Watu watatu wameuawa kwa
kupigwa risasi na watu wanaosadikiwa kuwa majambazi usiku wa kuamkia jana
katika matukio na maeneo tofauti ya wilaya za Kahama na Shinyanga mkoani Shinyanga.
Kamanda wa Polisi mkoani
Shinyanga Evaresti Mangala alisema, watu wakiwa na bunduki moja aina ya SMG
majira ya saa 1.30 za usiku huko katika mtaa wa Ndala Manispaa ya Shinyanga
walimvamia mfanyabiashara Kulwa Cosmas (42) wakati akiwa kwenye ofisi yake ya
huduma ya kuweka na kutoa pesa kwa simu.
Katika uvamizi huo
majambazi walimpiga risasi shingoni na kusababisha kifo chake papo hapo.
Alisema, siku hiyo hiyo
majira ya saa 2.45 watu waliokuwa na bunduki moja ya kivita aina ya SMG
walivamia nyumbani kwa mfanyabiashara mwingine Yahaya Mrisho (46)
wakampora Sh 300,000, vocha za simu za kiganjani za mitandao mbali mbali zenye
thamani ya Sh 150,000 na simu nne za kiganjani.
Kamanda Mangala alisema,
katika tukio jingine lililotokea majira ya saa mbili za usiku huko katika
kijiji cha Nyabusalu Kata ya Bulungwa wilayani Kahama watu wasiofahamika
walivamia nyumbani kwa mwanamke Milembe Masanja (60) wakati akiwa jikoni na
mtoto wake Kulwa Mdirisha (40) wakiandaa chakula cha jioni.
Katika uvamizi huo
wavamizi Milembe na mtoto wake Kulwa walipigwa risasi sehemu mbali mbali za
miili yao na kusababisha vifo vyao papo hapo na kwamba polisi mkoani hapa
inawahoji watu wanne kuhusu tukio la uvamizi wa Ndala.
No comments:
Post a Comment