Kampuni ya Simon Group inayoendesha Shirika
la Usafiri Dar es Salaam (UDA),
imewaomba radhi wabunge wa Dar es Salaam akiwemo Mbunge wa Ubungo, John Mnyika
(CHADEMA) kutokana na habari
zilizoandikwa kwamba Mwenyekiti wake, Robert Kisena aliwatuhumu wabunge hao
kuhongwa ili kuihujumu UDA.
Akizungumza na vyombo vya habari jana,
mwenyekiti huyo Robert Kisena amesema kuwa haikuwa lengo la Simon Group katika
mkutano wake na waandishi wa habari ulioitishwa
Mei 18, mwaka huu kuwakashifu wabunge wala mtu yeyote.
Alisema ajenda kubwa katika mkutano huo
ilikuwa uhalali wa umiliki wa hisa za Shirika la UDA, kutokana na mjadala
uliokuwa umeibuka bungeni juu ya uuzwaji wa hisa za shirika hilo.
Katika kipindi cha maswali na majibu bungeni,
serikali ilitamka kupitia kwa Naibu Waziri wa Fedha, kwamba mwaka 2010 ilitoa
maagizo kwa Bodi ya Wakurugenzi ya UDA kusitisha mpango wa kuiuzia Simon Group
hisa zozote kwa kuwa utaratibu wa kumpata mwekezaji huyo ulikuwa umekiuka
taratibu na misingi ya sheria.
Serikali ilitamka bungeni kuwa kampuni ya
Simon Group haimiliki hisa za UDA bali zinamilikiwa na wabia wawili ambao ni
serikali yenyewe kupitia Msajili wa Hazina (asilimia 49) na Halmashauri ya Jiji
la Dar es Salaam (asilimia 51).
Kisena alisema kwa kuzingatia kauli ya
serikali, uongozi wa Simon Group uliona haja ya kuueleza umma upate kufahamu
taarifa za upande wa pili, kwa sababu kampuni hiyo haikuwa na fursa ya
kujitetea bungeni.
Alisema baada ya mkutano huo na waandishi wa
habari, kumetokea mkanganyiko katika jamii juu ya masuala kadhaa ambayo baadhi
ya vyombo vya habari havikuripoti kwa usahihi taarifa husika.
“Miongoni mwa kasoro zilizojitokeza ni baadhi
ya vyombo vya habari vilitoa tuhuma kwa baadhi ya wabunge binafsi, kwa kuwataja
majina kwamba walitajwa wanajihusisha na vitendo vya rushwa.
“Kwa ujumla baadhi ya maudhui katika baadhi
ya habari si tu kwamba yamesababisha mkanganyiko kwa umma, lakini pia
kusababisha usumbufu mkubwa kwa Mbunge wa
Ubungo, John Mnyika na baadhi ya wabunge wa Mkoa wa Dar es Salaam kwa
ujumla wao.
“Natumia nafasi hii kumwomba radhi Mbunge wa
Ubungo, Mheshimiwa Mnyika, wananchi wake wa Ubungo na Watanzania kwa ujumla kwa
maneno hayo ambayo kama tulivyoeleza yameleta usumbufu kwake binafsi na
wananchi hao,” alisema.
Akizungumza, Kisena alisema amechukua hatua
hiyo ya kuwaomba radhi wabunge wa Dar es Salaam, hususan Mnyika ili kujenga
uhusiano mzuri baina ya kampuni hiyo na wadau mbalimbali kwa lengo la
kuiwezesha Simon Group kupata ushirikiano na wadau wote wa maendeleo katika
mipango yake ya uwekezaji mkubwa ndani ya UDA.
“Kwa kweli tumeona tuwaangukie wabunge na
watu wengine wote walioguswa na habari hizi ili kujenga uhusiano mwema na
wabunge, hususan Mheshimiwa Mnyika, wananchi wa Ubungo, wakazi wa Dar es Salaam
na Watanzania wote hasa kwa kuzingatia kwamba kampuni yetu ni ya Watanzania na
hivyo inahitaji kuungwa mkono na Watanzania wote ili iweze kutekeleza mipango
yake,” alisema.
No comments:
Post a Comment