MAKABURI YA SHEIKH YAHYA, SHEIKH KASSIM YAJENGWA UPYA


Serikali imesema imetimiza ahadi ya kujenga makaburi ya  marehemu Shehe Yahya Hussein na Shehe Kassim Bin Juma, yaliyovunjwa na watu wasiojulikana  wakati wa 'Operesheni  Safisha Jiji' hivi karibuni kwa Sh milioni 3.9. 
Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Said Meck Sadik alisema Manispaa ya Ilala ilipewa kazi ya kujenga makaburi hayo na baada ya kukadiria  gharama za ujenzi, walitaka zaidi ya Sh milioni 9.7, lakini  haikukubaliwa. 
Alisema baada ya familia za marehemu hao kusikia gharama hizo, hawakukubali na kueleza kuwa makaburi ya Kiislamu, hayajengwi kifahari kiasi hicho na kuamua kutafuta mjenzi wao.
Alisema walipomleta mjenzi huyo, alikadiria gharama hiyo ya Sh milioni 3.9, ambapo mjenzi huyo alikubalika na kupewa fedha hizo na kuanza ujenzi wa kaburi la Shehe Kassim Bin Juma.
Sadik alisema kaburi hilo, limejengwa na kumalizika kwa kiwango cha hadhi ya shehe huyo, ambacho  familia imeridhia, kisha kuanza ujenzi wa kaburi la pili.
Alisema  mjenzi alipoanza kujenga kaburi la Shehe Yahya Hussein na kufika kozi ya tatu, watoto wa marehemu huyo, walifika na kusimamisha ujenzi, kutaka wapewe fedha ili wajenge wenyewe.
Alisema watoto hao, walitaka Sh milioni 4.5 kwa mujibu wa makadirio ya awali ya Manispaa. Lakini  alisema serikali haikuahidi kuwapa pesa, bali kujenga makaburi.
“Tumefanya hivyo na jana (juzi), nimeenda kuwatembelea pale na kumuagiza fundi kuendelea na ujenzi, kwani hatukuwa na ahadi ya kuwapa fedha na kama wakikataa, ni kwa ridhaa yao,” alisema.
Alisema kuna upotoshaji wa suala hilo unaoendelea,  jambo ambalo sio zuri. Alisema  serikali imetimiza ahadi yake ya kujenga makaburi ya marehemu hao, yaliyovunjwa.
Usiku wa Aprili 10 mwaka huu  katika viwanja vya Makaburi ya Tambaza, jirani na Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, makaburi hayo yalivunjwa na watu wasiojulikana, wakati wa 'Operesheni Safisha Jiji' na serikali kuamua kuyajenga upya.

No comments: