Benki ya Posta Tanzania (TPB) Tawi la
Morogoro, imetoa msaada wa madawati 32 yenye thamani ya Sh milioni tano kwa
Shule ya Msingi Magole iliyopo wilayani
Kilosa baada ya madawati mengi kuharibiwa na mafuriko.
Meneja wa Benki ya TPB Tawi la
Morogoro, Fumbuka Ng'onge, alikabidhi msaada huo juzi kwa Mkuu wa Wilaya ya
Kilosa, Elias Tarimo katika viwanja vya Shule ya Sekondari Magole.
Meneja huyo alisema uongozi wa benki
hiyo, umeguswa baada ya kupata taarifa ya
maafa yaliyowakuta wakazi wa Tarafa ya Magole, yaliyotokana na mafuriko
hayo ya mvua ambayo pia yaliharibu
miundombinu, yakiwemo majengo ya Shule ya Msingi Magole.
"Uongozi na wafanyakazi wa Benki
ya Posta unatoa pole kwenu wananchi wa
Magole na uongozi wa Serikali ya Wilaya ya Kilosa ...katika kufanya hivyo
tumeona tutoe msaada kwa upande wa shule ya msingi kwa madawati 32 yenye
thamani ya Shilingi milioni tano na leo tunayakabidhi," alisema Meneja huyo.
Alisema licha ya kutoa huduma za
kibenki, Benki ya Posta imeendelea kuwa karibu na wananchi siku zote kwa kusaidia masuala mbalimbali ya
kijamii, ikiwemo sekta ya elimu.
Kwa upande wake, baada ya kupokea
msaada huo, Tarimo aliishukuru Benki ya Posta Tanzania na kusema msaada huo ni mkubwa
na umepunguza uhaba wa madawati katika
shule hiyo.
Awali, Kaimu Ofisa Elimu Msingi wa
Wilaya ya Kilosa, Chidelinga Julius, aliwasihi walimu wa shule hiyo kuwa
wavumilivu na kufundisha kwa bidii baada ya kupatiwa majengo ya Shule ya
Sekondari Magole, kwa vile jambo hilo ni la mpito.
Mwalimu Mkuu wa shule hiyo, Colletha
Mahululu aliishukuru Benki ya Posta kwa msaada wa madawati hayo.
Alisema bado idadi kubwa ya wanafunzi, wanaketi
sakafuni na kubanana wanafunzi watatu hadi wanne kwenye dawati.
No comments:
Post a Comment