HOTUBA YA WAZIRI WA UCHUKUZI, MHE. DKT. HARRISON G. MWAKYEMBE (MB), AKIWASILISHA
BUNGENI MAKADIRIO YA MAPATO NA MATUMIZI YA FEDHA KWA MWAKA 2014/2015
1.0 UTANGULIZI
1. Mheshimiwa Spika, baada ya Kamati ya
Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuchambua bajeti ya Wizara ya Uchukuzi na kuweka
mezani taarifa ya Kamati mbele ya Bunge lako Tukufu, naomba sasa Bunge lako
likubali kupokea, kujadili na kupitisha Mpango na Makadirio ya Mapato na
Matumizi ya Fedha ya Wizara ya Uchukuzi kwa mwaka 2014/2015.
2. Mheshimiwa Spika, naomba hotuba nzima ya
makadirio ya mapato na matumizi ya fedha ya Wizara ya Uchukuzi kwa mwaka
2014/2015 iingizwe yote kwenye kumbukumbu rasmi za bunge na uniruhusu
niwasilishe muhtasari tu unaobeba maudhui ya hotuba nzima. Vitabu vya Hotuba
yangu na andiko maalum la ukanda wa kati (The Central Corridor: A Wider Concept
Note) vimesambazwa kwa waheshimiwa Wabunge.
3.
Mheshimiwa
Spika,
nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia zawadi ya uhai na
kutuwezesha kukutana tena kujadili utendaji wa Sekta za Uchukuzi na Hali ya
Hewa kwa mwaka 2013/2014 na mipango ya Sekta hizo kwa mwaka 2014/2015 kwa
maendeleo ya Taifa letu.
4. Mheshimiwa
Spika, kabla
sijawasilisha hoja ya Wizara yangu, naomba niungane na Wabunge wenzangu
kuwalilia Wabunge wenzetu waliotutangulia mbele za haki. Ninaomba Mwenyezi
Mungu azilaze roho zao peponi. Aidha, nawapongeza Wabunge wapya waliojiunga
nasi kwenye Mkutano huu wa Bunge.
5.
Mheshimiwa Spika, naomba nitumie fursa
hii vilevile kuwapa pole wananchi wa jimbo la uchaguzi la Kyela kwa mafuriko
makubwa yaliyoikumba Wilaya ya Kyela na kuwashukuru kwa kunipa ushirikiano
mkubwa katika kutekeleza shughuli mbalimbali za maendeleo ya Jimbo na Taifa kwa
ujumla. Naomba tuendelee kushirikiana katika kipindi hiki kigumu ili kurudisha
hali ya miundombinu yetu ya kiuchumi na kijamii iliyoharibiwa na mafuriko hayo.
6.
Mheshimiwa
Spika,
kwa namna ya pekee kabisa naomba kumpongeza Mhe. Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, Rais wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania kwa msukumo alioutoa katika kuanzisha na kusimamia kwa
karibu utekelezaji wa Programu ya Matokeo Makubwa Sasa (Big Results Now - BRN)
ambayo imechochea mabadiliko makubwa katika kuufungua Ukanda wa Kati wa
Uchukuzi kwa kutekeleza miradi ya reli, bandari na barabara. Waheshimiwa Dkt. Mohamed Gharib Bilal, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mizengo Kayanza
Peter Pinda (Mb), Waziri Mkuu wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania nao nawapongeza kwa
uchapakazi na uongozi wao thabiti wa mfano uliotutia nguvu na matumaini katika
kufikia malengo ya BRN.
7. Naomba nimalizie Mheshimiwa Spika, kukupongeza
wewe na uongozi mzima wa Bunge kwa kazi nzuri mnayoifanya. Vilevile naishukuru Kamati ya Kudumu ya
Bunge ya Miundombinu chini ya Mwenyekiti wake Mhe. Peter Joseph Serukamba, Mbunge wa Kigoma
Mjini na Makamu wake Mhe. Prof. Juma Athuman Kapuya, Mbunge wa Urambo
Magharibi kwa kuendelea kunipa ushirikiano mimi na viongozi wenzangu wa Wizara
katika kuiongoza Wizara ya Uchukuzi. Ushirikiano na ushauri wao umesaidia kwa
kiasi kikubwa katika kuboresha utendaji wa sekta za Uchukuzi na Hali ya Hewa. Binafsi nina imani kubwa na Kamati na
naichukulia kama think tank ya Wizara. Ninaihakikishia Kamati hii kuwa
Wizara itaendelea kutoa ushirikiano wa karibu kwa lengo la kuendeleza Sekta za
Uchukuzi na Hali ya Hewa.
8. Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo hayo mafupi ya utangulizi,
napenda kutoa ufafanuzi wa kina kuhusu taarifa ya utekelezaji wa mipango ya maendeleo
ya Sekta za Uchukuzi na Hali ya Hewa kwa mwaka 2013/2014 na mipango ya mwaka
2014/2015.
2.0 HALI YA UTENDAJI NA MAPITIO YA UTEKELEZAJI WA MIPANGO YA WIZARA KWA MWAKA 2013/2014 NA MALENGO YA MWAKA 2014/2015
9. Mheshimiwa
Spika, katika mwaka wa fedha
2013/2014, Wizara iliidhinishiwa bajeti ya Shilingi bilioni 529.41. Kati ya
fedha hizo, Shilingi bilioni 420.52 ni kwa ajili ya miradi ya maendeleo na
shilingi bilioni 108.88 ni kwa ajili ya matumizi ya kawaida. Fedha za maendeleo
zinajumuisha Shilingi bilioni 252.68 fedha za ndani na Shilingi bilioni 167.84
fedha za nje. Hadi kufikia Aprili, 2014 Wizara ilikuwa imepokea fedha za
maendeleo Shilingi bilioni 201.21. Kati ya fedha zilizopokelewa, Shilingi
bilioni 180.13 ni fedha za ndani sawa na asilimia 71.29 na Shilingi bilioni
21.08 ni fedha za nje sawa na asilimia 12.56. Kwa kuzingatia mwenendo huo wa
upatikanaji wa fedha ni dhahiri kuwa sehemu kubwa ya utekelezaji wa Bajeti
umefanywa kwa fedha za ndani.
2.1 UTEKELEZAJI WA PROGRAMU YA MATOKEO MAKUBWA SASA (BIG RESULTS NOW – BRN)
10.
Mheshimiwa
Spika, itakumbukwa kuwa katika mwaka 2013/2014 Wizara yangu
iliteuliwa kuwa moja kati ya Wizara sita kuanza kutekeleza Programu ya BRN.
Katika kipindi hicho, Wizara imepata mafanikio na kufanya maandalizi yote
muhimu katika kufikia malengo ya BRN. Wizara itaendelea kutekeleza miradi ya
reli na bandari na kufikia malengo ya BRN katika mwaka 2014/2015.
2.1.1 BANDARI
11.
Mheshimiwa
Spika, kwa upande wa bandari katika mwaka 2013/2014, Mamlaka
imekamilisha majadiliano na Benki ya Dunia wakishirikiana na TradeMark East
Africa (TMEA) na Idara ya Serikali ya Uingereza ya Maendeleo ya
Kimataifa (DFID) ili kupata fedha kwa
ajili ya kugharamia ujenzi wa mradi wa kupanua na kuchimba lango la kuingilia
na kutokea meli katika bandari ya Dar es Salaam. Nilibainisha kuwa Mradi huu
utatekelezwa sambamba na uboreshaji wa gati namba 1-7. Kazi za ujenzi
zinatarajiwa kuanza mwezi Desemba, 2014 na kukamilika mwezi Agosti, 2016.
Aidha, kazi za uchimbaji na upanuzi wa lango la bandari ya Dar es Salaam zinatarajiwa
kuanza mwezi Agosti, 2015 na kukamilika mwezi Agosti, 2016.
12.
Mheshimiwa
Spika, miradi mingine inayoendelea kutekelezwa kwa lengo la
kuboresha utendaji wa Bandari ya Dar es salaam ni pamoja na: ujenzi wa jengo
lenye ghorofa 35 (one stop center building) la kuwaweka pamoja wadau muhimu
wanaotoa huduma katika Bandari ya Dar es Salaam, ambalo hadi Mei, 2014 lilikuwa
tayari na ghorofa 26 zilizojengwa na kazi inatarajiwa kukamilika ifikapo Juni
2015; kuanza kwa utekelezaji wa mradi wa kuwaunganisha pamoja watoa huduma kwa
njia ya mtandao (Electronic Single Window System) mwezi Aprili, 2014 na mradi
huu unatarajiwa kukamilika mwezi Novemba, 2014; kuanza kuweka (installation)
mfumo wa malipo kwa njia ya mtandao (Electronic Payment System) ifikapo mwezi
Juni, 2014 na mradi huu unatarajiwa kukamilika mwezi Novemba, 2014.
13.
Mheshimiwa
Spika, katika juhudi za kupunguza msongamano bandarini, Mamlaka
imepata maeneo kwa ajili ya kutumiwa katika shughuli za kibandari ikiwa ni
pamoja na vituo vya kupokelea na kuhifadhia mizigo kwa muda kwa nchi jirani za
DR Congo, Burundi, Rwanda, Uganda na Zambia. Maeneo hayo ni pamoja na eneo
lenye ukubwa ekari 132 linalomilikiwa na Jitegemee Trading Co. Ltd lililopo katika bonde
la mto Msimbazi na eneo lenye ukubwa wa ekari 39 lililopo Kiwalani
linalomilikiwa na TAZARA. Mamlaka vilevile kwa kushirikiana na Halmashauri ya
Manispaa ya Temeke, inaanzisha mradi wa maegesho ya magari makubwa ya mizigo
eneo la Kurasini linalomilikiwa na Manispaa ya Temeke lenye ukubwa wa ekari 7.5.
Aidha, Mamlaka ya Bandari ipo katika hatua za mwisho kupata eneo la Katosho na
Kibirizi mkoani Kigoma. Vilevile, taratibu za kupata maeneo mengine
zinaendelea.
14.
Mheshimiwa
Spika, utendaji wa Mamlaka ya Bandari umeendelea kuwa bora kama
inavyooneshwa katika viashiria mbalimbali vya utendaji. Muda wa meli kukaa
bandarini (Ship Turnround Time) umepungua kutoka wastani wa siku 6.3 mwaka 2012
hadi wastani wa siku 4.8 mwaka 2013; muda wa Makasha kukaa bandarini (Dwell
time) umepungua kutoka wastani wa siku 9.6 mwaka 2012 hadi wastani wa siku 9.3
mwaka 2013. Uwezo wa bandari wa kupakua magari (Roll On Roll Off capacity) kwa
kila shifti moja ya saa 8 uliongezeka na kufikia magari 671 Desemba, 2013
ikilinganishwa na magari 400 Desemba, 2012. Mwezi Februari, 2014 ulisainiwa
mkataba wa wadau wote wa Bandari kuanza utaratibu wa utoaji wa huduma katika
bandari ya Dar es Salaam kwa saa 24 kwa siku zote na Mamlaka ya Bandari tayari
inatekeleza utaratibu huo. Benki mbili, NMB na CRDB, tayari zimehamishia huduma
za kibenki ndani ya bandari na ni matarajio ya Wizara kuona benki zingine
zikifanya hivyo.
15.
Mheshimiwa
Spika, katika mwaka 2014/2015 Mamlaka ya
Bandari itaendelea na utekelezaji wa miradi iliyoainishwa katika Programu ya
BRN. Miradi hiyo ni: uboreshaji wa Gati Na. 1-7, uongezaji wa kina na upanuzi
wa lango la Bandari ya Dar es salaam, ujenzi wa kituo cha kuhudumia mizigo
Kisarawe, mradi wa kuwaunganisha wadau pamoja kwa njia ya elektroniki, kuweka
mfumo wa ukaguzi wa mizigo inayoingia na kutoka (scanning), kuboresha barabara
na reli za kuingia na kutoka bandarini, kuongeza nafasi ya kuhudumia mizigo kwa
kuhamisha maghala yaliyopo Bandarini na kukamilisha ujenzi wa jengo la bandari
(one stop center).
2.1.2. RELI
16.
Mheshimiwa
Spika, kwa upande wa miundombinu ya reli, ujenzi wa madaraja
matatu umekamilika. Ujenzi wa daraja lililopo kati ya stesheni za Bahi na Kintinku
ulikamilika Novemba, 2013 na ujenzi wa madaraja mawili yaliyopo km 303 na km
293 kati ya stesheni za Kilosa na Gulwe ulikamilika kwa kiwango cha kuweza kupitika
kuanzia Machi, 2014. Kukamilika kwa madaraja haya kumeongeza uhakika na usalama
wa huduma ya usafiri wa reli ya Kati ambao kwa nyakati tofauti ulikuwa
ukikwamishwa kutokana na ubovu na uchakavu wa madaraja hayo.
17.
Mheshimiwa
Spika, Serikali inaendelea kushirikiana na Benki ya Dunia
kugharamia mradi wa kuinua uwezo wa madaraja yaliyo chini ya tani 15 kwa ekseli
ili kufikia tani 25 kwa ekseli kati ya Dar es Salaam na Isaka. Mshauri
mwelekezi atakayefanya kazi ya uthamini na usanifu wa madaraja yote yaliyo
katika reli ya kati ili yawe na uwezo wa kubeba mzigo wenye uzito wa tani 25
kwa ekseli amepatikana. Aidha, katika mwaka 2014/2015 ujenzi madaraja 16 kati
ya madaraja 25 yaliyo katika hali mbaya kati ya stesheni za Dar es Salaam na
Tabora utaanza.
18. Mheshimiwa
Spika, mradi wa kutandika reli za ratili 80 kwa yadi kati ya
stesheni za Kitaraka na Malongwe urefu wa km 89 umekamilika na matengenezo ya
eneo la reli kati ya Kilosa na Gulwe lililoathiriwa vibaya na mafuriko, nayo
yamekamilika. Kukamilika kwa ujenzi wa njia ya reli kati ya stesheni za
Malongwe na Kitaraka nilikoelezea hivi punde, kunafanya reli zilizotandikwa
zenye uzito wa ratili 80 kwa yadi kati ya Dar es Salaam na Tabora kufikia jumla
ya km 527. Katika mwaka 2014/2015, Serikali itaendelea na utandikaji
wa reli za uzito wa ratili 80 kwa yadi kati ya stesheni za Igalula na Tabora
(km 37) na maeneo mbalimbali kati ya stesheni ya Dar es Salaam na Munisagara
(Km 283). Faida ya kuwa na reli nzito ni pamoja na kupunguza ajali za treni,
kuongeza mwendokasi na uwezo wa treni kubeba mizigo.
19.
Mheshimiwa
Spika, kuhusu tatizo la kujaa
mchanga kwenye makaravati yaliyopo kati ya stesheni za Gulwe na Godegode kila
mara mvua inaponyesha, Serikali imechukua hatua zifuatazo ili kudhibiti hali
hiyo:
·
Ujenzi
wa daraja na miundombinu mingine
ya kuepusha kujaa kwa mchanga karibu na karavati lililopo Km 349/450c. Rasimu
ya mkataba wa Mshauri Mwelekezi atakayefanya usanifu wa kina wa mradi huo ndani
ya mwaka ujao wa fedha, imewasilishwa kwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa
ushauri;
·
Kufanya
usanifu na ujenzi wa mabwawa mawili makubwa ya kupunguza kasi ya maji maarufu
kama “punguza”. Bwawa la kwanza litajengwa sehemu ya Kimagai karibu na stesheni
ya Godegode na bwawa la pili litajengwa karibu na stesheni ya Msagali kuanzia mwaka
wa fedha 2014/2015: na
·
Shirika
la Maendeleo la Ushirikiano wa Kimataifa la Japan (JICA) kwa kushirikiana na
Serikali kupitia mradi wa Tanzania Intermodal Rail Project (TIRP) litatuma timu ya
wataalam mwezi Julai mwaka huu kutafuta ufumbuzi wa kudumu wa tatizo la
uharibifu wa mara kwa mara wa miundombinu ya reli kutokana na mvua kati ya
stesheni za Kilosa na Gulwe.
20.
Mheshimiwa
Spika, mwaka 2013/2014, Wizara ilipanga kuanza maandalizi ya
kuunda Mfumo wa Kusimamia na Kufuatilia Mizigo na Vyombo vya Uchukuzi (Cargo
Tracking & Management System). Napenda kutoa taarifa kuwa, awamu ya kwanza
ya usambazaji wa mfumo huu itaanza mwaka 2014/2015. Kukamilika kwa mfumo huu
kutarahisisha ukusanyaji na utunzaji wa kumbukumbu za kiutendaji kuhusu wingi
wa shehena, usalama wake, mwendo wa vyombo vya uchukuzi wa shehena (pamoja na
treni) na usalama wake.
21.
Mheshimiwa
Spika, kuhusu uboreshaji wa huduma za reli, Serikali imefanya
maandalizi yafuatayo:
·
Ununuzi
wa vichwa vipya vya treni 13. Mkataba wa manunuzi ulisainiwa
Aprili, 2013 na malipo yote yamefanyika. Vichwa hivyo vinatarajiwa kuanza
kuwasili nchini Desemba, 2014;
·
Ununuzi
wa mabehewa mapya 22 ya abiria. Mkataba ulisainiwa Machi,
2013 na malipo yote yamefanyika. Mabehewa hayo yanatarajiwa kuanza kuwasili
nchini mwishoni mwa Septemba, 2014;
·
Ununuzi
wa mabehewa 274 ya mizigo. Mkataba ulisainiwa Machi, 2013 na
malipo ya awali yalikamilika Februari, 2014. Malipo ya mwisho yanatarajiwa
kukamilika kabla ya mwisho wa Juni, 2014 na mabehewa hayo 274 yataanza kuwasili
nchini Septemba, 2014;
·
Ununuzi
wa mabehewa 34 ya breki ulisainiwa Machi, 2013 na malipo yote
yamekamilishwa. Mabehewa hayo yanatarajiwa kuanza kuwasili nchini mwezi Julai,
2014;
·
Ununuzi
wa mabehewa 25 ya kubebea kokoto. Malipo yote yamekamilika na mabehewa hayo
yanatarajiwa kuanza kuwasili nchini Julai, 2014;
·
Kujenga
upya vichwa vinane vya treni. Kazi ilianza Machi, 2013 kwenye karakana yetu ya
Morogoro na hadi kufikia Aprili, 2014 vichwa vitatu vilikuwa vimekamilika.
Vichwa vitano vilivyobaki vinatarajiwa kukamilika kufikia Septemba, 2014.
22.
Mheshimiwa
Spika, katika kutekeleza miradi ya reli chini ya BRN, kwa mwaka
2013/2014 Wizara iliidhinishiwa bajeti ya maendeleo ya Shilingi bilioni 165.68.
Hadi kufikia Aprili 2014, Wizara ilikuwa imepokea jumla ya Shilingi bilioni
145.08 sawa na asilimia 88 ya bajeti iliyoidhinishwa kwa ajili ya kugharamia
utekelezaji wa miradi. Napenda kuchukua fursa hii kuishukuru Serikali kwa
kuweka kipaumbele katika utoaji wa fedha za utekelezaji wa miradi ya BRN.
23.
Mheshimiwa
Spika, Katika mwaka ujao wa fedha wa 2014/2015, Serikali imetenga
shilingi bilioni 126.9 chini ya Mpango wa BRN kwa ajili ya kuunda upya vichwa
vya treni vingine nane; kununua mabehewa mengine mapya ya mizigo 204; kununua
vichwa vingine vya treni vipya 11 na kuendelea na matengenezo ya njia ya reli
ya kati yenye mtandao wa urefu wa km 2,707.
2.2 HUDUMA ZA UCHUKUZI KWA NJIA YA NCHI KAVU
2.2.1 Usafiri na Uchukuzi kwa Njia ya Barabara
24.
Mheshimiwa
Spika, katika
mwaka 2013/2014, Sekta ya usafiri na uchukuzi kwa njia ya barabara imeendelea
kuimarika na kutoa mchango wake katika kutekeleza shughuli za kiuchumi, kijamii
na kimaendeleo. SUMATRA kwa kushirikiana na wadau mbalimbali, imeendelea
kuchukua hatua kukabiliana na matukio ya ajali barabarani. Hatua hizo ni pamoja
na kununua vifaa kwa ajili ya kupima ulevi na mwendo kasi na kuvikabidhi kwa Jeshi
la Polisi. Hatua nyingine ni kusimamisha leseni za mabasi yaliyohusika katika
matukio ya ajali ambapo katika kipindi cha Julai, 2013 hadi Machi, 2014, jumla
ya leseni 34 za usafirishaji wa abiria zilisimamishwa na wamiliki wa mabasi
walitakiwa kuwasilisha kwa maandishi mpango utakaotumika katika kudhibiti ajali
za barabarani. Wizara inaendelea kufuatilia utekelezaji wa mipango hiyo ili
kupima matokeo na mafanikio yake.
2.2.2 Huduma za Usafiri na Uchukuzi Mikoani na Vijijini
25.
Mheshimiwa
Spika, Wizara
kupitia SUMATRA imeendelea kuruhusu aina mbalimbali za usafiri kama vile
pikipiki za magurudumu mawili na matatu, magari aina ya Noah n.k. Hatua hizo
zinaenda sambamba na ukaguzi wa kushtukiza wa vyombo vyote vya usafiri, kutoa
nauli elekezi, na kutoa elimu, mafunzo na ushauri kwa watumiaji na watoaji wa
huduma za usafiri wa barabara. Aidha, Wizara imeendelea kushirikiana na
wasafirishaji wa abiria na mizigo kupitia vyama vyao ili kuboresha huduma za
uchukuzi wa barabara.
2.2.4 Huduma za Usafiri wa Reli Jijini Dar es Salaam
26.
Mheshimiwa
Spika,
huduma za usafiri wa reli katika Jiji la Dar es Salaam kati ya stesheni za Dar
es Salaam hadi Ubungo Maziwa na Mwakanga hadi Kurasini zimeendelea kukua na
kupendwa na wananchi. Kampuni ya Reli (TRL) ilisafirisha abiria 1,343,763
katika mwaka 2013 ikilinganishwa na abiria 230,009 waliosafirishwa katika mwaka
2012. Aidha, kwa upande wa TAZARA, abiria 1,460,506 walisafirishwa katika mwaka
2013 ikilinganishwa na abiria 148,524 waliosafirishwa katika mwaka 2012. Wizara
inaendelea na mikakati mbalimbali ya kuboresha huduma hii ikiwemo mpango wa
kuvutia sekta binafsi kuwekeza kwenye usafiri wa treni Jijini. Mikakati hiyo inalenga kuongeza eneo la
ujenzi wa miundombinu na uboreshaji wa usafiri jijini kutoka umbali wa kilometa
20 za sasa hadi kilometa 50 ili kujumuisha wilaya za Kibaha, Kisarawe, Mkuranga
na Bagamoyo. Kuhusu uwekezaji katika usafiri wa treni Jijini Dar es Salaam kwa
utaratibu wa PPP, kampuni kadhaa za ndani na nje ya nchi zimeonyesha ari ya
dhati. Aidha, Wizara kwa kushirikiana na TRL na RAHCO inaangalia uwezekano wa
kuanzisha kampuni tanzu ya kutoa huduma za usafiri wa reli mijini ambayo itatoa
fursa kwa sekta binafsi kushiriki. Katika mwaka 2014/2015, Serikali itakamilisha upembuzi
yakinifu wa ujenzi wa njia mpya za reli Jijini Dar es Salaam zikiwemo zile za
kwenda maeneo ya Pugu, Mbagala/Chamazi, Luguruni/Kibaha na Bunju/Kerege.
2.3 Usafiri na Uchukuzi kwa Njia ya Reli
27.
Mheshimiwa
Spika,
licha ya sekta ya reli kukabiliwa na changamoto mbalimbali, miundombinu na
huduma za reli zimeendelea kuboreshwa ili ziendelee kuchangia katika pato la
Taifa na kuongeza mchango wa sekta ya uchukuzi kwa kupitia njia ya reli.
Mwelekeo uliopo katika sekta ya uchukuzi ni kuhakikisha kuwa mizigo mizito na
mingi inayosafirishwa umbali mrefu inatumia usafiri wa reli.
28.
Mheshimiwa
Spika, katika
mwaka 2013/2014, mshauri mwelekezi (Kampuni ya COWI kutoka Denmark)
alianza kazi ya usanifu wa uboreshaji wa njia ya reli ya Tanga – Arusha (km
438) Septemba, 2013 na anatarajiwa kukamilisha kazi hiyo Julai, 2014. Mshauri
mwelekezi (Kampuni ya H.P. Gauff kutoka Ujerumani) alianza kazi ya kufanya
upembuzi yakinifu na usanifu wa awali wa ujenzi wa reli mpya ya Arusha – Musoma
(km 660) Septemba, 2013. Kazi hii inatarajiwa kukamilika Septemba, 2014. Aidha,
katika mwaka 2014/2015, Serikali imetenga Shilingi bilioni 7.55 kwa ajili ya
kukamilisha kazi ya kufanya usanifu wa ujenzi wa reli ya Tanga – Arusha;
kukamilisha upembuzi yakinifu kwa ajili ya ujenzi wa reli mpya kati ya Arusha –
Musoma pamoja na matawi ya kwenda Engaruka na Minjingu; kukarabati njia ya reli
ya Tanga hadi Arusha na kufanya usanifu wa kina wa kuinua kiwango cha reli
itakayounganisha reli ya kati na ile ya kaskazini (yaani Tanga-Arusha), kutokea
stesheni ya Ruvu Junction hadi Mruazi kuwa katika kiwango cha kimataifa na
kuunganisha reli ya Mruazi na Bandari ya Mbegani, Bagamoyo.
29.
Mheshimiwa
Spika,
kuhusu ulipaji fidia kwa wakazi wa eneo la Mwambani-Tanga ili kupisha ujenzi wa
sehemu ya kupanga mabehewa na kugeuzia (marshalling yard), jumla ya wakazi 607
kati ya 619 wamekwisha lipwa fidia ya jumla ya shilingi bilioni 4.7. Aidha,
hadi Aprili, 2014 hundi 187 kati ya 188 za fidia ya makaburi zilikuwa
zimelipwa. Hundi 13 zenye thamani
ya shilingi milioni 231.4 bado hazijachukuliwa kutokana na zuio la mahakama au
wahusika kutojitokeza.
30.
Mheshimiwa
Spika,
katika mwaka 2013/2014, kazi ya ukarabati wa tuta la reli linalokatiza mto
Ugala pamoja na daraja lake ilifanywa na Kampuni ya R & A Works Ltd na kukamilika Oktoba,
2013. Aidha,
kazi ya kuondoa reli nyepesi na zilizochakaa zenye uzito wa ratili 45 kwa yadi
na kuweka reli zenye uzito wa ratili 56.12 kwa yadi kwa umbali uliobaki wa km
4.59 kati ya 9 zilizobainishwa kuhitaji ukarabati wa haraka kati ya sehemu ya
Lumbe - Mto Ugala - Katumba ilikamilika Februari, 2014. Katika mwaka 2014/2015,
Serikali imetenga shilingi bilioni 5 kwa ajili ya kuendelea na matengenezo ya
njia ya reli kati ya Kaliua - Mpanda, kufanya usanifu wa kina wa uboreshaji wa
njia ya reli kati ya Kaliua – Mpanda kuwa kiwango cha kimataifa na kufanya
upembuzi yakinifu wa ujenzi wa reli mpya ya kutoka Mpanda hadi Karema.
31.
Mheshimiwa
Spika,
Serikali imeendelea kushirikiana na Serikali za Rwanda na Burundi katika
uendelezaji wa mradi wa ujenzi wa reli ya Dar es salaam – Isaka – Keza - Kigali
(Km 1,464) na Keza – Musongati (km 197) kwa kiwango cha kimataifa. Mshauri
mwelekezi, Kampuni ya CANARAIL kutoka Canada alikamilisha kazi ya kufanya
upembuzi wa kina Februari, 2014. Serikali inaendelea na juhudi zake za kupata
wawekezaji/fedha kwa ajili ya ujenzi wa reli ya hiyo. Aidha, Machi, 2014
Serikali za Tanzania na Burundi zilitiliana saini ya Makubaliano ya Awali (MoU)
ili kuendeleza mradi wa ujenzi wa reli ya kutoka Uvinza hadi Musongati.
32.
Mheshimiwa
Spika,
kazi ya usanifu wa kina wa kuinua kiwango cha reli ya Isaka - Mwanza ilianza
Septemba, 2013 na inatarajiwa kukamilika Julai, 2014. Aidha, Halmashauri ya
Jiji la Mwanza imetenga eneo lenye ukubwa wa hekta 148 sehemu ya Buhongwa kwa
ajili ya ujenzi wa sehemu ya kupanga mabehewa na kugeuzia treni (marshalling
yard). Mshauri mwelekezi anayefanya tathmini ya ulipaji fidia anaendelea na
kazi. Vilevile, katika mwaka 2014/2015, Serikali imetenga Shilingi bilioni 4 kwa
ajili ya kufanya usanifu wa kina wa kuinua kiwango cha njia ya reli kati ya
Tabora – Kigoma na kufanya upembuzi yakinifu wa ujenzi wa reli za kutoka Uvinza
hadi Musongati.
33.
Mheshimiwa
Spika, kuhusu upembuzi
yakinifu na usanifu wa awali wa ujenzi wa reli ya Mtwara – Songea – MbambaBay
na michepuko ya kwenda Mchuchuma na Liganga, Mtaalam mwelekezi wa kufanya kazi
hii ameshapatikana. Mkataba wa kutekeleza kazi hii utasainiwa wakati wowote
kabla ya mwisho wa Juni, 2014 na kazi hiyo ya usanifu itakamilika baada ya
miezi 12.
34.
Mheshimiwa
Spika, ujenzi wa kituo cha
kupakua na kupakia makasha (ICD) cha Mwanza ulikamilika Desemba, 2013. Kituo
hicho kimepata mwendeshaji Kampuni ya Transpark Ltd. Kukamilika kwa kituo
hiki pamoja na kile cha Shinyanga kutasaidia kufikia malengo ya Programu ya
Matokeo Makubwa Sasa (BRN) ya kuongeza mzigo unaosafirishwa katika njia ya reli
ya kati na pia kupunguza muda wa mzunguko wa mabehewa.
35.
Mheshimiwa
Spika, katika
mwaka 2013/2014, TAZARA ilianza kutekeleza Itifaki ya 15 kwa kuagiza vichwa vya
treni vipya 4; vichwa vya sogeza vipya 4; mabehewa ya abiria mapya 18; mashine
za okoa 2, mitambo na vifaa vya usalama. Vifaa hivyo vinatarajiwa kuanza
kuwasili nchini Desemba, 2014.
36.
Mheshimiwa
Spika, katika
mwaka 2013/2014 nilitoa taarifa kuhusu Serikali za Tanzania na Zambia kuendelea
kurekebisha Sheria ya TAZARA Na. 23 ya mwaka 1975 kama ilivyohuishwa na Sheria
Na. 4 ya mwaka 1995 Sura ya 143. Napenda kutoa taarifa kuwa marekebisho ya
Sheria hiyo yalifanyika na Rasimu kuwasilishwa katika kila nchi mwanahisa ili
kuboresha na kutoa maoni. Aidha, rasimu hii ya Sheria itawasilishwa kwenye Bodi
ya TAZARA Juni, 2014 na kuwasilishwa katika Baraza la Mawaziri la TAZARA
litakalokutana Julai, 2014 kwa ajili ya kupata idhini ya kuendelea na mchakato
wa kutunga sheria.
2.4 Udhibiti wa Huduma za Usafiri
wa Nchi Kavu na Majini
37.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka
2013/2014, udhibiti wa huduma za usafiri wa nchi kavu na majini umeendelea
kusimamiwa na kutekelezwa na SUMATRA kwa kusogeza huduma zake karibu na wananchi.
Hadi Machi, 2014, SUMATRA ilikuwa imefungua ofisi zake katika mikoa hiyo na
hivyo kufanya Mamlaka kuwa na ofisi katika mikoa yote 25 ya Tanzania Bara.
2.6 Udhibiti wa Huduma za Usafiri kwa Njia ya Barabara
38.
Mheshimiwa
Spika,
kupitia Hotuba ya mwaka 2013/2014 nilitoa maagizo kwa SUMATRA kuhakikisha kuwa
inaandaa utaratibu stahiki utakaowezesha kutoa leseni kwa magari aina ya Noah
kwa kuzingatia usalama wa abiria na mali zao. Ninapenda kuliarifu Bunge lako
Tukufu kuwa, SUMATRA iliandaa utaratibu huo na sasa magari aina ya Noah
yamesajiliwa na kutoa huduma za abiria katika mikoa 18 ya Tanzania Bara.
39.
Mheshimiwa
Spika,
katika mwaka 2013/2014, SUMATRA ilizifuatilia Halmashauri saba ambazo zilikuwa
hazijasaini mkataba wa Uwakala wa kusimamia utekelezaji wa kanuni za usafiri wa
pikipiki za magurudumu mawili na matatu katika maeneo ya halmashauri zao.
SUMATRA sasa imekwishaingia makubaliano na Halmashauri 135. Baada ya kusaini
makubaliano na Halmashauri hizo, kwa sasa SUMATRA inaendelea kusaini makubaliano
na Halmashauri nyingine mpya 29. Utekelezaji wa makubaliano hayo utapunguza
ajali na uhalifu unaohusisha matumizi ya pikipiki hizo.
2.7 Udhibiti wa Usalama wa Vyombo vya Usafiri Majini
40.
Mheshimiwa
Spika,
katika mwaka 2013/2014, Wizara kupitia SUMATRA iliendelea kusimamia usalama wa
vyombo vya usafiri majini, abiria na mizigo yao. SUMATRA na Mamlaka ya Usafiri
Baharini Zanzibar (ZMA) wameendelea kushirikiana katika kufanya ukaguzi na
uhakiki wa ubora wa vyombo vya usafiri majini na kubadilishana taarifa kuhusu
usalama wa vyombo vya usafiri majini bandarini na uhifadhi wa mazingira. Aidha,
Kituo cha kuratibu taarifa za Utafutaji na Uokoaji, ulinzi na usalama Majini
(MRCC) kilichopo Dar es Salaam kiliendelea kupokea na kuratibu taarifa za
utafutaji na uokoaji. Kwa upande wa Tanzania Bara kituo hicho kiliripoti ajali
13 ambazo watu 125 waliokolewa na wengine 24 kupoteza maisha.
3.0 USAFIRI NA UCHUKUZI MAJINI
3.1 Huduma za Uchukuzi Katika Maziwa
41.
Mheshimiwa
Spika,
wakati nawasilisha bajeti ya mwaka 2013/2014, niliahidi kuanza ujenzi wa meli
mpya tatu katika maziwa ya Victoria, Tanganyika na Nyasa na ukarabati wa meli
za MV. Victoria, MV. Umoja na MV. Serengeti. Pamoja na kwamba mradi huu mkubwa
tayari una Mshauri Mwelekezi (Kampuni ya OSK Shiptech ya Denmark),
umechelewa kuanza kutokana na gharama zake kupanda kwa asilimia 163 ya gharama
zilizokadiriwa awali. Serikali inajadiliana na Serikali ya Denmark inayofadhili
mradi huo kuhusu ongezeko hilo la gharama. Aidha, kutokana na mahitaji makubwa
ya uchukuzi katika ziwa Tanganyika, mradi huo sasa utajenga meli mpya nne, moja
katika Ziwa Victoria, mbili Ziwa Tanganyika na moja Ziwa Nyasa pamoja na
kukarabati meli tatu.
3.3 Huduma za Bandari
42.
Mheshimiwa
Spika,
katika mwaka 2013/2014, niliahidi kuhudumia shehena ya tani milioni 13.84
ikijumuisha makasha 430,600 yatakayohudumiwa katika kitengo cha TICTS. Napenda
kutoa taarifa kuwa katika kipindi cha Julai, 2013 hadi Aprili, 2014, Mamlaka
ilihudumia shehena ya tani milioni 13.7 ambazo ni sawa na asilimia 99 ya lengo
la mwaka. Matarajio ni kwamba kufikia mwishoni mwa mwezi Juni, 2014 tutakuwa
tumefikia lengo la tani milioni 13.84. Katika kipindi hicho kitengo cha makasha
(TICTS) kilihudumia makasha 348,811 ambapo ni sawa na asilimia 76 ya lengo la
mwaka.
43.
Mheshimiwa
Spika,
shehena iliyohudumiwa kwenda na kutoka nchi jirani za Zambia, Malawi, Jamhuri
ya Kidemokrasia ya Kongo, Burundi, Rwanda na Uganda katika kipindi cha Julai,
2013 hadi Aprili, 2014 ilikuwa ni tani milioni 3.654, ikilinganishwa na tani
milioni 3.182, (sawa na ongezeko la asilimia 12.9) zilizohudumiwa katika
kipindi kama hicho mwaka 2012/2013. Ongezeko la shehena hii limetokana na
jitihada zinazofanywa na Wizara kwa kushirikiana na wadau mbalimbali katika
kuvutia wateja toka nchi jirani kuendelea kutumia bandari zetu. Aidha,
uboreshaji wa huduma, uimarishaji wa usalama wa mizigo ya wateja na utoaji
huduma za bandari kwa saa 24 kila siku umesaidia kurudisha imani kwa wateja
kutoka nchi hizo.
44.
Mheshimiwa
Spika,
katika hotuba ya mwaka 2013/2014
tuliahidi utekelezaji wa miradi ya bandari kama ifuatavyo:
i.
Ujenzi
wa gati la bandari ya Mafia ambao ulikamilika Septemba, 2013 na gati hilo
kufunguliwa rasmi na Mhe. Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, Rais wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania, Oktoba, 2013. Vilevile, katika mwaka 2014/2015 Mamlaka
imetenga kiasi cha shilingi milioni 400 kwa ajili ya kuweka kivuko cha kupanda
na kushuka kwenye vyombo vidogo vidogo kwa kutumia gati lililopo na kuimarisha
usalama wa abiria kwa kuziba uwazi uliopo pembezoni mwa gati. Aidha, katika mwaka
2014/2015 TPA itakarabati na kuboresha gati la Nyamisati (Mkuranga) ili
kuhudumia wasafiri wanaokwenda Mafia;
ii.
Ujenzi
wa gati la bandari ya Kipili katika Ziwa Tanganyika, umekamilika kwa zaidi ya
asilimia 90 na unatarajiwa kuisha Julai, 2014. Kazi za ujenzi wa magati ya
Karema, Lagosa na Sibwesa (Kalya) katika Ziwa Tanganyika zimetelekezwa na
Mkandarasi M/S Modspan. Aidha, kazi za ujenzi wa magati ya Kagunga katika Ziwa
Tanganyika na Kiwira katika Ziwa Nyasa zilizokuwa zinatekelezwa na Mkandarasi
Canopies International hazijakamilika na Mkandarasi amekimbia eneo la kazi.
Serikali imeiagiza Mamlaka ya Bandari kuchukua hatua zifuatazo mapema
iwezekanavyo:
·
Iwanyang’anye
Makandarasi hao kazi hizo na kuzitangaza upya na washindi waanze ujenzi mwezi
Agosti, 2014 na kukamilisha kazi mwezi Julai, 2015 chini ya usimamzi wa karibu
wa Mamlaka. Kazi hizo zimetangazwa upya tarehe 17 Aprili, 2014;
·
Iwashtaki
Makandarasi hao kwa Mamlaka ya Ununuzi wa Umma (PPRA), Bodi ya Usajili wa
Makandarasi (CRB) ili kuzifutia usajili Kampuni hizo. Kazi hiyo imefanyika;
·
Mamlaka
iitishe dhamana walizoweka Makandarasi hao (Advance guarantee and Performance
Bonds) ili kufidia sehemu ya gharama. Wakati kazi hii inafanyika, imebainika
kuwa Mkandarasi M/S Canopies International aliwasilisha Mamlaka ya Bandari
nyaraka za kughushi za dhamana ya malipo ya awali na hivyo kupata kazi hiyo.
Mamlaka imeagizwa imfungulie Mkandarasi huyo kesi ya jinai haraka iwezekanavyo
na ichunguze misingi ambayo watendaji wake walizipokea dhamana hiyo ya Benki;
Vilevile,
katika mwaka 2014/2015 Mamlaka imetenga kiasi cha shilingi milioni 500 kwa
ajili ya ujenzi wa gati katika bandari ya Ndumbi katika Ziwa Nyasa ili
kurahisisha usafirishaji wa abiria na makaa ya mawe kutoka eneo la Ngaka.
iii.
Ujenzi
wa bandari ya Mbegani Bagamoyo. Mnamo Desemba, 2013 Serikali ilisaini
makubaliano ya kutekeleza mradi huo (Implementation Agreement) na Februari,
2014 Kampuni ya China Merchants Holdings International Limited iliwasilisha andiko la
mradi. Hivi sasa Serikali ipo
katika hatua za mwisho za kukamilisha uchambuzi wa andiko hilo ili kuendelea na
hatua zinazofuata ikiwa ni pamoja na kukabidhi eneo la mradi kwa mwekezaji
huyo. Kazi ya tathmini ya mali zilizo kwenye eneo husika itakamilika Juni, 2014
na malipo ya fidia yatafanyika katika mwaka wa fedha 2014/2015.
iv.
Kuendelea
na maandalizi ya kuanza kwa ujenzi wa Bandari za Mwambani (Tanga) na Mtwara,
ambapo zabuni zilitangazwa tarehe 27 Machi, 2014 na zitafunguliwa tarehe 26
Juni, 2014. Kazi zinatarajiwa kuanza ifikapo Septemba 2014 na kukamilika
Mwishoni mwa mwaka 2016.
v.
Kuanza
maandalizi ya ujenzi wa magati ya Pangani (Tanga) katika bahari ya Hindi, Ntama
na Lushamba katika Ziwa Victoria na Kabwe katika Ziwa Tanganyika. Gati la
Pangani Mkandarasi amepatikana ambaye ni M/S Alpha Logistics na ataanza kazi mwezi
Juni, 2014 na muda wa utekelezaji ni miezi 12 na hivyo kazi zitakamilika mwezi
Julai, 2015. Magati ya Ntama na Lushamba utekelezaji wake utaanza mwezi Juni,
2014. Kuhusu ujenzi wa gati la Kabwe utekelezaji wake utaanza mwezi Novemba,
2014;
vi.
Kuimarisha
usalama wa mizigo na bandari. Mamlaka imepanga kuanza utekelezaji wa mradi wa electronic
cargo Tracking system
ambapo zabuni za mradi zimeshaandaliwa na zinatarajiwa kutangazwa mwezi Julai,
2014.
vii.
Ununuzi
wa Scanners
kwa ajili ya ukaguzi wa mizigo. Scanners tatu zimeagizwa na zinatarajiwa
kuwasili Septemba, 2014: na
viii.
Ulipaji
fidia kwa wakazi wa Kibirizi ili kupisha ujenzi wa gati. Umeanza na unatarajiwa
kukamilika kabla ya Juni, 2014.
45.
Mheshimiwa
Spika, katika jitihada za
Serikali za kusogeza huduma za kibandari karibu na wateja, tarehe 1 Mei, 2014,
Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari ilifungua ofisi mjini Lubumbashi nchini DR
Congo. Kupitia ofisi hii, wateja walioko DRC hawatalazimika kusafiri kwenda Dar
es Salaam wakiwa wamebeba fedha kwa ajili ya kulipia mizigo yao. Badala yake,
wataweza kulipia huduma za bandari wakiwa nchini kwao DRC na kupokea mizigo yao
kule kule. Aidha katika mwaka wa fedha 2014/15, Mamlaka imepanga kufungua ofisi
nyingine katika nchi za Zambia, Burundi na Rwanda. Wizara inawasiliana na
Wizara ya Fedha na Mamlaka ya Mapato Tanzania kuona uwezekano wa kuwa na
watumishi wa TRA katika ofisi hizo ili kuboresha ufanisi. Vile vile ili
kuboresha huduma za forodha (Single Customs Territory – SCT) kwa nchi za
Jumuiya ya Afrika Mashariki, Mamlaka imetenga eneo la ofisi katika jengo la
Ex-NASACO katika bandari ya Dar es Salaam kwa ajili ya wafanyakazi kutoka
katika nchi za Jumuiya. Taratibu za kubadilishana taarifa kwa njia ya
kielektroniki zimeshakamilika ili kuwezesha utekelezaji wa kituo kimoja cha
forodha (SCT).
46.
Mheshimiwa
Spika, kuhusu uendelezaji wa kituo
cha mizigo cha Kisarawe (Kisarawe Freight Station) mtaalam mwelekezi wa kufanya
upembuzi yakinifu na usanifu wa kina wa kuendeleza eneo la Kisarawe amepatikana.
Mtaalam huyo (Royal Haskoning wa Uholanzi) anatarajiwa kuanza kazi mwezi
Julai, 2014 na kukamilisha mwezi Januari, 2015.
47.
Mheshimiwa
Spika, katika
hotuba ya mwaka 2013/2014 niliahidi kuanza ujenzi wa gati Na. 13 na 14. Napenda
kutoa taarifa kuwa mradi huu umechelewa kuanza kutokana na sababu kubwa tatu:
(i)
Gharama
za ujenzi wa gati hizo mbili ya Dola za Marekani milioni 523 (karibu shilingi
bilioni 837), bado ni juu mno na inayoendelea kuzua maswali mengi yasiyojibika
pale gharama za miradi mingine ya aina hiyo hiyo zinapoangaliwa ambazo ni chini
ya nusu ya gharama hiyo ya Dola za Marekani milioni 523;
(ii)
Gharama
hiyo ya ujenzi ya Dola za Marekani milioni 523 ilifikiwa ili kujenga gati mbili
za kisasa (na vifaa vyake) zinazoweza kuhudumia meli kubwa hata za aina ya Panamax zenye urefu wa mita
294.13, upana wa mita 32.31 na kina cha mita 12.04. Lakini mkandarasi CCCC/CHEC
hakuwa mkweli kwani aliendelea na mchakato wa usanifu wa awali (hydrographical
and topographical surveys) huku akijua kuwa gati namba 13 na 14 zisingeweza kuhudumia
meli kubwa za aina hiyo ya Panamax kwani kipenyo cha kugeuza meli za ukubwa huo
sehemu hiyo hakitoshi, mita 440 tu badala ya 600 ambazo kuzipata lazima tumege
mita 160 za ardhi ya jeshi upande wa pili wa bandari. Aidha, gharama za kundoa
mabomba ya mafuta chini ya bahari na kuyahamishia sehemu nyingine (pamoja na
kituo chake cha KOJ) ili kuruhusu dredging ambayo ni lazima ifanyike kuweza
kuhudumia meli kubwa zenye kina cha mita 12.04 haikuzingatiwa kwenye gharama za
Dola za Marekani milioni 523. Vilevile kwa kuzingatia taratibu za kiusalama
katika Bandari na kwa watumiaji bandarini, huduma kama hiyo ya KOJ kuwa
katikati ya Magati ya Bandari haiashirii mazingira salama. Hivyo kwa kufumbia
macho gharama hizo bayana, kampuni hizi mbili hazina nia njema ya kufanya
biashara ya kiungwana.
(iii)
Mchakato
wa ujenzi wa gati namba 13 na 14 ulisimama mwezi Septemba, 2013 baada ya
kampuni hizo mbili za CCCC na CHEC, kuanza kuvutana kuhusu utekelezaji wa mradi
huo. CCCC, kampuni mama ya CHEC ambayo ilikuwa imefungiwa (black-listed) na
PPRA na hivyo kutakiwa kuwaachia CHEC mradi, haikutaka kuiachia CHEC mradi huo,
hivyo ikateua afisa wake na kumpatia vitambulisho vya CHEC na CHEC ikamteua
afisa mwingine. Mvutano huo ukapelekea tuwe na watu wawili bandarini wote
wakiwa na nguvu za kisheria za kuiwakilisha CHEC. Kitendo hicho kikasababisha Deed
of Novation
iliyoandaliwa na TPA na kuridhiwa na Mwanasheria Mkuu wa Serikali kutosainiwa
kati ya Mamlaka na Mkandarasi mpaka sasa.
Kutokana na sababu
hizo, Mamlaka ya Bandari inakusudia kuachana na Kampuni za CCCC na CHEC na
hivyo kuanza taratibu za kushirikisha Kampuni zingine kutekeleza mradi huu kwa
masharti yanayokubalika. Tayari Mwanasheria Mkuu wa Serikali ameombwa ushauri
kuhusu suala hili.
Aidha, Benki ya Dunia
kupitia International Bank for Reconstruction and Development (IBRD) kwa kushirikiana na
DFID na TMEA zimekubali kutoa mkopo wenye masharti nafuu (soft loan) wa
asilimia 65 na msaada (grant) wa asilimia 35 kwa ajili ya uendelezaji wa Gati
namba 13 na 14, uboreshwaji wa Gati namba 1 – 7 na uongezaji wa kina cha lango
la Bandari ya Dar es Salaam.
Kutokana na nia hiyo
ya Benki na Washirika wake, TPA imeandaa Rasimu za Nyaraka za Zabuni (Draft
Tender Documents) za utekelezaji wa miradi hii kwa njia ya Usanifu na Ujenzi
(design and Build). Nyaraka zimewasilishwa Benki ya Dunia kwa ajili ya kupata
kibali. Mradi huu unatarajiwa kuanza mwaka wa fedha 2014/2015.
48.
Mheshimiwa
Spika, kuhusu ukarabati wa bandari za Mwanza na
Kigoma kazi ya kukarabati chelezo (slipway) katika bandari ya Kigoma inaendelea
na inatarajiwa kukamilika Agosti, 2014. Aidha, mkandarasi wa kufanya ukarabati
wa kreni ya kupakua na kupakia mizigo amepatikana na ataanza kazi Juni, 2014 na
kukamilisha ukarabati mwezi Septemba, 2014. Kwa upande wa bandari ya Mwanza mshauri
mwelekezi wa kufanya upembuzi yakinifu wa kubainisha mahitaji ya kuendeleza
bandari za Mwanza, Bukoba na Kemondo ataanza kazi Julai, 2014 na kukamilika
mwezi Februari, 2015.
49.
Mheshimiwa
Spika
kutokana na kazi nzuri na ya ufanisi ambayo Mamlaka ya Bandari imefanya ndani
ya kipindi kifupi, Mamlaka imeamua kutumia faida iliyopata kuchochea nyenzo za
uchukuzi pale zilipolala ili kuijengea Mamlaka mazingira ya kufanya kazi vizuri
zaidi na hivyo kuchochea uchumi wa nchi:
(i) Ili kuondoa msongamano wa mizigo bandarini
baada ya nchi kadhaa za jirani kuonesha nia ya kupitisha mizigo mingi zaidi
katika Bandari ya Dar es Salaam, TPA imeamua kugharamia uundaji upya wa vichwa
vitatu vya treni ambavyo vitatumika kuendeshea treni maalumu za mizigo (block
trains) kwenda Kigoma kila wiki kuhudumia wafanyabiashara wa DRC, Burundi na wa
Kigoma na kuendeshea treni maalumu zingine za mizigo kwenda Mwanza kila wiki
kuhudumia wafanyabiashara wa Rwanda na Uganda kwa kushushia mizigo yao Isaka na
Mwanza. TPA inatarajia wafanyabiashara wa Kigoma na Mwanza kuchangamkia fursa
hii kwa hamasa.
(ii) TPA vilevile inaendelea na mazungumzo na
uongozi wa TAZARA ili kutoa huduma za namna hiyohiyo kwa wafanyabiashara wa
Zambia, Malawi na Mbeya ambapo vichwa viwili vya treni vinatarajiwa kuundwa
upya. TPA inatarajia wafanyabiashara wa Mbeya watachangamkia fursa hii endapo
mazungumzo kati yake na TAZARA yakifanikiwa.
(iii) Ili kuchochea uchukuzi wa majini ambapo bandari
zake kwenye maziwa hazina shughuli za kutosha kutokana na uchache wa meli, TPA
inaanza mkakati wa kununua meli za abiria na mizigo kwa awamu katika maziwa
yote makubwa matatu kwa njia ya ubia. Kwa kuzingatia ratiba ya Serikali ya
miradi ya utengenezaji wa meli mpya ambayo inaanzia Ziwa Viktoria na Tanganyika
mwaka ujao wa fedha, TPA itaanza mradi wake wa kwanza mwaka wa fedha wa
2014/2015 katika Ziwa Nyasa ambako usafiri wa majini ni wa mashaka. Mamlaka
itanunua meli yenye uwezo wa kubeba abiria 200 na tani 100 za mizigo.
4.0 USAFIRI NA UCHUKUZI KWA NJIA YA ANGA
4.1 Udhibiti wa Usafiri wa Anga
50.
Mheshimiwa
Spika,
Wizara kupitia Mamlaka ya Usafiri wa Anga imeendelea kusajili ndege nchini
kulingana na masharti ya usajili ambapo hadi Aprili, 2014, ndege 23
zilisajiliwa kwa mara ya kwanza hapa nchini. Vilevile, viwanja vya ndege vya
Mwanza, Musoma, Bukoba, Kigoma, Tabora, Arusha, Tanga, Lindi, Mtwara, Iringa,
Songea, Nachingwea na Kilwa Masoko vilikaguliwa na kupewa leseni za uendeshaji.
Lengo la utoaji wa leseni ya uendeshaji ni kuhakikisha kuwa utekelezaji wa
sheria na kanuni za kitaifa na kimataifa za uendeshaji wa viwanja vya ndege
zinazingatiwa.
51.
Mheshimiwa
Spika,
nia
ya Serikali
ya kuanzisha Mfuko maalum kwa ajili ya kufadhili mafunzo ya urubani na uhandisi
wa ndege imeendelea kutekelezwa. Katika mwaka 2013/2014, Mfuko ulianza kutumika
kwa kufadhili Wanafunzi 5 katika mafunzo ya urubani. Katika mwaka 2014/2015
wanafunzi 10 watafadhiliwa kupitia Mfuko huu. Pamoja na kufadhili mafunzo hayo,
Mfuko unakabiliwa na changamoto ya ufinyu wa bajeti kuweza kupeleka wanafunzi
wengi mafunzoni. Wizara kwa kushirikiana na Mamlaka ya Usafiri wa Anga
inaendelea kutafuta vyanzo vingine vya mapato ili kutunisha fedha za Mfuko huu.
52.
Mheshimiwa
Spika,
limejitokeza tatizo kubwa la uhaba wa ajira kwa marubani vijana ambao
wamesomeshwa na wazazi wao au wadhamini wengine huku ongezeko la marubani
vijana kutoka nje ya nchi likionekana. Serikali inaiagiza TCAA kuhakikisha kuwa
utoaji wa leseni kwa marubani kutoka nje ya nchi unaambatana na vibali vya kazi
(work permits) na Chama cha Marubani kishirikishwe katika mchakato wa kutoa
vibali hivyo ili kuleta uwiano wa marubani wa ndani na nje wanaofanya kazi
nchini. Aidha, TCAA isimamie kikamilifu utekelezaji wa Kanuni za uendeshaji
ndege (Civil Aviation Operation of Aircraft Regulation) za mwaka 2012 ili idadi
ya marubani katika ndege wakati wowote isiwe chini ya mwongozo wa aina ya ndege
husika (aircraft flight manual) na cheti kinachoruhusu ndege kuruka
(Certificate of Airworthiness) kinachotambuliwa na TCAA.
53.
Mheshimiwa
Spika, idadi
ya abiria wanaosafiri kwenda na kutoka nje ya nchi iliongezeka kutoka abiria
2,010,240 mwaka 2012/2013 hadi kufikia abiria 2,251,469 mwezi Aprili, 2014. Hii
ni sawa na ongezeko la abiria kwa asilimia 12. Aidha, abiria wanaosafiri ndani
ya nchi waliongezeka kutoka abiria 2,420,922 katika mwaka 2012/2013 hadi
kufikia abiria 2,808,270 mwezi Aprili, 2014, sawa na ongezeko la asilimia 16. Sababu ya ongezeko la
abiria wa safari za ndani ya nchi ni pamoja na kukua kwa uchumi, kuongezeka kwa mashirika yanayotoa
huduma ya usafiri wa anga, kufunguliwa kwa viwanja vipya kama Songwe - Mbeya,
kukarabatiwa kwa viwanja vya Kigoma, Tabora na Arusha pamoja na kukua kwa
utalii. Katika mwaka 2014/2015, idadi ya abiria wanaotumia usafiri huu
inatarajiwa kufika 5,717,505. Vilevile, idadi ya abiria wa safari za nje
inategemewa kuongezeka baada ya kupitia upya na kusaini mikataba
ya usafiri wa anga kati ya Tanzania na nchi mbalimbali pamoja na mashirika ya Fastjet,
Mango na Proflight
kuanza safari za kimataifa.
54.
Mheshimiwa
Spika, katika
mwaka 2013/2014, safari za ndege
(aircraft movements) ziliongezeka kwa asilimia 7.8 kutoka safari 242,745 mwaka
2012/2013 hadi safari 261,763
Aprili, 2014. Kati ya hizo, safari za kimataifa ziliongezeka kutoka safari 40,426
mwaka 2012/2013 hadi kufikia safari 41,235 mwezi Aprili, 2014. Hii ni sawa na
ongezeko la asilimia 2. Safari za ndani ya nchi pia ziliongezeka kutoka safari
202,319 mwaka 2012/2013 hadi kufikia 220,528 mwezi Aprili, 2014. Hili ni
ongezeko la asilimia 9. Kuongezeka kwa safari za ndege kwa kiasi kikubwa
kulichangiwa na mashirika kama Fast Jet na Tropical Air kuanza safari katika
Kiwanja cha ndege cha Songwe na viwanja vya ndege vya Kigoma na Tabora
kufunguliwa baada ya ukarabati.
55.
Mheshimiwa
Spika, katika
hotuba ya mwaka 2013/2014, niliahidi kuboresha mikataba ya usafiri wa anga
(Bilateral Air Services Agreements - BASA) kati ya Tanzania na nchi mbalimbali
na kuanzisha mikataba mipya ili kukidhi mahitaji ya soko na kurahisisha usafiri
katika sekta hii muhimu. Hadi Aprili, 2014, Tanzania ilikuwa imeingia
makubaliano ya BASA na nchi 52 ikilinganishwa na nchi 48 zilizokuwa zimesaini
mkataba huo Aprili, 2013. Kati ya mikataba hiyo, mikataba 21 ndiyo ambayo
kampuni au mashirika yake ya ndege yanatoa huduma kati ya Tanzania na nchi
husika. Aidha, hadi Aprili, 2014,
mashirika ya ndege ya ndani na nje yanayotoa huduma nchini kwa utaratibu wa
BASA yalifikia 25 ambapo safari za ndege kati ya nchi hizo na Tanzania zilikuwa
175. Katika mwaka 2014/2015, Tanzania inatarajia kuingia mikataba mipya ya
usafiri wa anga au kupitia upya mikataba iliyopo na nchi za Australia, Italia,
Sudan ya Kusini na Mauritius.
56.
Mheshimiwa
Spika,
pamoja na majukumu ya kudhibiti na kusimamia shughuli na taratibu za usafiri wa
anga nchini, Mamlaka ya Usafiri wa Anga pia hutoa huduma za uongozaji wa ndege
katika anga lote la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kutokana na mwingiliano wa
majukumu ya kudhibiti na kutoa huduma, katika mwaka 2014/2015, Wizara
itaangalia uwezekano wa kutenganisha majukumu ya udhibiti na utoaji huduma ya
uongozaji wa ndege ili majukumu haya mawili yasikae chini ya Mamlaka moja. Aidha,
ili kuimarisha usalama wa usafiri wa anga, Wizara imetenga shilingi bilioni
11.14 kwa ajili ya kununua rada mbili (2) za kuongozea ndege za kiraia.
4.2 Huduma za Viwanja vya Ndege
57.
Mheshimiwa
Spika,
ujenzi wa jengo la tatu la abiria (Terminal III) katika Kiwanja cha Ndege cha
Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA) umeanza rasmi Januari, 2014 baada ya
kukamilika kwa kazi ya kufanya usanifu wa kina. Aidha, tarehe 24 Aprili, 2014
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Jakaya M. Kikwete
aliweka jiwe la msingi kuashiria kuanza kwa awamu ya kwanza ya ujenzi wa jengo
la tatu la abiria. Mradi huu ambao ni mkubwa katika historia ya usafiri wa anga
nchini unatekelezwa kwa awamu mbili. Awamu ya kwanza itahusu ujenzi wa jengo
lenye uwezo wa kuhudumia abiria milioni 3.5 kwa mwaka kwa gharama ya shilingi
bilioni 293. Awamu hii inatarajiwa kukamilika Oktoba, 2015. Ujenzi wa awamu ya
pili utaongeza uwezo wa jengo hadi kuhudumia abiria milioni 6 kwa mwaka na
hivyo JNIA kuwa na uwezo wa kuhudumia abiria milioni 7.2 kwa mwaka. Mradi huu
utakuwa na maegesho ya ndege za aina zote ikiwemo ndege kubwa kuliko zote aina
ya Airbus 380.
58.
Mheshimiwa
Spika,
kuhusu Kiwanja cha ndege cha Songwe, katika mwaka 2013/2014 Wizara kupitia
Mamlaka ya Viwanja vya Ndege imempata mkandarasi wa kutoa huduma za mafuta na
sasa anaendelea na maandalizi ya kuanza kutoa huduma hiyo. Aidha, kazi za
ujenzi wa maegesho ya ndege na jengo la abiria zinaendelea na zitakamalika
Desemba, 2014.
59.
Mheshimiwa
Spika,
awamu ya kwanza ya uboreshaji na upanuzi wa viwanja vya ndege vya Kigoma na
Tabora iliyowekewa jiwe la msingi na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Mheshimiwa Dkt. Jakaya M. Kikwete ilikamilika Juni, 2013. Zabuni kwa ajili ya kuwapata
makandarasi na wahandisi washauri kwa ajili ya utekelezaji wa awamu ya pili ya
ukarabati wa viwanja hivi chini ya ufadhili wa Benki ya Dunia zilifunguliwa
Mei, 2014. Kazi za awamu ya pili zitahusisha ujenzi wa jengo la abiria, maegesho
ya magari, barabara za kuingia viwanjani na upanuzi wa maegesho ya ndege.
Kukamilika kwa awamu ya pili kutawezesha viwanja hivyo kuwa vya kisasa na
kutumika kwa saa 24.
60.
Mheshimiwa
Spika,
mwaka 2013/2014 niliahidi kukamilisha ukarabati wa kiwanja cha ndege cha Mafia
kwa kiwango cha lami. Napenda kutoa taarifa kuwa ukarabati wa kiwanja hiki
uliogharamiwa kwa pamoja kati ya Serikali ya Tanzania na Serikali ya Marekani
kupitia Shirika la Changamoto za Milenia (MCAT) ulikamilika na kufunguliwa
rasmi na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Jakaya M.
Kikwete Oktoba, 2013. Aidha, katika mwaka 2014/2015, Serikali imetenga Shilingi
bilioni 1.05 kwa
ajili ya kuanza ujenzi wa jengo jipya la abiria, maegesho ya magari, ukarabati
wa barabara ya kuingia na kutoka kiwanjani pamoja na kituo cha umeme.
61.
Mheshimiwa
Spika,
mwaka 2013/2014 Bunge lako Tukufu liliidhinisha fedha kwa ajili ya kukamilisha
ukarabati wa Kiwanja cha ndege cha Bukoba. Napenda kutoa taarifa kuwa kazi za
ukarabati na upanuzi wa kiwanja hiki kwa kiwango cha lami zinaendelea na
zinatarajiwa kukamilika Septemba, 2014. Aidha, tarehe 24 Julai, 2013, Rais wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete aliweka
jiwe la msingi kuashiria kuanza kwa ujenzi wa kiwanja hiki. Kazi zilizokamilika
ni pamoja na ujenzi wa barabara ya kuruka na kutua ndege, barabara za viungio
na maegesho ya ndege kwa kiwango cha lami.
62.
Mheshimiwa
Spika,
katika Hotuba ya mwaka 2013/2014 niliahidi kufanya upembuzi yakinifu na usanifu
wa kina kwa viwanja kumi na moja (11) vya Iringa, Kilwa Masoko, Lake Manyara,
Moshi, Musoma, Lindi, Njombe, Songea, Singida, Bariadi (Mkoani Simiyu) na
Tanga. Napenda kutoa taarifa kuwa, tayari Mhandisi Mshauri ameanza kazi hiyo
Aprili, 2014 na inatarajiwa kukamilika Februari, 2015.
63.
Mheshimiwa
Spika,
katika mwaka 2013/2014, Bunge lako Tukufu liliidhinisha fedha kwa ajili ya
kuboresha kiwanja cha ndege cha Mwanza; kukarabati viwanja vya ndege vya
Shinyanga na Sumbawanga pamoja na upanuzi wa kiwanja cha ndege cha Mtwara.
Napenda kutoa taarifa kuwa:
i.
Kazi
zinazoendelea katika kiwanja cha ndege cha Mwanza ni pamoja na kuchimba eneo la
kurefusha barabara ya kuruka na kutua ndege, ujenzi wa nguzo za jengo la mizigo na jengo la kuongozea ndege, na
ujenzi wa kalavati la kutolea maji ya mvua kutoka upande mmoja wa barabara ya
kutua na kuruka ndege kwenda upande mwingine;
ii.
Zabuni
za kuwapata makandarasi wa kazi za ukarabati na upanuzi wa viwanja vya ndege
vya Shinyanga na Sumbawanga zinatarajiwa kutangazwa Juni, 2014. Aidha, taratibu
za kumpata mhandisi mshauri kwa ajili ya kufanya usanifu wa majengo ya abiria
katika viwanja hivyo zinaendelea; na
iii.
Kazi
ya kufanya upembuzi yakinifu wa ujenzi wa kiwanja cha ndege cha Mtwara
unaendelea na unatarajiwa kukamilika Julai, 2014. Aidha, kazi ya ukarabati wa
muda katika barabara ya kuruka na kutua ndege ili kuwezesha kiwanja kitumike
katika msimu mzima wa mwaka ilikamilika Novemba, 2013.
64.
Mheshimiwa
Spika,
Wizara imeendelea kuhakikisha kuwa kiwanja cha Ndege cha Arusha kinakuwa na
uwezo wa kuhudumia ndege za kubeba hadi abiria 70 ili kiendelee kuchangia
katika uboreshaji na ukuaji wa sekta ya utalii nchini. Katika mkakati wa
kukifanya kiwanja cha ndege cha Arusha kuwa katika viwango vya kimataifa, Machi
2014, Mamlaka ilifungua zabuni ya kumpata Mhandisi Mshauri wa kufanya marejeo
ya usanifu wa miundombinu ya kiwanja pamoja na kuandaa makabrasha ya zabuni kwa
ajili ya kumpata Mkandarasi. Aidha, zabuni kwa ajili ya kumpata Mkandarasi wa
kazi ya kurefusha barabara ya kuruka na kutua ndege kwa urefu wa mita 200
itatangazwa Juni, 2014.
65.
Mheshimiwa
Spika,
Serikali imeendelea kuimarisha na kuboresha ulinzi na usalama katika viwanja
vya ndege nchini hasa baada ya kushamiri kwa matukio ya usafirishaji wa madawa
ya kulevya kupitia viwanja vyetu vya ndege. Ili kufanikisha azma hiyo, katika
mwaka 2013/2014, Serikali kupitia Mamlaka ya Viwanja vya Ndege ilipata msaada
wa vifaa vya kisasa vya utambuzi wa milipuko (Explosive Trace Detectors) kutoka
Serikali ya Uingereza na Mamlaka imenunua mashine za kisasa za ukaguzi wa
mizigo zenye uwezo wa kutambua madawa ya kulevya (Rapscan X-ray machines 600
series). Vifaa hivyo vilisimikwa katika kiwanja cha ndege cha Kimataifa cha
Julius Nyerere. Serikali inaendelea na taratibu za kufunga vifaa kama hivyo
katika viwanja vya ndege vya Kilimanjaro, Mwanza, Songwe na Arusha.
66.
Mheshimiwa Spika, kuhusu Kiwanja cha
ndege cha Kimataifa cha Kilimanjaro Serikali za Tanzania na Uholanzi
zilitiliana saini ya msaada wa Shilingi bilioni 34.5 (sawa na Euro milioni 15)
kwa ajili ya ukarabati wa Kiwanja hiki. Kazi zitakazotekelezwa ni pamoja na
ukarabati na upanuzi wa maegesho ya ndege, njia za viungio, jengo la abiria,
njia ya kuruka na kutua ndege na ujenzi wa mfumo mpya wa maji taka. Aidha,
Serikali inaendelea kutafuta fedha kiasi cha Shilingi bilioni 47.15 (sawa na
Euro milioni 20.5) kwa ajili ya kuendelea na awamu ya pili ya ukarabati wa KIA.
Mradi huu utakapokamilika utaongeza uwezo wa KIA kuhudumia ndege nyingi, kwa
ufanisi mkubwa na usalama zaidi.
67.
Mheshimiwa
Spika,
katika mwaka 2014/2015, Mamlaka ya Viwanja vya Ndege imepanga kutekeleza kazi
zifuatazo:
i.
Kuendelea
na ujenzi wa jengo jipya la abiria (Terminal III) pamoja na miundombinu yake
katika kiwanja cha JNIA. Shilingi
bilioni 44 zimetengwa kwa ajili ya kuendelea na ujenzi;
ii.
Kukamilisha ujenzi wa maegesho ya ndege na jengo
kubwa la abiria, kuendelea na ujenzi wa uzio wa usalama na kusimika taa na
mifumo ya kuongozea ndege katika
kiwanja cha Ndege cha Songwe
(Mbeya) ambapo Shilingi bilioni 9.05 zimetengwa;
iii.
Kuendelea
na ukarabati wa kiwanja cha ndege cha Mwanza. Serikali imetenga shilingi
bilioni 12.05 kwa ajili ya kazi hiyo;
iv.
Kukamilisha
ukarabati wa Kiwanja cha ndege cha Bukoba na kulipa fidia kwa wakazi waliobaki.
Shilingi bilioni 3.33 zimetengwa;
v.
Kuendelea
na ukarabati na upanuzi wa Kiwanja
cha ndege cha Kigoma katika kiwango cha lami ambapo Serikali imetenga shilingi
bilioni 4.05 ili kukamilisha kazi hii;
vi.
Kuendelea
na ukarabati na upanuzi wa Kiwanja
cha ndege cha Tabora ambapo Shilingi bilioni 12.87 zimetengwa kwa kazi hii;
vii.
Kuanza
ukarabati na upanuzi wa kiwanja cha ndege cha Shinyanga kwa kiwango cha lami
ambapo Shilingi bilioni 12.07 zimetengwa;
viii.
Kuanza
ukarabati na upanuzi wa kiwanja cha ndege cha Sumbawanga kwa kiwango cha lami
ambapo Shilingi bilioni 11.75 zimetengwa;
ix.
Kufanya
kazi ya usanifu wa kina wa ujenzi wa Kiwanja kipya cha Ndege cha Msalato katika
kiwango cha lami ambapo Serikali imetenga shilingi bilioni 1.1 kwa ajili ya
kazi hiyo.
x.
Kufanya
matengenezo ya kiwanja cha ndege cha Mtwara. Katika mwaka 2014/2015, Serikali
imetenga Shilingi bilioni 2.1 kwa ajili ya kufanya ukarabati wa barabara ya
kuruka na kutua ndege;
xi.
Kuendelea na taratibu za maandalizi ya ulipaji fidia,
upimaji na upatikanaji wa hati miliki ya ardhi kwa maeneo ya viwanja vipya vya
ndege vya Bagamoyo (Pwani), Isaka (Shinyanga), Kisumba (Rukwa), Msalato
(Dodoma), Ngungungu (Manyara), Omukajunguti (Kagera), Bariadi (Simiyu) na
Nyansurura (Mara);
xii.
Kukamilisha
ufungaji wa majenereta mapya, kuweka madaraja mapya ya kupandia na kushuka
abiria (aerobridges) katika kiwanja cha ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere;
na
xiii.
Kuboresha
mitambo na mifumo ya kufuatilia mienendo ya shughuli za usalama na uendeshaji
wa kiwanja (CCTV) katika kiwanja cha ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere,
Mwanza na Arusha.
xiv.
4.3 Huduma za Usafiri wa Ndege
68.
Mheshimiwa
Spika,
Serikali imeendelea kusaidia Kampuni ya Ndege Tanzania (ATCL) ili iweze
kuboresha huduma zake na kujiendesha kibiashara. ATCL imeendelea kutoa huduma
ya kusafirisha abiria katika viwanja vya ndege vya Dar es Salaam, Mtwara, Tabora,
Kigoma na Hahaya-Comoro kwa kutumia ndege yake aina ya Dash 8 Q300. Aidha,
kuwasili kwa ndege ya kukodi aina ya CRJ-200 yenye uwezo wa kubeba abiria 50
mwezi Machi, 2014 kumeimarisha na kuboresha huduma za ATCL na hivyo kuanzisha safari za ndege
kwenda Bujumbura, Mwanza, Arusha, Songwe na Zanzibar. ATCL inatarajia kununua
ndege nyingine mbili zenye uwezo wa kubeba abiria zaidi ya 50 kila moja kwa
ajili ya kuboresha huduma za usafiri wa anga ndani ya nchi. Ujio wa ndege hizi
utaimarisha utendaji na kuongeza mapato ya ATCL. Katika mwaka 2014/2015,
Serikali imetenga Shilingi bilioni 2 ili kuboresha utendaji wa ATCL.
5.0 HUDUMA ZA HALI YA HEWA
69.
Mheshimiwa
Spika,
Mamlaka
ya Hali ya Hewa imeendelea kutekeleza majukumu yake ya kuhakiki na kuratibu
utoaji wa huduma za hali ya hewa pamoja na kutoa tahadhari dhidi ya matukio ya
hali mbaya ya hewa ili kuongeza mchango wa sekta hii katika kuendeleza sekta
nyingine za kiuchumi na kijamii na kupunguza athari zitokanazo na mabadiliko ya
hali ya hewa na tabianchi.
70.
Mheshimiwa
Spika,
katika mwaka 2013/2014, Wizara ilipanga kukamilisha malipo ya kuunda na kufunga
Rada ya hali ya hewa mkoani Mwanza. Napenda kutoa taarifa kuwa kazi ya ufungaji
wa Rada hii imeanza na inatarajiwa kukamilika Juni, 2014. Rada hii ni muhimu
kwani itasaidia katika shughuli za kiuchumi zinazofanyika katika Ziwa Victoria
na kutoa tahadhari juu ya matukio ya hali mbaya ya hewa.
71.
Mheshimiwa
Spika,
Wizara kupitia Mamlaka ya Hali ya Hewa ilifunga mitambo 11 ya kupima hali ya
hewa inayojiendesha yenyewe katika sehemu mbalimbali nchini. Aidha, ofisi ya
utoaji wa huduma za hali ya hewa kwa watumiaji wa Bahari ya Hindi katika
Bandari ya Zanzibar ilianzishwa na maandalizi ya kuanzisha ofisi za kutoa
huduma za hali ya hewa katika Bandari za Mwanza, Kigoma na Itungi yanatarajiwa
kukamilika Julai, 2014. Mamlaka pia iliboresha studio ya kuandaa taarifa za
hali ya hewa iliyoko Dar es Salaam kwa kufunga vifaa vya kisasa.
72.
Mheshimiwa
Spika,
baadhi ya kazi zilizotekelezwa na Mamlaka ya Hali ya Hewa katika mwaka
2013/2014 ni kama ifuatavyo:
i.
Kukamilisha
ukarabati wa vituo vya hali ya hewa vya Dodoma, Tabora, Mlingano pamoja na
ofisi ya Hali ya Hewa iliyoko Kiwanja cha JNIA;
ii.
Kufanya
upembuzi yakinifu wa ujenzi wa Kituo Kikuu cha Utabiri wa Hali ya Hewa (central
forecasting office) ilikamilika Machi, 2014. Aidha, kazi ya kufanya usanifu wa
Michoro ya jengo hilo kwa ajili ya kuanza ujenzi inatarajiwa kukamilika Juni,
2014; na
iii.
Kushirikiana
na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam katika kutoa mafunzo ya Shahada ya Hali ya Hewa
(BSc. Met). Mwezi Oktoba 2013, jumla ya wanafunzi 15 walichaguliwa kujiunga na
kozi hiyo. Kuanzishwa kwa kozi hii kutaboresha utoaji wa huduma za hali ya hewa
na kulipunguzia Taifa gharama za kusomesha wanafunzi nje ya nchi.
73.
Mheshimiwa
Spika,
katika mwaka 2014/2015, Mamlaka imetengewa jumla ya Shilingi bilioni 5.6 kwa
ajili ya utekelezaji wa mipango mbalimbali ikiwa ni pamoja na kuongeza vifaa
vya hali ya hewa, kujenga na kukarabati vituo vya hali ya hewa, kujenga uwezo
wa watumishi, kuanza ujenzi wa Jengo la Utabiri wa Hali ya Hewa na kutekeleza
programu ya Taifa ya kukabiliana na mabadiliko ya hali ya hewa na tabianchi. Mikakati mingine ni kuanza kutumia rada ya pili ya hali ya hewa iliyoko
Mwanza na mifumo ya kisasa ya utoaji wa utabiri.
74.
Mheshimiwa
Spika,
kuhusu ushikiri wa kikanda, Wizara imeendelea kushiriki katika mikutano na
shughuli mbalimbali za Jumuiya za Kikanda kama za Africa Mashariki (EAC) na
Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Africa (SADC), kwa lengo la kujenga
uhusiano bora katika kuendeleza Sekta za Uchukuzi na Hali ya Hewa.
8.0 TAASISI ZA MAFUNZO
75.
Mheshimiwa
Spika,
Wizara
imeendelea kuvihudumia vyuo vyetu vya mafunzo kwa lengo la kuviwezesha kutoa
taaluma na wanataaluma wa kada mbalimbali katika sekta za uchukuzi na hali ya
hewa. Vyuo vilivyo chini ya Wizara ya Uchukuzi ni Chuo cha Taifa cha
Usafirishaji (NIT), Chuo cha Bahari Dar es Salaam (DMI), Chuo cha Hali ya Hewa
- Kigoma, Chuo cha Usafiri wa Anga Dar es Salaam, Chuo cha Bandari Dar es
Salaam na Chuo cha Reli Tabora. Katika mwaka 2014/2015 Wizara itaendelea kutoa
kipaumbele katika kuhudumia vyuo hivyo ili viendelee kutoa wataalam wa Sekta ya
Uchukuzi na Hali ya Hewa na kuboresha utendaji wa Sekta hiyo.
9.0 MASUALA MTAMBUKA
9.1 Kuzingatia masuala ya Jinsia
76.
Mheshimiwa
Spika, Wizara
yangu imeendelea kulipa kipaumbele suala la ushirikishwaji wa wanawake katika
sekta ya uchukuzi kwa kuzingatia Itifaki na Mikataba ya Kimataifa ambayo
Tanzania imeridhia. Katika kuhakikisha ushirikishwaji wa wanawake katika
utekelezaji wa majukumu ya Sekta ya Uchukuzi, hivi sasa tuna wanawake madereva
wa treni wanane. Kati ya hao, wawili wameajiriwa TRL na sita wameajiriwa na
TAZARA; Marubani wanawake saba; kati ya hao, mmoja yuko ATCL, wanne wako
Precision Air, mmoja yuko TCAA na mmoja yuko TGFA. Pia tuna waongoza ndege
wanawake 16 ambao wako TCAA. Aidha, tuna wahandisi wanawake 39 wanaotumikia Taifa
katika Taasisi mbalimbali za Wizara ya Uchukuzi. Kati ya hao wawili wanafanya
kazi TRL, mmoja yuko ATCL, mmoja TGFA, watatu NIT, wawili TPA na mwingine yuko
TMA. Wahandisi mitambo ya kuongozea ndege wanawake 15 wako TCAA na Wahandisi 14
wa fani umeme, mitambo, ujenzi na mawasiliano ambao wako TAA. Waendesha boti za
kusukuma meli (tug) ni mmoja ambaye yupo TPA. Pamoja na ugumu wa kazi ya udereva
wa magari ya masafa marefu, nafurahi kuwaarifu kuwa tuna madereva wanawake
watatu wa mabasi na wawili wa malori.
9.2 Utunzaji wa Mazingira
77.
Mheshimiwa
Spika,
uharibifu
wa mazingira umeendelea kuwa changamoto kubwa kwa Wizara yangu. Shughuli za
kijamii zinazofanyika katika milima karibu na njia ya reli sehemu za Kilosa
hadi Gulwe zimeendelea kuathiri huduma za uchukuzi wa Reli ya Kati kwa kiasi
kikubwa. Naomba Waheshimiwa Wabunge, Madiwani na Viongozi wa Serikali za Mitaa
waungane na Wizara katika kuelimisha Wananchi na kukemea vitendo vya kukata
miti ovyo, kulima bila kufuata ushauri wa Wataalam na kulima kwenye kingo za
mito na reli. Vitendo hivyo vinaharibu miundombinu hiyo hasa wakati wa mvua
hivyo kuigharimu Serikali fedha nyingi za kufanya matengenezo.
10.0 SHUKRANI
78.
Mheshimiwa
Spika,
ningependa
sasa kutoa shukrani zangu za dhati kwa wale wote waliotoa ushirikiano katika
kufanikisha malengo ya sekta. Hawa ni pamoja na Washirika wa Maendeleo ambao
tunasaidiana nao katika kufanikisha utekelezaji wa program na mipango
mbalimbali ya maendeleo ya sekta za uchukuzi na hali ya hewa. Shukrani za dhati
ziende kwa nchi na mashirika ya kimataifa yaliyochangia katika maendeleo ya
sekta yetu. Nchi na mashirika hayo ni pamoja na Shirika la Bahari Duniani (IMO),
Shirika la Kimataifa la Usafiri wa Anga (ICAO), Shirika la Hali ya Hewa Duniani
(WMO), UNESCO, Benki ya Dunia (WB), Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB), Benki
ya Kiarabu ya Maendeleo ya Uchumi kwa Afrika (BADEA), Shirika la Maendeleo la
Ushirikiano wa Kimataifa la Japan (JICA) Kuwait Fund, Malaysia, Jamhuri ya
Korea, OPEC Fund, Umoja wa Nchi za Ulaya, Afrika Kusini, Uingereza, Marekani,
Uholanzi, Japan, Benki ya Uwekezaji ya Ulaya (EIB), TMEA, DFID, India, China,
Denmark, Norway, Ubelgiji, Ujerumani, Urusi, Sweden, Ufaransa, Finland,
Singapore na wengine wengi. Napenda kuwaomba waendelee kushirikiana nasi katika
kuimarisha sekta za uchukuzi na hali ya hewa.
79.
Mheshimiwa
Spika,
kwa namna ya pekee naomba kuwashukuru viongozi wenzangu wa Wizara ya Uchukuzi,
nikianza na Naibu Waziri, Mheshimiwa Dkt. Charles John Tizeba (Mb.), Katibu
Mkuu Dkt. Shaaban Ramadhan Mwinjaka, Naibu Katibu Mkuu, Bi. Monica Lyanda
Mwamunyange, Wakuu wa Idara na Vitengo, Watendaji Wakuu na Wenyeviti wa Bodi za
SUMATRA, TCAA, TGFA, KADCO, TAA, TPA, TRL, RAHCO, MSCL, TMA, SINOTASHIP, ATCL,
DMI, NIT, TAZARA na TTFA, pamoja na watumishi wote wa Wizara na Taasisi.
Ninafarijika kwa ushirikiano wanaonipa katika jitihada za kuendeleza sekta za
uchukuzi na hali ya hewa. Nikiri kuwa bila mchango wao mkubwa, kazi yangu ya
kuongoza sekta hii, ingekuwa ngumu.
11.0 MAOMBI YA FEDHA
80.
Mheshimiwa
Spika,
ili Wizara yangu iweze kutekeleza majukumu na malengo yake kwa mwaka 2014/2015,
Ninaomba Bunge lako Tukufu liidhinishe jumla ya Shilingi 527,933,790,000. Kati ya fedha hizo,
Shilingi 93,306,391,000 zimetegwa kwa ajili ya Matumizi ya Kawaida na
Shilingi 434,627,399,000 ni kwa ajili ya Miradi ya Maendeleo. Fedha za
Matumizi ya Kawaida zinajumuisha Shilingi 33,027,291,000 kwa ajili ya Mishahara ya Watumishi
na Shilingi 60,279,100,000 fedha za Matumizi Mengineyo (OC). Fedha za
Miradi ya Maendeleo zinajumuisha Shilingi 273,140,000,000 fedha za ndani na
Shilingi 161,487,399,000 fedha za nje.
81.
Mheshimiwa
Spika,
naomba nimalize hotuba yangu kwa kukushukuru wewe binafsi, pamoja na
Waheshimiwa Wabunge wote kwa kunisikiliza wakati nikiwasilisha hoja ya Wizara
yangu. Hotuba hii pia inapatikana katika tovuti ya Wizara kwa anuani ya: www.mot.go.tz.
82.
Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja.
No comments:
Post a Comment