HOTUBA
YA WAZIRI WA NISHATI NA MADINI MHE. PROF. SOSPETER MWIJARUBI MUHONGO (MB.),
AKIWASILISHA BUNGENI MAKADIRIO YA MAPATO NA MATUMIZI KWA
MWAKA 2014/15
A.
UTANGULIZI
1.
Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja kwamba, Bunge lako Tukufu sasa lipokee
na kujadili Taarifa ya Utekelezaji ya Mwaka 2013/14 na kupitisha Makadirio ya
Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati na Madini na Taasisi zilizo chini yake
kwa Mwaka 2014/15.
2.
Mheshimiwa Spika, awali ya yote namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia
afya njema na kuniwezesha kutekeleza
majukumu yangu kwa ajili ya maendeleo ya Taifa letu.
3.
Mheshimiwa Spika, kipekee nawashukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania, Mhe. Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, Makamu wa Rais, Mhe. Dkt. Mohamed Gharib Bilal na Waziri Mkuu,
Mhe. Mizengo Kayanza Peter Pinda (Mb.) kwa uongozi na juhudi zao katika kuleta
maendeleo ya Taifa letu na kwa ushirikiano wanaonipa katika kusimamia na
kutekeleza majukumu ya Wizara ya Nishati na Madini.
4.
Mheshimiwa Spika, naomba kumpongeza kwa dhati Rais wetu Mhe. Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete kwa
kupewa Tuzo ya Utumishi Bora kwa kuwa Kiongozi mwenye mchango mkubwa zaidi
katika maendeleo ya Bara la Afrika kwa Mwaka 2013. Hii ni heshima kubwa na Tunu
kwa Watanzania wote kwa ujumla kwa kuthaminiwa na kutambuliwa kwa kiongozi wetu
katika medani za kimataifa. Tunamwombea kwa
Mwenyezi Mungu ili azidi kumpa nguvu na hekima zaidi ya kutekeleza majukumu
yake.
5.
Mheshimiwa Spika, napenda pia kukupongeza wewe binafsi, Naibu Spika,
Wenyeviti wa Bunge na Wenyeviti wote wa Kamati za Kudumu za Bunge kwa
kuliongoza Bunge hili Tukufu kwa hekima, busara, umahiri na bila kuyumba katika kusimamia Kanuni tulizojiwekea
sisi wenyewe. Vilevile, namshukuru sana Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge
ya Nishati na Madini, Mhe. Victor Kilasile Mwambalaswa (Mb.), Makamu Mwenyekiti
Mhe. Jerome Dismas Bwanausi (Mb.), na wajumbe wote wa Kamati hiyo kwa kazi
kubwa wanayoifanya ya kuishauri na kuisimamia Wizara katika utekelezaji wa
majukumu yake, pamoja na kuchambua na kupokea Taarifa ya Utekelezaji wa
Majukumu ya Wizara kwa Mwaka 2013/14 na Makadirio ya Mpango na Bajeti kwa Mwaka
2014/15. Napenda kulihakikishia Bunge lako Tukufu kuwa Wizara ya Nishati na
Madini imezingatia ushauri na mapendekezo ya Kamati ya Bunge ya Kudumu ya
Nishati na Madini katika kuandaa Bajeti inayowasilishwa kwenu.
6.
Mheshimiwa Spika, naomba
vilevile kuungana na Waheshimiwa Wabunge wenzangu kuwapongeza Mhe.
Godfrey William Mgimwa, Mbunge wa Jimbo la Kalenga na Mhe. Ridhiwan Jakaya Kikwete, Mbunge wa Jimbo la
Chalinze kwa kuchaguliwa kwa kishindo kuwa wawakilishi wa wananchi katika
Majimbo hayo. Aidha, napenda kuwapa pole familia, ndugu, jamaa na wananchi kwa
kuondokewa na wapendwa wetu, Mhe. Dkt.William Augustao Mgimwa, aliyekuwa Mbunge
wa Jimbo la Kalenga na Waziri wa Fedha; Mhe. Said Ramadhani Bwanamdogo,
aliyekuwa Mbunge wa Chalinze; na Mhe. John Gabriel Tupa, aliyekuwa Mkuu wa Mkoa
wa Mara. Tunaomba Mwenyezi Mungu awarehemu na awapumzishe kwa amani.
7.
Mheshimiwa Spika, baada ya utangulizi huo, naomba sasa kuwasilisha Taarifa
ya Utekelezaji wa Shughuli za Wizara ya Nishati na Madini kwa Mwaka 2013/14; na
Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka 2014/15.
B. TAARIFA YA
UTEKELEZAJI KWA MWAKA 2013/14 PAMOJA NA MAKADIRIO
YA MAPATO NA MATUMIZI KWA MWAKA 2014/15
8. Mheshimiwa Spika, utekelezaji wa Mpango na
Bajeti kwa Mwaka 2013/14 katika Sekta za Nishati na Madini ulilenga kufanya yafuatayo: kuimarisha
upatikanaji wa umeme wa uhakika; kuongeza wateja wanaotumia umeme hususan
vijijini; ujenzi wa miundombinu ya gesi asilia; kuongeza kasi ya upelekaji
umeme katika Makao Makuu ya Wilaya ambazo hazijapatiwa umeme; kusimamia na
kudhibiti biashara ya mafuta; kuvutia uwekezaji
katika Sekta za Nishati na Madini; kuimarisha ukusanyaji wa maduhuli ya
Serikali; na kujenga uwezo wa usimamizi na ufuatiliaji katika Sekta za Nishati
na Madini ili kukuza uchumi na kuharakisha maendeleo ya Taifa letu.
9.
Mheshimiwa Spika, kazi nyingine zilizotekelezwa ni pamoja na: kuboresha
utoaji na usimamizi wa leseni za madini; kuendeleza uchimbaji mdogo wa madini;
kuimarisha usimamizi wa afya, usalama na utunzaji wa mazingira migodini;
kuhamasisha shughuli za uongezaji thamani madini; na kuziwezesha Taasisi na
Mashirika yaliyo chini ya Wizara ya Nishati na Madini kutekeleza majukumu yake
ipasavyo na kwa manufaa ya Watanzania wote.
10. Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2014/15, pamoja na
masuala mengine, Wizara imelenga kukamilisha ujenzi wa miundombinu ya gesi
asilia inayojumuisha ujenzi wa Bomba la Gesi kutoka Mtwara na Lindi hadi Dar es
Salaam na mitambo ya kusafisha gesi asilia; kuendelea na utekelezaji wa miradi
ya kipaumbele chini ya mfumo wa Matokeo Makubwa Sasa (Big Results Now -
BRN);
kuendelea na utekelezaji wa miradi ya kupeleka umeme vijijini na Makao Makuu ya
Wilaya; kuimarisha ukusanyaji wa maduhuli katika Sekta za Nishati na
Madini; kuendeleza uchimbaji mdogo
na wa kati wa madini; kuimarisha usimamizi wa biashara ya madini; na kuvutia
uwekezaji katika Sekta za Nishati na Madini, hususan nishati jadidifu (renewable
energies) na makaa ya mawe.
Taarifa ya
Ukusanyaji wa Mapato kwa Mwaka 2013/14
11. Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha Mwaka
2013/14, Wizara ya Nishati na Madini ilipangiwa kukusanya jumla ya Shilingi
bilioni 220. Hadi kufikia tarehe 23 Mei, 2014 jumla ya Shilingi bilioni 147.14 zilikusanywa, sawa na asilimia
67 ya
lengo. Juhudi zinaendelea ili kuhakikisha kuwa lengo la ukusanyaji linafikiwa
kama ilivyopangwa na hivyo kuongeza mapato ya Serikali.
Matumizi ya
Wizara kwa Mwaka 2013/14
12. Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2013/14, Wizara iliidhinishiwa jumla ya Shilingi
1,289,329,129,000. Kati ya fedha hizo, Shilingi 110,216,384,000 zilikuwa ni Matumizi ya Kawaida
na Shilingi 1,179,112,745,000 zilikuwa ni fedha za maendeleo.
13. Mheshimiwa Spika, hadi kufikia tarehe 23 Mei, 2014
jumla ya Shilingi 83,202,288,459 sawa na asilimia 75 ya fedha za Matumizi ya Kawaida zilipokelewa. Aidha, jumla ya Shilingi 577,526,232,810 sawa na asilimia 49 ya Bajeti yote ya Maendeleo zilipokelewa.
Kati ya fedha hizo, Shilingi 431,010,106,443 ni fedha za ndani, sawa na asilimia
58 ya
fedha za ndani zilizotengwa na Shilingi 146,516,126,367 ni fedha za nje, sawa na
asilimia 34 ya fedha za nje zilizotengwa. Hivyo, Wizara imepokea jumla ya Shilingi
660,728,521,269 sawa na asilimia 51 ya Bajeti yote iliyoidhinishwa kwa Wizara ya Nishati na
Madini kwa Mwaka 2013/14.
14.
Mheshimiwa
Spika, kutokana na
usimamizi mzuri wa matumizi ya fedha za Serikali, naomba kulitaarifu Bunge
lako Tukufu kuwa Wizara ya Nishati na Madini ni miongoni mwa Wizara zilizopata
Hati Safi ya Hesabu za Mwaka 2012/13 isiyokuwa na swali lolote. Wizara itaendelea kusimamia ipasavyo Sheria
mbalimbali ili kuhakikisha fedha za walipa kodi zinatumika kwa manufaa ya Taifa
letu na kwa Watanzania wote bila upendeleo wa aina yoyote.
Malengo ya
Ukusanyaji wa Mapato ya Serikali kwa Mwaka 2014/15
15. Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2014/15 Wizara ya
Nishati na Madini inatarajia kukusanya jumla ya Shilingi bilioni 240.59. Kiasi hiki ni sawa na
ongezeko la asilimia 9.36 ya lengo la Mwaka 2013/14 la Shilingi bilioni 220. Mipango na mbinu
zitakazotumika katika ukusanyaji wa mapato ni pamoja na: kuboresha Mfumo wa
Utoaji na Usimamizi wa Leseni za Madini; kuhakikisha kuwa wamiliki wote wa
leseni za madini nchini wanatimiza masharti ya leseni zao; na kuimarisha
ushirikiano na taasisi nyingine za Serikali katika kuzuia utoroshaji wa madini.
16. Mheshimiwa Spika, mipango mingine ni kuongeza udhibiti katika
kukusanya mapato yatokanayo na madini ya ujenzi na viwandani; kuimarisha
usimamizi wa wachimbaji wadogo kwa kuwatambua na kutoa huduma za ugani ili
kuongeza tija katika uzalishaji madini; na kuwahamasisha Wananchi kuzingatia
Sheria, Kanuni na Taratibu za Sekta za Nishati na Madini kuhusu umuhimu wa
kulipa kodi na ada mbalimbali.
SEKTA YA
NISHATI
UKUAJI WA
SEKTA YA NISHATI
17. Mheshimiwa Spika, Dira ya Maendeleo ya
Taifa (Tanzania Development Vision, 2025) ilianza kutekelezwa Mwaka 2000.
Kupitia Dira hiyo, Serikali ya Chama cha Mapinduzi (CCM) imedhamiria kujenga
uchumi wa kisasa utakaoiwezesha Tanzania kuongeza kipato cha mtu mmoja mmoja (GDP
per capita) kutoka wastani wa Dola za
Marekani 640 hadi 3,000 ifikapo Mwaka 2025. Ili kufikia lengo hilo, nchi inahitaji kuwa na nishati
ya kutosha, yenye uhakika na ya gharama nafuu. Kwa kutambua hilo, Serikali
imeendeleza jitihada za kuboresha upatikanaji wa nishati bora vijijini na
mijini kwa kuongeza uwekezaji katika miundombinu ya nishati ikiwemo ya umeme,
gesi asilia na mafuta.
18. Mheshimiwa Spika, sambamba na azma hiyo,
Sekta ya Nishati imejumuishwa kwenye Mpango wa Matokeo Makubwa Sasa (BRN) ulioanzishwa na Serikali
Mwaka 2013/14. Katika Sekta hiyo, miradi 29 iliainishwa ambayo inahusisha
miradi 7 ya ufuaji, miradi 7 ya usafirishaji na miradi 14 ya usambazaji umeme
pamoja na mradi mmoja wa miundombinu ya gesi asilia. Utekelezaji wa miradi ya
BRN utachangia kufikiwa kwa malengo ya Dira ya Maendeleo ya Taifa ya Mwaka
2025.
19. Mheshimiwa Spika, Serikali pia imeendelea
kudurusu na kuandaa Sera na Sheria mbalimbali katika Sekta ya Nishati ikiwemo
Sera ya Taifa ya Nishati. Lengo ni kujenga mazingira yanayochochea uwekezaji
kwa kushirikisha Sekta Binafsi, na hivyo kuongeza ufanisi na ushindani wa
kibiashara katika Sekta ya Nishati.
Mafanikio
yaliyopatikana katika Sekta ya
Nishati
20.
Mheshimiwa Spika, mafanikio yaliyopatikana katika Sekta ya Nishati kwa
Mwaka 2013/14 ni pamoja na: kuongezeka kwa idadi ya Watanzania waliounganishiwa
umeme (connection level)
kutoka asilimia 21 Mwaka 2012/13 hadi
kufikia asilimia 24 Mwezi Machi, 2014.
Ikumbukwe kwamba kiwango cha uunganishwaji wa umeme kilikuwa asilimia 10 mwaka 2005 wakati Mhe. Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, Rais
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania alipoingia madarakani. Mafanikio mengine ni
pamoja na kuongezeka kwa idadi ya watu waliofikiwa na huduma ya umeme (access
level) kufikia asilimia 36 Mwezi Machi, 2014; kukamilika kwa ujenzi wa mtambo wa
kufua umeme MW 60 huko Nyakato, Mwanza; kufunga vipozea umeme (transformers) vyenye uwezo wa MVA 15 katika vituo vya Bahari Beach,
Gongolamboto, Kigamboni na Kunduchi; kufunga vipozea umeme viwili
vyenye uwezo wa MVA 90 kila kimoja katika vituo vya Kipawa na Ubungo; kusainiwa
kwa mikataba 35 ya utekelezaji wa Awamu ya Pili
ya Mradi Kabambe wa Kusambaza Umeme
Vijijini (Turnkey
Phase II); kuwasili
kwa mitambo miwili ya kufua umeme yenye uwezo wa MW 75,
kati ya mitambo minne ya mradi wa MW150 wa Kinyerezi – I; na kuboresha hali ya
upatikanaji wa
umeme nchini na hivyo kuchochea ukuaji wa shughuli za kiuchumi na kijamii.
21.
Mheshimiwa Spika, mafanikio mengine ni pamoja na: kupitishwa kwa Sera ya
Gesi Asilia Mwezi Oktoba, 2013; kukamilika kwa ujenzi wa Bomba la
kusafirishia gesi asilia kutoka Mtwara
na Lindi hadi Dar es Salaam kwa asilimia 77.8;
kukamilika kwa maandalizi ya kufunga mitambo ya kusafisha gesi asilia kwa asilimia
44.8; kugunduliwa kwa gesi asilia inayofikia futi
za ujazo trilioni 4.8 kwenye visima vilivyopo kina kirefu cha
Bahari na hivyo kufanya jumla ya kiasi cha gesi asilia kilichogundulika hapa
nchini hadi sasa kufikia futi za ujazo trilioni
46.5; kuzinduliwa kwa duru ya nne ya utafutaji
mafuta na gesi asilia katika kina kirefu baharini na Kaskazini mwa Ziwa
Tanganyika; na kuanzishwa kwa kitengo
maalumu (Ministerial Delivery Unit - MDU) cha kufuatilia utekelezaji wa
miradi ya BRN katika Sekta ya Nishati.
22. Mheshimiwa Spika, mafanikio yote hayo ni matokeo ya
utekelezaji thabiti wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya Mwaka 2010 - 2015 inayosisitiza upatikanaji wa nishati
ya uhakika kwa ajili ya kujenga uchumi wa kisasa na imara unaozingatia
maendeleo ya sayansi, teknolojia na ubunifu. Ukuaji wa uchumi imara ndio
utakaotoa ajira mpya na matumaini mapya kwa vijana na maskini katika nchi yetu.
SEKTA NDOGO
YA UMEME
Hali
ya Uzalishaji Umeme
23. Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2013/14, Serikali
iliendelea kuchukua hatua mbalimbali za kuboresha upatikanaji wa umeme nchini. Hadi mwishoni mwa
mwezi Aprili, 2014 uwezo wa mitambo yote ya kufua umeme (total installed capacity) ulifikia MW 1,583 (maji - asilimia 35, gesi asilia - asilimia
34 na
mafuta - asilimia 31). Uwezo huo wa mitambo yote ni sawa na ongezeko la asilimia
78
ikilinganishwa na MW 891 zilizokuwepo mwaka 2005 wakati Serikali ya Awamu ya Nne
inaingia madarakani. Hili ni jambo la
kujivunia kwa Serikali ya Chama cha Mapinduzi.
24. Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2013 kiasi cha umeme
kilichoingizwa kwenye Gridi ya Taifa kiliongezeka na kufikia GWh 5,997.41
ikilinganishwa na GWh 5,760 za
Mwaka 2012, sawa na ongezeko la asilimia 4. Aidha, mahitaji ya juu ya
matumizi ya umeme kwa Mwaka 2013/14 yalifikia wastani wa MW 898.72 ikilinganishwa na MW
851.35
kwa mwaka 2012/13, sawa na ongezeko la asilimia 6.
Miradi ya
Kufua Umeme
Mradi wa MW
60 Nyakato - Mwanza
25.
Mheshimiwa Spika, Serikali imekamilisha mradi wa ujenzi wa mitambo ya MW
60 inayotumia mafuta mazito katika eneo la Nyakato, Jijini Mwanza. Mradi huo
ulizinduliwa rasmi na Mhe.
Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, tarehe 8
Septemba, 2013. Kuzinduliwa kwa mradi huo kumeimarisha upatikanaji wa umeme
katika Kanda ya Ziwa Victoria.
Mradi wa Kinyerezi I
- MW 150
26. Mheshimiwa Spika, katika Mwaka
2013/14 utekelezaji wa mradi wa kufua umeme wa MW 150 kwa kutumia gesi asilia
katika eneo la Kinyerezi, Jijini Dar es Salaam unaendelea vizuri. Mradi huo utakapokamilika utapunguza
utegemezi wa mitambo ya kukodi inayotumia
mafuta kufua umeme ambayo ni ghali. Pia, mitambo miwili yenye uwezo wa kufua MW 75 kati ya
mitambo minne (4) iliwasili nchini Mwezi Februari, 2014. Aidha, ujenzi wa misingi ya kuwekea mitambo na matenki mawili (2)
ya kuhifadhi mafuta kwa matumizi ya dharura umekamilika. Kazi nyingine
zinazoendelea ni ujenzi wa jengo la utawala, karakana pamoja na miundombinu ya
barabara na maji.
27. Mheshimiwa Spika, kazi zilizopangwa katika Mwaka 2014/15 ni pamoja na
kukamilisha ufungaji wa mitambo ya kufua umeme; kujenga kituo cha kupozea umeme chenye uwezo wa kV
220/kV 400; kujenga njia ya kusafirishia umeme ya msongo wa kV 220 kutoka
Kinyerezi hadi Kimara; na ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme ya msongo wa kV
132 kutoka Kinyerezi hadi kituo cha kupozea umeme cha Gongolamboto. Gharama za
mradi huu ni Dola za Marekani milioni 183 sawa na Shilingi bilioni 301. Katika Bajeti ya
Mwaka 2014/15 Shilingi bilioni 90 sawa na Dola za
Marekani milioni 55 ikiwa ni fedha za ndani zimetengwa kwa ajili ya
kukamilisha mradi huu. Mradi
unatarajiwa kukamilika katika Mwaka 2014/15 ikiwa ni sehemu ya kutekeleza uamuzi wa Serikali wa
kuondoa kero ya umeme nchini.
Mradi
wa Kinyerezi II - MW 240
28.
Mheshimiwa Spika, katika
Mwaka 2013/14, Serikali ilikamilisha majadiliano na Benki ya Maendeleo ya Afrika ya Kusini (DBSA), ambapo mkopo
wa asilimia 15 ya
gharama ya mradi uliidhinishwa. Aidha, majadiliano kwa ajili ya mkopo wa asilimia
85 ya gharama za mradi,
kati ya Serikali na Benki za Sumitomo Mitsui Banking Corporation (SMBC) na
Japan Bank of International Cooperation (JBIC) za Japan yamekamilika.
29. Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2014/15, Serikali itaanza
kutekeleza mradi huo ikiwa ni pamoja na kuagiza mitambo na kuandaa eneo itakapofungwa mitambo hiyo. Mkandarasi wa mradi ni Kampuni ya
Sumitomo Corporation kutoka Japan. Gharama za mradi huo ni Dola za Marekani milioni 344, sawa na Shilingi bilioni 564. Ili kuanza
utekelezaji wa mradi, fedha za nje Shilingi bilioni 1, sawa na Dola za Marekani
609,756
zimetengwa. Ujenzi wa mradi umepangwa kukamilika katika Mwaka 2015/16.
Mradi wa Kinyerezi III
- MW 300
30. Mheshimiwa Spika, makubaliano ya ubia (Joint
Venture Agreement) kwa ajili ya kuendeleza mradi wa
Kinyerezi III kati ya TANESCO na Kampuni ya China Power Investment (CPI) yamekamilika na kusainiwa Mwezi Oktoba, 2013. Taratibu za
uundwaji wa Kampuni ya ubia zimekamilika, ambapo Serikali kupitia TANESCO
itamiliki asilimia 40 ya hisa na CPI asilimia 60. Katika Mwaka 2014/15, TANESCO na CPI
zitateua wajumbe wa Bodi ya Wakurugenzi kwa ajili ya kuanza kusimamia utekelezaji wa mradi huo. Gharama
za mradi zinakadiriwa kuwa ni Dola za Marekani milioni 389 sawa na Shilingi
bilioni 638.
Mradi wa Kinyerezi IV - MW 300
31. Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia TANESCO
iliingia Makubaliano ya Awali (MoU) na Kampuni ya Poly
Technologies kutoka China Mwezi Septemba, 2013 kwa ajili ya kuendeleza mradi wa
Kinyerezi IV. Mradi utatekelezwa kwa njia ya ubia utakaozihusisha Kampuni za Golden Concord
Development Limited (asilimia 40), China – Africa Development Limited (asilimia
30) za
China na TANESCO (asilimia 30).
32. Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2014/15,
kazi zitakazofanyika ni pamoja na kukamilisha upembuzi yakinifu wa mradi na
Tathmini ya Athari za Mazingira na Kijamii (ESIA); kukamilisha mkataba wa ubia
na uundwaji wa Kampuni ya ubia; pamoja na uteuzi wa Wajumbe wa Bodi ya
Wakurugenzi.
33. Mheshimiwa Spika, miradi niliyoieleza hapo
juu inatekelezwa kupitia mfumo mpya wa usimamizi na ufuatiliaji wa miradi ya kimkakati ya Kitaifa yaani BRN.
Mradi wa
Kuzalisha MW 600 Mkoani Mtwara
34. Mheshimiwa Spika, Mwezi Novemba, 2013
Bodi ya Wakurugenzi ya TANESCO iliidhinisha utekelezaji wa mradi wa kufua umeme
wa MW 600 Mkoani Mtwara. Mradi huo utahusisha ujenzi wa njia ya kusafirisha
umeme ya msongo wa kV 400 kutoka Mtwara hadi Songea. Kampuni ya Symbion ya Marekani inayotekeleza mradi huo
imeajiri Kampuni ya MPR Associates kutoka Marekani kwa ajili ya kufanya
upembuzi yakinifu wa mradi. Kazi hiyo imeanza na inategemewa kukamilika Mwezi
Juni, 2014. Baada ya kazi hiyo kukamilika Kampuni ya Symbion na TANESCO
zitaanza majadiliano kuhusu masuala ya kiufundi na fedha. Utekelezaji wa mradi
huo utaimarisha upatikanaji wa umeme katika Mikoa ya Lindi, Mtwara na Ruvuma
pamoja na kuingiza katika Gridi ya Taifa. Aidha, ujenzi wa mradi huo utawezesha
kuuza umeme wa ziada nchi jirani zikiwemo Malawi na Msumbiji.
Mradi wa Kufua Umeme
wa Rusumo – MW 80
35. Mheshimiwa Spika, mradi wa Rusumo
unatekelezwa kwa pamoja na nchi za Rwanda na Burundi. Mradi pia unahusisha
ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme wa msongo wa kV 220 kutoka Rusumo hadi
kwenye mifumo ya usafirishaji umeme kwa nchi husika. Kwa upande wa Tanzania
njia ya kusafirisha umeme itaunganishwa katika Gridi ya Taifa katika kituo cha
Nyakanazi. Kazi zilizokamilika katika Mwaka 2013/14 ni zifuatazo: upembuzi
yakinifu; Tathmini ya Athari ya Mazingira na Kijamii (ESIA); kusainiwa kwa
Mkataba wa Utekelezaji Mradi (Implementation Agreement); na Mkataba wa Wana Hisa (Share
Holding Agreement). Aidha, majadiliano ya mkopo kati ya Serikali za Burundi, Rwanda
na Tanzania, pamoja na Benki ya Dunia na Benki ya Maendeleo ya Afrika
yalikamilika. Mradi utaanza kutekelezwa Mwaka 2014/15, na utagharimu kiasi cha Shilingi bilioni
164, sawa na Dola za Marekani milioni 100. Fedha za nje zilizotengwa na Serikali ni Shilingi bilioni 2, sawa na Dola za Marekani milioni 1.22 kwa ajili ya kuanza utekelezaji wa mradi
huu.
Miradi ya Kufua Umeme Kutokana na
Makaa ya Mawe
36. Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea
kusimamia uendelezaji wa miradi ya kufua umeme kutokana na makaa ya mawe ya Kiwira
- MW 200, Mchuchuma - MW 600 na Ngaka - MW 400. Miradi ya Mchuchuma na Ngaka
inatekelezwa na Wizara ya Viwanda na Biashara kupitia Shirika la Maendeleo ya
Taifa (NDC). Kwa upande wa mradi wa Kiwira unaosimamiwa na STAMICO, kazi zilizofanyika Mwaka 2013/14 ni kudurusu taarifa za
kitaalamu za utafiti, upembuzi yakinifu na mazingira zilizofanyika miaka ya
nyuma. Kazi zilizopangwa kufanyika katika Mwaka 2014/15 ni pamoja na: kufufua
mgodi wenye uwezo wa kuzalisha tani 150,000 za makaa ya mawe kwa mwaka;
kukarabati mtambo wa kufua umeme uliopo mgodini wa MW 6; kukamilisha
upatikanaji wa mbia kwa ajili ya mradi mkubwa wa kuzalisha MW 200; na kulipa
fidia kwa watakaopisha mradi na njia ya umeme wa msongo wa kV 400 wa urefu wa
kilomita 100 kutoka mgodini hadi eneo la Uyole, Mbeya ili kuunganishwa kwenye
Gridi ya Taifa. Gharama za
mradi zinakadiriwa kuwa Dola
za Marekani milioni 400,
sawa na takriban Shilingi bilioni 656. Katika Mwaka 2014/15, Shilingi bilioni 5 zimetengwa kwa ajili ya kutekeleza baadhi
ya kazi zilizotajwa hapo juu.
Ukarabati wa Mitambo ya
Kufua Umeme katika Kituo cha
Hale
37.
Mheshimiwa
Spika, mradi huu wa
ukarabati wa mitambo ya kufua umeme
katika kituo cha Hale unaofadhiliwa na Serikali ya Sweden. Lengo ni kuwezesha
kituo hicho kufua umeme kufikia uwezo wake wa juu kabisa wa MW 21 badala ya MW
10 zinazofuliwa sasa. Katika Mwaka 2014/15 Shilingi bilioni 3, sawa na Dola za
Marekani milioni 1.83 zimetengwa kwa ajili ya ukarabati wa mitambo hiyo.
Kuimarisha Njia za Kusafirisha na
Kusambaza Umeme
(i)
Mradi
wa Iringa - Shinyanga kV 400 (Backbone)
38.
Mheshimiwa Spika, mradi huu unahusu ujenzi wa kilomita 670 za usafirishaji umeme wa msongo wa kV
400 kutoka Iringa kupitia Dodoma na Singida hadi Shinyanga. Aidha, vituo vya kupozea umeme wa msongo wa kV
400/220/33 pamoja na njia za usambazaji umeme za msongo wa kV 33 zitajengwa. Mwezi
Novemba, 2013 TANESCO ilisaini mikataba ya ujenzi na Kampuni za KEC
International Limited na Jyoti Structures Limited za India. TANESCO pia
ilisaini mkataba na umoja (consortium) wa Kampuni za GS Engineering and Construction na
Hyosung kutoka Korea Kusini kwa ajili ya utekelezaji wa mradi huu. Kazi
nyingine iliyofanyika ni ulipaji wa fidia katika maeneo ya Igunga, Kishapu na
Shinyanga. Pia, kazi za upimaji (detailed survey), utayarishaji usanifu na uidhinishaji wa michoro
zinaendelea.
39.
Mheshimiwa Spika, kazi
zilizopangwa kufanyika katika Mwaka 2014/15 ni pamoja na ununuzi wa vifaa vya
mradi; maandalizi ya usambazaji wa umeme wa
Gridi katika vijiji zaidi ya 90 ambako mradi utatekelezwa; na kuanza ujenzi wa
njia za usafirishaji umeme. Jumla ya Shilingi bilioni 2.50 sawa na Dola za Marekani milioni 1.52 zimetengwa kwa Mwaka 2014/15 ili kutekeleza
mradi huu. Kati ya fedha hizo, Shilingi milioni 500 ni fedha za ndani na Shilingi bilioni 2 ni fedha za nje kutoka Benki ya Dunia
(WB), Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB), Shirika la Maendeleo la Japan
(JICA), Benki ya Uwekezaji ya Ulaya (EIB) na Shirika la Maendeleo la Korea
(EDCF). Mradi utagharimu Dola za Marekani milioni 224 sawa na Shilingi bilioni 367.36 na unatarajiwa kukamilika Mwaka 2015/16.
(ii) Mradi wa
Makambako - Songea kV 220
40.
Mheshimiwa Spika, katika kutekeleza Ibara 63 (u) ya Ilani ya Uchaguzi ya
CCM ya Mwaka 2010 - 2015, Wizara inaendelea na taratibu za kuanza utekelezaji wa mradi huo. Mradi utahusisha ujenzi wa
kilomita 250 za njia za kusafirisha umeme wa msongo wa kV 220 kutoka Makambako
hadi Songea; kujenga vituo vikuu viwili
(Madaba na Songea) vya kupozea umeme wa msongo wa kV 220/33 na kuongeza uwezo wa kituo cha kupozea
umeme cha Makambako; ujenzi wa kilomita 900 za njia za usambazaji umeme za
msongo wa kV 33. Lengo la mradi huu ni kuunganisha Wilaya za Ludewa, Mbinga,
Namtumbo, Njombe, Songea Mjini na Songea Vijijini katika Gridi ya Taifa. Mradi
pia utahusisha kuwaunganishia wateja wa awali 30,000 ambao watatakiwa kulipia
kodi ya ongezeko la thamani (VAT) pekee.
41.
Mheshimiwa Spika, Mwezi Januari, 2014 TANESCO ilisaini mkataba na
Kampuni ya Isolux kutoka Hispania kwa ajili ya kutekeleza mradi wa usambazaji
umeme. Aidha, uchambuzi wa zabuni kwa ajili ya ujenzi wa njia ya usafirishaji
umeme umekamilika na maombi ya “no objection” yamewasilishwa Shirika la Maendeleo la Sweden (Sida).
Vilevile, ulipaji fidia kwa watakaopisha mradi katika maeneo ya Mkoa wa Ruvuma
umekamilika kwa asilimia 95 na uhakiki wa malipo kwa Mkoa wa Njombe unaendelea.
42.
Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2014/15, kazi zilizopangwa kutekelezwa ni kuanza ujenzi
wa njia ya usafirishaji umeme na vituo vya kupozea umeme pamoja na njia za
kusambaza umeme. Jumla ya Shilingi bilioni 16.30 sawa na Dola za Marekani milioni 9.94 zimetengwa ili kutekeleza kazi
zilizopangwa. Kati ya fedha hizo, fedha za ndani ni Shilingi milioni 300 na fedha za nje ni Shilingi bilioni 16. Mradi umepangwa kukamilika Mwaka 2015/16.
(iii) Mradi wa North -
East Grid kV 400
43. Mheshimiwa Spika, mradi huu ni wa ujenzi wa njia ya
kusafirishia umeme wa msongo wa kV 400 yenye urefu wa kilomita 664 kutoka
Kinyerezi hadi Arusha kupitia Chalinze na Segera. Pia, mradi utahusisha ujenzi
wa njia za kusafirishia umeme wa msongo wa kV
220 zenye jumla ya kilomita 104 kutoka Segera kwenda Tanga na kutoka Kibaha
kwenda Bagamoyo. Aidha, vituo vikubwa vya kupozea umeme vya Bagamoyo, Chalinze,
Segera na Tanga vitajengwa kwa ajili ya kuwezesha usambazaji umeme katika
Wilaya na Miji Midogo ambayo njia za umeme zitapita. Kazi zilizokamilika Mwaka 2013/14
ni upembuzi yakinifu wa mradi; Tathmini ya Athari za Mazingira na Kijamii (ESIA); na upimaji wa awali wa
ardhi. Aidha, kazi za usanifu wa michoro ya mradi na uchambuzi wa zabuni kwa
ajili ya kumpata mshauri wa mradi zinaendelea.
44. Mheshimiwa Spika, kazi zilizopangwa kwa Mwaka 2014/15 ni pamoja na kukamilisha upimaji wa ardhi na kuweka
mipaka ya eneo la mradi; kulipa fidia kwa wananchi watakaopisha eneo la mradi;
na kumpata mshauri kwa ajili ya kusimamia utekelezaji wa mradi. Jumla ya Shilingi
bilioni 1.50 sawa na Dola
za Marekani 914,630 zimetengwa
ili kutekeleza mradi huu. Kati ya fedha hizo, Shilingi bilioni 1.0 ni fedha za ndani na Shilingi milioni
500 ni fedha za nje. Mradi
unatarajiwa kukamilika Mwaka 2016/17.
(iv) Mradi wa North -
West Grid kV 400
45. Mheshimiwa Spika, mradi huu unahusisha
ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme ya msongo wa kV 400 kutoka Mbeya kupitia Sumbawanga – Mpanda - Kigoma hadi Nyakanazi yenye
urefu wa kilomita 1,148. Awamu ya kwanza ya mradi itahusisha ujenzi wa njia ya kusafirisha
umeme yenye urefu wa kilomita 340 kutoka Mbeya hadi Sumbawanga, na vituo vikubwa
vipya vya kupozea umeme vya Uyole (Mbeya) na Sumbawanga.
46. Mheshimiwa Spika, kazi zilizofanyika kwa
Mwaka 2013/14 ni pamoja na kutathmini upya Athari za Mazingira na Kijamii (ESIA); kudurusu upembuzi
yakinifu baada ya kubadilisha njia ya kusafirisha umeme kutoka msongo wa kV 220
kwenda kV 400; upimaji wa mkuza itakakojengwa njia ya kusafirisha umeme; na
kutathmini fidia kwa watakaopisha awamu ya kwanza ya mradi.
47. Mheshimiwa Spika, kazi zilizopangwa kufanyika Mwaka 2014/15 ni pamoja na
kukamilisha upembuzi yakinifu na usanifu wa mradi ili kuwiana na mahitaji ya sasa ya
msongo wa kV 400; upimaji wa mkuza itakakojengwa njia ya kusafirisha umeme kutoka Mbeya hadi
Sumbawanga; na kulipa fidia kwa watakaopisha mradi. Fedha za ndani Shilingi
bilioni 1.0, sawa na Dola za Marekani 609,756 zimetengwa. Mradi huu unatarajiwa kukamilika Mwaka
2016/17.
(v) Mradi wa
Singida – Arusha - Namanga kV 400
48.
Mheshimiwa Spika, Ibara ya 63 (b) na (t) ya Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya
Mwaka 2010 - 2015 inatoa msisitizo kuhusu kuunganisha Gridi yetu ya Taifa na
nchi jirani ili kuimarisha upatikanaji wa umeme wa uhakika. Mradi wa Singida -
Arusha - Namanga ni sehemu ya
mradi wa Zambia – Tanzania – Kenya (ZTK interconnector) yenye urefu wa kilomita 2,047. Kwa upande wa Tanzania, mradi utahusisha ujenzi
wa njia ya kusafirisha umeme ya msongo wa kV 400 kutoka Singida hadi Arusha na
kutoka Iringa hadi Mbeya.
49.
Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2013/14, kazi zilizofanyika ni zifuatazo:
kukamilika kwa upembuzi yakinifu wa mradi na Tathmini ya Athari za Mazingira na
Kijamii (ESIA); na
upimaji wa mkuza kwa ajili ya njia ya kusafirisha umeme. Kazi zilizopangwa
kufanyika Mwaka 2014/15 ni pamoja na kukamilisha tathmini ya mali na kulipa fidia; ujenzi wa kituo
kipya cha kupozea umeme katika eneo la Kisongo, Mkoani Arusha na upanuzi wa
kituo cha kupozea umeme Mkoani Singida. Kazi nyingine ni kuajiri mshauri wa
mradi na kupata wakandarasi wa ujenzi wa vituo vya kupozea umeme na njia ya
kusafirisha umeme; na kuandaa mpango wa kusambaza umeme kwenye vijiji vilivyo
kando kando ya njia ya kusafirisha umeme. Fedha za nje zilizotengwa ni Shilingi
milioni 500, sawa na Dola za Marekani 304,878 ambazo ni mkopo kutoka AfDB na JICA. Mradi
umepangwa kukamilika Mwaka 2016/17.
50. Mheshimiwa Spika, sambamba na jitihada
hizo, Serikali kupitia TANESCO itatekeleza mradi wa upanuzi wa njia ya usambazaji umeme ya Tunduma hadi
Nakonde (Zambia) ya msongo wa kV 33 na urefu wa mita 100. Mradi pia utahusisha
ufungaji wa kipozea umeme chenye uwezo wa kVA
200 na ukarabati wa njia ya kusambaza umeme kutoka Mbeya hadi Tunduma yenye
urefu wa kilomita 40. Katika Mwaka 2013/14, upimaji na tathmini ya njia ya usambazaji umeme
vilikamilika. Aidha, Kitengo cha kusimamia mradi kimeundwa na taarifa ya Tathmini ya Athari za
Mazingira na za Kijamii imewasilishwa Baraza la Usimamizi wa Mazingira la Taifa
(NEMC) kwa ajili ya kupata idhini ya utekelezaji wa mradi. Katika Mwaka 2014/15,
Serikali imetenga Shilingi bilioni 5, sawa na Dola za Marekani
milioni 3.05 ili kuendelea na utekelezaji
wa mradi huu.
(vi) Mradi wa
Bulyanhulu – Geita kV 220
51.
Mheshimiwa Spika, mradi unahusu ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme ya
msongo wa kV 220 yenye urefu wa kilomita
55 kutoka Bulyanhulu hadi Geita. Mradi pia unahusisha ujenzi wa kituo cha
kupozea umeme cha Geita chenye uwezo wa kV 220/33, usambazaji umeme katika
vijiji vilivyopo ndani ya eneo la mradi na kubadilisha mita za umeme za kawaida
(conventional meters)
zipatazo 2,000 Mkoani Geita kwa kufunga mita za LUKU. Kazi zilizofanyika Mwaka 2013/14
ni pamoja na: kuundwa kwa Kitengo cha usimamizi wa mradi (Project
Implementation Unit) na kuanza kwa taratibu za upimaji wa eneo la mradi. Aidha, tathmini ya
zabuni ya kumpata mshauri wa mradi inaendelea.
52.
Mheshimiwa Spika, kazi zitakazofanyika Mwaka 2014/15 ni zifuatazo:
kukamilisha upimaji wa eneo la mradi; kulipa fidia kwa watakaopisha mradi;
kumpata mshauri na mkandarasi wa mradi; na kuanza utekelezaji wa mradi. Gharama
za mradi ni Shilingi bilioni 41 sawa na Dola za Marekani milioni 25. Jumla ya Shilingi bilioni 2.50 sawa na Dola za Marekani milioni 1.52 zimetengwa ili kutekeleza mradi huu. Kati
ya fedha hizo, Shilingi bilioni 2 ni fedha za ndani na Shilingi milioni 500 ni fedha za nje kutoka Bank of Arab for
Economic Development in Africa (BADEA). Mradi umepangwa kukamilika Mwaka 2015/16.
(vii)
Mradi wa Electricity V
53. Mheshimiwa Spika, mradi unalenga kuunganisha wateja wa awali 8,600
kwenye Wilaya za Bukombe, Busega, Kwimba, Magu, Mbogwe, Misungwi na Sengerema katika Mikoa ya Geita,
Mwanza na Simiyu. Ujenzi wa njia za usambazaji wa umeme wa msongo wa kV 33
zenye urefu wa kilomita 480, kV 0.4 zenye urefu wa kilomita 231 na ufungaji wa
vipozea umeme 109 utafanyika chini ya mradi huu. Shughuli nyingine ni ukarabati
wa vituo vya kupozea umeme vya Ilala kV 132/33/11 na Sokoine kV 33/11, katika
Jiji la Dar es Salaam pamoja na upanuzi wa kituo cha kupozea umeme cha kV
220/132/33 Njiro, Mkoani Arusha.
54. Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2013/14 kazi
zilizofanyika ni pamoja na: kuanza kwa ukarabati wa kituo cha kupozea umeme cha
Sokoine Drive, Ilala (Dar es Salaam); kukamilisha ukaguzi wa maeneo na michoro
ya kazi za usambazaji umeme; kukamilika kwa utafiti wa udongo kwenye vituo vya kupozea umeme vya Sokoine Drive,
Ilala (Dar es Salaam) na Arusha;
kuanza kwa ulipaji fidia kwa watakaopisha mradi; kuwasili kwa vifaa vya
usambazaji umeme ikiwa ni pamoja na nguzo 890 katika maeneo ya mradi; na
kuendelea kwa kazi ya usanifu wa mradi.
55.
Mheshimiwa Spika, kazi zitakazotekelezwa katika
Mwaka 2014/15 ni zifuatazo: kukamilisha ukarabati wa kituo cha Sokoine Drive,
Ilala (Dar es Salaam) na Arusha. Gharama za mradi huu ni Dola za Marekani milioni 45 sawa na Shilingi
bilioni 73.80. Jumla ya Shilingi bilioni 4, sawa na Dola za Marekani milioni 2.44 zimetengwa ili
kutekeleza kazi zilizopangwa. Kati ya fedha hizo, Shilingi bilioni 3.50 ni fedha za ndani na Shilingi
milioni 500 ni fedha za nje kutoka Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB). Mradi umepangwa kukamilika Mwaka
2014/15.
Mradi wa Kuboresha Upatikanaji
wa Umeme Jijini Dar es
Salaam
56. Mheshimiwa Spika, mradi huu unafadhiliwa na Serikali za Finland na Japan
na unahusu ujenzi wa kituo kipya cha kupozea umeme mkabala na kituo cha City Centre cha msongo wa kV 132/33/11, ujenzi wa njia
ya usafirishaji umeme wa msongo wa kV 132 kutoka kituo cha Ilala na kuunganisha
mfumo wa vituo vya kupozea umeme wa kV 33/11 vya City Centre, Kariakoo, Railway
na Sokoine. Lengo la mradi huu ni kuboresha miundombinu ya umeme ili kuwezesha
upatikanaji wa umeme wenye ubora na uhakika zaidi katika Jiji la Dar es Salaam.
57. Mheshimiwa Spika, kazi zilizotekelezwa kwa Mwaka
2013/14 ni zifuatazo: kupatikana kwa eneo la ujenzi wa kituo cha kupozea umeme
cha City Centre; kukamilisha upembuzi
yakinifu wa mradi; ulipaji fidia kwa watakaopisha mradi; na kuanza kwa ujenzi
wa kituo. Kazi zifuatazo zitatekelezwa kwa Mwaka 2014/15: kuendelea na ujenzi
wa kituo cha City Centre
na njia za usafirishaji na usambazaji umeme. Gharama za mradi ni Shilingi
bilioni 123 sawa na Dola za Marekani milioni 75. Fedha za nje zilizotengwa ni
Shilingi
bilioni 1.0 na mradi umepangwa kukamilika Mwaka 2014/15.
Mradi
wa Ufuaji na Usambazaji Umeme – Biharamulo, Mpanda na Ngara (ORIO)
58.
Mheshimiwa Spika, mradi unahusisha ufungaji wa jenereta zenye uwezo wa
MW 2.5 kila moja katika Wilaya za Biharamulo, Mpanda na Ngara na hivyo kufanya
jumla ya uwezo wa MW 7.5. Pia, ukarabati wa njia zilizopo na ujenzi wa njia
mpya za usambazaji umeme zenye msongo wa kV 33 utafanyika. Lengo la mradi huu ni
kuongeza uwezo wa ufuaji na usambazaji umeme katika Wilaya hizo.
59. Mheshimiwa Spika, kazi zilizofanyika katika Mwaka 2013/14 ni pamoja na:
kusainiwa kwa mkataba kwa ajili ya ufungaji jenereta hizo kati ya TANESCO na
Kampuni ya M/s Zwart Techniek B.V. ya Uholanzi Mwezi Oktoba, 2013; kusainiwa
kwa mikataba kati ya TANESCO na Kampuni ya Nakuroi Investment ya Tanzania kwa ajili ya ujenzi na
ukarabati wa mifumo ya usambazaji umeme
Mpanda; na Kampuni ya NAMIS ya Tanzania kwa ajili ya ujenzi na ukarabati wa
mifumo ya usambazaji umeme katika Wilaya za Biharamulo na Ngara. Mikataba
husika ilisainiwa Mwezi Desemba, 2013.
60. Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2014/15 kazi
zitakazofanyika ni zifuatazo: kufunga
jenerata katika Wilaya za Biharamulo, Mpanda na Ngara; kukarabati na kujenga njia mpya za usambazaji umeme
katika Wilaya za Mpanda, Biharamulo na Ngara; na kutoa mafunzo kwa ajili ya usimamizi wa miradi kwa
wajasiriamali na watumiaji wa umeme katika Wilaya hizo. Mradi huo
utakapokamilika unatarajiwa kuwaunganishia umeme wateja wapya zaidi ya 100,000.
61. Mheshimiwa Spika, gharama za mradi huo ni EURO milioni 33.15 sawa na Shilingi bilioni 81.55. Jumla ya Shilingi bilioni 22.50 sawa na Dola za Marekani milioni 13.72 zimetengwa kwa ajili ya kutekeleza mradi
huu Mwaka 2014/15. Kati ya fedha hizo
Shilingi bilioni 22 ni fedha za ndani na Shilingi milioni 500 ni fedha za nje kutoka Serikali ya
Uholanzi. Mradi umepangwa kukamilika Mwaka 2015/16.
Usambazaji Umeme kupitia TANESCO na Wakala
wa Nishati Vijijini (REA)
62.
Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kutekeleza
Ibara ya 63 (c) ya Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya Mwaka 2010 – 2015, inayohamasisha kuongeza idadi ya
wananchi waliounganishiwa
umeme mijini na vijijini. Wakati
Serikali ya Awamu ya Nne inaingia madarakani kiwango cha uunganishwaji (connection
level) nchini kilikuwa
asilimia 10. Kufuatia
jitihada mahsusi za Serikali ikiwemo punguzo la gharama za kuunganisha umeme
pamoja na uwezeshaji chini ya Mfuko wa Nishati Vijijini (Rural Energy Fund -
REF), kiwango cha
uunganishwaji umeme kimeongezeka na kufikia asilimia 24 Mwezi Machi 2014. Lengo la Serikali ni kuwawezesha
Watanzania asilimia 30 kuunganishiwa
umeme (connection) ifikapo Mwaka 2015/16. Aidha, kiwango cha
uunganishwaji umeme vijijini kimeongezeka kutoka asilimia 2 Mwaka 2005 hadi asilimia 7 mwishoni mwa Mwaka 2013.
63. Mheshimiwa Spika, hadi kufikia Mwezi Machi, 2014 watu wanaopata huduma
ya umeme (access level) walifikia asilimia 36 ya Watanzania waishio Bara. Hivyo,
Watanzania wanashauriwa kutumia fursa ya huduma ya umeme ili ichangie katika
shughuli za kiuchumi na kijamii na hivyo kuinua hali ya maisha yao mijini na
vijijini na kuanza kupunguza na hatimaye kutokomeza umaskini.
64.
Mheshimiwa Spika, pamoja na juhudi nyingine,
mafanikio hayo yametokana na utekelezaji wa Awamu ya Kwanza ya Mradi Kabambe wa Kusambaza Umeme
Vijijini uliokuwa na miradi midogo 41 katika Mikoa 16 ya Tanzania Bara (Arusha,
Dodoma, Kagera, Kigoma, Kilimanjaro, Manyara, Mara, Mbeya, Morogoro, Mwanza,
Pwani, Rukwa, Shinyanga, Singida, Tabora na Tanga). Kuanzia Mwezi Julai 2013
hadi Aprili 2014, wateja wapya 15,817 walikuwa wameunganishiwa umeme kati ya
wateja 22,000 waliotarajiwa. Aidha, kupitia lengo la BRN la kuunganisha wateja
150,000 kwa mwaka, jumla ya wateja wapya 138,931 waliunganishiwa umeme sawa na asilimia
92.62 ya lengo hilo. Ongezeko
hili linatokana na uamuzi wa Serikali kupunguza gharama za kuunganishia umeme
wa wateja wa njia moja (single phase) mijini na vijijini kwa wastani wa kati ya asilimia
30 hadi 77 ulioanza kutekelezwa Mwezi Januari, 2013.
65. Mheshimiwa Spika, REA imesaini mikataba na wakandarasi 35 wa
kutekeleza Awamu ya Pili ya Mradi Kabambe wa Usambazaji Umeme Vijijini katika mikoa mbalimbali Tanzania Bara. Utekelezaji wa mradi huo
utaendelea katika Mwaka 2014/15, ambapo jumla ya Shilingi bilioni 290.20 sawa na Dola za Marekani 176.95 zimetengwa kutekeleza miradi hiyo. Kati ya
fedha hizo, Shilingi bilioni 269.20 ni fedha za ndani na Shilingi bilioni 21 ni fedha za nje kutoka Shirika la Maendeleo
la Norway (NORAD).
Mpango wa Kitaifa wa Kuhamasisha Uwekezaji
kwenye Usambazaji Umeme
66. Mheshimiwa Spika, Serikali imeandaa Mpango
wa Usambazaji Umeme Nchini kwa kipindi cha miaka 10 kuanzia Mwaka 2013 hadi
2022 (The National Electrification Programme Prospectus). Katika kipindi hicho,
Mpango huo utakuwa ndiyo mwongozo wa miradi ya Serikali ya kusambaza umeme
vijijini. Maandalizi ya Mpango huo yamefadhiliwa na Serikali ya Norway.
Mradi wa
Kusambaza Umeme katika Mikoa ya Lindi na Mtwara
67. Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia REA
inaendelea na utekelezaji wa jumla ya miradi 52 ya kusambaza umeme katika Mikoa
ya Lindi na Mtwara. Hadi Mwezi Aprili, 2014 miradi 47, sawa na asilimia 97 ilikamilika, ambapo
wateja 1,925 waliunganishiwa umeme. Kati ya hao wateja 1,135 ni kutoka Mkoa wa
Lindi na wateja 790 ni kutoka Mkoa wa Mtwara. Gharama za miradi hiyo ni Shilingi
bilioni 6.10, sawa na Dola za Marekani milioni 3.72. Katika Mwaka 2014/15, Serikali
itakamilisha miradi mitano (5) iliyobaki. Gharama ya kuunganisha umeme kwa
Mikoa ya Lindi na Mtwara ni Shilingi 99,000 kwa umbali usiozidi mita 30.
Gharama hizi zitatumika hadi kufikia Mwezi Juni, 2015. Natoa ushauri kwa
wananchi wa Mikoa ya Lindi na Mtwara kutumia fursa hiyo kuunganishiwa umeme ili
kuboresha maisha yao kupitia shughuli endelevu za kiuchumi na kijamii.
Tanzania Energy Development and Access Expansion
Project (TEDAP)
68.
Mheshimiwa Spika, mradi huu ni wa uboreshaji wa mifumo ya Gridi (on-grid)
na kuhamasisha matumizi ya
nishati jadidifu kama vyanzo mbadala vya kufua umeme nje ya Gridi (off-grid). Kazi zilizotekelezwa Mwaka 2013/14 kwa upande wa Gridi
ni zifuatazo: kukamilika kwa ufungaji wa vipozea umeme viwili vyenye uwezo wa MVA 20
katika kituo cha umeme cha Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA).
Kukamilika kwa kazi hiyo kumeboresha upatikanaji umeme katika maeneo ya
Mererani, Usa River na Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro. Gharama za
mradi huo kwa upande wa on-grid ni Dola za Marekani milioni 114.50 sawa na Shilingi bilioni 187.78. Aidha, kwa upande wa
mifumo ya nje ya Gridi, kazi zilizofanyika ni zifuatazo: kuwezesha ukamilishaji
wa mradi wa maporomoko madogo ya maji wa Mapembasi (Njombe) unaotekelezwa na Sekta Binafsi;
kuwezesha wafuaji wa umeme wa uwezo mdogo (small power producers) kutumia mkopo kutoka
Benki ya Dunia (IDA Credit Line); kugharamia ukamilishaji mradi wa pamoja na
kufunga mifumo ya Umeme Jua katika Wilaya za Bunda, Geita na Tandahimba; na
kukagua mifumo ya Umeme Jua katika Wilaya ya Sumbawanga chini ya Awamu ya
Kwanza ya Sustainable Solar Market Packages (SSMP). Gharama za mradi kwa upande wa off-grid ni Dola za Marekani milioni 47.50 sawa na Shilingi
bilioni 77.90. Mradi huu unafadhiliwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,
Benki ya Dunia na Serikali ya Korea ya Kusini.
69. Mheshimiwa Spika, kazi zitakazotekelezwa
kwa Mwaka 2014/15 ni zifuatazo: kuendelea kuboresha miundombinu ya umeme katika
Mikoa ya Arusha, Dar es Salaam na
Kilimanjaro; kuendelea kuhamasisha na kuwezesha matumizi ya nishati bora; na kufadhili
ujenzi wa mitambo ya kufua umeme kwenye maporomoko madogo ya maji. Aidha, Awamu ya Pili ya SSMP itahusisha ufungaji wa
mifumo ya Umeme Jua kwenye taasisi za kijamii, makazi ya watu na sehemu za
biashara. Wilaya zitakazonufaika ni Biharamulo, Bukombe, Chato, Kasulu,
Kibondo, Namtumbo, Sikonge na Tunduru. Jumla ya Shilingi bilioni 4.7, sawa na Dola za
Marekani milioni 2.87 zimetengwa ili kutekeleza kazi zilizopangwa. Kati ya
fedha hizo, fedha za ndani ni Shilingi milioni 700, sawa na asilimia 15; na fedha za nje ni Shilingi
bilioni 4, sawa na asilimia 85 ya gharama zote za mradi.
70. Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea
kuhamasisha uendelezaji wa miradi ya kufua umeme kwa kutumia maporomoko madogo ya
maji. Katika Mwaka 2013/14, Serikali kupitia EWURA ilitoa leseni tatu kwa
Kampuni za Mwenga Hydro Limited ya Mufindi (MW 4); Ngombeni Power Limited ya
Kisiwani Mafia (MW 1.5); Mapembasi ya Njombe (MW 10); na Tangulf Express
Limited ya Njombe (MW 10).
71. Mheshimiwa Spika, ili kuboresha mazingira
ya uwekezaji katika miradi midogo isiyozidi MW 10 ya kufua umeme kwa kutumia
nishati jadidifu, katika Mwaka 2014/15, Serikali kupitia EWURA itakamilisha durusu ya Mwongozo
wa mikataba ya kuuziana umeme (Standardised Power Purchase Agreement - SPPA) na Kanuni ya kukokotoa
bei ya kuuziana umeme kwa miradi yenye uwezo wa kufua umeme kati ya kW 100 mpaka MW 10. Kukamilika kwa
Kanuni na Mwongozo huo kutaimarisha uwekezaji nchini kwani bei itazingatia
gharama halisi za kufua umeme pamoja na aina ya teknolojia itakayotumika. Lengo
ni kuongeza kasi ya kuwapatia wananchi huduma ya umeme, hususan vijijini.
Ujenzi wa
Miundombinu ya Umeme Kilombero na Ulanga
72.
Mheshimiwa Spika, mradi huu unatekelezwa chini ya Mpango wa Southern Agriculture Growth Corridor of Tanzania
(SAGCOT) katika maeneo ya
Kilombero na Ulanga. Katika Mwaka 2013/14 upembuzi yakinifu ulikamilishwa. Katika
Mwaka 2014/15, kazi zitakazofanyika ni pamoja na zifuatazo: kusimamia
utekelezaji wa ujenzi wa njia kubwa ya kusafirisha umeme ya msongo wa kV 220;
ujenzi wa kituo cha kupozea umeme cha kV 220/33 chenye uwezo wa MVA 20; na
ujenzi wa njia za kusambaza umeme. Ili kutekeleza mradi huu, jumla ya fedha za
nje Shilingi bilioni 1.0,
sawa na Dola za
Marekani 609,756
zitatolewa na Umoja wa Nchi za Ulaya.
Kuboresha Upatikanaji wa
Umeme
73. Mheshimiwa Spika, kutokana na umuhimu wa huduma ya umeme katika shughuli
za kiuchumi na kijamii, Serikali imeendelea kutekeleza miradi ya kuiwezesha TANESCO
kutoa huduma bora. Miradi hiyo ni
ya kipindi cha mpito wakati Serikali inakamilisha ujenzi wa miundombinu ya
umeme wa gesi asilia. Katika Mwaka 2014/15, jumla ya Shilingi bilioni 145, sawa na Dola za
Marekani milioni 88 zimetengwa kwa ajili ya kutekeleza miradi hiyo. Kati ya
fedha hizo, Shilingi bilioni 20, sawa na asilimia 14 ni fedha za ndani na Shilingi
bilioni 125, sawa na asilimia 86 ni fedha za nje kutoka Benki ya Dunia.
74. Mheshimiwa Spika, Serikali pia imeendelea
na zoezi la kutathmini muundo wa TANESCO na kuandaa Mwelekeo Mpya wa Sekta
Ndogo ya Umeme (Electricity Supply Industry Reform Roadmap). Vilevile, Serikali
imempata mshauri Kampuni ya PriceWaterCoopers (PWC) kutoka Uingereza, ambaye ametoa
ushauri kuhusu zoezi hilo. Serikali
inategemea kutangaza Roadmap hiyo ifikapo Mwezi Juni, 2014.
75.
Mheshimiwa Spika, napenda kutumia fursa
hii kuupongeza uongozi wa TANESCO na watumishi wote kwa mabadiliko ambayo
wameanza kuyatekeleza katika Shirika hilo na matokeo kuanza kuonekana. Mabadiliko hayo ni
pamoja na kuhamisha shughuli za ununuzi, utekelezaji wa Bajeti na Mipango
kutoka Makao Makuu kwenda Ofisi za Kanda na Mikoa kwa nia ya kuboresha huduma
zinazotolewa kwa wananchi. Utaratibu huu utasaidia
kuongeza kasi ya kupeleka umeme wilayani na vijijini pamoja na kuharakisha
matengenezo na ukarabati wa miundombinu ya umeme.
Uboreshaji wa Huduma kwa Wateja
76.
Mheshimiwa
Spika, pamoja na mahitaji ya juu ya umeme (Maximum Demand) kuongezeka kwa asilimia
8 kati ya Mwaka 2011 na 2013, TANESCO imehakikisha kuwa huduma ya umeme
inaendelea kupatikana nchini. Sambamba na jitihada za TANESCO, inatarajiwa kuwa
umeme wa uhakika utaendelea kupatikana kwa Mwaka 2014/15 kama ilivyokuwa kwa
2013/14. Pamoja na kuwa na changamoto
mbalimbali, naipongeza TANESCO kwa kuboresha utoaji huduma ya umeme nchini na
hivyo kuimarisha shughuli za kiuchumi na kijamii.
77. Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia
TANESCO inaendelea kuhakikisha kuwa vifaa vyote muhimu vya kuunganishia umeme
wateja vikiwemo nguzo, mita na nyaya vinapatikana kwa wakati. TANESCO pia imeendelea
kuboresha huduma mbalimbali kwa wateja zikiwemo: kutumia mtandao (on-line) kupata fomu za maombi ya
mwanzo ya kuunganishiwa umeme na kulipia ankara kwa wateja wanaolipa baada ya
kutumia umeme; utoaji wa taarifa za katizo la umeme kwa ujumbe mfupi wa simu (sms);
kuanzisha vituo maalum (point of sales) vya kulipia umeme karibu na wanachi;
kulipia umeme kupitia benki; mpango wa kuwaunganishia wateja majumbani na Ofisi
za Serikali mita za LUKU utakaotekelezwa na kukamilishwa ndani ya kipindi cha
miaka mitatu pamoja kuongeza
matumizi ya mita za kisasa zijulikanazo kama Automatic Meter Reading (AMR).
(i) Uendelezaji wa Umeme wa Jua
78.
Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2013/14, wasambazaji wa mifumo ya Umeme wa Jua
nchini waliongezeka kufuatia kukua
kwa mahitaji na matumizi ya aina hiyo ya nishati. Aidha, wawekezaji
wengi walionesha nia ya kujenga mifumo ya Umeme wa Jua yenye uwezo wa kuanzia
MW 50 hadi MW 500 kwa ajili ya kuunganishwa kwenye Gridi ya Taifa. Katika Mwaka
2014/15, Serikali itaendelea kuhamasisha matumizi ya Umeme wa Jua.
79.
Mheshimiwa Spika, Mwezi
Januari, 2014 Serikali ilisaini Mkataba
na Kampuni ya Elektro-Merl kutoka Austria kwa ajili ya kuleta na kufunga
jenereta 14 za Umeme wa Jua (Photovoltaic Generators) zitakazotumika kusambaza umeme
vijijini. Mradi huo utatekelezwa katika Mikoa ya Dodoma, Katavi, Ruvuma na
Tabora. Gharama za mradi huo ni Euro milioni 5.38
sawa na Shilingi bilioni 14.20.
(ii) Uendelezaji wa Nishati ya Upepo
80.
Mheshimiwa Spika,
taratibu za uendelezaji wa nishati ya upepo kupitia Sekta Binafsi zipo katika
hatua mbalimbali. Majadiliano ya kuuziana umeme (Power Purchase Agreement -
PPA) kati ya TANESCO na Kampuni ya Geo Wind
Power (Singida) yanaendelea. Katika awamu
ya kwanza (2015/16), Kampuni hiyo inatarajia kufua umeme wa MW 50 ambapo Dola
za Marekani milioni 136,
sawa na Shilingi bilioni 223 zitatumika.
Aidha, Kampuni ya Wind East Africa Limited (Singida) iliendelea na maandalizi
ya kufua umeme wa MW 100 na kulipa fidia kwa watakaopisha mradi. Vilevile,
Kampuni ya Sino-Tan Renewable Energy Limited inatarajia kutekeleza mradi wa
kufua umeme MW 100 katika eneo la Makambako, Mkoani Njombe. Kwa sasa Kampuni
hizo zinatafuta fedha kwa ajili ya kutekeleza miradi yao. Katika Mwaka 2014/15,
Kampuni hizo zitakamilisha mikataba ya kuuziana umeme na TANESCO pamoja na
taratibu za kupata mikopo.
(iii) Uendelezaji Tungamotaka (Biomass)
81.
Mheshimiwa Spika, Watanzania wengi bado
wanategemea tungamotaka hasa kuni na mkaa kama chanzo cha nishati ya kupikia.
Katika Mwaka 2013/14, Serikali
ilikamilisha Mpango wa Kuendeleza Tungamotaka, ambao unalenga kuboresha matumizi ya nishati hiyo.
Katika Mwaka 2014/15, kazi zitakazofanyika ni pamoja na kukusanya taarifa kuhusu
viwanda vinavyofua au vinavyoweza kufua umeme kutokana na mabaki yatokanayo na
shughuli za viwanda vya sukari, mbao na karatasi.
(iv) Uendelezaji wa Bioenergies
82.
Mheshimiwa Spika, Serikali imeandaa
Rasimu ya Sera na Sheria ya Bioenergies, na kufanya tathmini ya kina kuhusu uzalishaji wa bio-diesel kwa kutumia mafuta ya mimea. Katika Mwaka 2014/15,
utekelezaji utalenga kuhamasisha uendelezaji wa Bioenergies na kukamilisha Sheria ya Bioenergies.
Jumla ya Shilingi milioni 800, sawa na Dola za
Marekani 487,805 zimetengwa kwa ajili ya kutekeleza kazi
hizo. Kati ya fedha hizo, Shilingi milioni 300, sawa
na asilimia 37.5 ni fedha za ndani; na Shilingi milioni
500, sawa na asilimia 62.5 ni
fedha za nje kutoka Sida (Sweden) na NORAD (Norway).
83.
Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2013/14,
Serikali kwa kushirikiana na Kituo
cha Zana za Kilimo na Teknolojia (CARMATEC) ilitekeleza Mpango wa uendelezaji
wa biogas katika ngazi ya kaya. Kupitia Mpango huo, jumla ya
mitambo 9,000 ilijengwa katika Mikoa 22 nchini. Katika Mwaka 2014/15, Serikali
itaendelea kuhamasisha matumizi ya biogas majumbani, vituo vya
afya, zahanati na katika shule mbalimbali.
(v) Uendelezaji Jotoardhi (Geothermal)
84.
Mheshimiwa Spika,
Serikali imeanzisha Kampuni inayoitwa Tanzania Geothermal Development Company
Limited (TGDC). Kampuni hiyo itaratibu utafiti,
uchorongaji visima, uendelezaji wa jotoardhi na kutoa ushauri wa kitalaamu. Serikali pia inatekeleza Mpango unaoitwa Scaling-Up
Renewable Energy (SREP) unaofadhiliwa na mfuko wa Climate
Investment Funds (CIF) na kuratibiwa na
AfDB. Serikali imepata Dola za Marekani 700,000 sawa na Shilingi bilioni 1.15 kwa ajili ya maandalizi ya mradi huu. Miongoni mwa
shughuli zitakazotekelezwa ni uendelezaji wa nishati jadidifu vijijini (Renewable
Energies for Rural Electrification)
pamoja na matumizi ya jotoardhi kama chanzo kipya cha nishati nchini. Thamani
ya mradi huu ni Dola za Marekani milioni 50, sawa na Shilingi
bilioni 82.
85.
Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2014/15,
Serikali kupitia TGDC itachoronga visima vyenye kina kifupi katika Mkoa wa Mbeya kwa ajili ya
kupima mwongezeko wa joto chini ya ardhi. Aidha, Mpango wa kuendeleza Jotoardhi
nchini utaandaliwa. Katika kuendeleza ushirikiano na nchi wanachama wa African
Rift Geothermal (ARGeo) pamoja na kuhamasisha uendelezaji
wa jotoardhi nchini, Serikali kwa kushirikiana na UNEP inaandaa kongamano la
kikanda kuhusu Jotoardhi litakalofanyika Jijini Arusha Mwezi Oktoba, 2014.
Katika Mwaka 2014/15, Shilingi bilioni 11.0, sawa na Dola za Marekani milioni 6.71 zimetengwa kwa ajili ya kazi hizo. Kati ya fedha hizo Shilingi bilioni 10.0, sawa na asilimia 90.9 ni fedha za ndani; na Shilingi bilioni 1.0, sawa na asilimia 9.1 ni fedha za nje.
(vi) Matumizi Bora ya Nishati
86.
Mheshimiwa Spika,
matumizi bora ya nishati (Energy Conservation and Efficiency)
ni mpango muhimu katika kuhakikisha upatikanaji wa nishati na kupunguza
uharibifu wa mazingira. Jitihada za kuendeleza matumizi bora ya nishati zimeelekezwa katika sekta za kiuchumi zikiwemo: afya,
biashara, elimu, makazi, migodi, kilimo, usafirishaji na viwanda. Lengo la
mradi huu ni kupunguza upotevu wa nishati hasa ya umeme. Katika Mwaka 2014/15,
Serikali kupitia TANESCO itatekeleza mradi wa kusimamia matumizi bora ya umeme (Demand
Side Management) katika Taasisi za Serikali kwa kubadilisha
jumla ya taa milioni 3.2 zitumiazo umeme mwingi (Incandescent bulbs) na
kuweka taa zitumiazo umeme kidogo (Compact Fluorescent Light - CFL)
na hivyo kuwezesha kuokoa takriban MW 37.9 baada ya mradi huu kukamilika. Kiasi
hiki cha umeme kinaweza kutosheleza mahitaji ya Mkoa wa Mbeya. Mradi huu
utatekelezwa katika Mikoa ya Arusha, Dar es Salaam, Kilimanjaro, Mwanza na
Tanga ambapo matumizi ya umeme ni makubwa. Gharama ya kutekeleza mradi huu ni Shilingi
bilioni 24, sawa na Dola za Marekani milioni
14.63.
87.
Mheshimiwa Spika,
sambamba na mradi huo, TANESCO pia inafanya juhudi za kupunguza upotevu wa
umeme katika njia za usafirishaji na usambazaji umeme (Supply Side
Management), kwa kuboresha miundombinu yake. Katika
Mwaka 2014/15, Serikali
inakusudia kufanya yafuatayo: kujenga uwezo wa kitaasisi katika masuala ya
matumizi bora ya nishati; kuratibu tafiti za kupunguza upotevu wa nishati; na
ukaguzi wa matumizi ya nishati (Energy Audit) kwa
kushirikiana na Kampuni ya KEMCO
kutoka Korea Kusini ambayo imesaini Makubaliano ya Awali (MoU)
na Wizara ya Nishati na Madini. Shilingi milioni 600,
sawa na Dola za Marekani 365,854 zimetengwa kwa ajili
ya kutekeleza mradi huu, ambapo Shilingi milioni 400,
sawa na asilimia 66.67
ni fedha za ndani na Shilingi milioni 200,
sawa na asilimia 33.33
ni fedha za nje kutoka Sida (Sweden).
SEKTA NDOGO
YA GESI ASILIA NA MAFUTA
Mradi wa Ujenzi wa Bomba la Gesi Asilia
kutoka Mtwara na Lindi hadi Dar es
Salaam
88.
Mheshimiwa Spika, hadi
kufikia Mwezi Aprili, 2014 mabomba yote 45,693
kwa ajili ya ujenzi wa Bomba
la kusafirishia gesi asilia kutoka Mtwara
(Madimba) na Lindi (Songo Songo) hadi Dar es Salaam yalikuwa yameletwa nchini.
Ufukiaji wa mabomba hayo umekamilika kwa umbali wa kilomita 182 kati ya 542
sawa na asilimia 34. Kazi ya ujenzi wa Bomba la kutoka Songo
Songo kupitia baharini hadi Somanga Fungu, lenye urefu wa kilometa 25.6
imekamilika kwa asilimia 100. Kwa ujumla ujenzi wa
Bomba la gesi asilia umekamilika kwa asilimia 78.
Kazi ya kuweka mkongo wa mawasiliano (Fibre Optic Cable)
inafanyika sambamba na ufukiaji wa Bomba. Aidha, mtambo wa kuchimbia mabomba
katika Mto Rufiji (horizontal drilling) uliletwa
nchini Mwezi Aprili, 2014.
89.
Mheshimiwa Spika, shughuli
za ujenzi wa mitambo ya kusafisha gesi asilia katika eneo la Madimba, Mtwara na
Songo Songo, Lindi zinaendelea.
Hadi kufikia Mwezi Aprili, 2014 ujenzi wa nyumba za kuishi wafanyakazi kwa eneo
la Madimba ulikuwa umekamilika kwa asilimia 90
na Songo Songo kwa asilimia 78. Aidha, ujenzi wa
misingi (foundations) ambako mitambo ya kusafisha gesi asilia
itafungwa umekamilika. Vilevile, utengenezaji (manufacturing)
wa mitambo yote ya kusafisha gesi
asilia umekamilika kwa asilimia 60. Mitambo hiyo itaanza
kuwasili nchini kuanzia Mwezi Julai, 2014 kutoka Jamhuri ya Watu wa China. Kwa
ujumla maandalizi ya kufunga mitambo ya kusafisha gesi asilia yamekamilika kwa asilimia
45.
90.
Mheshimiwa Spika, Serikali imedhamiria
kwa dhati kukamilisha ujenzi wa Bomba ifikapo Mwezi Julai, 2014 na mitambo ya kusafisha gesi asilia ifikapo Mwezi
Desemba, 2014. Mradi huu utagharimu Dola za Marekani bilioni 1.2, sawa na takriban Shilingi trilioni 2. Fedha za ndani
zilizotengwa kwa Mwaka 2014/15 ni Shilingi bilioni 148,
sawa na Dola za Marekani
milioni 90.
Usambazaji
wa Gesi Asilia Lindi, Mtwara na Pwani
91.
Mheshimiwa Spika, mradi wa ujenzi wa Bomba la gesi asilia kutoka
Mtwara hadi Dar es Salaam umeweka matoleo (tie - out) kwa
ajili ya kusambaza gesi asilia katika miji mikubwa yote ambapo Bomba hilo
linapita ikiwemo miji ya Mtwara, Lindi, Kilwa na Kisarawe. Serikali itawezesha
ujenzi wa miundombinu ya kusambaza gesi asilia kwa ajili ya mitambo ya kufua
umeme, matumizi viwandani, Taasisi mbalimbali, majumbani na kwenye magari
katika Mikoa hiyo. Katika Mwaka 2013/14, zabuni ilitangazwa kwa ajili ya kumpata
Mshauri atakayefanya upembuzi yakinifu wa mradi na Tathmini ya Athari za
Mazingira na Kijamii (ESIA) kwa ajili ya usambazaji wa gesi asilia katika miji
ya Mtwara, Lindi, Kilwa na Kisarawe. Mshauri amepatikana na anatarajiwa kuanza
kazi Mwezi Juni, 2014 na kukamilisha kazi hiyo baada ya miezi mitatu (3). Kazi
zitakazofanyika katika Mwaka 2014/15 ni pamoja na utafiti wa mahitaji ya gesi asilia katika viwanda,
Taasisi mbalimbali, magari na majumbani; na mfumo na miundombinu ya kufikisha
gesi asilia katika maeneo yatakayoainishwa. Aidha, baadhi ya viwanda na kampuni
mbalimbali zimeanza majadiliano ya mikataba na TPDC ili kupatiwa gesi asilia.
Kampuni hizo ni pamoja na Dangote (Mtwara) na MEIS (Lindi) kwa ajili ya
uzalishaji wa saruji; na Kilwa Energy (Kilwa) kwa ajili ya kufua umeme.
92.
Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2014/15,
Serikali itaendelea kusimamia ukamilishaji wa upembuzi yakinifu wa mradi.
Vilevile, Serikali itampata mshauri atakayefanya usanifu na michoro (Detailed Engineering
Design and Drawings) ya miundombinu pamoja
na vituo vya kujazia gesi asilia iliyoshindiliwa (Compressed Natural Gas) kwenye magari.
Mshauri huyo ataongoza
zoezi la kumpata mkandarasi na atasimamia ujenzi wa mradi. Fedha za ndani
zilizotengwa kwa ajili ya kutekeleza kazi hizo ni Shilingi bilioni 5.
Shughuli za Utafutaji wa Mafuta
93.
Mheshimiwa Spika, utaratibu wa awali wa kupata Kampuni za
kuja kufanya utafiti wa mafuta na gesi asilia nchini toka miaka ya 1952 ulikuwa
kwa Kampuni husika kuomba eneo inalolitaka kufanya utafiti na kupewa bila
ushindani. Kwa wakati huo, maeneo yaliyohusika yalikuwa ya nchi kavu na siyo
kwenye kina kirefu cha Bahari. Kuanzia Mwaka 1973 hadi 1999, TPDC ilianza
kujitangaza Kimataifa kwa nia ya kupata wawekezaji na kushawishi Kampuni za nje
zenye uwezo, kuja nchini kwa ajili ya utafutaji mafuta. Kampuni zilizojitokeza
ni: Agip ya Italia; Aminex, BP,
Heritage, Petrodel, Tullow za Uingereza; Ammoco na Exxon za Marekani; Artumas
ya Canada; Beach Petroleum, Ndovu Resources na Swala za Australia; Bubin ya
Ireland; KUFPEC na IEDC za Kuwait; Maurel and Prom ya Ufaransa; Motherland ya
India; Shell ya Uholanzi; na Tanganyika Oil ya Misri yalikuja nchini kufanya
utafiti katika nyakati tofauti. Tafiti hizo zilifanyika nchi kavu na Bahari ya
kina kifupi.
94.
Mheshimiwa Spika, vitalu kwenye kina
kirefu cha Bahari vilianza kutangazwa Mwaka 2000. Katika zabuni ya kwanza, Kampuni
moja ilipatikana ambayo ni Petrobras ya Brazil.
Katika Duru ya Pili iliyofanyika Mwaka 2001, Kampuni moja
ilipatikana ambayo ni Shell ya Uholanzi. Katika Duru ya Tatu iliyofanyika Mwaka
2004, Kampuni tatu zilipatikana ambazo ni Ophir (Uingereza),
Statoil (Norway) na Petrobras (Brazil). Duru zote hizo tatu zilifanyika nje
ya nchi.
95.
Mheshimiwa Spika,
katika Mwaka 2013/14, Serikali ilidurusu Mwongozo wa Mkataba wa Uzalishaji na
Ugawanaji Mapato yatokanayo na Mafuta na Gesi Asilia (Model Production Sharing
Agreement – MPSA, 2013). Kufuatia Mwongozo huo, uzinduzi
wa Duru ya Nne ya Kuitisha Zabuni za Utafutaji Mafuta (Fourth Petroleum
Licensing Round) kwenye vitalu saba (7)
katika Bahari Kuu na kimoja (1) kwenye Ziwa Tanganyika Kaskazini ulifanyika
hapa nchini Mwezi Oktoba, 2013. Shughuli hiyo ilizinduliwa rasmi na Mhe. Dkt.
Jakaya Mrisho Kikwete, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Zoezi hilo
lilifanyika kwa mara ya kwanza nchini baada ya kufanyika nje ya nchi mara tatu
mfululizo. Kampuni za ndani na nje
ya nchi zilizokidhi vigezo zilishiriki, ambapo hadi Aprili, 2014 kampuni 19
zilinunua taarifa za vitalu vilivyotangazwa. Zoezi hilo lilifungwa tarehe 15
Mei, 2014 ambapo kampuni 5 zilirudisha nyaraka za Zabuni (bidding documents), limesaidia kuitangaza Tanzania kimataifa na kutoa fursa
ya Watanzania kushiriki. Katika zabuni hiyo, Kampuni za kitanzania zilipewa
upendeleo maalum wa kisheria wa alama za ziada. Hata hivyo, hakuna Kampuni ya
Kitanzania iliyojitokeza kushiriki. Nitoe wito kwa Kampuni za Kitanzania
kujitokeza kushiriki katika fursa mbalimbali zilizopo katika Sekta Ndogo ya
Mafuta na Gesi Asilia. Hii
itaondoa dhana kwamba uwekezaji katika sekta hiyo ni kwa ajili ya
kampuni za nje pekee. Nashauri Kampuni
nyingine za kitanzania ziige mfano wa Kampuni za Swala Energy na Petrodel za
nchini mwetu ambazo zinafanya shughuli za utafutaji wa mafuta na gesi asilia
nchini.
Ugunduzi wa Gesi Asilia
96.
Mheshimiwa Spika, katika
Mwaka 2013/14, jumla ya futi za ujazo trilioni 4.8
za gesi
asilia ziligunduliwa katika visima vya Mkizi – 1, Ngisi – 1, Tangawizi – 1, na
Mlonge – 1. Hadi
kufikia Mwezi Aprili 2014, kiasi cha gesi asilia
kilichogunduliwa nchini ni futi za ujazo trilioni 46.5, sawa na mapipa ya mafuta bilioni 8.37. Kiasi hiki ni takriban
mara tano ya gesi asilia iliyokuwepo Mwaka 2005 wakati Serikali ya Awamu ya Nne
inaingia madarakani. Kati ya kiasi
hicho, asilimia 83 ni kutoka kina kirefu cha
maji Baharini na asilimia 17 ni
nchi kavu.
Mradi wa Uzalishaji Mbolea kwa Kutumia
Gesi Asilia
97.
Mheshimiwa Spika,
katika kutekeleza kauli mbiu ya “Kilimo Kwanza” Serikali itawezesha uanzishwaji
wa kiwanda cha mbolea kitakachotumia malighafi ya gesi asilia inayopatikana hapa nchini.
Jitihada hizi ni katika kuhakikisha upatikanaji mzuri na wa uhakika wa mbolea
ili kuboresha kilimo chetu. Mwezi Agosti, 2013 Serikali kupitia TPDC ilitangaza
zabuni ya kujenga kiwanda cha mbolea na
kampuni 19 zilionesha nia. Kati ya Kampuni hizo, 12 zilikidhi vigezo
na hivyo kupelekewa Request for Proposal (RFP)
ili ziwasilishe project write-up kwa ajili ya uchambuzi.
Kampuni 6 zimeleta mapendekezo ya utekelezaji wa mradi
na uchambuzi unaendelea wa kumpata mshindi. Taratibu za kumpata mwekezaji kwenye kiwanda cha
mbolea zitakamilika kabla ya Julai, 2014 na maandalizi ya ujenzi yataanza Mwaka
2014/15.
98.
Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea
kuratibu uanzishwaji wa Hifadhi ya Taifa ya Mafuta kwa kuandaa Rasimu ya Kanuni za Uratibu wa Mafuta ya Akiba (National
Strategic Petroleum Reserve Regulations).
Kampuni ya Oman Trading International (OTI) ilishinda zabuni ya kuiuzia mafuta
TPDC. Kampuni ya OTI imekubali kuleta mafuta kwa mkopo, ambapo TPDC itailipa
Kampuni hiyo fedha baada ya kuuza mafuta hayo. Lengo la
utaratibu huu ni kuhakikisha nchi yetu inakuwa na mafuta ya akiba wakati wote.
Katika Mwaka 2014/15, Serikali itakamilisha maandalizi ya Kanuni za Uratibu wa
Mafuta ya Akiba na kuanza utekelezaji wake.
Hisa za Serikali
katika Kampuni ya Puma Energy Limited, TAZAMA na TIPER
99.
Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2013/14, Serikali
iliendelea kusimamia na kushiriki katika shughuli za uendeshaji wa Kampuni za Puma Energy Tanzania
Limited (asilimia 50), Tanzania Zambia Pipeline Limited (TAZAMA, asilimia
30) na Tanzania International Petroleum Reserve (TIPER, asilimia
50). Gawiwo litakalolipwa Serikalini katika kipindi husika kutoka Kampuni ya Puma
Energy Tanzania Limited ni Shilingi bilioni 3.28. Kampuni za TAZAMA na TIPER
hazijawasilisha gawiwo Serikalini kwa kuwa bado hazijakamilisha hesabu zake za
Mwaka 2013. Serikali itaimarisha usimamizi wa Kampuni hizo ili kuongeza gawiwo
katika miaka ijayo. Kufuatia kumalizika
kwa vipindi vya Wajumbe wa Bodi hizi tatu (3), Serikali imeteua wajumbe wapya
wa Bodi hizo Mwezi Machi, 2014.
Sera na Sheria katika Sekta Ndogo ya Mafuta na Gesi Asilia
100.
Mheshimiwa Spika,
kama nilivyoahidi katika Hotuba yangu ya Mwaka 2013/14 mbele ya Bunge lako
Tukufu, Serikali iliidhinisha Sera ya Gesi Asilia Mwezi Oktoba, 2013 ili
kuimarisha usimamizi wa Sekta Ndogo ya Gesi Asilia. Aidha, Rasimu ya Sera ya Uwezeshaji na Ushirikishaji
Wazawa (Local Content Policy)
ziliandaliwa. Lengo la Sera hiyo ni kuhakikisha kuwa Watanzania wanashiriki
ipasavyo katika shughuli zote za rasilimali za mafuta na gesi asilia kwa
manufaa ya kizazi cha sasa na vijavyo. Rasimu ya Sera hiyo imesambazwa kwa
wadau mbalimbali wakiwemo Waheshimiwa Wabunge, Wizara, Taasisi za Serikali na
Washirika wa Maendeleo ili kupata maoni yao. Wizara ingependa kupata maoni yenu
kabla ya tarehe 30 Juni, 2014.
101.
Mheshimiwa Spika, Vilevile, Serikali imekamilisha Rasimu ya Kwanza ya
Sera ya Petroli itakayotoa mwongozo kuhusu
usimamizi wa shughuli za utafutaji, uzalishaji na
ugawanaji mapato yanayotokana na Mafuta na Gesi Asilia pamoja na usafishaji,
uhifadhi, usafirishaji na usambazaji mafuta. katika Mwaka 2014/15 Rasimu hizo
zitawasilishwa katika Mamlaka husika kwa ajili ya kuidhinishwa. Kukamilika kwa
Sera husika kutaimarisha usimamizi wa Sekta Ndogo ya Mafuta na Gesi Asilia kwa
maendeleo ya kizazi cha sasa na vijavyo.
102.
Mheshimiwa Spika, napenda
kulijulisha Bunge lako Tukufu kuwa Rasimu ya Sheria ya Gesi Asilia imekamilika.
Rasimu imepelekwa kwa wadau ili kupata maoni yao kabla ya kuikamilisha na
kuiwasilisha katika kikao cha Bunge cha
Mwezi Novemba, 2014.
Kudurusu Muundo wa TPDC
103.
Mheshimiwa Spika, kutokana
na kuongezeka kwa shughuli za utafutaji mafuta na gesi asilia, uendelezaji wa matumizi ya gesi asilia na kusudio la kuongeza
ufanisi katika utendaji wa TPDC, Bodi ya Wakurugenzi na Menejimenti ya TPDC
iliwasilisha Serikalini mapendekezo ya muundo mpya wa Shirika Mwezi Mei, 2013.
Serikali ilitathmini mapendekezo hayo kwa kuangalia miundo na uzoefu kutoka
nchi mbalimbali zilizonufaika na uwepo wa rasilimali ya mafuta na gesi asilia.
Baada ya tathmini hiyo Mwezi Aprili, 2014, Serikali kupitia Msajili wa Hazina
iliidhinisha muundo mpya wa TPDC ili kuliwezesha Shirika hilo kushiriki
kikamilifu kwenye shughuli zote za utafutaji, uzalishaji na usambazaji wa mafuta na gesi asilia (Upstream,
Mid and Down-streams). Ili kutekeleza majukumu hayo, TPDC
itaanzisha kampuni tanzu zikiwemo Kampuni ya Usafirishaji na Usambazaji wa Gesi
Asilia (GASCO) na Kampuni ya Mafuta (COPEC). Ushiriki wa TPDC katika maeneo
hayo utaimarisha mapato ya Serikali kwenye shughuli za mafuta na gesi asilia
pamoja na kuboresha usimamizi wa Sekta Ndogo ya Mafuta na Gesi Asilia.
Shughuli za
Udhibiti wa Sekta ya Nishati
104.
Mheshimiwa Spika, katika
Mwaka 2013/14, EWURA iliendelea kusimamia shughuli za udhibiti katika Sekta
Ndogo za Umeme, Mafuta na Gesi Asilia. Serikali kupitia Kampuni ya Petroleum Importation
Coordinator Limited (PICL) iliendelea kusimamia Mfumo wa Uagizaji wa Mafuta kwa
Pamoja (BPS). Kati ya Mwezi Julai, 2013 na Aprili, 2014 mafuta yaliendelea
kupatikana kulingana na mahitaji yetu. Katika kipindi cha Januari hadi Desemba,
2013 jumla ya lita bilioni 4.66 za aina mbalimbali za mafuta ziliingizwa nchini
kupitia Bandari ya Dar es Salaam. Kati ya kiasi hicho, lita bilioni 2.76 sawa
na asilimia 59 yalikuwa ni mafuta kwa
matumizi ya ndani na kiasi cha lita bilioni 1.90, sawa na asilimia 41 yalikuwa kwa ajili ya nchi jirani. Aidha, kutokana na
kuimarika kwa mfumo huo, wastani wa gharama (weighted average premium) za uagizaji mafuta ya petroli zimeshuka kutoka Dola
za Marekani 59 kwa tani Mwezi Novemba, 2011 hadi
Dola za Marekani 36 kwa tani Mwezi Aprili, 2014.
105.
Mheshimiwa Spika, katika Mwaka
2013/14 Serikali kupitia EWURA iliendelea kudhibiti ubora wa bidhaa za
mafuta ya petroli nchini na kuchukua hatua stahiki za kisheria kwa wale
waliothibitika kutozingatia viwango vilivyowekwa. Aidha, EWURA iliendelea kusimamia bei za
mafuta katika soko la ndani ili kuhakikisha bei hizo zinaendana na mabadiliko
ya bei katika Soko la Dunia na mwenendo wa thamani ya Shilingi ya Tanzania
ikiwianishwa na Dola ya Marekani. Bei ya mafuta ya petroli nchini imeendelea
kushuka kutokana na kuimarika kwa Mfumo wa Uagizaji Mafuta kwa Pamoja na
shughuli za udhibiti.
106.
Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2013/14,
Idara ya Uchumi ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam ilifanya tathmini kuhusu
manufaa ya uwekaji vinasaba katika mafuta, uanzishwaji wa matumizi ya Kanuni ya
Kukokotoa Bei Kikomo pamoja na Mfumo wa Uagizaji Mafuta kwa Pamoja. Matokeo ya
tathmini hiyo yanaonesha kuwa nchi imenufaika na shughuli za udhibiti wa Sekta
Ndogo ya Mafuta kwa kupunguza uchakachuaji ambapo kati ya Mwaka 2010 na 2011,
mapato ya Serikali yameongezeka kwa Shilingi bilioni 33.5. Aidha, kutokana na udhibiti wa uuzaji mafuta yaliyoagizwa
kwa ajili ya nchi jirani (transit)
mapato ya Serikali yameongezeka kwa Shilingi bilioni 468.5 kwa kipindi cha kati ya Mwaka 2010/11 na
2012/13.Vilevile, shughuli za udhibiti zimeongeza ufanisi katika uagizaji
mafuta na matumizi ya miundombinu bandarini; pamoja na kuondoa upandaji holela
wa bei za mafuta nchini.
107.
Mheshimiwa Spika, katika
Mwaka 2014/15 EWURA itaendelea kuboresha usimamizi na udhibiti wa ubora wa
mafuta pamoja na Mfumo wa Uagizaji wa Mafuta kwa Pamoja. Aidha, katika Mwaka
2014/15, Serikali itaboresha muundo wa PICL ili kuongeza ufanisi kwa kuzingatia
uzoefu wa nchi jirani za Kenya na Msumbiji zinazotumia mfumo kama huo.
Changamoto katika Sekta ya Nishati na Mipango ya Kukabiliana Nazo
108. Mheshimiwa Spika, pamoja na mafanikio yaliyopatikana,
Sekta ya Nishati imeendelea kukabiliwa na changamoto mbalimbali zikiwemo
upatikanaji wa fedha za kutosha kutekeleza miradi; mahitaji makubwa ya umeme;
kupunguza upotevu wa umeme; vivutio mwafaka kwa wawekezaji; gharama kubwa za
umeme unaofuliwa kutokana na mafuta; uzingatiaji matumizi bora ya nishati; na
mabadiliko ya tabia nchi.
109. Mheshimiwa Spika, Mpango na Bajeti ya Mwaka
2014/15 katika Sekta ya Nishati unalenga kukabiliana na changamoto hizo kwa
kutekeleza mipango na miradi iliyotajwa katika Hotuba hii, pamoja na kudurusu, kutunga
na kusimamia Sera na Sheria
zinazohusu Sekta ya Nishati kwa manufaa ya Watanzania wa kizazi cha sasa na
vizazi vijavyo.
SEKTA YA
MADINI
Mafanikio katika Sekta ya Madini kwa
Mwaka 2013/14
110. Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha Mwaka
2013/14, Wizara iliendelea kutekeleza vipaumbele vyake katika Sekta ya Madini.
Mafanikio yaliyopatikana katika Sekta hii ni pamoja na yafuatayo: kukamilika kwa zoezi la high
resolution airborne geophysical survey katika Mikoa ya Dodoma, Manyara,
Mbeya, Morogoro, Pwani, Singida, Tabora na Tanga Mwezi Oktoba, 2013; kukamilika
kwa ground geophysical survey (kwenye Quarter Degree Sheet (QDS) - 7, geological
mapping kwa QDS 18 na geochemical mapping kwa QDS 7) katika maeneo ya Dodoma, Mbeya, Morogoro, Njombe, Pwani,
Singida na Tanga; na kusainiwa kwa Makubaliano ya Awali (MoU) na Serikali ya
Finland kwa ajili ya mkopo nafuu kuwezesha utafiti wa kijiosayansi na maeneo
yenye madini katika Mikoa ya Lindi, Mtwara na Pwani utakaoanza Mwezi Agosti,
2015.
111. Mheshimiwa Spika, mafanikio mengine ni
kukamilika kwa Rasimu ya Sheria ya kusimamia shughuli za Mpango wa Uhamasishaji
Uwazi na Uwajibikaji katika Tasnia ya Uziduaji (TEITI); kusainiwa kwa makubaliano
kwa STAMICO kumiliki mgodi wa dhahabu wa Tulawaka (Biharamulo) kutoka Kampuni
ya African Barrick Gold; kutolewa kwa leseni nane (8) za uchenjuaji madini
katika Wilaya za Bunda (2), Misungwi (1), na Mkoa wa Geita (5); Serikali
kukusanya Shilingi bilioni 50.6 kama Kodi ya Mapato kutoka Kampuni ya Geita Gold
Mining Limited na Shilingi bilioni 3.38 kutoka Kampuni ya Resolute
Tanzania Limited; na malipo ya jumla ya Shilingi milioni 178.9 kwa Serikali kama Alternative
Minimum Tax kutoka Kampuni ya Williamson Diamonds Limited.
112. Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea
kusimamia upatikanaji wa malipo ya ushuru wa huduma (service levy) kwa Halmashauri za
Geita, Kahama, Kishapu, Nzega na Tarime. Mapato yaliyolipwa tangu migodi hiyo
ianze hadi Aprili, 2014 kwa Halmashauri hizo ni jumla ya Dola za Marekani
milioni 10.58, sawa na Shilingi bilioni 17.35 kwa mchanganuo ufuatao: Mgodi wa
Geita Dola za Marekani milioni 1.6, sawa na Shilingi bilioni 2.62 kwa Halmashauri ya Geita;
Mgodi wa Bulyanhulu Dola za Marekani milioni 2.53, sawa na Shilingi bilioni 4.15 kwa Halmashauri ya Kahama; Mgodi
wa Buzwagi Dola za Marekani
800,000, sawa na Shilingi bilioni 1.31 kwa Halmashauri ya Kahama; Mgodi
wa North Mara Dola za Marekani milioni 2.4, sawa na Shilingi bilioni 3.94 kwa Halmashauri ya Tarime; Mgodi wa Resolute Dola za
Marekani milioni 3.04, sawa na Shilingi bilioni 4.99 kwa Halmashauri ya Nzega;
na Mgodi wa Almasi wa Mwadui Dola za Marekani 202,469 sawa na Shilingi milioni 332.05 kwa Halmashauri ya Kishapu.
113. Mheshimiwa Spika, Mafanikio mengine ni
kukusanywa kwa mrabaha wa Shilingi bilioni 116.64 kutokana na madini
yaliyozalishwa na kuuzwa; kukamilika kwa Mpango wa Uendelezaji wa Uchimbaji
Mdogo wa Madini; kuandaliwa kwa
Mtaala wa utafiti wa madini na programu za uchimbaji mdogo wa madini; kufadhili
mafunzo ya wanafunzi 148 katika
ngazi ya cheti na diploma katika fani za Madini, Petroli na Gesi Asilia;
kuanza ujenzi wa madarasa mawili (2) katika Chuo cha Madini Dodoma kila moja
likiwa na uwezo wa kuchukua wanafunzi 140; na kuanzishwa kwa ofisi mbili za
Wakala wa Ukaguzi wa Madini Tanzania (TMAA) katika Mikoa ya Arusha na Mbeya.
114. Mheshimiwa Spika, kwa Mwaka 2013/14,
Serikali kwa upande wa Sekta ya Madini iliendelea kutekeleza majukumu yake kwa
kufuata Mpango Kazi uliowekwa na Wizara. Katika Mwaka 2014/15 maeneo mahsusi
yatakayoleta matokeo makubwa katika Sekta hii ni pamoja na: kuimarisha
makusanyo ya maduhuli yatokanayo na madini; kuendeleza shughuli za uchimbaji
mdogo; kuboresha utoaji na usimamizi wa leseni za madini; kuimarisha usimamizi
wa afya, usalama na utunzaji wa mazingira migodini; kuhamasisha shughuli za
uongezaji thamani madini; kuimarisha usimamizi wa biashara ya madini; kuwezesha Mashirika na Taasisi za
Serikali katika Sekta ya Madini; na kuendelea kuboresha mazingira ya kazi
katika Ofisi za Madini za Kanda.
Mauzo na Thamani ya Madini yaliyouzwa nje ya Nchi
115. Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2013/14
Wizara iliendelea kusimamia shughuli za utafutaji, uchimbaji na biashara ya
madini nchini kwa lengo la kuongeza mchango wa Sekta hii kwenye Pato la Taifa.
Kutokana na mipango na miradi mbalimbali inayoendelea kutekelezwa na Serikali,
Sekta ya Madini imeendelea kuwa chachu katika ukuaji wa uchumi nchini. Hata
hivyo, Sekta ya Madini ni mojawapo ya sekta zilizoathiriwa kwa kiasi kikubwa na
mtikisiko wa uchumi Duniani ambao uliambatana na kushuka kwa bei ya madini
mbalimbali, hususan dhahabu na pia kushuka kwa upatikanaji wa mitaji ya nje
(FDI).
116. Mheshimiwa Spika, thamani ya mauzo ya
madini nje ya nchi yaliyouzwa na Migodi Mikubwa ya Dhahabu iliongezeka kutoka Dola
za Marekani milioni 640 Mwaka 2005 hadi kufikia Dola za Marekani bilioni 1.79 Mwaka 2013. Uzalishaji
wa madini ulipungua kutoka wakia 1,398,406 Mwaka 2005 hadi wakia 1,244,743 Mwaka
2013, sawa na punguzo la asilimia 10.9. Aidha, asilimia 69.27 ya mauzo ya madini yote
ya migodi mikubwa nje ya nchi kwa Mwaka 2013 ilitokana na mauzo ya dhahabu.
117. Mheshimiwa Spika, kwa upande wa uzalishaji
na mauzo ya madini katika migodi mikubwa nchini katika kipindi cha Mwaka 2013,
jumla ya wakia milioni 1.24 za dhahabu, wakia 380,000 za fedha na ratili
milioni 17.70 za shaba zilizalishwa na kusafirishwa nje ya nchi kutoka migodi
mikubwa ya Bulyanhulu, Buzwagi, Geita, Golden Pride, New Luika, North Mara na
Tulawaka. Jumla ya thamani ya madini hayo ni Dola za Marekani bilioni 1.79 pungufu kwa asilimia
17.7
ukilinganisha na mauzo ya madini yaliyofanywa na migodi hiyo kwa Mwaka 2012 ya Dola
za Marekani bilioni 2.17. Vilevile, jumla ya karati 158,562 za almasi na gramu milioni
3.24 za Tanzanite zilizalishwa na migodi ya Mwadui na TanzaniteOne, sawia. Mauzo yote ya almasi na
Tanzanite yaliyofanywa na migodi hiyo kwa Mwaka 2013 yalifikia Dola za
Marekani milioni 50.53. Mrabaha uliolipwa Serikalini na wamiliki wote wa migodi
mikubwa nchini katika kipindi hicho ni Dola za Marekani milioni 72.90, sawa na Shilingi
bilioni 116.64. Mgodi wa Tulawaka uliopo Wilaya ya Biharamulo, Mkoa wa Kagera ulifungwa
rasmi Mwezi Julai, 2013. Aidha, mgodi wa Golden Pride uliopo Wilaya ya Nzega,
Mkoa wa Tabora ulifungwa rasmi Mwezi Februari, 2014. Ni wazi kuwa, kufungwa kwa
migodi hiyo kutapunguza uzalishaji wa dhahabu na mapato ya Serikali.
Kuimarisha
Makusanyo ya Maduhuli Yatokanayo na Madini
118. Mheshimiwa Spika, katika kuimarisha
makusanyo ya maduhuli ya Serikali yatokanayo na madini, Wizara ililenga kukusanya
kiasi cha Shilingi bilioni 199.96 katika Mwaka 2013/14. Hadi kufikia tarehe 23 Mei,
2014 kiasi cha Shilingi bilioni 137.9 kimekusanywa, sawa na asilimia
69 ya
lengo. Kushuka kwa makusanyo
hayo kumetokana na kushuka kwa bei ya dhahabu katika Soko la Dunia.
119. Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2014/15
Serikali inategemea kukusanya jumla ya Shilingi bilioni 209.96 kutoka katika Sekta ya
Madini. Ili kufikia lengo hilo, Wizara itaimarisha ukaguzi na usimamizi wa
Sekta ya Madini ili kuhakikisha kwamba wachimbaji wakubwa, wa kati, wadogo na
wafanyabiashara wa madini wanalipa ada za leseni na mrabaha stahiki. Pia,
Wizara itafungua ofisi mpya mbili (2) za Kanda ambazo ni Kanda ya Ziwa Viktoria
Mashariki, ambayo Makao Makuu yake yatakuwa Musoma; na Kanda ya Ziwa Nyasa ambayo
Makao Makuu yake yatakuwa Songea. Aidha, Ofisi nne (4) za Maafisa Madini Wakazi
zitafunguliwa huko Bariadi, Moshi, Nachingwea na Njombe. Kufunguliwa kwa Ofisi
hizo kumelenga kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi na ukusanyaji wa maduhuli
ya Serikali.
120. Mheshimiwa Spika, Wizara pia itaendelea
kutekeleza mpango wake wa kuanzisha vituo vya ukaguzi wa madini ya ujenzi na
viwandani katika Kanda zote za Madini nchini. Mpango huo umewezesha jumla ya Shilingi
bilioni 1.71 kukusanywa Mwaka 2012/13 kutoka Kanda za Mashariki, Ziwa Viktoria, Kati na
Kusini ikilinganishwa na wastani wa Shilingi milioni 4 kwa mwaka zilizokuwa
zinakusanywa hapo awali katika Kanda hizo kabla ya mpango huo kuanzishwa. Aidha,
Wizara itaimarisha usimamizi wa uchimbaji na biashara ya Tanzanite ili
kuhakikisha kuwa Taifa linapata manufaa stahiki ya uvunaji wa madini hayo
yanayopatikana Tanzania pekee.
Majadiliano na Kampuni za Madini
121. Mheshimiwa Spika, katika Hotuba yangu ya
Mwaka 2013/14, niliahidi kuendelea kufanya majadiliano na baadhi ya wamiliki wa migodi mikubwa nchini
wenye Mikataba ya Uendelezaji Migodi (Mineral Development Agreements – MDAs). Majadiliano hayo ni
kuhusu kubadilisha baadhi ya vipengele vya mikataba
ili kuleta mapato zaidi ya fedha kwa Taifa.
122.
Mheshimiwa Spika, Serikali
imefanikiwa kujadiliana na Kampuni ya African Barrick Gold (ABG) inayomiliki migodi mikubwa ya Bulyanhulu
katika Halmashauri ya Msalala, Wilaya ya Kahama, Buzwagi katika Halmashauri ya
Mji wa Kahama na North Mara katika Halmashauri ya Wilaya ya Tarime. Napenda
kulitaarifu Bunge lako Tukufu kuwa kutokana na majadiliano hayo, Kampuni hiyo
imekubali kuwa kuanzia Julai, 2014 italipa asilimia 0.3 ya mapato (turnover) kama ushuru wa huduma (service levy) kwa Halmashauri husika, badala ya malipo ya Dola za Marekani
200,000 kwa mwaka iliyokuwa inalipwa hapo awali kulingana na MDA. Napenda kutumia fursa hii kuipongeza
Kampuni ya ABG kwa uamuzi huo na kuzishauri Kampuni nyingine kuiga mfano huo.
123. Mheshimiwa Spika, Kampuni ya ABG itaendelea kulipa moja kwa
moja Dola za Marekani 200,000 kwa Halmashauri husika na ziada ya malipo
yatakayotokana na asilimia 0.3 ya mapato itawekwa kwenye Mfuko Maalum
utakaoanzishwa na kusimamiwa na Halmashauri husika. Mfuko huo utatumika kwa
ajili ya kuendeleza miundombinu kwenye maeneo ya Halmashauri hizo katika nyanja
za afya, barabara, elimu, maji na nishati. Ili kuhakikisha kuwa fedha hizo zinatumika
kama ilivyokusudiwa, Halmashauri husika italazimika kuwasilisha kwa Wizara ya
Nishati na Madini Mpango wa utekelezaji kwa ajili ya idhini. Lengo ni
kuhakikisha kuwa fedha hizo zinatumika kwa miradi ya maendeleo tu.
Kuendeleza Shughuli za Uchimbaji Mdogo wa Madini
124. Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2013/14,
shughuli za uchimbaji mdogo zimeendelea kukua na kutoa mchango mkubwa katika kupunguza
umaskini, ambapo zaidi ya Watanzania milioni moja wamejiajiri katika shughuli
hizo. Katika kutekeleza Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya Mwaka 2010 – 2015, Ibara ya
56 (d) ambayo pamoja na mambo mengine, inasisitiza juu ya kuwawezesha
wachimbaji wadogo kupata mikopo na mitaji, Wizara imeendelea kutoa mikopo ya
masharti nafuu na ruzuku kwa wachimbaji wadogo kupitia Benki ya TIB. Mwezi
Aprili, 2014 Mhe. Mizengo Kayanza Peter Pinda, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania, alikabidhi hundi zenye jumla ya Dola za Marekani
537,000
sawa na Shilingi milioni 880.68 kwa miradi kumi na moja (11) ya wachimbaji wadogo
ambayo ilikidhi vigezo vya kupata ruzuku. Vilevile, Wizara inatarajia kuipatia
miradi mingine 18 ya wachimbaji wadogo mikopo yenye jumla ya Shilingi
bilioni 2.3 ifikapo mwishoni mwa Mwezi Juni, 2014. Nawasihi wachimbaji wadogo
kuandaa michanganuo yao ya miradi kwa ajili ya kuomba mikopo na ruzuku kupitia
TIB ili watakaokidhi vigezo wapate ruzuku ama mikopo kwa ajili ya kuendesha
shughuli zao za uchimbaji mdogo kwa tija. Wachimbaji wadogo wanashauriwa
kupata ushauri wa bure wa kitaalamu kutoka Shirika la Taifa la Madini
(STAMICO). Wizara
itaendelea kushirikiana kwa karibu sana na wachimbaji wadogo waaminifu watakaotumia
vizuri ruzuku wanazopewa, na watakaorejesha mikopo na kulipa kodi za Serikali.
125. Mheshimiwa Spika, ili kuendelea
kuwawezesha wachimbaji wadogo kwa mitaji na mikopo, Wizara imetenga kiasi cha Shilingi
bilioni 2.5 katika Bajeti yake ya Mwaka 2014/15 kwa ajili ya kukopesha wachimbaji hao.
Pamoja na fedha hizo za mikopo, Serikali, kupitia Mradi wa Usimamizi Endelevu
wa Rasilimali za Madini (SMMRP) unaofadhiliwa na Benki ya Dunia imetenga jumla ya
Dola za Marekani milioni 3.5, sawa na Shilingi bilioni 5.74 kama ruzuku kwa ajili ya
wachimbaji wadogo, na kiasi cha Dola za Marekani milioni 1.1, sawa na Shilingi
bilioni 1.8 kwa ajili ya kununua mitambo miwili (2) ya uchorongaji miamba (drilling
rigs).
Mitambo hiyo itapelekwa katika Ofisi za Madini za Kanda ya Ziwa (Mwanza) na
Kanda ya Kusini Magharibi (Mbeya) ili kuwezesha utambuzi wa kiasi cha mashapo
yaliyopo katika maeneo ya wachimbaji wa kati na wadogo yaliyogunduliwa kuwa na
madini. Kiasi hicho kinafanya jumla ya fedha zilizotengwa kwa Mwaka 2014/15 kwa
ajili ya wachimbaji wadogo kufikia jumla ya Shilingi bilioni 10.04.
126. Mheshimiwa Spika, katika juhudi za
kuendeleza shughuli za uchimbaji mdogo, kwa Mwaka 2013/14 Wizara iliendelea
kutoa mafunzo kwa nadharia na vitendo kwa wachimbaji wadogo ambapo jumla ya
wachimbaji wadogo 420 walipatiwa mafunzo katika maeneo ya Handeni na Kilindi
(250), Musoma (90) na Tunduru (80). Pia, katika kupanua wigo wa kutoa elimu kwa
wadau wengi zaidi, vitabu 2,000 vya kuelimisha wachimbaji wadogo vilichapishwa
na kusambazwa. Kwa Mwaka 2014/15, Wizara imepanga kutoa mafunzo kwa nadharia na
vitendo kwa wachimbaji wapatao 1,000. Vilevile, Wizara itaendelea kutoa huduma
za ugani ili kuboresha utendaji kazi wa wachimbaji wadogo nchini.
127. Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2013/14
jumla ya maeneo 10 yenye ukubwa wa hekta 67,677.61 yametengwa kwa ajili ya
wachimbaji wadogo. Maeneo hayo ni Nyamwironge (Kakonko), Ibaga (Mkalama),
Makanya (Same), Mwajanga (Simanjiro), Itumbi B na Saza (Chunya), Ilujamate
(Misungwi), Kalela/Kigogwe/Samwa (mpakani mwa Wilaya za Kasulu, Buhigwe na
Kigoma Vijijini), Maguja (Nachingwea) na Nyangalata (Kahama/Nyang’hwale). Jumla
ya maeneo yaliyotengwa hadi sasa kwa ajili ya wachimbaji wadogo ni 25 yenye
ukubwa wa kilomita za mraba 2,166.24. Aidha, jumla ya viwanja 8,800 vyenye
ukubwa wa jumla ya kilomita za mraba 2,047.14 vimegawiwa kwa wachimbaji wadogo.
128. Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2014/15,
Wizara itaendelea kutenga maeneo kwa ajili ya wachimbaji wadogo kadri
itakavyoonekana inafaa. Pamoja na kuongeza ajira kwa wachimbaji wadogo,
utengaji wa maeneo unalenga kupunguza migogoro ya maeneo kati ya wachimbaji
wadogo na wakubwa na kati ya wachimbaji wadogo na wadogo (wenyewe kwa wenyewe).
Vilevile, Wizara itafanyia tathmini maeneo yote yaliyotengwa kwa ajili ya
wachimbaji wadogo na yatakayobainika kuwa hayafanyiwi kazi yatatenguliwa na
kugawiwa kwa waombaji wengine kwa mujibu wa Sheria.
Kuboresha Utoaji na Usimamizi wa Leseni za Madini
129. Mheshimiwa Spika, katika kuboresha mfumo
wa utoaji wa leseni za madini, Wizara iliwezesha wamiliki wa leseni kupata
taarifa za leseni kupitia tovuti maalum ya leseni (Mining Tenements Portal) na pia kuwawezesha
wateja kupokea taarifa za maombi kupitia ujumbe mfupi wa simu (sms) na barua pepe. Hatua
hizi zimelenga hatimaye kuwawezesha waombaji wa leseni kuwasilisha maombi kwa
njia ya mtandao (on-line applications of mineral rights and payments). Pamoja na maboresho
hayo, Wizara imeendelea kuhakiki taarifa za leseni kwenye mfumo wa utoaji wa
leseni (data cleaning), kuondoa mlundikano wa maombi ya leseni na kuimarisha
miundombinu ya mfumo wa leseni (MCIMS).
130. Mheshimiwa Spika, katika kipindi kati ya
Julai, 2013 na Aprili, 2014 jumla ya maombi 7,640 ya utafutaji na uchimbaji madini
yalipokelewa na kuingizwa kwenye Mfumo wa Utoaji na Usimamizi wa Leseni za
Madini, ikilinganishwa na maombi 9,889 katika Mwaka 2012/13. Kati ya
maombi yaliyopokelewa, 715 ni kwa ajili ya leseni za utafutaji wa madini; 6,909
yalikuwa ni ya uchimbaji mdogo; na 16 ni ya uchimbaji wa kati. Jumla ya maombi
3,994 ya leseni yalikataliwa kwa sababu ya kushindwa kutimiza masharti ya
Sheria ya Madini ya Mwaka 2010. Aidha, jumla ya leseni 5,418 zilitolewa, kati
ya hizo 482 kwa ajili ya utafutaji wa madini; 4,913 za uchimbaji mdogo; 22 za
uchimbaji wa kati; na moja (1) ya uchimbaji mkubwa.
131. Mheshimiwa Spika, hadi kufikia Mwezi
Aprili, 2014 jumla ya leseni hai za madini nchini zilikuwa ni 39,958. Kati ya hizo, leseni za
uchimbaji mkubwa ni 13; uchimbaji wa kati ni 381; uchimbaji mdogo ni 36,094; na
leseni za utafutaji madini ni 3,470. Eneo la leseni hizo zote ni kilometa za
mraba zipatazo 240,000 sawa na asilimia 27 ya eneo lote la nchi kavu ya
Tanzania Bara.
132. Mheshimiwa Spika, wakati Sekta ya Madini
ikiendelea kukua na kuongezeka kwa uwekezaji, imejengeka dhana kwamba
wawekezaji wageni wanamiliki maeneo mengi kuliko Watanzania. Aidha, ipo fikra
kwamba Serikali haijachukua hatua ya kuwawezesha Watanzania kushiriki
kikamilifu katika uwekezaji kwenye Sekta hii muhimu. Ukweli ni kwamba, Watanzania
wanamiliki asilimia 70 ya leseni za madini, wageni asilimia 25 na asilimia 5 ya
leseni hizo zinamilikiwa kwa ubia kati ya Watanzania na wageni.
133. Mheshimiwa Spika, katika kuimarisha
usimamizi wa leseni za madini, Wizara imeendelea kuchukua hatua za kutoa Hati
za Makosa (Default Notices) kwa wamiliki wa leseni za utafutaji na uchimbaji madini
ambao hawatimizi masharti ya leseni. Aidha, Wizara imechukua hatua dhidi ya
wamiliki waliohodhi maeneo makubwa ya leseni za madini nchini. Hadi kufikia Mwezi
Aprili, 2014 Hati za Makosa 336
zilitolewa zikihusisha leseni 253 za utafutaji madini na leseni 83 za uchimbaji
madini. Aidha, jumla ya leseni 174 za utafutaji madini na leseni moja ya
uchimbaji mkubwa wa madini zilifutwa. Vilevile, leseni 78 za utafutaji madini na
leseni 34 za uchimbaji wa kati ziko katika utaratibu wa kisheria wa kufutwa. Kati ya leseni zote
zilizofutwa na zinazotarajiwa kufutwa, leseni 67 ni za wamiliki 10 waliobainika kuhodhi
maeneo makubwa ya leseni za madini. Pamoja na hatua ya kufuta leseni, Wizara pia imechukua hatua ya
kutomilikisha leseni mpya 214 kwa kampuni zenye leseni zinazozidi ukomo wa eneo
la leseni la kilomita za mraba 2,000. Hatua hii imechukuliwa ikiwa ni sehemu ya
usimamiaji wa Sheria ya Madini ya Mwaka 2010.
134. Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2014/15,
Wizara itaendelea kuimarisha Mfumo wa Utoaji na Usimamizi wa Leseni za Madini
ikiwa ni pamoja na kukamilisha uanzishwaji wa Data Recovery Center mjini Morogoro. Kituo
hicho kitaimarisha usalama wa taarifa za leseni. Aidha, Wizara itaanza kupokea
maombi ya leseni na malipo ya ada za leseni kwa njia ya mtandao. Utaratibu huu
utapunguza muda wa kushughulikia maombi ya leseni na kuongeza mapato ya
Serikali. Vilevile, utapunguza ushawishi wa rushwa na upendeleo kwa waombaji wa
leseni za madini. Wizara pia itaendelea kuwachukulia hatua za kisheria wamiliki
wanaokiuka masharti ya leseni zao na wale wanaohodhi maeneo makubwa ya leseni
bila kuyaendeleza.
Kuimarisha
Usimamizi wa Afya, Usalama na Utunzaji wa Mazingira Migodini
135. Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2013/14
Wizara iliendelea kuhakikisha kuwa shughuli za uchimbaji madini zinaendeshwa
kwa kuzingatia Kanuni za Usalama, Afya na Utunzaji wa Mazingira. Hadi kufikia Mwezi
Machi 2014, jumla ya migodi 351 ilikaguliwa, ikijumuisha migodi mikubwa mitano
(5); migodi ya kati 56; na migodi midogo 290. Kaguzi hizo zimesaidia kuimarisha
usalama na afya migodini. Wizara itaendelea kusimamia Sheria ya Madini ya Mwaka
2010 na Kanuni zake kwa kuimarisha ukaguzi katika migodi mikubwa, ya kati na
midogo. Aidha, ukaguzi utafanywa katika maeneo ya uchenjuaji na leseni za
utafutaji wa madini. Pia, leseni za biashara ya madini na maduka ya usonara
yatakaguliwa kwa lengo la kuhakiki ulipaji wa maduhuli ya Serikali.
136. Mheshimiwa Spika, katika kuimarisha
utunzaji wa mazingira katika migodi mikubwa nchini, migodi ya Bulyanhulu,
Buzwagi, Golden Pride, North Mara, Tulawaka na WDL imekamilisha Mipango ya
Ufungaji Migodi (Mine Closure Plans) kwa mujibu wa Kanuni za Usalama,
Afya na Utunzaji wa Mazingira na imeidhinishwa na Kamati ya Kisekta ya Ufungaji
Migodi. Migodi ya Geita na TanzaniteOne imewasilisha Mipango ya Ufungaji Migodi
ili kupitiwa na Kamati ya Kisekta kwa ajili ya uidhinishaji. Migodi ya El Hilal,
New Luika na TANCOAL inatarajiwa kuwasilisha Mipango ya Ufungaji Migodi kabla
ya mwisho wa Mwaka 2014.
137. Mheshimiwa Spika, kufuatia kufungwa kwa
shughuli za uzalishaji katika migodi ya Tulawaka na Golden Pride, Wizara
ilisimamia taratibu za makabidhiano ya mgodi wa Tulawaka kwa STAMICO kupitia
Kampuni yake tanzu ya “STAMIGOLD Mining Company Ltd” ili kuendelea kuchimba
mashapo ya dhahabu yaliyobaki baada ya Kampuni ya ABG kufunga shughuli za
uchimbaji. Pia, taratibu za kufungwa na kukabidhi eneo la mgodi wa Golden Pride
kwa Chuo cha Madini Dodoma zinaendelea.Ukarabati wa maeneo yote yaliyoathiriwa
na shughuli za mgodi huo unaendelea na utakamilika ifikapo Mwezi Desemba, 2014.
Aidha, maandalizi katika eneo la mgodi wa Golden Pride yataanza Mwezi Agosti,
2014 ili kuwezesha Wanafunzi 200 kuanza mafunzo katika eneo hilo. Baada ya
majadiliano ya kina na Serikali, Kampuni ya Resolute imekubali kukipatia Chuo
cha Madini Dodoma Dola za Marekani milioni 1.0, sawa na Shilingi bilioni
1.64 ili
kuendeleza miundombinu ya kuanzisha Kampasi ya Chuo cha Madini kwenye eneo la
mgodi wa Golden Pride na kuimarisha ulinzi. Kwa upande wake, Serikali imetenga Shilingi
bilioni 1.0 katika Bajeti ya Mwaka 2014/15 kwa ajili hiyo.
138. Mheshimiwa Spika, kwa Mwaka 2014/15,
Wizara itaendelea kukamilisha mikataba ya uwekaji wa Hati Fungani ya Ufungaji
Migodi (Rehabilitation Bond for Mine Closure) kwa ajili ya migodi mikubwa
nchini. Aidha, wachimbaji wadogo wataendelea kupewa elimu ya namna ya kuandaa
mipango ya utunzaji wa mazingira (Environmental Protection Plans) ili kutimiza matakwa ya
Sheria ya Madini ya Mwaka, 2010.
139. Mheshimiwa Spika, Wizara imeendelea
kusimamia shughuli za utafutaji na uchimbaji wa madini ya Urani nchini. Hata
hivyo, kumekuwapo na mtazamo hasi kuhusu utafutaji na uchimbaji wa madini ya
Urani nchini. Kutokana na hali hiyo, Wizara kwa kushirikiana na wadau
mbalimbali ilitekeleza mpango wa elimu kwa umma kuhusiana na madini ya Urani na
shughuli za uchimbaji wa madini hayo. Elimu hiyo ilitolewa kwa njia ya
makongamano katika maeneo ya Bahi na Namtumbo ambako shughuli za utafutaji
zinaendelea. Kutolewa kwa elimu hiyo kumewezesha jamii husika kuwa na taarifa
sahihi juu ya madini hayo na faida zake. Katika kipindi cha Mwaka 2014/15,
Wizara itaendelea kutoa elimu kwa jamii kwa njia ya semina na vyombo vya habari
kuhusu uvunaji, uhifadhi, usafirishaji, matumizi ya madini ya Urani.
Usimamizi wa Shughuli za Baruti Nchini
140. Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha Mwaka
2013/14, Wizara iliendelea kuimarisha usimamizi wa uingizaji, usafirishaji,
uhifadhi na matumizi ya baruti nchini. Katika kutekeleza jukumu hilo, katika
kipindi cha kuanzia Julai 2013 hadi Machi 2014, jumla ya tani 15,628.8 za
baruti na fataki 2,177,062 ziliingizwa nchini kwa ajili ya utafutaji wa mafuta na
gesi asilia na uchimbaji wa madini. Vibali 114 vilitolewa kwa ajili ya kuingiza
baruti nchini; vibali 44 vilitolewa kwa ajili ya kusafirisha baruti nje ya nchi;
vibali 85 vya kulipulia baruti; na vibali 12 vya maghala ya kuhifadhia baruti.
Aidha, Wizara ilitoa mafunzo kwa wachimbaji wadogo wa madini wanaotumia baruti
wapatao 420 katika Mikoa ya Mara (90), Ruvuma (80) na Tanga (250). Mafunzo hayo
yalihusu utaratibu wa kisheria wa upatikanaji, usafirishaji, utunzaji na
matumizi salama ya baruti. Lengo ni kuwaelekeza na kuwaelimisha watumiaji wa baruti juu ya mambo muhimu ya
usalama katika kufanya shughuli za uchimbaji wa madini kwa kutumia baruti.
141. Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha Mwaka
2014/15 Wizara itaimarisha mipango na taratibu za usimamizi wa masuala ya
baruti kwa kuzingatia Sheria ya Baruti ya Mwaka 1963; kuendelea kutoa elimu na
mafunzo kwa wachimbaji wadogo wapatao 1,000 kuhusu matumizi bora na salama ya
baruti; na kuendelea kufanya kaguzi mbalimbali kwenye maghala ya kuhifadhia
baruti. Pia, Sheria ya Baruti ya Mwaka 1963 itaboreshwa ili iendane na wakati.
Kuhamasisha Shughuli za Uongezaji Thamani Madini
142. Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha Mwaka
2013/14, Wizara iliendelea kuhamasisha shughuli za uongezaji thamani madini
nchini ambapo hadi kufikia Mwezi Machi, 2014 jumla ya leseni 32 za uchenjuaji
wa madini ya dhahabu (Vat Leaching), leseni 1 ya uchenjuaji wa madini
ya coltan na leseni 1 ya
uyeyushaji wa madini ya shaba
(copper smelter) zimetolewa. Pia, viwanda vitatu (3) vya kuchenjua madini ya shaba vyenye uwezo wa kuchenjua wastani wa tani
90,000 za shaba ghafi (Copper Oxide) kwa mwaka vimeanzishwa. Viwanda
hivi vipo Dar es Salaam (Danformation), Mkuranga (Horus) na Mpanda (TPM Mining). Viwanda hivyo vina
uwezo wa kuzalisha shaba katika kiwango cha ubora wa kati ya asilimia 80 hadi 95. Maeneo yanayozalisha
shaba ghafi kwa wingi kwa sasa ni Mbesa (Tunduru); Dreef, Kapanda, Kasakalawe na
Sikitiko (Mpanda); Burega, Gagwe, Ilagala, Lusunu, Kabulanzwila na Mkanga
(Kigoma); Ibaga na Ilangida (Mkalama); na Sufu (Chamwino). Makisio ya
uzalishaji wa shaba ghafi kwa mwaka ni tani 1,200.
143. Mheshimiwa Spika, Wizara imeanza
kukarabati na kukiboresha kituo cha Jimolojia kilichopo Arusha (Tanzania
Gemological Centre) ili kiwe cha kisasa zaidi ikiwa ni pamoja na kununua vifaa
vya ukataji wa madini ya vito (lapidary) na usanifu wa mawe (carving).
Aidha,
katika kukiimarisha kituo hicho, Wizara imenunua mashine 37 za aina mbalimbali
zikiwemo faceting machine 20, triming machine 4, stone carving
machine 4, bead making machine 6 na carbochon machine 3 kwa ajili ya kutoa mafunzo ya
ukataji na usanifu wa vito kwa vitendo. Pia, Serikali kupitia Wizara ya Nishati
na Madini imesaini makubaliano ya ushirikiano na Chuo cha Jimolojia cha nchini
Thailand (GIT) kwa kipindi cha miaka miwili (2) kuanzia Mwezi Julai 2013 hadi
Juni 2015. Aidha, Chama cha Wafanyabiashara wa Madini Tanzania (TAMIDA)
kimesaini hati ya ushirikiano na Chama cha Wafanyabiashara wa Vito na Usonara
cha Thailand (TGJTA) Mwezi Februari, 2014 ili kusaidia maendeleo ya tasnia ya
vito nchini mwetu.
144. Mheshimiwa Spika, Wizara imeendelea
kuendesha maonesho ya Vito na Usonara huko Arusha yakiwa na malengo ya kuvutia masoko
ya uhakika hapa nchini; fursa ya kutangaza rasilimali za madini ya vito yapatikanayo Tanzania; kukuza
kazi za uongezaji thamani madini nchini kupitia programu mbalimbali kwa kutoa
elimu ya uongezaji thamani madini kwa vikundi mbalimbali vya kinamama
wanaojishughulisha na biashara ya madini ya vito; wazalishaji na wafanyabiashara wa madini wa ndani kupata fursa ya kupata
masoko ya kimataifa; kuifanya Arusha kuwa kituo cha biashara ya vito na usonara
barani Afrika; na kukusanya mapato ya Serikali. Katika maonesho yaliyofanyika
Arusha kuanzia tarehe 28 hadi 30 Oktoba 2013, nchi 29 zilishiriki ambapo jumla
ya washiriki walikuwa ni 550 wakiwemo waoneshaji, wageni waalikwa na wanunuzi.
Aidha, madini yenye thamani ya Shilingi bilioni 6.9 yaliuzwa na kuiwezesha Serikali kukusanya kiasi cha Shilingi
milioni 227.4 ikiwa ni mrabaha. Ili kuboresha zaidi maonesho yajayo, Wizara ilishiriki
kwenye maonesho ya vito nje ya nchi yakiwemo Maonesho ya 53 ya Bangkok, Thailand; na Maonesho ya Tucson, Marekani. Ushiriki
huo umesaidia kujifunza namna bora ya kuandaa maonesho ya vito na kuwashawishi
wafanyabiashara wakubwa kuja kushiriki kwenye maonesho yajayo ya vito ya Arusha
ambayo yamepangwa kufanyika Mwezi Novemba, 2014.
145. Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2014/15,
Wizara itaendelea kuhamasisha shughuli za uongezaji thamani madini hapa nchini
yakiwemo madini ya shaba, vito, dhahabu na madini ya viwandani ili kuongeza
ajira, kipato kwa wananchi na mapato kwa Serikali. Aidha, Wizara itakamilisha Sheria
na Kanuni za Uongezaji Thamani Madini ili kusaidia kukuza na kusimamia shughuli
za uongezaji thamani madini hapa nchini. Pamoja na juhudi hizo, baada ya
kukamilisha ukarabati wa kituo cha Jimolojia kilichopo Arusha, Wizara itatekeleza mpango wa mafunzo ya uongezaji
thamani kwa vitendo kwa Watanzania na hivyo kuifanya fani hiyo kuchangia
ipasavyo katika ukuaji wa Sekta ya Madini na upatikanaji wa ajira mpya kwenye
tasnia hiyo.
Kuimarisha Usimamizi wa Biashara ya Madini
146. Mheshimiwa Spika, katika juhudi za
kuimarisha usimamizi wa biashara ya madini nchini, Serikali imeendelea
kusimamia shughuli hizo kwa kukagua na kuhakiki madini yanayozalishwa,
kuthaminisha, na kutoa vibali vya kuruhusu kusafirishwa kwenda nje. Katika kutekeleza lengo hilo,
jumla ya leseni 621 za biashara ya madini (dealers - 361 na brokers - 260) zimetolewa kwa mujibu wa Sheria
ya Madini ya Mwaka 2010. Aidha, katika kupambana na wimbi la utapeli na
udanganyifu katika biashara ya madini, Wizara imeanzisha
mpango wa kutangaza wamiliki wa leseni halali za biashara ya madini kupitia
tovuti yake ili kusaidia wanunuzi wa madini kuwafahamu wafanyabiashara halali
wa madini.
147. Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2014/15
Wizara itaimarisha ukaguzi wa biashara ya madini ili kupunguza udanganyifu
unaoikosesha Serikali mapato. Pia, Serikali itakamilisha mazungumzo na nchi za
India, Kenya na Marekani ili kuzishawishi kukubali kutambua Certificate of
Origin
ya Tanzanite. Hatua hii itapunguza utoroshaji wa madini. Aidha, Wizara kwa
kushirikiana na mamlaka nyingine za umma itaimarisha msako kwa ajili ya
kuwabaini na kuwakamata wanaojihusisha na utapeli katika biashara ya madini.
Kuendelea Kuvutia Uwekezaji katika Sekta ya Madini
148. Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2013/14,
Serikali imeendelea kuvutia uwekezaji katika Sekta ya Madini kwa kushiriki
kwenye warsha na maonesho ya ndani na nje ya nchi yanayokutanisha wawekezaji
katika Sekta ya Madini, kwa mfano INDABA (Afrika Kusini), PDAC (Canada) na ADUC
(Australia). Kupitia fursa hii, Serikali imetoa taarifa mbalimbali kuhusu
mazingira wezeshi ya uwekezaji katika Sekta ya Madini ikiwa ni pamoja na
taarifa za kijiolojia ili kuvutia wawekezaji.
149. Mheshimiwa Spika, ili kuendelea kuvutia
uwekezaji katika Sekta ya Madini, kwa Mwaka 2014/15 Wizara itaendelea kushiriki
katika warsha na maonesho mbalimbali ya ndani na nje ambayo huhudhuriwa na
wawekezaji mbalimbali. Aidha, Wizara itaendelea kutoa taarifa za kijiolojia
kupitia Wakala wa Jiolojia Tanzania (GST) zinazohitajika katika shughuli za
utafutaji wa madini pamoja na kuboresha huduma za utoaji wa leseni ili
zipatikane kwa wakati.
Kuimarisha
Mazingira ya Kazi katika Ofisi za Madini za Kanda
150. Mheshimiwa Spika, Wizara imeendelea
kuimarisha Ofisi za Madini za Kanda ikiwa ni pamoja na kujenga ofisi za kudumu.
Katika Mwaka 2013/14, taratibu za kujenga Ofisi za Dodoma, Mpanda na Mtwara
zimeanza. Lengo la Wizara ni kuboresha mazingira ya kazi ili kuongeza ufanisi
wa utekelezaji majukumu likiwemo ukusanyaji wa maduhuli. Kwa Mwaka 2014/15,
Wizara itaendelea kuimarisha na kuboresha vitendea kazi kwenye Ofisi zote za
Madini za Kanda na Maafisa Madini Wakazi na kukamilisha ujenzi wa ofisi za
Dodoma, Mpanda na Mtwara.
Asasi ya
Uwazi katika Tasnia ya Uziduaji (Tanzania Extractive Industries Transparency
Initiative – TEITI)
151. Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2013/14 Kamati
Tekelezi ya TEITI ilikamilisha rasimu ya Sheria itakayosimamia shughuli zake.
Nchi wanachama wa EITI ambazo tayari zina Sheria hiyo zilishirikishwa katika
maandalizi ya rasimu hiyo. Nchi hizo ni Ghana, Liberia na Nigeria. Lengo
lilikuwa ni kupata maoni na uzoefu wa nchi hizo katika utekelezaji wa Sheria
hiyo. Maoni yaliyopatikana Mwezi Oktoba, 2013 yametumika kuboresha rasimu hiyo,
na taratibu za maandalizi ya muswada zinaendelea ili uwasilishwe katika kikao
cha Bunge kabla ya Mwezi Novemba, 2014.
152. Mheshimiwa Spika, katika jitihada za
Serikali za kuweka wazi mapato yanayotokana na shughuli za kampuni zinazofanya
utafutaji na uchimbaji wa madini, mafuta na gesi asilia, TEITI iliendesha
warsha kwa Waandishi wa Habari, Asasi za Kiraia na wananchi juu ya matokeo ya Ripoti ya Tatu ya TEITI
katika maeneo yenye uwekezaji. Jitihada hizi zinalenga kuwajengea wananchi
uwezo wa kuhoji Serikali katika usimamizi wa rasilimali hizo. Warsha
hizi zilifanyika tarehe 28 Juni, 2013 na 03 Julai, 2013 Jijini Dar es Salaam;
tarehe 03 - 05 Julai, 2013 Jijini Arusha; tarehe 30 Septemba - 02 Oktoba, 2013
Jijini Mwanza; na tarehe 04 - 06 Novemba, 2013 Lindi na Mtwara.
153. Mheshimiwa Spika, napenda kuliarifu Bunge
lako Tukufu kuwa asasi ya EITI imefanya marekebisho ya masharti ya uanachama
ili kuongeza kasi ya kuleta mabadiliko yanayokusudiwa katika kuongeza manufaa
ya uvunaji wa rasilimali kwa wananchi kwenye nchi wanachama. Kuanzia Mwezi
Julai, 2013 utekelezaji katika nchi wanachama ulianza kupimwa kwa kutumia
viwango (EITI Standard) badala ya Kanuni za
Mwaka 2011. Katika mabadiliko hayo, nchi wanachama zinatakiwa pamoja na hatua
nyingine kuweka wazi rejista ya majina ya watu na kampuni zinazomiliki leseni za utafutaji na
uchimbaji wa madini, mafuta na gesi asilia.
154. Mheshimiwa Spika, utekelezaji wa mpango wa
EITI umekuwa na changamoto mbalimbali ikiwa ni pamoja na utoaji wa takwimu zilizo nje ya kipindi husika
na ucheleweshaji wa upatikanaji wa takwimu hizo kutoka kampuni za uchimbaji wa madini
na gesi asilia; na kutoka katika Taasisi za Serikali zinazokusanya mapato, na
hivyo kuathiri utoaji wa ripoti za TEITI kwa wakati. Ili kuondoa tatizo hili, natoa
wito kwa kampuni na Taasisi za Serikali kuwasilisha takwimu sahihi na kwa
wakati.
155. Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2014/15, Kamati
Tekelezi ya TEITI itaendelea kuandaa Sheria ya TEITI pamoja na kujenga uwezo
juu ya uendeshaji wa EITI kwa wajumbe wa Kamati na Sekretarieti Tekelezi ya
TEITI. Katika kipindi hiki Kamati
imepanga kuelimisha na kuhamasisha wananchi juu ya maeneo yafuatayo:
utekelezaji wa EITI kwa kuchapisha na kusambaza taarifa za TEITI kwa Mwaka 2011/12 na 2012/13; kukamilisha
matayarisho ya Taarifa ya Tano ya TEITI inayohusisha malipo ya kodi na mapato
ya Mwaka 2012/13; kusimamia tafiti mbalimbali za kupanua wigo wa utekelezaji wa
EITI; kutekeleza mpango wa mawasiliano na kuendesha warsha na semina juu ya
utekelezaji wa mpango wa TEITI; na kuiwezesha kifedha Sekreterieti na Kamati
Tekelezi ya TEITI. Aidha, Kamati itazijengea uwezo Asasi za Kiraia, Idara za
Serikali na kampuni za uziduaji juu ya utekelezaji wa mpango wa TEITI.
Uchambuzi na Uthamanishaji wa Madini ya Vito Kupitia TANSORT
156. Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha
kuanzia Julai 2013 hadi Machi 2014, TANSORT ilithamini na kusimamia uuzwaji wa
karati 128,000 za almasi zenye thamani ya Dola za Marekani milioni 33.3, sawa na Shilingi
bilioni 54.61. Mauzo ya almasi hizo yaliingizia Serikali mapato ya Dola za Marekani
milioni 1.7, sawa na Shilingi bilioni 2.79 ikiwa ni mrabaha. Aidha, Kitengo
kilithamini tani 24,000 za madini ya mapambo; gramu milioni 10 za vito ghafi;
na karati 166,000 za vito vilivyochongwa vikiwa na thamani ya Dola za
Marekani milioni 25.2, sawa na Shilingi bilioni 41.33. Mauzo ya madini hayo
yote ya vito yaliingizia Serikali mapato ya Dola za Marekani milioni 0.98, sawa na Shilingi
bilioni 1.61.
157. Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2014/15,
TANSORT itaendelea kutekeleza majukumu yake yakiwemo: kuthamanisha almasi na
madini ya vito ili kuwezesha Serikali kupata malipo stahiki ya mrabaha;
kutayarisha miongozo ya bei ya almasi na madini ya vito; kutoa huduma za
kijemolojia kwa wachimbaji wadogo
na wa kati; kusimamia mauzo ya almasi na madini ya vito ndani na nje ya nchi;
kufanya tafiti za masoko na bei za vito; na kutoa ushauri kwa wachimbaji wadogo
na wa kati kuhusu masoko, ukataji na ukadiriaji thamani ya vito.
Kuwezesha
Mashirika na Taasisi za Serikali katika Sekta ya Madini
Chuo cha Madini cha Dodoma - MRI
158. Mheshimiwa Spika, uamuzi wa kukigeuza Chuo
cha Madini Dodoma kuwa Polytechnic umeanza kutekelezwa katika Mwaka
2013/14. Jambo muhimu katika hatua hii ni kukipa Chuo mamlaka ya kujiendesha (autonomy), ambapo Wizara ya Nishati
na Madini imewasilisha mapendekezo Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi kwa
hatua zaidi. Aidha,
maandalizi ya kukikabidhi Chuo cha Madini eneo la Mgodi wa Golden Pride (Nzega)
uliofungwa yanaendelea ambapo makabidhiano rasmi yatafanyika Mwezi Desemba,
2014. Pamoja na juhudi hizo, Chuo cha Madini kimeandaa Makubaliano ya Awali (MoU)
yatakayowezesha
kushirikiana na Chuo cha Southern Alberta Institute of Technology (SAIT Polytechnic) cha Canada. Lengo la
hatua hii ni kuwezesha Chuo hiki kupata uzoefu wa kimataifa.
159. Mheshimiwa Spika, Chuo cha Madini Dodoma
kimeendelea kuongeza idadi ya wanafunzi kutoka 35 Mwaka 2005/06 hadi 547 kwa
Mwaka 2013/14 katika ngazi ya Cheti na Stashahada. Chuo hiki kinatoa mafunzo
katika fani za Jiolojia na Utafutaji Madini; Uhandisi Uchimbaji Madini;
Uhandisi Uchenjuaji Madini; Sayansi za Mafuta na Gesi Asilia; na Uhandisi
Usimamizi wa Mazingira Migodini. Aidha, katika Mwaka 2014/15, Chuo kitaanzisha
kozi mpya ya Upimaji Migodi (Mine Surveying) na Jimolojia (Gemology) katika ngazi ya Cheti na
Stashahada.
160. Mheshimiwa Spika, kuanzia Mwaka 2012/13
Serikali kupitia Wizara ya Nishati na Madini iliamua kwa makusudi kudhamini
wanafunzi wa Tanzania kusomea fani za mafuta na gesi asilia ndani na nje ya
nchi. Lengo ni kuhakikisha kwamba Wataalam wa Kitanzania wa kuhudumia Sekta ya
Mafuta na Gesi Asilia wanapatikana. Hadi sasa, wanafunzi 109 wanapata udhamini katika
Chuo cha Madini katika ngazi ya Stashahada. Aidha, katika kujenga uwezo wa Chuo
hicho, jumla ya Wakufunzi 6 wanahudhuria mafunzo ya Shahada za Uzamili na
Uzamivu katika nchi za Australia, Kenya, Sweden na hapa nchini. Aidha, Chuo
kitaendeleza watumishi kitaaluma na kitaalamu ili waweze kutoa mafunzo
yaliyokusudiwa ipasavyo kwenye Sekta za Nishati na Madini.
Shirika la Madini la Taifa - STAMICO
161. Mheshimiwa Spika, katika Hotuba yangu ya
Mwaka 2013/14 niliahidi kuwa Serikali itafanya kila linalowezekana ili
kuimarisha utendaji wa Shirika hilo. Miongoni mwa hatua zilizochukuliwa na
Wizara ni kuwezesha STAMICO kuajiri watumishi wapya 78 ili kutekeleza majukumu
yake ipasavyo. Aidha, Shirika liliendeleza mradi wa Buckreef kwa ubia na Kampuni ya
TANZAM 2000 kwa kukamilisha utafiti wa kimaabara wa njia bora za uchenjuaji miamba
(metallurgical studies) katika maeneo ya Bingwa, Buckreef na Tembo Mines katika
Mkoa wa Geita. Taratibu za uagizaji wa vifaa na mitambo kwa ajili ya uchimbaji
na uzalishaji dhahabu zimeanza kwa lengo la kuanza uzalishaji Mwezi Novemba,
2014.
162. Mheshimiwa Spika, pamoja na kukamilisha
utafiti wa Buckreef, Mwezi Aprili, 2014 Shirika lilianza maandalizi ya
kuchenjua mabaki ya uchimbaji wa zamani (tailings) katika eneo la Buhemba. Aidha,
mkataba rasmi wa ubia kati ya STAMICO na TanzaniteOne Mining Limited
ulisainiwa Mwezi Desemba, 2013.
Chini ya ubia huo, mgawanyo wa faida ni asilimia 50 kwa 50 na watumishi wa STAMICO
wamepelekwa mgodini kusimamia maslahi ya Taifa. Vilevile, STAMICO kupitia Kampuni
yake tanzu ya STAMIGOLD imeshaanza uendelezaji wa maeneo ya “West Zone na Moja
Moja” kwa kujenga barabara inayounganisha maeneo hayo na mitambo ya uchenjuaji
ya mgodi wa Tulawaka uliopo Wilaya ya Biharamulo.
163. Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2014/15 STAMICO imepanga
kufanya yafuatayo: kuendeleza migodi ya Buckreef (Geita), Buhemba (Butiama), Tulawaka
(Biharamulo) na TanzaniteOne (Simanjiro). Aidha, Shirika litaanzisha ununuzi na
uchenjuaji wa madini ya bati (tin ore) katika Mkoa wa Kagera na kufanya utafiti wa madini Rare
Earth Metals katika leseni zake zilizopo Wilaya ya Nkasi.
Wakala wa Ukaguzi wa Madini Tanzania - TMAA
164. Mheshimiwa Spika, katika kutekeleza Mpango
na Bajeti kwa Mwaka 2013/14, TMAA ilitekeleza majukumu yake na kuwezesha
kupatikana mafanikio mbalimbali. Katika kipindi cha kuanzia Julai 2013 hadi
Aprili 2014, baadhi ya migodi mikubwa iliendelea kulipa kodi ya mapato kutokana
na ukaguzi uliofanywa na TMAA kwa kushirikiana na TRA. Baadhi ya Kampuni hizo
ni Resolute Tanzania Limited (Nzega, Tabora) iliyolipa Shilingi bilioni 3.38 na Kampuni ya Geita Gold
Mining Limited (Geita) iliyolipa Shilingi bilioni 50.6 kama kodi ya mapato.
Aidha, ukaguzi uliofanywa na Wakala umewezesha jumla ya Shilingi bilioni 4.86 kulipwa Serikalini na baadhi ya
wamiliki wa migodi mikubwa na ya kati. Malipo hayo yanajumuisha mrabaha, ushuru
wa huduma, ada ya mwaka ya leseni na kodi ya zuio.
165. Mheshimiwa Spika, ukaguzi uliofanywa na
TMAA uliwezesha kukusanywa kwa mrabaha kutokana na madini ya ujenzi na
viwandani katika Kanda za Mashariki, Kusini, Magharibi, Kati na Ziwa Victoria
ambapo jumla ya Shilingi bilioni 1.72 zililipwa kama mrabaha katika
kipindi cha Julai 2013 hadi Aprili 2014. Malipo hayo yametokana na uzalishaji
wa jumla ya tani milioni 5 za madini ya ujenzi na viwandani yaliyokaguliwa na
Wakala yenye thamani ya Shilingi
bilioni 56.8.
166. Mheshimiwa Spika, Serikali iliendelea
kupata mrabaha na takwimu sahihi za madini yaliyozalishwa na migodi mikubwa
kutokana na ukaguzi na uhakiki wa
madini yaliyozalishwa na kuuzwa na migodi mikubwa ya Bulyanhulu (Shinyanga),
Buzwagi (Shinyanga), Geita (Geita), Golden Pride (Tabora), New Luika (Mbeya),
North Mara (Mara), Mwadui (Shinyanga), TanzaniteOne (Manyara) na Tulawaka
(Kagera). Ukaguzi huo ulisaidia kujua kiasi na thamani halisi ya madini
yaliyozalishwa na kuuzwa katika kipindi husika. Ukaguzi huo umewezesha
kukusanywa mrabaha wa jumla ya Dola za Marekani milioni 72.90, sawa na Shilingi
bilioni 119.56 kwa Mwaka 2013.
167. Mheshimiwa Spika, katika kudhibiti
utoroshaji wa madini na ukwepaji wa mrabaha, Wakala umeendelea kufanya ukaguzi
kupitia madawati maalum kwenye Viwanja vya Ndege vya Dar es Salaam, Kilimanjaro
na Mwanza. Kwa Mwaka 2013, ukaguzi huo umewezesha kukamatwa kwa watoroshaji wa
madini katika matukio 32 yaliyoripotiwa katika viwanja hivyo. Matukio hayo
yanahusu utoroshaji wa madini nje ya nchi yenye thamani ya Shilingi bilioni 2.1.
Wahusika wamefikishwa mahakamani na baadhi yao wamehukumiwa na madini yao
kutaifishwa na Serikali kwa mujibu wa Sheria za nchi.
168. Mheshimiwa Spika, kwa Mwaka 2014/15,
Serikali itaendelea kuimarisha ukaguzi wa shughuli za uzalishaji na biashara ya
madini kwa migodi mikubwa, ya kati na midogo kupitia Wakala wa Ukaguzi wa
Madini Tanzania (TMAA) ili kuhakikisha kuwa Taifa linanufaika ipasavyo na
rasilimali yake ya madini. Aidha, Wizara kupitia TMAA itaendelea kuchukua hatua
za makusudi kuelimisha umma kuhusu manufaa yanayopatikana kwenye Sekta ya
Madini kama njia ya kukabiliana na udanganyifu unaofanywa na baadhi ya watu kwa
lengo la kupotosha umma.
169. Mheshimiwa Spika, Wakala pia utaendelea
kuboresha mazingira ya kazi kwa kununua vitendea kazi vinavyohitajika na
kuwaendeleza wafanyakazi kitaaluma na kujenga uwezo katika kubainisha maoteo ya
mapato ya Serikali kutoka kwenye Sekta ya Madini kwa kutumia mfumo wa kisasa (revenue forecasting model) ili kuwa na takwimu za
uhakika za mapato ya Serikali kutokana na Sekta ya Madini. Aidha, Wakala
utakamilisha taratibu za usajili wa Maabara ya Wakala katika Shirika la Viwango
vya Kimataifa (ISO 17025) ili iweze kutambulika kimataifa.
Wakala wa Jiolojia Tanzania - GST
170. Mheshimiwa Spika, kwa Mwaka 2013/14,
Wakala umefanya utafiti wa kijiolojia na upatikanaji madini katika QDSs kumi na
nane (18) kwenye Wilaya za Bagamoyo, Chamwino, Chunya, Dodoma, Handeni, Ikungi,
Iramba, Kilindi, Ludewa, Makete, Mbinga, Mkalama, Mvomero, Singida na Songea
Vijijini. Uchoraji wa ramani hizo unaendelea kukamilishwa. Aidha, Wakala
umekamilisha utafiti wa jiokemia katika QDSs saba (7) kwa ajili ya utafutaji
madini kwenye Wilaya za Dodoma, Ikungi, Iramba, Manyoni, Mkalama na Singida.
171. Mheshimiwa Spika, katika kuendeleza Sekta
ya Madini nchini, Wakala pia ulifanya utafiti wa kina wa kijiofizikia (ground geophysical surveys) kwenye QDSs saba (7) katika Wilaya
za Bagamoyo, Handeni, Iramba, Kilindi, Mkalama na Singida kwa ajili ya
kufuatilia maeneo yaliyoonesha kuwa na viashiria vizuri vya kuwepo madini kutokana na utafiti wa
kijiofizikia kwa kutumia ndege. Matokeo ya utafiti huo yanaendelea kutafsiriwa
na taarifa zake zinaandaliwa na zitakamilishwa kabla ya Mwezi Januari, 2015.
172. Mheshimiwa Spika, ili kujiimarisha
kiutendaji, Wakala umebadilisha mfumo wa kuhifadhi na kusambaza taarifa na
takwimu za jiosayansi kwa kuziweka kwenye Computer Based Centralized
Geo-Scientific Data and Information Management Systems. Mabadiliko hayo yanawezesha kuwa
na takwimu za uhakika, zinazopatikana kwa urahisi na kwa wadau wengi zaidi.
173. Mheshimiwa Spika, kwa Mwaka 2014/15,
Wakala umejipanga kuendeleza tafiti za kijiosayansi za upatikanaji madini,
hususan technology metals, upatikanaji wa nishati ya jotoardhi, gesi za Helium (Mara) na Carbon
Dioxide
(Mbeya) na kuchora ramani 4 za kijiolojia katika Wilaya za Kilwa, Liwale,
Nachingwea na Ruangwa pamoja na ramani mbili (2) za kijiokemia katika Wilaya za
Liwale na Ruangwa.
Changamoto katika Sekta ya Madini
174. Mheshimiwa Spika, pamoja na mafanikio
yaliyopatikana, Sekta ya Madini imekabiliwa na changamoto mbalimbali zikiwemo:
upatikanaji wa masoko ya uhakika ya baadhi ya madini yanayozalishwa na
wachimbaji wadogo; kiwango kidogo cha uwekezaji wa mitaji katika uchimbaji
mdogo wa madini; kiwango kidogo cha fungamanisho la Sekta ya Madini na sekta
nyingine za uchumi; utoroshaji wa madini nje ya nchi; na upungufu wa watumishi wenye
ujuzi katika kusimamia Sekta ya Madini.
Mipango ya Kukabiliana na
Changamoto Zilizojitokeza
175. Mheshimiwa Spika, katika kukabiliana na changamoto zilizojitokeza,
Wizara itaendelea kuboresha na kuimarisha Idara ya Madini kwa kuwezesha
upatikanaji wa vitendea kazi na watumishi katika Ofisi zake. Aidha, Wizara
itaimarisha ukaguzi wa shughuli za uzalishaji na biashara ya madini nchini ili kuendelea
kudhibiti vitendo vya utoroshaji wa madini nje ya nchi.
C. AJIRA NA MAENDELEO YA
RASILIMALI WATU
176. Mheshimiwa Spika, katika Mwaka 2013/14
Wizara imeendelea kuajiri na kuendeleza watumishi wake ili waweze kufanya kazi
kwa weledi na ufanisi zaidi ikilenga kuinua mchango wa Sekta za Nishati na
Madini kwenye Pato la Taifa. Katika kipindi hicho, jumla ya watumishi
walioajiriwa na Wizara na Taasisi zake katika kada mbalimbali ni 227. Kati ya
hao, Wizara iliajiri watumishi 36, TMAA 11, STAMICO 78, REA 4 na TPDC 51. Vilevile, TPDC inaendelea na
utaratibu wa kuajiri watumishi wapya 226. Aidha, katika kuendeleza watumishi,
Wizara ilipeleka watumishi 80 katika mafunzo ya muda mfupi na watumishi 60
katika mafunzo ya muda mrefu ndani na nje ya nchi. Katika Mwaka 2014/15, Wizara
na Taasisi zake inatarajia kuajiri jumla ya watumishi 508 katika kada
mbalimbali. Kati ya hao,
watakaoajiriwa na Wizara ni watumishi 207; TMAA 29; STAMICO 79; GST 52; MRI 74;
TPDC 51; na REA 16.
177. Mheshimiwa Spika, Wizara pia kwa kutambua
kwamba masuala ya mafuta na gesi asilia ni maeneo mapya nchini, itaendelea
kutekeleza Mpango Kabambe wa Uendelezaji wa Rasilimali Watu (Marshall Plan
on Capacity Building and Development in Oil and Gas Industry). Hii ni miongoni mwa
mipango ya Serikali kuhahakikisha kuwa nchi inakuwa na wataalamu wa Kitanzania
wa kutosha katika Sekta Ndogo ya Mafuta na Gesi Asilia. Mpango huu
unashirikisha vyuo mbalimbali nchini vikiwemo Chuo Kikuu cha Dar es Salaam; na
Chuo Kikuu cha Dodoma ambavyo pamoja na fani nyingine vimeanzisha pia mitaala
kuhusu mafuta na gesi asilia (BSc in Petroleum Engineering, Petroleum Chemistry na BSc Petroleum
Geology).
178. Mheshimiwa Spika, baada ya mitaala hiyo
kuanzishwa, Wizara kwa Mwaka 2013/14 ilitoa ufadhili kwa vijana wa Kitanzania 9
katika Chuo Kikuu cha Dodoma kusomea Shahada ya uhandisi wa Mafuta na Gesi Asilia;
109 Chuo cha Madini Dodoma kusomea Stashahada ya Sayansi ya Mafuta na Gesi
Asilia; 59 VETA – Mtwara kwa wanafunzi wanaotoka maeneo ya Lindi na Mtwara
kusomea ufundi stadi ambao utawawezesha kupata ajira sehemu za uzalishaji wa
mafuta na gesi asilia; na wanafunzi 9 kusomea Shahada ya Uzamili katika masuala
ya Mafuta na Gesi Asilia huko Uingereza. Aidha, Watanzania 8 walipata ufadhili
wa Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China na mmoja nchini Ufaransa kusomea Shahada
ya Uzamili ya Mafuta na Gesi Asilia. Vilevile, watumishi 38 kutoka Taasisi
mbalimbali walihudhuria mafunzo ya muda mfupi yaliyofadhiliwa na Serikali ya
Uholanzi ambayo yalifanyika nchini Tanzania na Uholanzi. Vilevile, Chuo Kikuu
cha Dar es Salaam (UDSM) kimewezesha jumla ya wanafunzi 19 kwenda nchini Norway
kusomea Shahada ya Uzamili ya Mafuta na Gesi Asilia. Kati ya wanafunzi hao, 11
wanasoma Msc. in Petroleum Engineering na 8 wanasoma Msc. in
Petroleum Geology.
179. Mheshimiwa Spika, ili kuendelea kuimarisha
utendaji wa watumishi wake, Wizara kwa Mwaka 2014/15 inatarajia kupeleka
mafunzoni watumishi 246 katika mafunzo ya muda mfupi na watumishi 95 katika
mafunzo ya muda mrefu ndani na nje ya nchi. Aidha, pamoja na kuendelea
kuwalipia wanafunzi wa Kitanzania
walioanza masomo katika vyuo mbalimbali ndani na nje ya nchi, Wizara kwa kushirikiana
na Washirika wa Maendeleo inatarajia kuwapeleka Watanzania katika nchi
mbalimbali kwenye mafunzo ya Shahada za Uzamili, ambapo 10 watasomeshwa na
Serikali ya Brazili; 10 Serikali
ya Jamhuri ya Watu wa China; na wawili (2) Serikali ya Thailand katika masuala
ya mafuta na gesi asilia. Aidha, Wizara itaendelea kushirikiana na nchi na
mashirika mbalimbali ili kuongeza idadi ya Watanzania watakaosomeshwa katika
Sekta Ndogo ya Mafuta na Gesi Asilia kwa ajili ya kusimamia Sekta hiyo.
180. Mheshimiwa Spika, katika kipindi hiki pia,
Wizara itaanzisha mpango maalum wa kutoa mafunzo ya kusimamia Sekta ya Nishati
kwa kushirikisha Washirika wa Maendeleo wa Umoja wa Ulaya (EU), Serikali ya
Sweden na Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP). Fedha zitakazotumika
kutekeleza mpango huo, ambazo zimetengwa katika Bajeti ya Mwaka 2014/15 ni Shilingi bilioni 7.80 sawa na Dola za
Marekani milioni 4.76.
181. Mheshimiwa Spika, katika kuongeza tija na
motisha kwa watumishi, kwa Mwaka 2013/14 Wizara iliwapandisha vyeo jumla ya watumishi 57 katika fani
mbalimbali na kuwathibitisha kazini watumishi 36. Katika Mwaka 2014/15 Wizara
inatarajia kuwapandisha vyeo watumishi 157 ambao wamepata sifa za kitaaluma na
wenye utendaji mzuri wa kazi kulingana na Sera ya Menejimenti na Ajira katika
Utumishi wa Umma ya Mwaka 1999. Aidha, ili kuongeza ufanisi wa masuala ya
Sheria katika Sekta za Nishati na Madini zinazokua kwa kasi, Serikali
imeboresha muundo wa Wizara ya Nishati na Madini kwa kukipandisha hadhi Kitengo
cha Sheria na kuwa Idara kamili.
182. Mheshimiwa Spika, katika kujali afya za
watumishi, kwa Mwaka 2013/14, Wizara ya Nishati na Madini imeendelea
kutekeleza Waraka wa Utumishi wa
Umma Na. 2 wa Mwaka 2006 kwa kuwahudumia watumishi wanaoishi na Virusi vya
Ukimwi (VVU) na wenye Ukimwi waliojitokeza kwa kuwapa lishe na madawa maalumu.
Katika Mwaka 2014/15, Wizara itaendelea kutoa elimu mahali pa kazi ili kuzuia
maambukizi mapya na kuwahudumia waathirika wa Ukimwi kadri watakavyojitokeza.
Sambamba na jitihada hizo, Wizara pia itaendelea kuhamasiha watumishi kupima
afya hususan kuhusiana na magonjwa ya shinikizo la damu (blood pressure), kisukari na saratani.
Elimu kwa Umma kuhusu Rasilimali za Nishati na Madini
183. Mheshimiwa Spika, ili kuongeza uelewa
kuhusu masuala mbalimbali katika Sekta za Nishati na Madini, kuanzia Mwaka 2013/14 Wizara imeweka Mpango wa
kutoa elimu kwa wananchi. Ili kuwafikia wananchi wengi zaidi, Wizara inatumia njia mbalimbali ikiwa
ni pamoja na vyombo vya habari na Viongozi wa aina mbalimbali wakiwemo Viongozi
wa Dini. Mpango huo ulizinduliwa rasmi Jijini Dar es Salaam na Mhe. Dkt Jakaya
Mrisho Kikwete, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mwezi Januari, 2014.
184. Mheshimiwa Spika, katika kutekeleza mpango huo, kati ya Mwezi Januari na
Machi 2014, Wizara imefanikisha kufanyika kwa makongamano matatu (3) katika Mikoa
ya Dar es Salaam, Lindi, Mtwara na Pwani kwa ajili ya kutoa elimu kwa umma
kuhusu Sekta Ndogo ya Mafuta na Gesi Asilia pamoja na Sekta ya Madini,
yakilenga pamoja na mambo mengine, kuonesha faida zinazopatikana kwa Watanzania
katika uwekezaji kwenye rasilimali hizo. Katika Makongamano hayo jumla ya washiriki
605
walihudhuria, kati ya hao 209 walikuwa katika Kongamano lililofanyika Dar es
Salaam, 227 Lindi na Mtwara na 169
Pwani.
185. Mheshimiwa Spika, kimsingi makongamano
hayo yamekuwa na mafanikio makubwa, ikiwa ni pamoja na washiriki kupata
ufafanuzi ulio sahihi katika masuala yanayohusu Sekta za Nishati na Madini.
Washiriki wengi wamekiri kuelimika na kuahidi kueneza elimu sahihi katika
maeneo yao. Aidha, kupitia makongamano haya, washiriki hao kwa niaba ya
Watanzania walishuhudia kwa vitendo juhudi zinazofanywa na Serikali katika
kuendeleza Sekta hizo kwa manufaa ya Watanzania. Moja ya ushuhuda ni ule
uliotokea wakati Washiriki wa kongamano la Mikoa ya Mtwara na Lindi
walipotembelea eneo la Madimba panapojengwa mitambo ya kusafisha gesi asilia,
ambapo mmoja wao alitamka wazi kuwa “kumbe Serikali inafanya mambo makubwa lakini wananchi kwa kutoyajua,
wanaendelea kudanganywa kila siku kwa kupewa taarifa zisizo sahihi”.
186. Mheshimiwa Spika, ili kuendeleza mafanikio hayo,
Wizara katika Bajeti yake ya Mwaka 2014/15 imeamua kwa dhati kuanzisha programu
maalum ya kuelimisha umma (Public Awareness Program), ambayo itawezesha Wizara kutoa
elimu juu ya utekelezaji wa shughuli zake kwa kutumia njia mbalimbali zikiwemo
luninga, magazeti, redio, makongamano, tovuti na mihadhara. Lengo la Wizara ni
kuendelea kutoa elimu kwa Watanzania juu ya Sekta hizo ili kuwa na taarifa
sahihi za shughuli zinazotekelezwa na Serikali yao na faida zinazopatikana.
D.USHIRIKIANO WA KIMATAIFA
187. Mheshimiwa Spika, katika utekelezaji wa
shughuli zake, Wizara ya Nishati na Madini inaendelea kushirikiana na wadau
mbalimbali. Kwa niaba ya Serikali napenda kutoa shukrani kwa Serikali za
Algeria, Brazil, Canada, China, Finland, Korea ya Kusini, Marekani, Norway,
Sweden, Thailand, Trinidad na Tobago, Ujerumani na Urusi. Vilevile, natoa
shukrani kwa Benki
ya Dunia (WB), Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB), Benki ya Exim ya China,
Benki ya Maendeleo ya Afrika Kusini (DBSA), Benki ya HSBC, Benki ya BADEA,
Benki ya Uwekezaji ya Ulaya (EIB), Umoja wa Ulaya (EU), pamoja na Taasisi na
Mashirika ya AFD (Ufaransa), CIDA (Canada), DANIDA (Denmark), ECDF (Korea
Kusini), FINIDA (Finland), JICA (Japan), MCC (Marekani), NORAD (Norway), OFID
(Saudi Arabia), ORIO (Uholanzi), Sida (Sweden), IFC, UNDP, Sekretarieti ya
Jumuiya ya Madola, Climate Investment Fund (CIF), USAID (Marekani) na JBIC (Japan).
E. SHUKRANI
188. Mheshimiwa Spika, naomba kutumia fursa hii
kuwashukuru Naibu Mawaziri wa Wizara ya Nishati na Madini, Mhe. Stephen Julius
Masele, Mbunge - Jimbo la Shinyanga Mjini, anayesimamia masuala ya Madini; na
Mhe. Charles Muhangwa Kitwanga, Mbunge - Jimbo la Misungwi, anayesimamia
masuala ya Nishati. Nikiri wazi kuwa Naibu Mawaziri hao wamekuwa msaada mkubwa
kwangu katika utekelezaji wa majukumu ya Wizara ya Nishati na Madini. Aidha,
namshukuru kwa dhati aliyekuwa Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Mhe. George
Boniface Simbachawene, Mbunge - Jimbo la Kibakwe kwa mchango mkubwa alioutoa
akiwa Wizara ya Nishati na Madini. Namtakia mafanikio katika majukumu yake
mapya aliyoaminiwa na Mhe. Rais katika Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya
Makazi.
189. Mheshimiwa Spika, nawashukuru Mwenyekiti,
Makamu na wajumbe wote wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kwanza
kwa ushauri na maelekezo yao wanayoyatoa katika kuongeza ufanisi wa Wizara
yangu. Kamati hii imekuwa chachu muhimu katika kutoa miongozo ya kusaidia
kutatua matatizo na changamoto zinazoikabili Wizara. Nawashukuru viongozi na
wajumbe wote wa Kamati hii na ni matumaini yangu kuwa wataendelea kutoa
ushirikiano ili kuendeleza Sekta za Nishati na Madini kwa faida ya Watanzania
wote.
190. Mheshimiwa Spika, kwa namna ya kipekee
nawashukuru Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini, Bw. Eliakim C. Maswi,
Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini, Mhandisi Ngosi X. Mwihava kwa
ushirikiano wanaonipa na kwa utendaji wao mahiri ambao unaiwezesha Wizara hii
kusonga mbele siku hadi siku. Nakiri kuwa viongozi hawa wamekuwa kiungo muhimu
na wenye umakini mkubwa katika timu yangu ya ushindi ya Wizara. Aidha,
nawashukuru Kamishna wa Nishati na wa Masuala ya Petroli; Kamishna wa Madini;
Wakuu wa Idara, Sehemu na Vitengo.
191. Mheshimiwa Spika, nawashukuru sana
Wenyeviti wa Bodi za Wakurugenzi za EWURA, PICL, PUMA, REA, STAMICO, TANESCO,
TIPER na TPDC; Wenyeviti wa Bodi za Ushauri za GST, TMAA na MRI pamoja na
Mwenyekiti wa Bodi ya Ushauri ya Madini kwa
ushirikiano wanaonipa katika kuongoza Wizara. Ili Bodi hizi zifanye kazi vizuri
zinahitaji Menejimenti nzuri na yenye mwono wa mabadiliko. Nawapongeza sana
Wakuu wa Taasisi zilizo chini ya Wizara; na watumishi wote kwa ujumla kwa
ushirikiano wao katika kufanikisha utekelezaji wa majukumu ndani ya Wizara,
Taasisi na Kampuni zetu.
192. Mheshimiwa Spika, kwa unyenyekevu kabisa
napenda kuwashukuru na kuwapongeza Viongozi wote wa Dini nchini kwa kukubali
kushirikiana na Wizara ya Nishati na Madini katika kuelimisha jamii kwa kauli
mbiu isemayo “Uendelezaji
wa Rasilimali za Gesi Asilia, Mafuta na Madini kwa Amani na Maendeleo ya Nchi
Yetu”. Kupitia viongozi hawa
Wizara imeendelea kuelimisha jamii juu ya rasilimali zake katika makongamano
mbalimbali nchini. Aidha, navishukuru vyombo vya habari na wadau wengine kwa
kushirikiana na Wizara ya Nishati na Madini katika kutoa habari na kuelimisha
wananchi juu ya uendelezaji wa rasilimali zetu kwa manufaa ya Taifa letu.
Nawaomba Viongozi wa Dini na wadau wengine tuendelee kushirikiana ili kuleta
maendeleo endelevu kupitia rasilimali za nishati na madini. Napenda kuwahakikishia kuwa
Wizara ya Nishati na Madini haitarudi nyuma katika kutafuta ufumbuzi wa
matatizo na changamoto mbalimbali zinazoikabili na itaendelea kushirikisha
jamii na wananchi kwa ujumla katika hatua zake za utekelezaji.
193. Mheshimiwa Spika, kwa dhati kabisa
namshukuru sana mke wangu Bertha Muhongo pamoja na wanangu Godfrey Chirangi,
Dkt. Musuto Chirangi, Dkt. Bwire Chirangi, Rukonge Muhongo, ndugu, marafiki na
Wananchi kwa ujumla kwa msaada mkubwa wanaonipa katika kutekeleza majukumu
yangu ya kusimamia Wizara ya Nishati na Madini kwa umakini na ubunifu wa hali
ya juu.
F: HITIMISHO
194. Mheshimiwa Spika, Bajeti ya Mwaka 2014/15
inakusudia kuimarisha na kuendeleza Sekta za Nishati na Madini ili kuongeza
zaidi mchango wake katika kujenga uchumi imara wa Taifa utakaotoa ajira mpya
kwa Watanzania na kupunguza umaskini nchini.
195. Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja kwamba
Bunge lako Tukufu sasa liidhinishe Bajeti ya jumla ya Shilingi
1,082,555,622,000.00 kama ifuatavyo:
(i) Bajeti ya Maendeleo ni Shilingi 957,177,170,000.00 sawa na asilimia 88.4 ya Bajeti
yote ya Wizara. Kati ya
fedha hizo, Shilingi 652,805,000,000.00 ni fedha za ndani, sawa na asilimia
68.2 ya fedha za maendeleo na Shilingi
304,372,170,000.00 sawa na asilimia 31.8 ni fedha za nje; na
(ii) Matumizi ya Kawaida ni Shilingi 125,378,452,000.00 sawa na asilimia 11.6 ya Bajeti yote ya
Wizara. Kati ya fedha hizo Shilingi 26,912,948,000.00 ni kwa ajili ya mishahara ya watumishi wa Wizara, Mashirika na Taasisi zake
(sawa na asilimia 21.47 ya Bajeti ya Matumizi ya
Kawaida au asilimia 2.49 ya Bajeti yote) na Shilingi
98,465,504,000.00 ni kwa ajili ya Matumizi Mengineyo
(O.C), sawa na asilimia 78.53 ya Bajeti ya Matumizi ya
Kawaida au asilimia 9.1 ya Bajeti yote.
196. Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja.
No comments:
Post a Comment