KESI DHIDI YA MAMENEJA WA BARCLAYS YAAHIRISHWA


Kesi ya wizi wa zaidi ya Sh milioni 479 katika Benki ya Barclays inayowakabili watu saba, wakiwemo mameneja wawili wa benki hiyo, imeahirishwa hadi Mei 28 mwaka huu. 
Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Nyigulila Mwaseba aliahirisha kesi hiyo jana, kwa kuwa upelelezi haujakamilika.
Washitakiwa hao ni Meneja wa benki hiyo tawi la Kinondoni, Alune Kasililika (28) na Meneja Neema Batchu. Wengine  ni wafanyabiashara Kakamie Julius (32), Iddy Khamis (32), Sezary Massawe (31), Boniphace Muumba (29) na Ruth Macha (30).
Wanadaiwa kupanga njama na Aprili 15 mwaka huu katika Benki ya Barclays tawi la Kinondoni. Washitakiwa hao wanatuhumiwa kuiba Sh 390,220,000, dola 55,000 za Marekani na Euro 2,150, mali ya benki hiyo. 
Inadaiwa kabla na baada ya kuiba ya wizi huo, washitakiwa walitumia silaha kuwatishia wafanyakazi wa benki hiyo, Anifa Ahmad na Anna Tegete ili wachukue fedha hizo bila pingamizi. 
Washitakiwa hao wanaendelea kusota rumande, kwa kuwa mashitaka ya unyang’anyi wa kutumia silaha yanayowakabili hayana dhamana.

No comments: