MBUNGE ASHAURI WAZIRI WA KILIMO ATAFUTE KAZI NYINGINE



Mbunge wa Mwibara, Kangi Lugola (CCM) amesema haiingii akilini kuona Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika kuendelea kuwa madarakani licha ya kushindwa kusimamia maeneo muhimu ya kilimo kama wakulima kupelekewa mbegu na mbolea bandia.
Alitoa kauli hiyo jana wakati akichangia hotuba ya makadirio ya matumizi ya fedha ya Wizara ya Kilimo, Chakula na Ushirika.
Alisema wakulima wamekuwa wakipelekewa pembejeo feki na Waziri amekuwa kimya.
“Inakuwaje Waziri, wakulima wanapelekewa pembejeo feki bado Waziri, analipa ruzuku mbegu ya pamba isiyoota haiingii akilini,” alisema. 
Alisema kuna raia wa China ambaye alikuwa mkandarasi katika daraja huko Kilombero na aliamua kujiua kwa ajili ya kujenga daraja lililokuwa chini ya kiwango.
Alisema hamshauri  Waziri ajiue, lakini kwa vitendo hivyo Waziri angeacha kazi  na kupumzika na kufanya kazi mbadala.
“Wizara hii itakigharimu Chama Cha Mapinduzi (CCM) ukiangalia hotuba ya Waziri Mkuu mwaka jana  ilisema Serikali iko kwenye mchakato wa kuanzisha bima ya bei ya pamba lakini kwenye hotuba ya Waziri hakuna mahali ambapo mfuko huo ulizungumziwa,” alisema na kuongeza.
“Nchi hii itaendeshwa kwa usanii mpaka lini? Itakuwaje Mbunge wa Mwibara nikuunge mkono kwenye jambo la kisanii kama hili? Kwenye jimbo langu tuna mabonde mazuri lakini mpaka leo tunataka tupewe skimu ya umwagiliaji, lakini Serikali ya CCM haitaki kutusikia katika mazingira ya kudanganyana, wananchi wa Mwibara Mbunge wao ni mimi nitakuwa mgeni wa nani? Alihoji mbunge huyo.
Alisema hawezi kukubaliana na hotuba kila wakati maneno ni yale yale  na utekelezaji wake umekuwa ni mdogo. “Nitawaambia nini wakulima wa Mwibara?” Akahoji. 
Mbunge wa Sumve, Richard Ndasa (CCM) alisema  Waziri alikuwa wa kwanza kupinga mbolea ya minjingu baada ya kuingia jikoni je hiyo mbolea ya minjingu inafaa?
Hata hivyo Mbunge wa Mbozi Magharibi, David Silinde alisema mwaka jana bajeti  ya kilimo ilitengewa bilioni 81 lakini iliyotoka ni bilioni 41 hali ambayo ilifanya baadhi ya miradi kushindwa kutekelezwa.
Mbunge wa Viti Maalum, Esther Bulaya (CCM) alisema si sera ya CCM kufumbia macho watu wanaofanya ubadhirifu kwenye sekta ya kilimo na kutaka kuchukuliwa kwa hatua kwa wote wanaohujumu miradi ya kilimo.
Mbunge wa Namtumbo, Vita Kawawa (CCM) alitaka Serikali kulipa fidia kwa wakulima waliopata hasara kutokana na kuuziwa mbegu feki kwani wakulima wengi ni masikini.
Huku Mbunge wa Maswa Magharibi, John Shibuda (CCM), alimtaka Waziri Mkuu na Waziri wa Kilimo kutembelea wakulima wa pamba ili kuona changamoto wanazokabiliana nazo.

No comments: