Wajumbe
wa Jumuiya ya Tawala za Mitaa (Alat), ambao wengi ni madiwani wamepinga
utaratibu wa Uchaguzi Mkuu, kutumiwa na wananchi kuchagua rais, wabunge na
madiwani.
Kutokana
na hatua hiyo, wajumbe hao sasa wamependekeza uchaguzi wa madiwani, utafutiwe
wakati mwingine, ili jamii itambue umuhimu wao katika kupatikana kwa ushindi wa
wabunge na rais.
Mwenyekiti
wa Halmashauri ya Wilaya ya Kigoma, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Chama Cha
Mapinduzi (CCM) wa wilaya hiyo, Hamis Said, aliwaambia wajumbe wa Alat kuwa
ongezeko la posho za wabunge haliwezi kuachwa likaendelea kufumbiwa macho, huku
thamani ya madiwani ikizidi kushuka.
Sababu
ya hatua hiyo zilitolewa jana katika Mkutano Mkuu wa Alat, kwamba ni ongezeko
la posho ya vikao kwa wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania la
hivi karibuni na viwango vya posho za wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba,
vinavyoonekana wao wamedharauliwa.
Huku
akiungwa mkono na kushangiliwa na zaidi ya wajumbe 500 wa Alat,
Said alisema hakuna maana tena kuendelea kutumika kwa kauli mbiu ya
mafiga matatu ambayo hutumiwa na CCM kwenye uchaguzi, ikiwahamasisha
wananchi kumpigia kura rais wa CCM, mbunge wa CCM na diwani wa CCM, wakati
baada ya uchaguzi madiwani hupuuzwa.
“Kuanzia
sasa wao wawe na uchaguzi wao na sisi tuwe na uchaguzi wetu. Haiwezekani kazi
kubwa tunafanya sisi kule kwenye mitaa, vitongoji, kata na tarafa lakini baada
ya kuisha uchaguzi wanaangalia maslahi yao tu, sisi tukibakia taabani.
“Tumeshuhudia
wabunge wa Katiba wakilipwa Sh 300,000 za vikao. Juzi juzi Wabunge wa Bunge la
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wanaanza vikao vya bajeti,
wameanza na posho mpya ya Sh 300,000. Yaani mtu alikuwa hana kitu lakini
anaanza na kiwango kikubwa cha fedha, sisi watendaji wa Serikali za Mitaa ambao
ndio tunahangaika na wananchi tunapuuzwa,” alisema.
Hata
hivyo hasira za wajumbe hao ambao wengi ni madiwani, wenyeviti wa halmashauri
za wilaya na mameya dhidi ya ongezeko la posho hizo za wabunge zinaweza kuisha
wakati wowote kutokana na ahadi ya juzi ya Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, ambaye
ameahidi kuwa Serikali itapandisha posho za madiwani katika bajeti ya
mwaka huu wa fedha.
Pinda
alisema hivyo alipokuwa akijibu kilio hicho cha posho finyu ya madiwani,
ambacho awali kiliwasilishwa na Mwenyekiti wa Alat Taifa, Dk Didas
Masaburi, kwa Pinda alipozindua Mkutano huo wa 30 wa Alat juzi.
Akijibu
hoja hiyo, Pinda alisema alichofurahishwa na maombi ya juzi ya Alat
kutaka madiwani kuongezewa posho ilikuwa ni hatua ya maombi hayo kutoshinikiza
kiwango fulani kama ambavyo wamekuwa wakishinikiza miaka ya nyuma.
No comments:
Post a Comment