Mkuu wa Wilaya ya Ngorongoro, Elias
Lali amesema haijathibitishwa kama madini, yanayodaiwa kugundulika Kijiji cha
Mgongo huko Samunge kuwa ni dhahabu au la.
Amesisitiza kuwa idadi ya watu
wanaofika wilayani hapo kusaka dhahabu
ni ndogo, ikilinganishwa na iliyojitokeza enzi za `Kikombe cha Babu wa Loliondo',
Mchungaji Ambilikile Mwaisapile.
Mkuu wa Wilaya alilazimika kutoa
ufafanuzi huo jijini hapa jana,
alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari, waliotaka kujua je, ni
kweli madini hayo yanapatikana juu juu, kama inavyoelezwa na baadhi ya vyombo
vya habari nchini.
Alisema ni kweli madini yamegundulika,
lakini haijathibitishwa kama madini hayo ni dhahabu kweli au ni madini ya aina
nyingine.
Alisema muda wowote kuanzia sasa,
wataalamu wa madini Kanda ya Kaskazini watatoa taarifa juu ya aina ya madini
waliyoyagundua. Alisema timu ya wataalamu imeshafika eneo hilo, kuchunguza na
kutoa elimu ya uchimbaji wa madini hayo.
Alisema, awali wakati taarifa hizo
zilipotoka kuwa madini yanapatikana `nje nje' karibu na mto Mgongo, alifika
eneo hilo akiwa na Kamati ya Ulinzi na
Usalama ili kujua kama ni kweli au la.
Lakini, waligundua kuwa madini hayo, si
kweli yapo juu juu kama inavyodaiwa, bali waliwakuta wachimbaji wadogo wanaoshi
maeneo hayo, wakiwa wanachimba madini hayo pembezoni mwa mto.
Alisema idadi ya watu si kubwa kama
inavyodaiwa, bali watu waliopo ni 400 hadi 600
huku asilimia 80 ya watu hao ni
wakazi wa Kijiji cha Mgongo, asilimia 10 wanatoka ndani ya Kata ya Samunge,
asilimia 5 wanaotoka nje ya wilaya ya Ngorongoro na asilimia 5 wanaotoka ndani
ya Wilaya ya Ngorongoro.
Alisema wamejipanga kuhakikisha kuwa
huduma muhimu za ulinzi na usalama, zinakuwepo ikiwemo huduma za maji na vyoo.
Alisitiza kuwa ni kweli madini hayo,
yapo, lakini bado hayajathibitishwa rasmi kama ni dhahabu au la.
Alitoa rai kwa watu wanaopenda kutoa
taarifa, hata kama ni za kweli, wawasiliane na mamlaka husika ili kutoa taarifa
za uhakika, badala ya kutoa taarifa wanazozijua wao.
No comments:
Post a Comment