DALADALA 1,800 KUONDOLEWA NJIA KUU



Daladala 1,800 zinazofanya safari zake kati ya Kimara na Kivukoni, zinatarajiwa kuondolewa katika barabara hiyo yenye wateja wengi, baada ya kuanza kwa awamu ya kwanza ya Mradi wa Mabasi Yaendayo Kasi (Dart).
Daladala hizo zitapangiwa njia nyingine za pembezoni, ambako hakuna wateja, kama barabara ya awali, huku madereva wake watakaojitokeza kuomba ajira,  watapewa kipaumbele katika mabasi ya kasi.
Meneja Uendeshaji wa Dart, Peter Munuo, alisema hayo jana wakati akizungumza na waandishi wa habari, kuhusu maendeleo ya mradi huo.
"Daladala hizo zitapangiwa ruti mpya, kama mnavyojua hapa kwetu (Dar es Salaam) usafiri ni wa tabu kidogo, hasa kwa maeneo ambayo yako pembezoni," alisema Munuo.
Meneja Msimamizi wa Matumizi ya Barabara wa Dart, Mohamed Kuganda, alisema mradi huo unatarajiwa kukamilika mwaka kesho.
Lakini, alisema jambo hilo litawezekana, endapo mkandarasi aliyepewa zabuni hiyo, Kampuni ya Strabag, atakomesha migogoro inayoendelea.
Alisema kwa sasa kampuni hiyo, imekuwa ikiingia katika migogoro na wafanyakazi wake, jambo ambalo kama kampuni hiyo haitachukua hatua za haraka, linaweza kukwamisha mradi huo kukamilika kwa wakati.
"Tunataka wakae na wafanyakazi wao, wajadili kwa sababu migogoro hii, inaathiri maendeleo ya mradi wakati mitambo ipo, lakini haifanyi kazi na hivyo inaweza kuchelewesha kazi," alisema Kuganda.
Alisema mradi huo, unakabiliwa na changamoto  mbalimbali, ikiwemo maandalizi ya huduma za awali.
Alisema kuwa wanatarajia kuanza kutoa huduma za awali kwa mabasi makubwa 20 na madogo 10. Alisema zinahitajika Sh bilioni 20 ili kufanikisha hatua za awali za kuanza mradi huo.
Meneja Uhusiano wa Dart, William Gatamba, alisema madereva daladala, watakaopewa vipaumbele watapelekwa katika mafunzo maalumu, ambapo baada ya hapo vigezo ndiyo vitawawezesha kupata ajira.

No comments: