Abiria
wa treni ya Mamlaka ya Reli ya Tanzania na Zambia (Tazara), ambayo inatakiwa
kuondoka leo kwenda Zambia, wako njia panda kutokana na wafanyakazi wa shirika
hilo kuendelea na mgomo wakidai mishahara yao.
Wakati
mgomo huo ukiendelea, leo treni ya abiria kwa mujibu wa ratiba ya shirika hilo
inatarajiwa kusafiri, hali inayotia wasiwasi kuwa huenda abiria watakwama
stesheni, kwasababu hawajarudishiwa fedha zao kama walivyorudishiwa abiria wa
treni iliyotarajiwa kuondoka Jumanne ya Mei 13 mwaka huu.
Wafanyakazi
wa Tazara jana waliendelea kukusanyika katika viwanja vya Tazara, wakisubiri
uamuzi wa Menejimenti ya shirika hilo kuhusu malipo yao, ndipo waendelee na
kazi hata hivyo hakujitokeza kiongozi yeyote katika Menejimenti kuzungumza nao.
Mwenyekiti
wa Chama cha Wafanyakazi wa Reli nchini (Trawu) Kanda, Yusuph Mandari aliwataka
wafanyakazi wenzake kuwa na uvumilivu katika kipindi hicho wakati wakisubiri
kikao kitakachofanyika leo cha Bodi ya Wakurugenzi wa Tazara kutafutia ufumbuzi
tatizo lao kama walivyoahidiwa na Mkurugenzi Mkuu wao Phiri.
No comments:
Post a Comment