Pengine si mgeni wa kichekesho cha Mkude Simba kilichoanza kuzagaa
pole pole katika jiji la Dar es Salaam
na hatimaye karibu nchi nzima.
Ni
kichekesho ambacho kilianza kupitia mitandao ya kijamii, taratibu
kikapokewa na madereva pikipiki na
sasa kwenye kituo cha redio mpya inayokwenda kwa jina la 'E' Fm.
Lakini
unaweza usijue sauti inayotumika katika
kichekesho hiki ni cha msanii maarufu ambaye anatambulika zaidi katika tasnia
ya filamu kwa mtindo wa kuigiza utumiaji wa dawa za kulevya 'teja' Kitale ambaye jina lake halisi ni Musa
Kitale.
Katika
mahojiano maalumu na mwandishi wa makala haya,
Kitale anasimulia sababu za kuanzisha kichekesho hicho ambacho sasa
kinatishia kulipoteza jina lake la Kitale.
Anasema
Mkude Simba ni kichekesho kinachotumia lafudhi ya Kiluguru ambaye anaonesha
ushamba wa hali ya juu na maswali ya kukosa majibu ya msingi.
Kitale
anasema yeye ni Mluguru na kwa muda mrefu
alikuwa na wazo na kulitangaza kabila lake kupitia sanaa, lakini hakuwa na njia
ya kutumia.
Anasema
kipindi hicho alitaka kutumia "Bwana mjomba... Mjomba Mkude" ambayo
hutumiwa na Waluguru na wazo lingine lilikuwa kutumia mtindo wa Uteja.
Aliamua
kuchagua Uteja akafikiria kutumia
kichekesho hicho ambacho kitakuwa
cha peke yake, kitakacholeta mabadiliko
katika tasnia ya sanaa.
"Niliweza
kupata umaarufu mkubwa na watu wengi wakanijua kupitia tasnia ya filamu, kwa
kuigiza kama mtumiaji wa madawa ya kulevya, mkorofi na mtu wa vurugu,"
anasema.
Lakini
tofauti na vile ambavyo alidhani mwanzo
wakati anatumia mtindo huo, kwani yalianza kuibuka matatizo mengi kutokana
na mtindo huo.
"Nilitumia
mtindo huo kwa muda mrefu na ndipo imani hiyo ikakaaa kichwani mwa watu,
nikaanza kuingia kwenye matatizo mengine," anasema.
Anasema
matatizo madogo madogo ni mengi, lakini miongoni mwa matatizo makubwa ni
kufuatiliwa na polisi wakidhani anahusika na biashara ya dawa ya kulevya.
Anasimulia
zaidi kwamba akiwa kwenye matembezi yake ya kawaida, alimtembelea rafiki yake
Mwananyamala ambapo alipoingia ndani dakika chache walivamiwa na polisi
waliokuja na gari nakuanza kupitisha msako wa nguvu mle ndani wakidhani Kitale
alikuwa na madawa ya kulevya.
"Hapo
ndipo nilipojua kwamba baadhi ya jamii inanichukulia tofauti sana, kufikia hadi
kuvamiwa na polisi na kukaguliwa," anasema Kitale kwa mshangao.
Anasema
matatizo mengine kuna baadhi ya watu hawana imani naye kabisa kwa kudhani ni
mwizi, ingawa anajaribu kuwaelewesha kwamba anaigiza na ni sehemu ya kazi.
Katika
tukio lingine anasema aliwahi kuwekwa polisi
katika ugomvi wa mtaani kisa
alikuwepo kuamualia ugomvi huo.
Anasema ugomvi huo ulikuwa mtaani kwao Mwananyamala ambapo
vijana wa kihuni walikuwa wakigombana na kupelekea kuvunja kioo cha gari
lililoegeshwa ofisi za CCM.
Anasema
baada ya ugomvi kuisha kila mtu alitawanyika, lakini polisi walipokuja na
kuchunguza aliyevunja kioo cha gari watu wakamtaja kutokana na kujulikana kama
raisi wa Mateja Mwananyamala.
"Nikiwa
nyumbani nilifuatwa na kukamatwa na kupelekwa polisi, ndipo nikawapa maelezo ya
kutosha na kuachiwa huru," anasema.
Anasema
lakini yote hayo yalitokea kutokana na Mwananyamala kujulikana zaidi kama raisi
wa mateja, ndio maana kila tatizo linaangukia kwake hata kama alikuwa akipita
njia.
Anasema
matatizo hayo na mengine mengi, ndiyo yaliyomfanya afikirie kutambulisha mtindo
mpya wa Mkude Simba.
Mtindo
wa Mkude Simba anasema anaamini anaweza kupunguza kasi ya Kitale teja na hata
jamii kumuelewa kwa mtindo tofauti.
"Kweli
hivi sasa jamii inanijua zaidi kwa jina la Mkude Simba na jina la Kitale
limepungua nguvu," anasema.
Anasema
alitumia mtindo huo, ili kujaribu kuleta tumaini kwa jamii na kumuona ni mtu
anayeigiza, na kwamba maisha ya uteja
sio halisi.
Kwa
sasa anasema kila sehemu anayopita humuita Mkude Simba sio Kitale kama zamani,
tena wanatamani kuwa karibu naye
kumsikiliza tofauti na zamani aliogopeka zaidi.
Kitale
anasema kwa sasa anatarajia kutumia mitindo yote miwili, akiwa kama Mkude Simba
na Kitale.
"Mkude
Simba nitakuwa tofauti na Kitale, na kazi zao zitakuwa tofauti kabisa kama
inavyojulikana sasa," anaelezea.
Pia
ana malengo ya kutengeneza filamu za Mkude Simba, ambazo zitakuwa na vichekesho
vya Mkude Simba.
Lakini
anasema ipo siku ataigiza filamu ya pamoja kati ya Mkude Simba na Kitale, jambo
ambalo anaamini ataleta mshangao kwa watu wengi.
Kitale
anasema kwa sasa hajaanza kupata faida ya vichekesho hivyo, ingawa vimeenea
karibu kila mahali.
Lakini
ana imani kwamba ipo siku vitamletea fedha kupitia miito ya simu, filamu,
matangazo ya redioni kwa kuwa watu wameshaanza kuvikubali.
Zaidi
ya sanaa ya kuigiza sauti na filamu, Kitale anasema muziki pia ni sehemu ya
kazi yake.
"Tayari
nilishafanya kazi nyingi, nikitumia mtindo wa Mchiriku na bado nafanya kazi
mpya zinakuja," anasema.
Miongoni
mwa kazi ambazo alishazifanya ni Hili Toto aliyomshirikisha Sharomilionea, Hili Dude na wimbo unaokuja sasa ni Mapenzi
yanauma.
"Mtindo
ninaotumia ni mchiriku kwa kuwa ndio unaozitambulisha nyimbo zetu nje ya nchi,"
anasema.
Kitale
anasema yeye ni mzaliwa na Morogoro, Matombo na kwamba alianza kupata elimu
yake Morogoro mjini kabla ya kuimalizia Dar es Salaam. Sanaa alianza katika
kundi la Kaole.
Makala
hii kwa mara ya kwanza imechapishwa kwenye gazeti la HabariLEO Jumamosi.
No comments:
Post a Comment