KORONGO KUTOWEKA ZIWA MANYARA KWA KUNYWA MAJI YA SUMU



Viumbe hai vinavyotumia maji katika ziwa Manyara lililopo ndani ya mbuga ya Hifadhi ya Taifa ya Manyara wakiwemo ndege aina ya korongo huenda wakatoweka kwa kufa kufuatia kunywa maji yanayodaiwa kuwa na kemikali yenye sumu ambayo hutiririka katika ziwa hilo kutoka katika mito inachimbwa na kuchekechwa madini ya dhahabu. 
Mbali ya athari kwa ndege hao ambao ni kivutio kikubwa cha watalii katika mbuga hiyo pia madhara mengine huenda yakawakuta walaji wa samaki wanaovuliwa katika ziwa Manyara.  
Kaimu Mhifadhi wa Hifadhi ya Manyara, Yustina Kiwango aliwaeleza waandishi wa habari kuwa ndege aina ya korongo ni kivutio kikubwa cha watalii katika mbuga hivyo jitihada za ziada zinahitaji kuhakikisha kemikali hizo zinadhibitiwa zisiweze kuingia kwa wingi katika ziwa Manyara. 
Kiwango alisema katika ziwa Manyara kuna vyakula muhimu sana ambavyo hupendwa na ndege hao hivyo sio rahisi kuzuia ndege hao kunywa maji hayo kufuatia kuwepo kwa kemikali hizo ambazo zipo katika madini aina ya dhahabu yanayochekechwa katika mbuga hiyo. 
Alisema wachimbaji wadogo wadogo wenye leseni halali zilizotolewa na wizara ya Nishati na Madini  huchimba madini ya dhahabu ndani ya hifadhi ya Manyara katika mito ya Magara na Giheri na maji yenye kemikali zenye suma huingia katika ziwa Manyara na kuua viumbe hai wakiwemo ndege na samaki na pia mlaji naye huathirika. 
Mbali ya kutojua kiwango rasmi cha ndege waliokufa mpaka sasa, Mhifadhi huyo alisema utafiti unaendelea kujua idadi yao, lakini  jitihada za ziada zinahitajika kuelimisha jamii juu ya hali hiyo ili ndege, samaki na viumbe wengine waliopo ndani ya ziwa hilo wasiweze kufa na hatimaye kutoweka kabisa. 
Mhifadhi huyo aliomba wadau wote kwa kushirikiana kwa pamoja na Wizara ya Utalii na Maliasili, Nishati na Madini,Wizara ya Ushirika na Kilimo na Mifugo kulichunguza suala hilo kwa kina na kulipatia ufumbuzi kabla ya kuleta madhara zaidi kwa ndege hao muhimu kwa utalii. 
Alisema mbali ya hilo pia uchimbaji huo hupeleka tope jingi katika ziwa Manyara na kufanya kina cha ziwa hilo kwa sasa kuwa mita moja badala ya mita 4 kama ilivyokuwa miaka 50 iliyopita. 
Kiwango alisema na kuomba wadau wote kudhibiti hali hiyo na kama hilo halitafanyika upo uwezekana mkubwa wa ziwa Manyara kutoweka hivyo aliiomba wizara ya nishati na madini kuacha kutoa leseni mpya za uchimbaji madini ndani mbuga hiyo pindi zinapokwisha ama kutoa leseni mpya.
 ‘’Hapa tunapaswa kushirikiana kwa pamoja ili kudhibiti kemikali zisiendelee kwenda ziwa Manyara kwani zitaua kwa wingi ndege aina ya flamingo na viumbe hai wengine waliopo katika        
Ziwa Manyara.’’ 
‘’Kuongezeka kwa tope katika ziwa hilo nalo ni tatizo lingine ambalo nalo linapaswa kudhibitiwa kwa kiasi kikubwa hivyo jitihada za ziada zinahitajika kwa wizara na sekta nyingine kukomesha hali hiyo’’alisema Kiwango 
Mhifadhi alitaja miji itayoathirika na hali hiyo ni pamoja na Oltukai, Esilalei, Mto wa Mbu, Makuyuni na Minjingu kwani kwa asilimia kubwa hufaidika na ziwa hilo.

No comments: