EKELEGE ABANWA NA TAKUKURU MAHAKAMANI



Ofisa Uchunguzi wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), Thadei Nzalalila, ameieleza Mahakama kwamba aliyekuwa Mkurugenzi wa Shirika la Viwango Tanzania (TBS), Charles Ekelege alikiri kutoa msamaha wa ada ya utawala kwa kampuni mbili.
Nzalalila alidai hayo jana katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, wakati akitoa ushahidi katika kesi ya matumizi mabaya ya madaraka na kulisababishia shirika hilo hasara ya Sh milioni 68, inayomkabili Ekelege.
Ekelege anadaiwa kusababisha hasara hiyo, baada ya kuondoa ada ya asilimia 50, ambayo ni sawa na Sh milioni 68 kwa kampuni za Jaffar Mohamed Ali na Quality Motors bila idhini ya Bodi.
Akiongozwa na Wakili kutoka Takukuru, Janeth Machulya, Nzalalila alidai kuwa alimhoji Ekelege na katika maelezo yake ya onyo, alikiri kusamehe kodi kampuni hizo na alitoa msamaha wa dola 27.380 kwa Kampuni ya Jaffar Mohamed Ali na dola 15.160 kwa Kampuni ya Quality Motors.
Alidai katika maelezo yake kuwa Ekelege alifanya hivyo kwa kuwa aliamini kampuni hizo, zipo chini ya kiwango, ambacho anaruhusiwa kufanya hivyo kisheria.
Awali alidai kuwa mwaka 2012 na 2013, alifanya uchunguzi kuhusu tuhuma dhidi ya Ekelege, na kugundua ni kweli kampuni hizo ziliandika barua za kuomba msamaha wa kodi, ambapo Ekelege alifanya hivyo, bila kushirikisha Idara ya Fedha na utawala ya shirika hilo.
Aidha, alidai hakukuwa na kikao chochote kilichofanywa na menejimenti kupitisha msamaha huo, pia ripoti ya ukaguzi wa ndani ya TBS, ilijadiliwa na Bodi ya Wakurugenzi ambayo iliidhinisha msamaha huo ambao tayari ulikuwa umeshatolewa.
Inadaiwa kuwa Machi 28, mwaka 2008 na Agosti 7, mwaka 2009, Ekelege alitumia madaraka vibaya kusamehe ada kampuni mbili kwa asilimia 50, ambayo ni sawa na Sh milioni 68 bila idhini ya Baraza la Utendaji, kinyume na utaratibu wa TBS na pia alilisababishia shirika hilo hasara ya fedha hizo.

No comments: