KUNA MADAKTARI 20 WA DAWA YA USINGIZI NCHINI



Chama cha Madaktari wa  Dawa  ya Usingizi Tanzania, kimeiomba serikali kuweka chombo maalumu kitakachofuatilia watoa huduma wenye weledi wa dawa hizo wakati wa upasuaji.
Imeelezwa kuwa, kwa Tanzania wapo  madaktari 20  na kati yao  17 wapo Dar es Salaam,  wawili wapo Hospitali ya Rufaa ya Bugando, Mwanza  na mwingine katika Hospitali ya Rufaa ya KCMC ya Moshi, Kilimanjaro.
Hayo yalisemwa Dar es Salaam na Rais  wa chama hicho, Mpoki  Ulisubisya katika mkutano wa kwanza wa kimataifa wa Madaktari wa dawa za usingizi uliohusisha nchi ya Uswisi, Marekani, Afrika Kusini na Kenya.
Alisema Tanzania wapo madaktari wengi lakini wanaotoa huduma ya dawa za usingizi wakati wa upasuaji ni wachache, hivyo wanahitaji madaktari wa kutosha kutoa huduma hiyo.
Alisema wameamua kufanya mkutano huo baada ya utafiti wa kisayansi uliofanywa na madaktari hao ili kujadili changamoto zinazowakabili.
‘’ Wapo wasaidizi wasioelewa matumizi ya dawa hizo kwa wagonjwa wakati wanafanya upasuaji hivyo wakati mwingine inaleta madhara kwa mgonjwa kwa kumsababishia matatizo mbalimbali,’’ alisema Ulisubisya.
Alitaja hospitali zilizopo Dar es Salaam ambazo zina madaktari wa kutoa huduma hiyo kuwa ni Lugalo, Aga Khan, Hospitali ya Taifa Muhimbili,  Kitengo cha Mifupa (Moi).
Alisema serikali iwasaidie madaktari kupata wataalamu watakaotoa mafunzo katika hospitali zote nchini, kuleta ari kwa madaktari kujifunza kutoa huduma hiyo.
 Mkurugenzi wa Tiba, Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, Margareth Mhando alisema serikali itafadhili mafunzo ya elimu ya juu kwa  madaktari wa dawa hizo. Alisema wanatarajia kuongeza wataalamu wa aina hiyo katika hospitali zote ili kuepusha madhara yanayojitokeza wakati wa upasuaji.

No comments: