MALAWI WAPIGA KURA LEO KUCHAGUA RAIS NA WABUNGE



Wananchi wa Malawi, leo wanapiga kura kuchagua rais atakayeiongoza nchi hiyo kwa kipindi kingine cha miaka mitano. Kadhalika, watachagua wabunge na madiwani.
Hii ni mara ya kwanza kwa wananchi wa Malawi kupiga kura tatu. Chaguzi za nyuma zilihusisha urais na ubunge pekee huku uchaguzi wa madiwani ukifanywa siku tofauti.
Katika siku za kuelekea uchaguzi wa leo, wagombea urais ambao ni 12 walikuwa wakifanya kampeni katika maeneo mbalimbali ya nchi hadi usiku ili kuvutia wapiga kura. Taratibu za Malawi zinaruhusu kufanya kampeni hadi usiku.
Kura za maoni za karibuni zilizotafitiwa na taasisi ya Afrobarometer zilionesha kwamba wagombea wanne wakubwa wanaowania urais wa nchi hiyo na kupewa nafasi kubwa ya kushinda wanazidiana kidogo sana.
Wagombea hao wanne ambao mmoja wao anatarajiwa kuwa rais kutokana na kura za leo ni Lazarus Chakwera wa chama cha upinzani cha Malawi Congress Party (MCP), Atupele Muluzi wa chama cha United Democratic Front (UDF), Peter Mutharika wa  Democratic Progressive Party (DPP) na Rais wa sasa wa nchi hiyo, Joyce Banda anayetokea chama tawala cha People’s Party (PP).
Takriban vyama hivyo vinne vikubwa vinavyotazamiwa kutoa rais vilishawahi kuongoza nchi hiyo huko nyuma na takriban vyote, wakati wa kampeni vilijikita katika kudhamiria kuondoa umaskini na njaa kupitia kilimo na kuongeza ajira kwa vijana.
Wagombea wote hawajawahi kugombea nafasi kubwa kama hiyo isipokuwa Rais Joyce Banda, maarufu kama  JB (kifupi cha majina yake),  katika uchaguzi wa mwaka 2009 alikuwa mgombea mwenza wa Rais wa zamani wa nchi hiyo, Bingu wa Mutharika. 
Hata hivyo, JB aliamua kuunda chama chake cha kisiasa baada ya kushindwa kuiva na rais Bingu wa Mutharika, ingawa aliendelea kuwa Makamu wa Rais 'kiubishiubishi'.
JB ambaye ni mke wa Jaji Mkuu mstaafu wa Malawi, Richard Banda, alitawazwa kuwa rais kufuatia kifo cha Mutharika mwaka 2012 kwani katiba ya Malawi inasema Makamu wa Rais ashike nafasi hiyo kama kitatokea kifo cha Rais.
Mgombea urais wa DPP, Profesa Peter Mutharika ni mdogo wa Hayati Bingu wa Mutharika wakati Atupele Muluzi ambaye ana miaka 35 na hivyo kuwa mgombea urais kijana zaidi kuwahi kutokea nchini humo ni mtoto wa Rais wa zamani wa nchi hiyo, Bakili Muluzi. 
Dk Chakwera ni sura mpya ambayo chama kilicholeta uhuru wa nchi hiyo kupitia kwa hayati Dk Kamuzu Banda cha Malawi Congress Party kimemsimisha mwaka huu. Huko nyuma, chama hicho kilikuwa kikimsimamisha mkongwe wa siasa nchini humo, John Tembo, lakini alikuwa hafanyi vizuri. Kabla ya kuingia kwenye siasa, Chakwera alikuwa mchungaji na Rais wa Kanisa la Assemblies of God.

No comments: