MEMBE ASHAURI WATANZANIA WAACHE KWENDA LIBYA



Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe ameshauri Watanzania kutokwenda sasa Libya, kutokana na mgogoro unaoikumba nchi hiyo. 
Alisema katika mgogoro wa Libya, hali ya usalama bado ni tete, jambo lililofanya ofisi za balozi mbalimbali  mjini Tripoli na Beghazi kufungwa. 
 Membe alisema hayo jana wakati akiwasilisha bungeni makadirio ya mapato na matumizi ya wizara hiyo mwaka wa fedha ujao ya Sh bilioni 191,919,748,000.00.
Aidha, alitoa msimamo wa Serikali juu ya mgogoro wa Ukraine na kusema Tanzania haitafungamana na upande wowote.
Alisema hatua hiyo, inalenga kuepuka kuingia kwenye  mgogoro huo unaotishia amani na usalama wa dunia kwa kuirudisha tena kwenye vita baridi.
 Membe alisema kuhusu mgogoro wa Ukraine unaotishia  kuigawa dunia katika pande mbili kwa zinazounga mkono kujitenga kwa jimbo la Crimea zikiongozwa na Urusi na zinazopinga zikiongozwa na mataifa ya Ulaya na Marekani. 
Alisisitiza, “msimamo wa Tanzania ni kutofungamana na upande wowote na inaendelea kuiomba Jumuiya ya Kimataifa kushughulikia  mgogoro huo kwa kutumia hekima na busara ambayo itaiepusha dunia kuingia kwenye vita.”
Akizungumzia uraia wa nchi mbili, Membe alisema,  “suala hili tayari limewekwa kwenye rasimu ya Katiba mpya na tutajadili kwa nguvu za hoja na kwamba umefikia wakati wa nchi yetu kuwa na sheria ya kuruhusu uraia pacha kwa maendeleo na maslahi ya taifa  na matumaini yangu ni  kuwa Bunge litaunga mkono pendekezo hilo.”
Kuhusu mgogoro wa Malawi, Waziri Membe alisema kwa sasa Wizara inaandaa majibu kwenye jopo la usuluhishi, kueleza hasara tutakazopata endapo itaamriwa kuwa mpaka upite kwenye ufukwe wa Ziwa Nyasa.
Hatua hiyo imetokana na jopo hilo linaloongozwa na  Rais mstaafu wa Afrika Kusini ,Thabo Mbeki kushauri hoja za kisheria kuwekwa pembeni  na kujadili hoja zinazogusa maisha ya kila siku ya kijamii.

No comments: