Wakati jamii ya Watanzania ikipigwa
butwaa na ukatili wa kutisha aliofanyiwa mtoto wa miaka minne kwa kufungiwa
ndani ya boksi kwa miaka mitatu mjini Morogoro, ukatili mwingine wa
kutisha dhidi ya watoto umeripotiwa
mkoani Kagera.
Katika mkoa huo, mganga wa kienyeji
ametiwa mbaroni, akituhumiwa kumuua kwa kumnyonga, kumkata mikono na kumzika
katika nyumba yake.
Mganga huyo, Mujingwa John (20) amekiri
mbele ya jeshi la polisi kuhusika na mauaji ya mtoto Fausta Geofrey (8),
mwanafunzi wa darasa la kwanza katika Shule ya Msingi Kitunga kata ya Muhutwe,
wilayani Muleba.
Anatuhumiwa kwamba, alimkamata kwa
nguvu akienda shule na wenzake, akamuua, kumkata mikono, nyama ya mgongo,
masikio na sehemu za siri kwa lengo la kuibanika na kutengeneza 'uchawi' wake,
kisha akachimba shimo na kuzika mwili ndani ya nyumba.
Tukio hilo lilithibitishwa na Kamanda
wa Polisi mkoa wa Kagera, George Mayunga aliyesema mganga huyo alikamatwa na
polisi kwa kushirikiana na wananchi, ambapo alikutwa akibanika viungo
alivyovikata kutoka kwa mtoto huyo.
Aidha, akiwa polisi, mganga huyo
alipewa fursa ya kueleza kilichotokea mbele ya waandishi wa habari, ambapo
alidai alifikia uamuzi wa kumuua mtoto
huyo, kutokana na hali ngumu ya umaskini inayomkabili.
Alisema baada ya kumkamata mtoto huyo,
alimkaba shingo na kumvuta hadi katika nyumba aliyokuwa akiishi, akamnyonga
hadi kufa na baada ya kufa, alimkata ngozi ya mgongoni, mikono akianzia na
mkono wa kushoto aliodai una bahati, sehemu za siri na masikio.
"Nilimkamata mtoto na kumuua,
maana niliona nikikamata mtu mzima atanizidi nguvu na kupiga kelele,"
alidai.
Alidai kuwa, "Nilipomaliza kumuua
nilichimba shimo chini ya kitanda changu nikamzika na kutandaza nyasi juu yake
ili isigundulike kama eneo hilo kuna shimo".
Mganga huyo aliyejitambulisha kuwa ni
Msukuma, alidai viungo hivyo ambavyo hadi polisi wanafika, alikuwa bado
akivikausha, angevichanganya na dawa ambayo angewapatia wateja wake ili
iwasaidie kufanikisha mambo yao, ikiwamo kupata bahati na utajiri na alitarajia
kuuza kwa Sh 500 kwa kila ujazo wa kijiko kimoja cha dawa yake.
Alisema hiyo ni mara yake ya kwanza
kufanya tukio la aina hiyo na kwamba alihamia Muleba mkoani Kagera miaka miwili
iliyopita akitokea Nyanguge wilaya ya Magu mkoani Mwanza. Alisema alirithi
uganga huo kutoka kwa babu yake mzaa mama na kuwa alianza uganga akiwa na umri
wa miaka minane na hakuwahi kwenda shule.
Ofisa Mtendaji wa Kijiji cha Bisole
katika Kata hiyo wilayani Muleba, Khamis Hassan, akizungumzia tukio hilo baada
ya mauaji hayo, alidai muuaji alimkata mtoto huyo mikono yake miwili kabla ya
kumzika.
Hassan alisema kuwa tukio hilo ni la
Mei 21 mwaka huu asubuhi katika kijiji hicho, wakati mtoto huyo akiwa na
wenzake wakielekea shuleni, ambapo inadaiwa aliitwa na kukamatwa na mganga
huyo, aliyetambulika kwa jina la Mujingwa John (20).
Alisema kuwa baada ya taarifa za mtoto
huyo kutoonekana kuzagaa, wanakijiji walikusanyana na kuanza msako, ambapo
walikamata kundi la watu waliokuwa wakiwahofia kuhusika, hasa vijana.
Alisema baada ya kuwakamata watu hao,
waliwaweka sehemu moja na kuwaita wanafunzi waliokuwa na marehemu, ambapo
walimtambua mganga huyo kuwa ndiye aliyemwita na kumkamata mtoto huyo.
Mtendaji huyo alidai baada ya mganga
huyo kutambuliwa, wananchi na polisi waliofika eneo hilo, walikwenda naye hadi
katika nyumba anayoishi na kumtaka awaonyeshe alipo mtoto huyo.
Alidai baada ya kumbana, aliwaonesha
sehemu alikomzika, ambapo walichukua jembe na kuanza kufukua mwili wa mtoto
huyo, uliokuwa umezikwa ndani ya nyumba aliyoishi mganga huyo.
Alidai baada ya mganga huyo kumuua
mtoto huyo, alimkata mikono yake miwili na kisha kuchimba shimo ndani ya
nyumba, ambapo baada ya kumzika alifukia shimo akatandaza nyasi juu yake na
kisha kuweka kitanda chenye godoro alilokuwa akilala.
Alisema kuwa alipohojiwa ili kujua nani
kamtuma kutekeleza unyama huo, mganga huyo alidai ilitokana na yeye kuoteshwa
na mizimu yake, iliyomtaka kumuua mtoto ili amkate viungo vyake kwa ajili ya
kuchanganya na dawa.
Alisema mikono hiyo alitaka kuibanika
kwenye moto ili aichanganye na dawa, ambayo angewapatia watu wanaohitaji kupata
utajiri.
Tukio hilo limekuja siku chache wakati
Jeshi la Polisi mkoani Morogoro, likiendelea na
uchunguzi wa kilichotokea mpaka mtoto mmoja mkoani hapa (jina
limehifadhiwa), akateswa na mama mlezi kwa kuwekwa katika boksi tangu akiwa na
miezi tisa, mpaka alipotimiza miaka minne.
No comments:
Post a Comment