Kamati ya Bunge ya Miundombinu,
imepitisha Bajeti ya Wizara ya Ujenzi kwa mwaka ujao wa fedha 2014/2015, ya Sh
trilioni 1.2, fedha zilizoelekezwa katika matumizi ya kawaida na ya maendeleo
katika wizara hiyo.
Akiwasilisha taarifa ya mapendekezo ya
bajeti kwa mwaka ujao wa Waziri wa Ujenzi, Dk John Magufuli, alifafanua kuwa
ili wizara yake iweze kutekeleza majukumu na malengo yake itahitaji kiasi hicho
cha Sh trilioni 1.2.
Awali akiwasilisha mapendekezo hayo
kwanza, alianza kwa kutoa taarifa ya utekelezaji kwa mwaka wa fedha
unaoishia 2013/14 ambapo wizara hiyo ilitengewa
Sh bilioni 381.2 kwa ajili ya matumizi ya kawaida.
“Hadi kufikia Aprili mwaka huu jumla ya
Sh bilioni 372 zilikuwa tayari zimetolewa na Hazina, kiasi hicho ni sawa na
asilimia 97.61 ya kiasi kilichokuwa kimepangwa.
Akizungumzia fedha za Mfuko wa Barabara
(Road Fund), Magufuli alibainisha kuwa katika mwaka wa fedha unaoishia mfuko
huo ulipangiwa kukusanya Sh bilioni
504.3 kwa ajili ya wizara hiyo ya ujenzi, Wakala wa Barabara (Tanroads) na
Wizara ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI).
Alisema hadi kufikia Aprili, mwaka huu
fedha zote zilizokusanywa zilikuwa zimefikia Sh bilioni 496.2 sawa na asilimia
98.4 ya malengo ya mwaka huo unaoishia wa fedha.
Kamati hiyo ya Bunge baada ya kupitia
vipengele vyote ilihitimisha kikao hicho kwa kupitisha mapendekezo ya wizara
hiyo ili yaweze kuwasilishwa rasmi katika Mkutano unaoendelea wa Bunge la
Bajeti.
Hata hivyo, Mwenyekiti wa kamati hiyo,
Peter Serukamba, aliitaka Wizara hiyo ya Ujenzi kuhakikisha inasimamia ipasavyo
sheria na taratibu zilizowekwa kwa lengo la kulinda miundombinu mbali mbali
inayosimamiwa na wizara hiyo.
No comments:
Post a Comment