Jeshi la Polisi nchini limewaagiza
Makamanda wa Polisi wa Mikoa, kuhakikisha wanavidhibiti na kuvitokomeza vikundi
vyote vinavyojihusisha na vitendo vya uhalifu, ikiwemo uporaji, unyang'anyi na
kujeruhi watu katika maeneo mbalimbali.
Agizo hilo limetolewa na Naibu Inspekta
Jenerali wa Polisi Nchini (DIGP), Abdulrahman Kaniki.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa kwa
vyombo vya habari na msemaji wa Jeshi la Polisi, Advera Senso, hatua hiyo
imetokana na kushamiri kwa matukio ya uhalifu na yanayojenga hofu miongoni mwa
jamii, ikiwa ni pamoja na vikundi vinavyozidi kuibuka na kutishia amani katika
Kanda Maalumu ya Dar es Salaam.
Vikundi hivyo ni pamoja na vile
vilivyojipachika majina ya mbwa mwitu, watoto wa mbwa au panya road, ambavyo
vimekuwa vikifanya uporaji, unyang'anyi wa kutumia nguvu na kuwajeruhi watu
katika maeneo mbalimbali.
Makamanda hao wametakiwa kuhakikisha
wanavitafuta vikundi hivyo popote vilipo na kuwakamata kisha kuwafisha katika
vyombo vya sheria.
"Naibu IGP amekemea vikali vikundi
hivyo na kuvitaka kuacha tabia hiyo mara moja, kwani vitendo hivyo ni vya
kihalifu na vinatakiwa kukemewa na kila mtu katika jamii," ilieleza
taarifa hiyo ya Senso.
Aidha, iliwataka wananchi kuondoa hofu
na badala yake watoe ushirikiano kwa kutoa taarifa za vikundi hivyo katika
vituo vya Polisi ili hatua za haraka ziweze kuchukuliwa.
No comments:
Post a Comment