Mafundi na vifaa kutoka nchini Canada kwa
ajili ya kutengeneza ya mashine mbili za
mionzi zilizoharibika katika Taasisi ya Saratani ya Ocean Road, watawasili
nchini wakati wowote na matengenezo hayo yatagharimu Sh milioni 740.
Imeelezwa matengenezo hayo, yatachukua siku
nne na tayari serikali imelipa Sh 365,046,000 ikiwa ni nusu ya gharama zinazotakiwa.
Naibu Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii,
Kebwe Stephen Kebwe aliliambia bungeni jana wakati akitoa kauli ya serikali
kuhusu hali ya mashine za mionzi za taasisi hiyo ya Ocean Road.
Alisema mashine zinazotoa tiba ya mionzi
katika taasisi hiyo ni mbili na hutibu asilimia 95 ya wagonjwa wa saratani na
wanaohitaji mionzi na nyingine ndogo
inayotumika kwa wagonjwa wachache, hasa wenye saratani ya ngozi.
“Kwa kawaida mashine hizi zinatakiwa
kufanyiwa matengenezo kila baada ya miezi mitatu, aidha mafundi wa kutengeneza
mashine hizo wanatoka nje ya nchi hivyo kuharibika kwa mashine hizo
kunasababisha wagonjwa kukosa huduma kwa muda” alisema
Kebwe alitaja mashine zinazohitaji
matengenezo ni Equinox no 2002, ambayo chanzo chake cha mionzi bado ni kizima,
lakini imeharibika na Equinox no 2004
inayohitaji chanzo kipya cha mionzi.
Alisema mtengenezaji pekee wa mashine hizo ni
kampuni ya Theratronics kutoka Canada na ilipewa zabuni kutengeneza mashine
hizo.
“Kampuni hiyo itatakiwa kuharibu vyanzo vyote
vya mionzi vitakavyotokana na utengenezaji wa mashine hizo za mionzi na
ubadilishaji wa vyanzo vya mionzi, ufungaji wa vipuri vipya na kubeba masalia
yote ya vipuri kutoka mashine zote mbili na kurudisha nchini Canada ili
kudhibiti isilete madhara kwa watanzania,” alisema.
Naibu waziri huyo alisema mwaka 2013/2014
taasisi hiyo ilihudumia wagonjwa 4,712 wa saratani, ikiwa ni ongezeko la
wagonjwa 976, ikilinganishwa na kipindi cha mwezi Julai hadi Machi mwaka
2012/2013.
Alisema wagonjwa 3,295 walitibiwa kama wagonjwa
wa nje na 1,417 walilazwa huku wanawake
4,985 walifanyiwa uchunguzi wa saratani ya shingo ya kizazi na matiti. Kati ya
hao wanawake 197 waligundulika na dalili za awali za saratani ya kizazi na 61 walikuwa
na dalili za kuwa na saratani ya matiti.
“Nia ya serikali ni kuona mashine hizo
zinaanza kufanya kazi mapema iwezekanavyo ili wananchi waendelee kupata huduma
hizo za mionzi,vile vile serikali itaajiri Biomedical Engineers katika
hospitali zetu za rufaa ikiwemo ORCA ili waweze kushirikiana na kupata elimu
kutoka kwa wataalamu hawa kutoka Canada watakaofika kutengeneza ili baadaye
kujenga uwezo wa kufanya matengenezo kinga wenyewe,” alisema Kebwe.
No comments:
Post a Comment