MENGI ASHAURI VIJANA WAACHE KUCHAGUA KAZI



Mwenyekiti wa Makampuni ya IPP amewataka wasomi nchini kuacha kubagua kazi badala yake wafungue macho na kuziona fursa zilizopo katika maeneo yao ili waweze kujiajiri.
Alisema iwapo vijana watafungua macho na kuona fursa zilizopo, nusu ya tatizo la ajira nchini litapungua kwa kuwa vijana watakuwa wanazitumia fursa hizo kujiajiri na kuajiriwa pia.
"Tatizo la vijana wetu wanachagua kazi, kwa usomi wao wanajiona hawawezi kufanya kazi fulani…wavulana hawataki kufanya kazi zingine kwa kudhani ni za wanawake na wanawake pia wanaona baadhi ya kazi ni za wanaume," alisema Mengi.
Alisema hayo wakati wa kutoa zawadi kwa tweet bora ya mwezi Aprili.
Mengi alisema fikra na mawazo ya vijana juu ya kazi ni lazima yabadilike ili macho yao yafunguliwe waone fursa nyingi zilizopo nchini.
Mengi pia alisema wazazi wanalo jukumu la kuwaandaa watoto wao namna ya kujitegemea, ikiwa ni pamoja na kumtanguliza Mungu na kuwa waaminifu katika shughuli zao.
Swali la tweet la Aprili lilihoji namna gani wazazi wanapaswa kuwaandaa watoto wao ili wawe na uchumi mzuri, mawazo mengi yaliyotolewa  waliacha kumtegemea Mungu na kuwa mwaminifu maishani.
Mshindi wa kwanza katika shindano hilo ni Abnery Mwogela ambaye ni mwalimu wa shule ya msingi kutoka Njombe aliyejinyakulia Sh 1,000,000. Mshindi wa pili aliyejinyakulia Sh 500,000 ni Samson Shila na mshindi wa tatu aliyepata Sh 300,000 ni Gerald Nyaissa wa Dar es Salaam.
Wazo la mshindi wa kwanza lilisema mzazi amuandae mwanawe kuishi kwa kujiamini, kuthubutu, kuanza kufanya anachodhani ni vyema akifanye kwa wakati huo cha kiuchumi, wazo la mshindi wa pili lilisema mzazi amwandae mtoto katika mambo makuu manne, elimu, kupenda kufanya kazi kwa bidii, ubunifu na kupenda kumcha Mungu.
Wazo lililoshinda nafasi ya tatu lilisema kila siku mzazi amnong'oneze mwanawe, Mungu amewapa matajiri saa 24 kwa siku sawa na anayokupa wewe, yatumie masaa hayo kwa faida."

No comments: