Mkuu
wa Wilaya ya Pwani, Halima Kiemba, ametoa mwito kwa kila Mtanzania
kujitolea kuwa balozi wa Fistula, ili kuunganisha nguvu katika kupambana
na tatizo hilo na kufikia malengo ya kulitokomeza ifikapo 2015.
Mkuu
huyo wa Wilaya alitoa mwito huo juzi, wakati akizindua mafunzo maalum kwa
mabalozi 100 kutoka mikoa mbalimbali nchini, ambayo ni sehemu ya maandalizi ya
maadhimisho ya Siku ya Fistula Duniani, inayoadhimishwa kila Mei 23.
“Niwapongeze,
Vodacom Foundation kwa kushirikiana na CCBRT pamoja na UNFPA na kuwezesha
mafunzo haya ambayo kwa mara ya kwanza yamefanyika katika Wilaya ya Pwani.
Tatizo hili limekuwa kikwazo kwa wanawake wengi ndani ya jamii yetu na bado
limeendelea kuwepo katika baadhi ya maeneo kutokana na imani zetu,” alisema
Kiemba.
Alisema
kunahitajika nguvu katika kupambana na ugonjwa huo na kusisitiza Mtanzania
ajitolee kuwa balozi kwa kutoa taarifa katika vituo vya afya, hasa pale anapo
gundua eneo alilopo kuna mgonjwa na kuwahimiza wagonjwa wenyewe wajitokeze ili
wapate matibabu.
Mafunzo
hayo yamelenga kuwajengea mabalozi hao uwezo wa kutoa elimu watakaporudi katika
jamii zao na kusambaza ujumbe kwamba ‘Fistula Inatibika’ kuelekea kilele cha
maadhimisho hayo.
Juhudi
hizo zinaratibiwa duniani kote ambapo watu wameungana katika kutoa elimu siku
hiyo na hapa nchini, sherehe hizo zitafanyika katika Wilaya ya Temeke
jijini Dar es Salaam.
Naye
Mkuu wa Vodacom Foundation, Yesaya Mwakifulefule, alisema wamejipanga kuwafikia
akinamama waliopo vijijini ambao wanaamini ugonjwa huu hautibiki kwa kuwaleta
mjini kupata matibabu.
Aidha
Ofisa Mtendaji Mkuu wa CCBRT, Erwin Telemans amesema kuwa mabalozi wao 500
wamefanya kazi kubwa na inayostahili pongeza kwa kuweza kuwatambua wanawake
wenye tatizo la fistula lakini mafunzo haya yanawataka mabalozi wetu 100
wamepiga hatua zaidi kwa kwenda kutoa semina kwenye sehemu zao ambazo
zitazinduliwa tarehe 23 nchi nzima.
No comments:
Post a Comment