Mfuko
wa Mitaji ya Wafanyabiashara (Mkoba Private Equity Fund), uliozinduliwa na Rais
Jakaya Kikwete hivi karibuni, umeelezwa kuwa ndio kimbilio kubwa kwa
wafanyabiashara wadogo na wa kati katika kupata mitaji ya kukuza biashara zao.
Balozi
wa Heshima wa Botswana Tanzania, Emmanuel ole Naiko, ameuelezea mfuko huo kuwa
kimbilio la wajasiriamali.
"Uzinduzi
wa mfuko huo umekuja wakati mwafaka kwa vile Tanzania tuna tatizo kwa
wajasiriamali wadogo na wakati kupata mitaji ya kuendeleza na kukuza shughuli
zao za kibiashara," alisema Ole Naiko mwishoni mwa wiki jijini Dar es
Salaam wakati akifungua semina ya siku moja ya wajasiriamali wa Asasi ya Diana
Women Empowerment Organization.
Alisema
Serikali kupitia Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC), imejitahidi kuweka mifumo
mizuri ya sheria kwa ajili ya wawekezaji wa ndani na nje, lakini tatizo
lililopo ni namna ya kupata mitaji kwa vile benki zina masharti magumu ya
kupata mikopo.
"Kwa
kweli uzinduzi wa mfuko huo utachochea shughuli za biashara na ujasiriamali
hapa nchini kwa vile kutakuwa na sehemu ya kupata mitaji," alisema na
kuongeza kuwa ni vyema wajasiriamali wachangamkie fursa za kuwepo kwa mfuko
huo.
Ole
Naiko ambaye pia ni mlezi wa asasi hiyo, aliwaasa pia wanasemina hao kuzingatia
mafunzo ya ujasiriamali na kwamba elimu, mbinu na maarifaĆ wanayoyapata
wayatumie kwa vitendo ili kuzidi kuendelea kibiashara.
"Mafanikio
katika biashara yanaanza kwa mtu mwenyewe na hakuna mtu anayeweza kuja
kuwaendeleza katika biashara zenu bila wenyewe kujitambua na kujiongezea
maarifa," alisema.
Aliwaasa
wajasiriamali hao kuzitumia fursa zinazojitokeza za kupata mikopo kwa ajili ya
kukuza biashara kwa faida yao na Taifa kwa ujumla, kwani mchango wa
wajasiriamali ni mkubwa sana.
Mwenyekiti
wa Taifa wa Asasi hiyo, Farida Khakoo alisema semina hiyo ilishirikisha
wajasiriamali 40 ambao ni wanachama wa asasi hiyo.
"Asasi
yetu inalea watoto yatima, walemavu na wajane na ina wanachama ambao ni
wajasiriamali," alisema.
Alisema
semina hiyo inalenga kuwafundisha namna ya kutunza kumbukumbu za hesabu za
biashara zao katika vitabu ili waendeshe vema biashara.
Mwanachama
na mjasiriamali wa asasi hiyo, Constance Chandende, alisema semina hiyo
itamwezesha kupata ujuzi zaidi wa kuendesha shughuli zake za ujasiriamali na
kufikia malengo.
"Mimi
biashara yangu ni ya kusindika matunda yakiwemo ya pilipili mbuzi, michaichai,
maembe na mbilimbi," alisema.
Alisema wanawake wengine nchini wasikae bila
kazi bali wajiingize katika biashara mbalimbali ili waweze kuwa na mchango
katika familia.
No comments:
Post a Comment