MAGARI YA KAMPUNI YA KAUDO SASA KUPIGWA MNADA

Magari ya iliyokuwa Kampuni ya Usafiri Dodoma (KAUDO) yanatarajiwa kuuzwa hivi karibuni baada ya kumalizika kwa kesi kati ya mmoja wa waliokuwa wafanyakazi wake aliyeishitaki Serikali.
Kwa mujibu wa Naibu Waziri wa Uchukuzi, Dk Charles Tizeba, hukumu ya kesi hiyo ilitoka mwaka 2011 ambapo Serikali ilishinda.
Alisema taratibu za Serikali za kupata kibali cha uuzaji wa magari hayo zimeshakamilika.
“Hivi sasa, zoezi la kufanya uthamini wa magari hayo linaendelea na linatarajiwa kukamilika mwishoni mwa mwezi Juni 2014. Baada ya tathimini kukamilika, magari hayo yatauzwa kwa uwazi na kwa njia ya ushindani,” alisema Dk Tizeba.
Alisema awali uuzaji wa mali za msingi za shirika hilo hususan magari haukufanyika kutokana na mmoja wa aliyekuwa mtumishi wa Kaudo kufungua shauri namba 352 la mwaka 2000 mahakamani akidai kulipwa mafao ya Sh milioni 98.
“Kutokana na kufunguliwa kwa shauri hilo, mahakama iliweka zuio ya kutouzwa kwa magari kumi (10) ya shirika hilo hadi hapo shauri litakaposikilizwa na kutolewa maamuzi,” alisema Dk Tizeba.
Naibu Waziri alikuwa akijibu swali la Mbunge wa Lushoto, Dk Henry Shekifu (CCM) aliyehoji Serikali inachukua hatua gani kunusuru vifaa vya magari ya kampuni hiyo.

No comments: