Wakati Muungano ukiwa hoja kuu
katika mchakato wa Katiba mpya uliofikia katika ngazi ya mjadala wa Bunge Maalumu,
Serikali imeandaa kitabu maalumu kinachoelezea historia, utekelezaji wa mambo
ya Muungano, mafanikio, changamoto, fursa na matarajio ya Muungano kwa miaka
ijayo.
Waziri Mkuu Mizengo Pinda alisema
hayo jana alipokuwa akiwasilisha Makadirio ya Bajeti ya Ofisi yake ya Sh
bilioni 105.5 kwa ajili ya matumizi ya
kawaida na maendeleo ya ofisi yake.
Kwa mujibu wa Pinda, kitabu hicho
kitatumika kama rejea kwa kizazi chetu na vizazi vijavyo, ili kuendelea kulinda
Muungano wa Tanganyika na Zanzibar uliodumu kwa miaka 50 sasa.
“Tutaendelea kuulinda Muungano
wetu kwa nguvu zote tukiwa na uelewa kwamba, katika kipindi cha miaka 50
iliyopita, Watanzania wameishi kwa amani na kufanya kazi zao za kujiletea
maendeleo wakiwa upande wowote wa Muungano,” alisema Pinda.
Akitetea hoja yake ya kulinda
Muungano, Pinda alisema takwimu zinaweka jambo moja wazi kwa Muungano kwamba zaidi ya asilimia 90 ya
Watanzania wote, wamezaliwa baada ya
Muungano.
“Sasa tuliozaliwa kabla ya
Muungano ni chini ya asilimia kumi. Kwa
mujibu wa takwimu hizo, Tanzania nzima ina watu 44,926,923. Kati yao, watu 40,640,425, sawa na Asilimia
90.6 ni wa umri wa siku moja hadi miaka 50.
“Takwimu hizo zina maana kwamba,
asilimia 90.6 ya watu wote wamezaliwa ndani ya Muungano na nchi wanayoifahamu
ni Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Sote
tunawajibika kuwatendea haki watu hawa kwa kuulinda, kuuimarisha na kuudumisha
Muungano wetu,” alisema Pinda.
Hata hivyo kwa mujibu wa Pinda,
takwimu hizo za Sensa ya Watu na Makazi ya mwaka 2012, zimebainisha jambo
lingine kwamba asilimia 7.7 ya Watanzania ambao ni watoto, ni yatima.
“Hali ya utegemezi nchini ni
kubwa kutokana na ukweli kuwa kati ya Watanzania milioni 44.9, asilimia 50.1 ni
watoto wenye umri chini ya miaka 18. Aidha, takwimu zimebainisha kuwa asilimia
7.7 ya Watanzania ni watoto yatima.
“Kutokana na hali hiyo, ni jukumu
letu kama Taifa kuweka mipango madhubuti ya kukabiliana na changamoto hizo
katika sekta za huduma za jamii, ili hatimaye kila mwenye uwezo wa kufanya kazi
achangie ipasavyo katika kukuza uchumi na maendeleo ya nchi yetu,” alisema.
Pinda alisema pato la Taifa
katika mwaka 2013, lilikua kwa asilimia 7
ikilinganishwa na ukuaji wa asilimia 6.9 mwaka 2012 na ongezeko hilo limetokana na ukuaji mzuri wa
shughuli za huduma za mawasiliano, viwanda, ujenzi na huduma za fedha.
Hata hivyo, alifafanua kuwa
pamoja na uchumi kukua kwa kasi ya
asilimia 7.0 kwa mwaka 2013 na pato la Mtanzania kuongezeka, kiwango hicho siyo
kikubwa kiasi cha kuwezesha umaskini wa wananchi kupungua kwa kasi.
“Utafiti wa kitaalamu unaonesha
kwamba, ili umaskini upungue kwa kasi kubwa, uchumi unatakiwa kukua kwa zaidi
ya asilimia nane kwa kipindi cha miaka 10 mfululizo. Ukuaji huo pia unatakiwa kulenga sekta ambazo
zinagusa maisha ya watu wengi, hususan kilimo, mifugo na uvuvi,” alisema Pinda.
Katika kuinua sekta ya kilimo,
Pinda alisema Serikali kupitia Mfumo wa Tekeleza Sasa kwa Matokeo Makubwa,
inategemea kuvutia uwekezaji na kuanzisha kilimo cha mashamba makubwa 25 ya
kilimo cha kibiashara kwa mazao ya mpunga na miwa kwa utaratibu wa
kuwaunganisha wakulima wakubwa na wadogo wanaozunguka mashamba hayo.
“Serikali imeendelea kushirikisha
Washirika wa Maendeleo kuchangia Programu ya Kuendeleza Kilimo katika Ukanda wa
Kusini mwa Tanzania (SAGCOT).
“Miongoni mwa malengo ya Programu
hiyo ni kuwaunganisha wakulima wadogo na mnyororo wa thamani wa kibiashara
wa kampuni kubwa za ndani na nje ya nchi. Ili kufikia
lengo hilo, Serikali imeanzisha Mfuko Chochezi wa Uendelezaji wa Kilimo katika
Ukanda wa Kusini mwa Tanzania,” alisema Pinda.
Alifafanua kwamba mfuko huo
utatoa mitaji itakayogharamia hatua za awali za miradi inayotoa tija ya haraka,
ambayo imebainishwa kwenye Mpango Mkakati wa Uwekezaji.
Vilevile alisema Mfuko huo
utahamasisha biashara inayolenga kumuinua mkulima mdogo kwa kumuunganisha na
mnyororo wa thamani na kampuni kubwa.
Mbali na makadirio ya bajeti kwa
ajili ya Ofisi yake, Pinda pia aliomba Bunge limuidhinishie Sh bilioni 479. 22 kwa ajili ya matumizi ya
kawaida na ya maendeleo ya Ofisi ya Waziri Mkuu - Tawala za Mikoa na Serikali
za Mitaa na taasisi zake.
Ofisi za wakuu wa mikoa
ziliombewa Sh bilioni 267. 90,
halmashauri zote zimeombewa Sh trilioni 4.23 na Bunge Sh bilioni 132.6 kwa ajili ya matumizi ya kawaida na maendeleo.
No comments:
Post a Comment