco, France Mchalange na Sophia
Misidai pamoja na Ofisa Ugavi, Naftali Kisinga.
Washitakiwa hao walifikishwa mahakamani hapo
jana na kusomewa mashitaka na Wakili kutoka Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na
Rushwa (Takukuru), Leornald Swai mbele ya Hakimu Mkazi, Frank Moshi.
Kwa mujibu wa mashitaka yaliyosomwa
mahakamani, Mhando alitumia vibaya madaraka yake kwa kutoa zabuni ya kusambaza
vifaa vya ofisi vyenye thamani ya Sh 884,550,000 kwa kampuni inayomilikiwa na
mkewe.
Wakili Swai alidai kati ya Aprili Mosi na
Desemba 31, mwaka 2011 katika Makao Makuu ya Tanesco, Mhando alitumia vibaya
madaraka kwa kushindwa kuelezea ana maslahi na kampuni ya Santa Clara ambayo
mkurugenzi wake ni mkewe Eva na mtoto
wake, hivyo kuiwezesha kupata mkataba
kusambaza vifaa vya ofisi wenye thamani ya Sh 884,550,000 na kuipa faida ya Sh
31,747,000.
Katika mashitaka yanayomkabili Eva, Swai
alidai kati ya Januari 6 na Julai 30, mwaka 2011, sehemu isiyofahamika Dar es
Salaam, alighushi ripoti ya ukaguzi wa fedha ya Kampuni ya Santa Clara kwa
mwaka 2007/2008, kuonesha kuwa Finx Capital House ilifanyia ukaguzi kampuni
hiyo jambo ambalo si kweli.
Aidha inadaiwa Agosti 9, mwaka 2011, kwa njia ya
udanganyifu, mke huyo wa Mhando alighushi nyaraka za uhamishaji wa hisa
kuonesha kwamba amehamisha hisa 200 ambazo kila moja ina thamani ya Sh 10,000
kutoka kwa kampuni yake kwenda kwa Eveta John Shing'oma, jambo ambalo si kweli.
Swai aliendelea kudai kuwa, Agosti 5, 2011,
katika Makao Makuu ya Tanesco, huku akijua ni kwa nia ya udanganyifu, aliwasilisha
kwa Katibu wa Bodi ya Zabuni ya shirika hilo, ripoti ya ukaguzi wa fedha wa
kampuni yake kuonesha imeandaliwa na Finx Capital House.
Pia anadaiwa alijipatia Sh 31,747,000 kwa njia ya udanganyifu. Anadaiwa
kujipatia fedha hizo, kwa kusambaza vifaa vya ofisi, baada ya kuwasilisha
nyaraka za kughushi.
Nyaraka hizo zinadaiwa kuwa ni ripoti ya
ukaguzi wa fedha na orodha ya mikataba
ya miaka miwili. Anadaiwa kuwasilisha nyaraka hizo kwa Katibu wa Bodi ya Zabuni
ya shirika hilo, kuonesha kwamba kampuni
yake ilistahili kupewa zabuni kusambaza mashine ya kutoa nakala za karatasi na
kompyuta kwa mwaka 2011.
Katika mashitaka mengine, Mchalange, Sophia
na Kisinga wanadaiwa Oktoba 17, mwaka 2011
katika makao makuu ya Tanesco, wakiwa wajumbe wa Kamati ya Tathimini ya
zabuni ya usambazaji wa vifaa vya ofisi kwa mwaka huo, walitoa taarifa za uongo
kuonesha Santa Clara, imekidhi vigezo vya kupatiwa zabuni ya kusambaza vifaa
hivyo, huku ikiwa ni kinyume cha sheria.
Washitakiwa hao walikana mashitaka na Wakili Swai
alidai upelelezi wa shauri hilo umekamilika.
Hakimu Mushi alisema washitakiwa watapata
dhamana endapo watakuwa na wadhamini wawili wa kuaminika ambao watasaini hati
ya Sh milioni nane kila mmoja. Aidha washitakiwa hawatakiwi kutoka nje ya mkoa
wa Dar es Salaam, bila ya kibali cha mahakama.
Wote wako nje kwa dhamana baada ya
kukamilisha masharti hayo ya udhamini.
No comments:
Post a Comment