Bomu limelipuka
katika nyumba ya kulala wageni iliyopo katika eneo la Kanisa la Kiinjili la
Kilutheri (KKKT), Usharika wa Imani, jijini Mwanza na kujeruhi vibaya mtumishi
wa kanisa hilo.
Akizungumza na
waandishi wa habari jana, Katibu wa KKKT Dayosisi ya
Mashariki ya Ziwa Victoria, Rogart Mollel,
alimtaja aliyejeruhiwa katika tukio hilo kuwa ni Bernadetha Alfred,
ambaye alikimbizwa katika Hospitali ya Rufaa ya Bugando.
Akizungumza kwa
masikitiko, Katibu huyo alisema bomu hilo lililipuka juzi saa 2 usiku na
kusababisha taharuki kubwa kwa wageni waliokuwa kwenye nyumba hiyo na watu
wanaoishi jirani na kanisa hilo.
Akifafanua zaidi
kuhusu bomu hilo, Mollel alisema lilifungwa katika kifurushi kilichopambwa na
karatasi za zawadi na kuwekwa katika mfuko uliotelekezwa katika korido ya
nyumba hiyo kwa takribani siku tatu.
Kwa mujibu wa
Mollel, eneo hilo la korido huwekwa kreti za soda na wageni wamekuwa wakiingia
na kutoka kutumia njia hiyo, na wakati mwingine hupata chakula na chai katika
eneo hilo, ndio maana watumishi hawakuhisi kwa haraka kama ni kitu cha hatari.
“Jana (juzi)
mhudumu huyo aliamua kufungua kifurushi hicho ili kuona ni nini na ndipo
lilipomlipukia na kumjeruhi vibaya sehemu mbalimbali za mwili, ikiwemo usoni na
miguuni na kukimbizwa Bugando kwa uchunguzi na tiba,” alisema Mollel.
Lakini Makamu Mwenyekiti wa Umoja
wa Makanisa ya Kikristo Mkoa wa Mwanza, Askofu Zenobius Isaya, alielezea kwa
undani kuwa Bernadetha aliamua kwenda kuchukua boksi hilo la zawadi juzi usiku,
kwa kuwa lilikuwa limetelekezwa tangu Ijumaa iliyopita.
Kwa mujibu wa Askofu Isaya, nia
ya Bernadetha ilikuwa kufahamu ni la nani na kwa nini lipo kwenye korido hiyo
kwa muda mrefu, ndio kufungua likamlipukia.
Alipoulizwa kuhusu ulinzi uliopo
katika eneo hilo la Kanisa Kuu la KKKT, Mollel
alisema ulinzi upo katika mageti yote mawili lakini upekuzi huwa haufanyiki kwa
kina.
“Kwa kweli tukio hili limetuchanganya sana,
tumekuwa
tukisikia matukio hayo yakitokea maeneo mengine
makanisani, kwetu limetokea kwenye nyumba ya kulala wageni, sina hakika
waliofanya hivyo walilenga nini,” alisema na kuongeza; “ tunashukuru Mungu
haijaleta madhara makubwa sana.”
Baadhi ya watu waliohojiwa walidai waliposikia
mlipuko huo, walidhani ni transfoma ya Shirika la Umeme (Tanesco) kwa kuwa mara
baada ya kulipuka, umeme ulikatika katika eneo hilo.
Mlinzi aliyekuwa zamu siku ya tukio, Charles
Mathayo, alidai baada ya mlipuko huo alisikia kilio cha mhudumu Bernadetha akiomba
msaada, na walipofika walimkuta akiwa amelala chini akilia huku damu
zikimtiririka huku kukiwa na misumari midogo midogo katika eneo hilo.
Shuhuda ambaye kwa wakati huo alikuwa amekaa nje
kwenye ngazi, Elina Emmanuel, alidai alisikia
mlipuko mkubwa na kuona moshi huku
waliokuwa vyumbani wakianza kutoka nje.
Elina ambaye ni mwanafunzi wa chuo cha kompyuta alidai alikuwa kwenye nyumba hiyo na baada ya mlipuko huo wageni walihamishiwa kwenye nyumba nyingine ya kulala wageni.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Valentine Mlowola, alithibitisha kutokea kwa mlipuko huo saa 2.20 usiku na kusema uchunguzi wa awali unaonesha kuwa bomu hilo limetengenezwa kienyeji.
Alisema uchunguzi wa Jeshi la Polisi mkoani hapa
unaendelea kubaini nani aliyefanya
kitendo hicho na kwa sababu gani, ili hatua za kisheria zichukuliwe dhidi yake
ingawa mpaka jana hakukuwa na mtu aliyekuwa akishikiliwa kwa tuhuma hizo.
Kamanda Mlowola ametoa mwito kwa wananchi
wanapoona vitu wasivyo na uhakika navyo na kuwa na wasiwasi navyo wasivishike,
badala yake watoe taarifa Polisi.
Mganga Msaidizi wa Idara ya Dharura katika Hospitali
ya Rufaa ya Bugando, aliyejulikana kwa
jina moja la Baraka alisema kwa sasa waandishi hawaruhusiwi kumuona, kuongea
wala kumpiga picha majeruhi kutokana na hali yake kuwa mbaya na kwa wakati huo
hakukuwa na ndugu yake hata mmoja.
No comments:
Post a Comment