MABALOZI 100 WA CCBRT KUELIMISHA KUHUSU FISTULA



Mabalozi 100 wa Taasisi ya CCBRT  wanatarajiwa kuendesha mafunzo ya wazi sehemu mbalimbali nchini, yenye lengo la kuzijengea jamii uelewa kuhusu ugonjwa wa fistula nawanawake wenye matatizo hayo, wametakiwa kujitokeza kupata matibabu.
Wiki iliyopita mabalozi 100 kutoka mikoa 25 Tanzania walihudhuria mafunzo ya namna bora ya kuendesha semina hizo za kijamii kwa mafanikio na kuwezeshwa vifaa vya kazi. Mabalozi hao wanasambaza ujumbe wa 'Fistula inatibika'.
Akizungumza jijini Dar es Salaam, Ofisa Mtendaji Mkuu wa CCBRT, Erwin Telemans alisema, "maelfu ya wanawake sehemu mbalimbali hapa nchini, wanaishi maisha ya aibu na kutengwa, kutokana na kusumbuliwa na fistula bila kufahamu kwamba CCBRT na wabia wake wanatoa matibabu bure, ikiwa ni pamoja na kubeba gharama zote za usafiri wa wagonjwa kufika Dar es Salaam, malazi na chakula".
Mtandao wa mabalozi wa CCBRT, hutumika kuwabaini na kuwasafirisha wanawake wenye tatizo la fistula kwa ajili ya matibabu.
Balozi wa fistula anapombainisha na kumthibitisha mgonjwa, hufanya mawasiliano na CCBRT kupitia namba maalum, ambayo ni bure kwa wateja wote wa Vodacom.
Baada ya hapo, CCBRT hufanya utaratibu wa kutuma fedha za nauli kusafiri kuelekea CCBRT Dar es Salaam au kwenye moja ya hospitali inazofanya kazi nazo za Kigoma, Arusha na Moshi.
Kwa kila mgonjwa mmoja anayefikishwa hospitali, balozi wa CCBRT hupata Sh 10,000 kama motisha kwa kusaidia kumaliza tatizo la fistula Tanzania.
Kwa sasa mtandao wa mabalozi wa fistula, unafikia mabalozi 500 wanaofanya kazi  kwa utaratibu wa kujitolea  na wameshafikisha hospitali wagonjwa wapatao 2,000.
Mkurugenzi Mtendaji wa Vodacom, Rene Meza alisema "Kutumika kwa teknolojia ya Vodacom kumesaidia kupunguza vikwazo kwa wanawake wanaotafuta matibabu na ni moja kati ya ubunifu mkubwa kwenye sekta ya afya kuwahi kushuhudiwa hapa Tanzania".
Siku ya kimataifa ya kutokomeza fistula huadhimishwa Mei 23 kila mwaka, kutambua umuhimu wa juhudi za kumaliza tatizo hilo na pia kuonesha nia ya dhati ya Umoja wa Mataifa kwa juhudi zote zinazofanywa za kutibu na kukinga fistula duniani.

No comments: