Rais
Jakaya Kikwete, amesema Serikali imebaini kuwepo kwa mchezo mchafu unaotumiwa
na baadhi ya watumishi wasio waaminifu, unaosababisha malimbikizo ya
madeni ya wafanyakazi hususani walimu kutomalizika, kwa maslahi yao binafsi.
Amesema
watumishi hao wamekuwa wakitumia fursa hiyo ya madai hasa ya walimu na
kurejesha Hazina madeni hata yaliyolipwa, huku walimu wenyewe wakiwa hawana
taarifa jambo linalofanya kuwepo na mkanganyiko wa takwimu halisi za deni la
malimbikizo ya walimu hao.
Alisema
hayo jana katika maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Duniani, ambapo awali
wakati wafanyakazi hao wakipita mbele yake na maonesho ya kazi zao, walimu
wakiongozwa na Chama cha Walimu (CWT), walipita mbele yake, na kudai
malimbikizo ya mishahara, likizo na uhamisho.
“Mashemeji
zangu kama mlivyoniita leo nawahakikishia tumeshabaini mzizi wa fitina,
Serikali imekuwa ikijitahidi kuhakiki madeni yenu ili kukamilisha malipo, lakini
kwa mshangao tumegundua deni halisi si Sh bilioni 19, ni kama Sh bilioni tisa
tu, kuna wajanja wanajinufaisha kupitia migongo yenu,” alisema Rais Kikwete.
Alisema
imebainika kuwa wapo walimu wengi wameshalipwa malimbikizo yao, lakini majina
yao na madeni yamerejeshwa upya Hazina huku walimu wenyewe wakiwa hawana
taarifa na watu wanaofanya hivyo wakiwa hawajulikani.
“Nimeshaielekeza
Wizara ya Fedha na Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi, kuchunguza kwa kina
ili wakaguzi na wahasibu wasio waaminifu wanaofanya mchezo huu mchafu
wabainishwe na kuchukuliwa hatua,” alisema.
Alisema
kwa sasa Serikali inaendelea na kazi ya kuhakiki madeni ya watumishi wasio
walimu, ambapo kati ya halmashauri 147 tayari, halmashauri 96 zimehakikiwa na
madeni yameanza kulipwa na halmashauri 51 zilizobaki zikiwa katika hatua ya
kuanza kuhakikiwa.
Awali
wakati maadhimisho hayo yanaanza, yalitawaliwa na nderemo na vifijo kutoka kwa
wafanyakazi waliojitokeza kwa wingi kuandamana na kupitisha bidhaa na kazi zao
mbele ya Rais na viongozi wa kitaifa.
Katika
maandamano hayo, walimu wakiongozwa na CWT walipofikia jukwaa la Rais Kikwete
walisimama huku wakicheza na kuimba walisikika wakiimba; “shemeji mshahara
bado” jambo lililomshitua Rais Kikwete ambaye alilazimika kufuatilia papo hapo
na kugundua mshahara wa mwisho wa mwezi uliopita umechelewa.
Hata
hivyo alifafanua tatizo lilivyotokea kwa kuwa kutoka Benki Kuu mishahara hiyo
ilishatoka na kuahidi kuwa halitatokea tena.
No comments:
Post a Comment