HOTUBA
YA WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI, MHESHIMIWA PROF. ANNA KAJUMULO TIBAIJUKA (MB),
AKIWASILISHA BUNGENI MAKADIRIO YA MAPATO NA MATUMIZI YA WIZARA YA ARDHI, NYUMBA NA
MAENDELEO YA MAKAZI
KWA
MWAKA WA FEDHA 2014/15
UTANGULIZI
1.
Mheshimiwa Spika, kutokana na taarifa iliyowasilishwa leo ndani ya Bunge
lako Tukufu na Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na
Mazingira, naomba kutoa hoja kwamba Bunge lako tukufu likubali kupokea na
kujadili taarifa ya utekelezaji wa kazi za Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo
ya Makazi ya mwaka wa fedha 2013/14 na malengo ya Wizara katika bajeti ya mwaka
wa fedha 2014/15. Aidha, naliomba Bunge lako Tukufu likubali kupitisha
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara kwa mwaka wa fedha 2014/15.
2.
Mheshimiwa Spika, awali ya yote namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia
Waheshimiwa Wabunge kuwa na afya njema na hivyo kuweza kushiriki mkutano wa
kumi na tano wa Bunge la Kumi la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Pia,
nampongeza Mhe. Dkt. Asha Rose Migiro kwa kuteuliwa kuwa Mbunge wa Bunge lako
na Waziri wa Katiba na Sheria. Aidha, nawapongeza Mhe. Ridhiwani Kikwete na
Mhe. Godfrey Mgimwa kwa kuchaguliwa kwa kishindo kuwa Wabunge wa Bunge lako
Tukufu na kuimarisha safu ya Wabunge vijana wa CCM.
3.
Mheshimiwa Spika, naomba nitangulize dua zangu kwa Mwenyezi Mungu kuwa azipokee na kuzilaza
mahala pema peponi roho za marehemu Mhe. Dkt. William Augustino Mgimwa
aliyekuwa Waziri wa Fedha, Mbunge wa Jimbo la Kalenga na Mhe. Saidi Bwanamdogo
aliyekuwa Mbunge wa Jimbo la Chalinze. Vilevile, kwa namna ya pekee natoa pole
kwa Watanzania wenzangu walioathirika na majanga mbalimbali likiwemo la
mafuriko yaliyotokea sehemu mbalimbali nchini kati ya mwezi Machi na Aprili,
2014. Sina budi kuwalilia na kuwakumbuka wananchi kadhaa wa Wilaya ya Muleba
Kata ya Mazinga, Nyakabango, Kimwani na Rulanda waliouawa na mamba na viboko
kutoka Hifadhi ya Taifa ya Rubondo. Maisha yao hayakupotea bure nimetoa taarifa
kuepusha mashambulizi mengine. Aidha kuna wananchi ambao wamepoteza maisha yao
katika migogoro ya ardhi sehemu mbalimbali nchini. Nichukue nafasi hii kuwapa
pole wafiwa, njia pekee ya kuwaenzi ndugu zetu hao ni kumaliza migogoro hii
tukawa taifa na jamii inayomaliza tofauti kwa majidiliano (...dialogue and
not confrontation).
4.
Mheshimiwa Spika, naomba nitumie fursa hii kuwapongeza Mhe. Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, Rais
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Mohammed Gharib Bilal, Makamu wa
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; na Mhe. Mizengo Kayanza Peter Pinda, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania na Mbunge wa Mpanda Mashariki, kwa uongozi wao mahiri.
Nawashukuru kwa ushauri, maelekezo na ushirikiano wanaonipa, ulioniwezesha
kutekeleza majukumu niliyokabidhiwa ya kuongoza sekta hii mtambuka na muhimu
katika maendeleo ya Taifa letu. Nawapongeza kwa dhati Mhe. Dkt. Ali Mohammed
Shein, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi; pia, Mhe. Maalim
Seif Shariff Hamad, Makamu wa Kwanza wa Rais wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar;
na Mhe. Balozi Ali Idd Seif, Makamu wa Pili wa Rais wa Serikali ya Mapinduzi
Zanzibar, kwa mafanikio makubwa yanayoendelea kupatikana katika Serikali ya
Umoja wa Kitaifa ya Zanzibar. Sherehe za miaka 50 ya Mapinduzi ya Zanzibar na
za miaka 50 ya Uhuru zilionesha jinsi gani taifa hili linasonga mbele kwa
amani, mshikamano na upendo. Tanzania imekuwa kisiwa cha amani si kwa
kubahatisha bali kwa uongozi imara chini ya Serikali ya Chama Cha Mapinduzi.
5.
Mheshimiwa Spika, nakupongeza wewe kwa kuongoza shughuli za Bunge kwa ufanisi. Mwenyezi
Mungu aendelee kukuongoza na kukupa nguvu, afya na hekima za kumudu zaidi
majukumu yako. Pia, nampongeza Mhe. Job Yustino Ndugai, Mbunge wa Kongwa na Naibu Spika wa
Bunge letu kwa utendaji mzuri katika uendeshaji wa shughuli za Bunge.
6.
Mheshimiwa Spika, napenda nitumie fursa hii kuwashukuru kwa dhati wananchi
wa Jimbo la Muleba Kusini kwa kunipa ushirikiano wa
karibu katika kutimiza majukumu yangu nikiwa Mbunge wao. Pamoja na kuwa na kazi
nyingi za kitaifa, wananchi wa Jimbo la Muleba Kusini wamekuwa wakinipa
ushirikiano mzuri na kujitahidi kukutana nami ninapopata nafasi kufika jimboni
kwa kuhudhuria vikao na mikutano katika tarafa zao au kupokea wageni na
wataalaam waelekezi ninaowatuma kufika kusukuma maendeleo yetu. Kama Waziri, tena
wa Ardhi, muda wa kuwa jimboni ni mdogo. Pamoja na hayo wananchi wa Muleba
wamekuwa wakijitokeza kwa wingi katika mikutano ya Kata ninapofika ili
tutathmini maendeleo, kujipanga vizuri na kula na kunywa pamoja. Muleba
tunasema “Ebitaina mahyo tibyela”. Au “Kazi bila pongezi haiendi”.
Ninawashukuru sana kwa moyo huo wa upendo ambao umewaumbua wanaodhani kuwa
kukaa mbali ni kukosa mahusiano.
7.
Mheshimiwa Spika, aidha, ninawashukuru ndugu, jamaa na marafiki wanaonisaidia na kunipa
ushirikiano wa karibu katika kutimiza majukumu ya Uwaziri na Ubunge. Nawashukuru wananchi na kuwahakikishia
popote pale mlipo, iwe Tarafa ya Nshamba, Kimwani au Muleba yenyewe, kwamba
tutayalinda mafanikio tuliyoyafikia na kuongeza kasi zaidi ili kufikia malengo
ya kulinda amani, utulivu na kufikia maisha bora. Namuomba Mwenyezi Mungu
amwezeshe kila mwananchi kulitambua hili na kuchangia katika nafasi yake kwa
kadri ya uwezo wake kufikia maisha bora. Mwisho, ninatuma salamu kwa mama yangu
mzazi Ma Aulelia Kajumulo hapo Muleba. Sala zake za kila siku zimeendelea
kuniimarisha katika kutekeleza majukumu yangu. Nasimama hapa nikiwa mzima wa
afya kwa sababu hiyo.
8.
Mheshimiwa Spika, napenda kuwashukuru kwa dhati viongozi wote wa Chama cha
Mapinduzi (CCM) ambao wamenisaidia katika kutekeleza majukumu yangu magumu hasa
katika utatuzi wa migogoro ya ardhi sehemu mbalimbali nchini. Hii imenipa nguvu
mpya katika kutekeleza ilani ya CCM. Aidha, sina budi kutambua mchango wa
viongozi wa dini na vyama vya hiari ambao nimeshirikiana nao katika kazi zangu
za kutatua migororo na changamoto nyingi za sekta ya ardhi ambazo zinahitaji
ushiriki wao, busara zao na kutambua na kutofautisha sheria na haki na uhusiano
wake.
9.
Mheshimiwa Spika, kwa namna ya kipekee natoa shukurani zangu za dhati kwa
wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Mazingira ikiongozwa na Mwenyekiti wake Mhe. James Daudi Lembeli, Mbunge wa
Kahama kwa ushirikiano mkubwa na ushauri wao ambao uliiwezesha Wizara
kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi. Natoa shukrani za pekee kwa Naibu Waziri,
Mhe. George Bonifance Simbachawene, Mbunge wa Kibakwe kwa ushirikiano na umoja
tuliojenga katika kutekeleza majukumu yetu. Nawashukuru pia Katibu Mkuu Bw.
Alphayo Japani Kidata; Naibu Katibu Mkuu, Dkt. Selassie David Mayunga; watendaji
katika Idara, Vitengo, Shirika na Taasisi zilizo chini ya Wizara kwa ushauri na
mshikamano wao katika kupanga na kutekeleza mipango ya Wizara. Zipo changamoto
nyingi zinazoikabili sekta yetu lakini kwa mshikamano na umoja wao naamini
tumeweza kuendelea kukabiliana nazo.
CHANGAMOTO ZINAZOIKABILI SEKTA YA ARDHI
10.
Mheshimiwa Spika, changamoto zinazoendelea kuikabili sekta yangu, kama
nilivyoziorodhesha mwaka jana, zinagawanyika katika maeneo manne (4) makubwa
kama ifuatavyo:
i.
Uelewa usiotosheleza wa wananchi kuhusu sekta yenyewe
hasa sheria zake, taratibu na miongozo iliyopo; haki zao na wajibu wao;
ii.
Nafasi ya vyombo mbalimbali vya usimamizi na utendaji wake;
iii.
Vitendea kazi vilivyopo na vinavyohitajika ili kukidhi
mahitaji ya sekta nyeti ya ardhi ambayo ni kiungo muhimu katika maendeleo; na,
iv.
Mazingira ya utendaji yaliyopo nje ya uwezo wa Wizara.
11.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2013/14 Wizara yangu iliahidi kuwa itaeleza jinsi ilivyojipanga
kukabiliana na changamoto za utekelezaji wa majukumu yake. Katika kutekeleza ahadi hiyo, Wizara
imeongeza utoaji wa elimu kwa umma kuhusu sheria za ardhi, kanuni na taratibu
pamoja na kuandaa miongozo mbalimbali; kupunguza kwa kiasi kikubwa ukosefu wa
vitendea kazi katika sehemu za kazi kwa mfano, ununuzi wa mtambo mpya wa
uchapaji wa ramani na nyaraka. Ili kuongeza mahusiano na wadau wake na kuboresha mazingira
ya utendaji yaliyoko nje ya uwezo wa Wizara, Wizara iliweza kuwashawishi
wahisani wa maendeleo ambao tayari wameanza kuipatia Wizara rasilimali fedha za
kutekeleza Mpango Mkakati wa Utekelezaji wa Sheria za Ardhi. Pia, Wizara ipo
katika hatua za kurekebisha muundo wake ili watumishi wa Sekta ya Ardhi walioko
Halmashauri wawajibike moja kwa moja Wizarani.
12.
Mheshimiwa Spika,
baada ya kueleza hayo, naomba sasa nieleze kwa kifupi utekelezaji wa Mpango wa
Wizara kwa mwaka wa fedha 2013/14 na Shabaha za Mpango wa mwaka wa fedha
2014/15. Napenda kulijulisha Bunge lako Tukufu kuwa takwimu nyingi za
utekelezaji zinaishia mwezi Aprili, 2014 na zitakuwa tofauti ifikapo mwisho wa mwezi
Juni, 2014.
MAPITIO
YA UTEKELEZAJI WA BAJETI YA MWAKA WA FEDHA 2013/14 NA MALENGO YA
MWAKA
WA FEDHA 2014/15
Ukusanyaji wa Mapato
13.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2013/14 Wizara ilikuwa na lengo la kukusanya jumla ya
Shilingi bilioni 100.05 kutokana na vyanzo
mbalimbali vya mapato yanayotokana na Sekta ya Ardhi. Hadi Aprili, 2014 jumla
ya Shilingi bilioni 37.03
zilikusanywa. Makusanyo
haya ni zaidi ya maduhuli yaliyokusanywa katika mwaka wa
fedha 2012/13
kwa shilingi bilioni 14.27. Hata hivyo, mwenendo wa makusanyo kwa mwaka wa fedha 2013/14
ni hafifu yakilinganishwa na lengo la kukusanya shilingi bilioni 100. Sababu zilizochangia
hali hiyo ni pamoja na kubainika kwamba makusanya ya nyuma yaliyopelekea
malengo ya ukusanyaji mpya kuwekwa yalitokana na vyanzo visivyojirudia, yaani
tozo kwa viwanja vipya wakati wa mradi wa viwanja elfu ishirini. Kwa hiyo
pamoja na juhudi za kukusanya maduhuli kuongezeka na kupanda kwa viwango vya
kodi, ada na tozo mbalimbali za ardhi bado malengo hayakufikiwa. Aidha
utaratibu wa ulipaji wa kodi usio rafiki kwa wananchi, tabia ya kusubiri kulipa
kodi dakika za mwisho wa mwaka wa fedha ambao bado unaendelea, na uelewa mdogo
wa wananchi juu ya wajibu wao wa kulipa kodi pia umechangia kutokufikia malengo
hadi sasa. Ili kukabiliana na changamoto hizo, Wizara inarekebisha viwango vya
kodi, ada na tozo za ardhi pale ambapo zitadhihirika kuwa juu ya uwezo wa
wananchi (affordability test); mazungumzo yamefanyika ili kuhakikisha
utaratibu wa kufanya malipo unarahisishwa; na, kuongeza kasi ya kutoa elimu kwa
umma kuhusu wajibu wa wamiliki wa viwanja na mashamba kulipa kodi. Aidha
wanaoshindwa kulipa kodi ya ardhi watachukuliwa hatua na kubatilisha milki zao
kwa kukiuka masharti ya miliki.
14.
Mheshimiwa Spika,
katika mwaka wa fedha 2014/15, baada ya kurekebisha
uhalisia wa vyanzo vya walipa kodi tofauti na walipa tozo, Wizara imeweka lengo la kukusanya Shilingi
bilioni 61.32. Maduhuli haya yatakusanywa kwa kutumia mikakati ifuatavyo: kuimarisha utunzaji wa kumbukumbu za ardhi; kupanga, kupima na kumilikisha
maeneo mapya; kuhamasisha wananchi kulipa kodi ya pango la ardhi; kurahisisha
ulipaji wa kodi kwa kutumia teknolojia za kisasa za malipo na kuhuisha viwango
vya kodi ya ardhi. Aidha, Wizara yangu itaendelea kuwachukulia hatua za
kisheria wadaiwa sugu wa kodi ya pango la ardhi. Nitumie fursa hii
kuwakumbusha wananchi kutimiza masharti ya umiliki wa ardhi ikiwa ni pamoja na
kulipa kodi ya pango la ardhi, ada na tozo nyingine kwa mujibu wa sheria.
Matumizi
15.
Mheshimiwa Spika,
katika mwaka wa fedha 2013/14 Wizara iliidhinishiwa matumizi ya jumla ya Shilingi
bilioni 108.3. Kati ya fedha hizo Shilingi bilioni 10.20 zilitengwa
kwa ajili ya mishahara; Shilingi bilioni 25.96
zilitengwa kwa ajili ya matumizi mengineyo; na Shilingi bilioni 72.17 zilitengwa kwa ajili ya miradi ya
maendeleo. Kati ya fedha za miradi ya maendeleo Shilingi bilioni 56.2 ni fedha za ndani na Shilingi bilioni 16
ni fedha za nje. Hadi Aprili, 2014 jumla ya fedha zilizopatikana ni Shilingi
bilioni 47.94 sawa na asilimia 44.25 ya fedha
zilizoidhinishwa. Jumla ya Shilingi bilioni 38.80
sawa na asilimia 81 ya kiasi kilichotolewa,
zilitumika (Jedwali Na. 1). Ni matarajio yangu
kwamba fedha zilizotolewa zitatumika hadi kufikia tarehe 30 Juni, 2014.
UTAWALA WA ARDHI
16.
Mheshimiwa Spika, Usimamizi
wa ardhi nchini unahusisha mamlaka kuu tatu ambazo ni Halmashauri za Vijiji,
Halmashauri za Wilaya na Miji na Wizara chini ya ofisi ya Kamishna wa Ardhi.
Majukumu na mamlaka za usimamizi yameainishwa vema katika Sheria za Ardhi. Lengo
la sheria ni kuhakikisha kuwa wananchi wanashirikishwa ipasavyo katika suala
zima la usimamizi wa rasilimali ardhi kuanzia ngazi ya Kijiji hadi Taifa.
Ofisi
za Ardhi za Kanda
17.
Mheshimiwa Spika,
katika jitihada za kusogeza huduma za ardhi karibu na wananchi, Wizara
imeendelea kuanzisha na kuimarisha Ofisi za Ardhi za Kanda. Hadi sasa Wizara
ina Ofisi za Ardhi za Kanda 7 ambazo ni Kanda ya Kusini (Mtwara), Ziwa
(Mwanza), Mashariki (Dar es Salaam), Kaskazini (Moshi), Kati (Dodoma), Nyanda
za Juu Kusini (Mbeya) na Magharibi (Tabora). Wizara imepanga kupeleka huduma za
Mipango Miji na Vijiji, Upimaji na Ramani na Uthamini wa Mali katika ofisi hizo
katika mwaka wa fedha 2014/15.
18.
Mheshimiwa Spika,
katika Hotuba ya Bajeti ya mwaka wa fedha 2013/14, Wizara yangu iliahidi kuanza
kutoa huduma za ardhi katika ofisi ya ardhi ya Kanda ya Magharibi iliyopo mjini
Tabora. Napenda kuliarifu Bunge lako Tukufu kuwa ofisi hiyo imeanza kazi rasmi
na inahudumia mikoa ya Tabora, Shinyanga, Kigoma na Katavi, ambayo awali
ilikuwa inahudumiwa na Kanda ya Ziwa (Mwanza) na Nyanda za Juu Kusini (Mbeya).
Ni matumaini yangu kwamba kwa kuanzishwa ofisi hiyo kutawawezesha wananchi
kupata huduma za ardhi karibu na maeneo yao.
19.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2014/15 Wizara yangu itaigawanya Kanda ya Mashariki
kuwa Kanda mbili; Kanda ya Dar es
Salaam na Kanda ya Mashariki. Kanda ya Dar es Salaam itahudumia Mkoa wa Dar es
Salaam pekee kutoka makao makuu ya Wizara na Kanda ya Mashariki itahudumia
Mikoa ya Pwani na Morogoro kutoka aidha mkoa wa Morogoro au Pwani kama
itakavyoamuliwa na wadau. Kanda ya Mashariki itaanza kutoa huduma za ardhi
kuanzia Julai, 2014. Hatua hii ni muendelezo wa kusogeza huduma za ardhi karibu
na wananchi na kuongeza ufanisi.
Mkakati
wa Kupima Kila Kipande cha Ardhi Nchini
20.
Mheshimiwa Spika, Sheria za ardhi zinatoa miongozo muhimu ya kusimamia ardhi na fursa ya
kuhakikisha kuwa ardhi yote nchini inamilikiwa kisheria. Wizara imeweka mkakati
wa kuhakikisha kuwa kila kipande cha ardhi nchini kinapangwa, kinapimwa,
kinamilikishwa na kinasajiliwa kisheria. Mkakati huu ambao umeanza kutekelezwa
katika Wilaya ya Mvomero katika Mkoa wa Morogoro utasaidia kupunguza migogoro
ya matumizi ya ardhi. Katika mwaka wa fedha 2014/15 utekelezaji utaendelea katika
Wilaya za Kilosa na Kilombero, Mkoa wa Morogoro. Natoa rai kwa wananchi na Halmashauri ambazo
maeneo yao yatahusika katika kufanikisha utekelezaji wa mkakati huu kutoa
ushirikiano wa dhati mara zitakapofikiwa. Aidha, ninawaomba wananchi pia
kutambua ardhi ikishapimwa na kumilikishwa itakuwa haramu kuivamia na kuitumia
kwa matumizi ambayo hayakupangwa. Migogoro haiwezi kuisha kama kila mwananchi
hatii matumizi yaliyopangwa.
Utekelezaji
wa Sheria ya Ardhi
21.
Mheshimiwa Spika, Sheria ya Ardhi ya mwaka 1999 inatoa fursa ya kuhakikisha kuwa ardhi yote
nchini inamilikiwa kisheria. Hadi Aprili 2014, vijiji 20 vimewezeshwa kuandaa mipango shirikishi ya matumizi ya ardhi ya kijiji,
Vyeti vya Ardhi ya Kijiji 972 vimetolewa kwa
kushirikiana na taasisi mbalimbali, Hati za Hakimiliki ya Kimila 24,945 zimetolewa na Hati Miliki 24,651
zimetolewa (Jedwali Na. 2). Katika mwaka wa fedha 2014/15,
Wizara yangu itaendelea na kazi ya uhakiki na upimaji wa vipande vya ardhi
wilayani Mvomero na inatarajia kupima na kuandaa hatimiliki za kimila 70,000
na Hati Miliki 40,000. Halmashauri zote nchini zihakikishe kuwa zinapanga, zinapima,
zinamilikisha viwanja na kuandaa Hati ili wananchi waweze kuwa na milki salama.
22.
Mheshimiwa Spika, Wizara ina jukumu la kushughulikia uteuzi wa wajumbe wa Kamati za Ugawaji
Ardhi katika ngazi ya Taifa, Miji na Wilaya. Kamati hizi ni vyombo muhimu
katika kushughulikia ugawaji wa ardhi nchini. Katika mwaka wa fedha 2013/14
Wizara imefanya uteuzi wa Wajumbe wa Kamati za Ugawaji Ardhi katika Halmashauri
za Magu, Musoma, Kigoma/Ujiji, Bukoba, Kilosa, Morogoro, Masasi, Tandahimba,
Bariadi, Lindi, Mpanda, Same, Kilolo, Sengerema, Manispaa ya Morogoro na
Manispaa ya Moshi. Aidha, Kamati ya Taifa ya Ugawaji Ardhi pamoja na majukumu
mengine inalo jukumu la kugawa ardhi kwa ajili ya uwekezaji. Katika mwaka wa fedha 2013/14 kamati
hii ilipokea maombi 96 na kutoa ushauri wa
kumilikisha viwanja 35 na mashamba 12 kwa ajili ya uwekezaji. Nazihimiza Halmashauri ambazo hazina Kamati za
Ugawaji Ardhi za Wilaya na Miji kuwasilisha mapendekezo ya majina ya wajumbe wa
kamati hizo Wizarani ili uteuzi uweze kufanyika.
23.
Mheshimiwa Spika, mojawapo ya majukumu ya Wizara yangu ni kusimamia uhamisho wa milki za
ardhi. Katika mwaka wa fedha 2013/14 Wizara iliahidi kushughulikia maombi ya
uhamisho wa milki 1,800. Hadi Aprili, 2014
Wizara imeshughulikia maombi ya uhamisho wa milki 3,079. Kwa mwaka wa fedha 2014/15 Wizara itashughulikia maombi ya uhamisho wa
milki 3,500. Vilevile, Wizara inaendelea na jukumu la kusimamia
masharti ya umiliki wa ardhi na kuhakikisha kuwa miliki zinaendelezwa ipasavyo.
Hadi Aprili, 2014 ilani za ubatilisho 3,581
zilitumwa kwa wamiliki waliokiuka masharti ya umiliki wakiwemo wamiliki wa
mashamba yasiyoendelezwa nchini. Kwa mwaka wa fedha 2014/15, Wizara itaendelea
kushughulikia ubatilisho wa milki zote zinazokiuka masharti ya uendelezaji. Napenda
kuwashauri wananchi wote wanaonunua milki za ardhi kuhakikisha wanafanya
uhamisho wa milki na kuzisajili.
Usajili wa Hati na Nyaraka za Kisheria
24.
Mheshimiwa Spika,
katika mwaka wa fedha 2013/14 Wizara ilikuwa na lengo la kusajili hati za
kumiliki ardhi pamoja na nyaraka za kisheria zipatazo 80,000. Kati ya hizo hati za kumiliki ardhi
ni 35,000 na nyaraka za kisheria ni 45,000. Hadi Aprili, 2014 jumla ya hatimiliki na nyaraka za kisheria 50,592 zilisajiliwa. Kati ya hizo
hatimiliki ni 21,285 na nyaraka za kisheria
ni 29,307, zilisajiliwa chini ya Sheria ya Usajili wa Ardhi Sura
Na. 334 (Jedwali Na. 3A). Aidha, nyaraka 5,072 zilisajiliwa chini ya Sheria ya Usajili wa Nyaraka, Sura117 (Jedwali
Na. 3B). Pia, rehani ya mali zinazohamishika zipatazo 2,077 zilisajiliwa chini ya Sheria ya Usajili wa Rehani ya Mali Zinazohamishika,
Sura 210 (Jedwali Na. 3C). Aidha, katika mwaka wa
fedha 2014/15, Wizara inakusudia kusajili Hatimiliki 42,000, Nyaraka za Kisheria 45,000
na Hati ya Sehemu ya
Jengo/eneo 2,000.
Kuboresha
Kumbukumbu za Ardhi na Teknolojia ya Habari na Mawasiliano
25.
Mheshimiwa Spika, Wizara yangu
imeendelea kutekeleza jukumu muhimu la utunzaji wa kumbukumbu za ardhi na
kuzisimamia ipasavyo kwa kuweka na kuimarisha mifumo ya kielektroniki. Mifumo
hiyo ni pamoja na mfumo unganishi wa kuhifadhi kumbukumbu za ardhi wa Integrated
Land Management Information System (ILMIS) na mfumo wa kutunza kumbukumbu za
kodi ya ardhi (Land Rent Management System - LRMS).
26.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2013/14
Wizara iliahidi kuendelea na kazi ya kuweka mfumo unganishi wa kuhifadhi
kumbukumbu za ardhi (Integrated Land Management Information System - ILMIS). Napenda kuliarifu
Bunge lako Tukufu kuwa Serikali imepata fedha za kujenga mfumo huo na ujenzi
utaanza rasmi katika mwaka wa fedha 2014/15.
27.
Mheshimiwa
Spika,
Wizara pia imeendelea na kazi ya kusimika mfumo wa kielekitroniki wa kuhifadhi
kumbukumbu na kukadiria kodi ya Ardhi. Katika mwaka wa
fedha 2013/14
Wizara ilipanga kusimika mfumo huo katika Ofisi za Ardhi za Halmashauri 20.
Hadi Aprili, 2014 mfumo huu ulisimikwa katika Ofisi za Ardhi za Halmashauri 75 (Jedwali Na. 4). Katika mwaka wa fedha 2014/15
Wizara itaendelea na kazi ya kusimika mfumo wa kielekitroniki wa kuhifadhi
kumbukumbu na kukadiria kodi ya ardhi katika ofisi za Ardhi za Halmashauri 30.
UTHAMINI WA MALI
28.
Mheshimiwa
Spika,
Wizara yangu inalo jukumu la kuthamini na kuidhinisha taarifa za uthamini wa mali
kwa madhumuni mbalimbali ya kuwezesha maendeleo ya kiuchumi na kijamii. Kuna
aina kuu mbili za uthamini ambazo ni Uthamini wa Kawaida na Uthamini wa
Kisheria.
Uthamini wa Kawaida
29.
Mheshimiwa
Spika,
Uthamini wa Kawaida hufanyika kwa kuzingatia misingi ya kitaaluma na hauna
maelekezo maalum ya sheria. Uthamini huu hufanyika ili kuwezesha maamuzi
mbalimbali kufanyika yakiwemo maamuzi ya mauzo au manunuzi ya mali, kuweka mali
rehani, kuomba mikopo benki, dhamana ya mahakama, mizania na bima. Katika mwaka
wa fedha 2013/14 Wizara iliweka lengo la kuthamini na kuidhinisha
taarifa za uthamini wa mali 15,000. Hadi Aprili, 2014, Wizara iliidhinisha
taarifa za uthamini wa kawaida wa mali 7,904 (Jedwali Na.5A). Kwa mwaka wa fedha 2014/15,
Wizara itafanya na kuidhinisha taarifa za uthamini wa mali 10,000 kwa matumizi
mbalimbali kadri maombi yatakavyowasilishwa.
Uthamini wa Kisheria
30.
Mheshimiwa Spika, Uthamini wa Kisheria
hufanyika ili kuwezesha utozaji wa ada na ushuru wa Serikali kutokana na mauzo
au uhamisho wa umiliki wa mali, utozaji malipo ya awali (premium) wakati wa kutoa
milki, utozaji kodi ya pango la ardhi na ukadiriaji fidia za mali zinazoguswa
na miradi mbalimbali inayotekelezwa nchini. Katika mwaka wa
fedha 2013/14,
Wizara ilipanga kufanya na kuidhinisha taarifa za uthamini wa fidia wa mali 40,000. Hadi Aprili, 2014
Wizara iliidhinisha taarifa za uthamini wa mali 29,898 kwa ajili ya kulipa
fidia (Jedwali Na. 5B). Katika mwaka wa fedha 2014/15 Wizara
itawezesha uthamini wa mali 30,000.
Viwango vya Thamani
31.
Mheshimiwa Spika, Wizara imeendelea na
zoezi la kuhakikisha uwepo wa viwango sahihi vya soko kwa ajili ya ukadiriaji
thamani ya ardhi na mazao. Katika mwaka wa fedha 2013/14, Wizara
ilipanga kuendelea kufanya uchambuzi wa takwimu za bei ya soko kwa lengo la
kuhuisha viwango vya thamani sambamba na kuweka utaratibu endelevu wa kuhuisha
viwango hivyo. Hadi Aprili 2014, Wizara imehuisha viwango vya thamani vya mazao
mbalimbali katika Wilaya za mikoa ya Mwanza, Geita, Kagera, Mara, Shinyanga,
Simiyu, Tabora na Kigoma kwa kushirikiana na Halmashauri za Mikoa hiyo. Aidha, Wizara imehuisha viwango vya
thamani ya ardhi katika eneo la Makongo Juu Wilaya ya Kinondoni na Kata tatu
(3) za Wilaya ya Temeke (maeneo ya Kimbiji, Pemba Mnazi na Kisarawe II).
Pia, Wathamini wa
Halmashauri zote nchini wamepatiwa Mafunzo na Miongozo ya utaratibu wa kufanya
uchambuzi wa takwimu za bei ya soko na kuweka viwango vya thamani ya ardhi na
majengo. Lengo ni kuhakikisha mfumo endelevu wa uhuishaji viwango vya thamani
kadri ya mabadiliko ya bei ya soko. Katika mwaka wa
fedha 2014/15,
Wizara imepanga kuimarisha mifumo ya kielektroniki ya uwekaji na uhuishaji
viwango vya thamani ya ardhi, majengo na mazao. Nawaagiza Wataalam wa
uthamini nchini kushiriki kikamilifu kuhuisha viwango vya thamani ili viendane
na mabadiliko katika soko la mali kwenye maeneo yao.
32.
Mheshimiwa Spika, Wizara ikiwa ni
msimamizi wa taaluma ya uthamini imeandaa miongozo mbalimbali ya kuwajengea
uwezo na weledi Wathamini wa kumudu majukumu yao kwa mujibu wa taratibu za
kisheria na kitaaluma. Miongozo hiyo ni pamoja na; Mwongozo wa Utaratibu wa
Uthamini wa Fidia; Mwongozo wa Uchambuzi na uwekaji viwango vya thamani ya soko
la ardhi, majengo na mazao; na, miongozo ya ukadiriaji malipo ya premium wakati wa kumilikisha
ardhi, kodi ya pango la ardhi na gharama za kuhamisha makaburi pale ardhi
husika inapotwaliwa kwa manufaa ya umma. Katika mwaka wa
fedha 2014/15
Wizara itasambaza miongozo hiyo kwa wataalam na wadau wa uthamini nchini. Hivyo,
nawaagiza wataalam na wadau wa uthamini kuzingatia yaliyomo kwenye miongozo
hiyo ili iwawezeshe kutimiza wajibu wao na kuleta tija kwa umma kiuchumi na
kijamii. Ninawataka wathamini kutambua kwamba baadhi yao wamekuwa chanzo cha
migogoro kwa kujihusisha na vitendo visivyofaa kama kudai rushwa na hongo
badala ya kuthamini mali za wananchi kwa ukweli na haki. Aidha, kumekuwa na
migogoro mingi baada ya shughuli za uthamini ikiwa ni pamoja na uthamini hewa.
Wizara tayari imeweka mikakati ya kuziba mianya hiyo kwa kutumia upimaji wa
kielektroniki wa kila kipande cha ardhi na pia kutaka malipo ya uthamini
yafanyike kupitia benki teule na hivyo kuwabana wale wanaotumia ujanja wa
malipo kwa wathaminiwa hewa. Ninawaomba wananchi watupe ushirikiano katika
utekelezaji wa malipo kupita benki kwa kufungua akaunti katika benki teule
inapohitajika kufanya hivyo.
MABARAZA YA ARDHI NA
NYUMBA YA WILAYA
33.
Mheshimiwa Spika, tangu Sheria ya
Mahakama ya Ardhi Sura 216 ianze kutumika tarehe 1 Oktoba, 2003 jumla ya
Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya 49 yameundwa. Kati ya hayo Mabaraza 42 yanafanya kazi. Mabaraza haya
yanasikiliza na kuamua migogoro ya ardhi na nyumba kwa lengo la kudumisha haki,
usalama na amani katika jamii.
34.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2013/14
Wizara ilipanga kununua samani na vitendea kazi pamoja na kukarabati majengo ya
Mabaraza saba (7) ili yaanze kufanya kazi. Aidha, Wizara ilikusudia kuunda
Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya katika Wilaya tano (5) za Kilindi, Mbulu,
Kahama, Sengerema na Kasulu. Napenda kuliarifu Bunge lako tukufu kuwa Wizara
imekamilisha ukarabati wa majengo/ofisi za Mabaraza sita (6) pamoja na ununuzi
wa samani na vitendea kazi zikiwemo seti za kompyuta. Hata hivyo, Mabaraza
matano (5) hayajaundwa kutokana na hitaji kubwa la kuboresha mabaraza 49 yaliyoundwa.
35.
Mheshimiwa
Spika,
Wizara iliendelea kushughulikia utatuzi wa migogoro ya ardhi na nyumba kupitia
Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya na iliahidi kuamua mashauri 11,000. Kuanzia Julai, 2013
yalikuwepo mashauri 18,328 na hadi kufikia Aprili, 2014 mashauri mengine
11,548
yalifunguliwa. Katika kipindi
hicho jumla ya mashauri 11,432 yaliamuliwa hivyo mashauri 18,444 yaliyobaki na
yatakayofunguliwa yataendelea kushughulikiwa katika mwaka wa
fedha 2014/15
(Jedwali Na. 6).
36.
Mheshimiwa
Spika,
katika mwaka wa fedha 2013/14 niliahidi kuendelea kufuatilia utendaji kazi wa
wenyeviti ili kuhakikisha kuwa wanazingatia maadili ya kazi zao. Napenda
kulijulisha Bunge lako Tukufu kuwa Wizara imeandaa Mwongozo wa maadili ya kazi
ya Wenyeviti wa Mabaraza ya Ardhi na Nyumba ya Wilaya (Code of Conduct) utakaotumika
kufuatilia utendaji wao wa kazi.
37.
Mheshimiwa
Spika,
katika mwaka wa fedha 2014/15 Wizara itaendelea kuimarisha Mabaraza ya Ardhi na
Nyumba ya Wilaya 49 kwa kuyapatia vitendea kazi ili kuyawezesha kutatua migogoro
kwa haraka na kufikia uamuzi wa haki.
Aidha, Wizara itakarabati majengo/ofisi za Mabaraza ili kuboresha
mazingira ya kufanyia kazi.
Vilevile, Wizara itayapatia Mabaraza yaliyopo watumishi na kuendelea
kuunda Mabaraza katika Wilaya zingine kwa lengo la kuharakisha utatuzi wa
migogoro.
HUDUMA ZA UPIMAJI NA
RAMANI
38.
Mheshimiwa
spika,
upimaji ardhi na utayarishaji ramani za msingi ni moja ya majukumu ya Wizara.
Ramani hizo ni chanzo muhimu cha taarifa zinazohitajika katika kubuni na
kutayarisha Mipango ya Matumizi ya Ardhi kwa sekta mbalimbali.
Utayarishaji Ramani
39.
Mheshimiwa
spika,
katika mwaka wa fedha 2013/14 Wizara ilipanga kukamilisha kujenga na kuimarisha
kanzi ya taarifa za kijiografia (geodata base) katika Wilaya mpya 19
za Mikoa mipya minne (4) ya Geita, Katavi, Njombe na Simiyu; pamoja na
kuendelea na utekelezaji wa kazi hiyo katika mikoa ya Mwanza, Shinyanga, Kagera
na Mara. Napenda kuliarifu Bunge lako tukufu kuwa kazi ya kujenga na kuimarisha
kanzi katika Wilaya zote 19 katika mikoa mipya minne (4) pamoja na mikoa ya
Kagera na Mara imekamilika. Kazi hiyo inaendelea katika Mikoa ya Shinyanga na
Mwanza. Katika mwaka wa fedha 2014/15 Wizara
itakamilisha kujenga na kuimarisha kanzi ya taarifa za kijiografia katika mikoa
ya Shinyanga na Mwanza na itaanza kazi hiyo katika mikoa ya Kigoma, Tabora na
Rukwa.
40.
Mheshimiwa
Spika,
katika mwaka wa fedha 2013/14 Wizara yangu iliahidi kukamilisha kufunga mtambo
mpya wa uchapaji ramani. Wizara imekamilisha ufungaji wa mtambo huo. Kuwepo kwa
mtambo huo kunaiwezesha Serikali kuwa na uwezo wa kuchapa ramani zenye viwango
stahiki kwa matumizi mbalimbali. Katika mwaka wa
fedha 2014/15
Wizara itaandaa na kuchapa ramani za msingi za uwiano wa 1:2,500 kwa ajili ya
Jiji la Dar es Salaam. Aidha,
Wizara itandaa ramani za kuelekeza (guide maps) katika jiji la Dar es
Salaam na maeneo ya utalii kwenye mbuga za wanyama za Mikumi na Serengeti.
Mipaka ya Ndani ya
Nchi
41.
Mheshimiwa
Spika,
Wizara yangu imeendelea kushughulikia utatuzi wa migogoro ya mipaka ya
kiutawala katika maeneo mbalimbali kwa mujibu wa Matangazo ya Serikali. Katika
mwaka wa fedha 2013/14 Wizara iliahidi kujenga na kuimarisha taarifa za
kijiografia kwa ajili ya kutafsiri Matangazo ya Serikali (GN) kwa kushirikiana
na wadau mbalimbali. Hadi Aprili, 2014 Wizara ilikamilisha kutafsiri Matangazo
ya Serikali kwa Hifadhi za Taifa za Selous, Serengeti na Saadani. Aidha, alama
za kudumu za mipaka kati ya Hifadhi ya Serengeti na vijiji vinavyopakana na
hifadhi hiyo zimesimikwa na zinasubiri upimaji. Katika mwaka wa fedha 2014/15
Wizara itafanya kazi ya upimaji wa mipaka kati ya hifadhi ya Serengeti na
vijiji inavyopakana navyo pamoja na kutafsiri Matangazo ya Serikali. Aidha,
Wizara itahakiki na kupima mipaka ya Hifadhi ya Taifa ya Ngorongoro kwa
kushirikiana na TANAPA, wanavijiji na wadau wengine. Natoa rai kwa wapima
wote nchini kutambua kwamba wanawajibu kuhalalisha upimaji wao kwa mujibu wa
Sheria kwa kupata Baraka za Mkurugenzi wa Upimaji na Ramani kwa kazi zao.
Migogoro imeibuka kwa upimaji holela bila kuzingatia matakwa hayo ya sheria.
Mipaka ya Kimataifa
42.
Mheshimiwa
Spika,
Wizara yangu ina jukumu la kuweka na kutunza alama za mipaka kati ya Tanzania
na nchi jirani. Katika mwaka wa fedha 2013/14 Wizara iliahidi
kuimarisha alama za mipaka saba ya kimataifa kati ya Tanzania na nchi za
Msumbiji, Malawi, Zambia, Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo, Burundi, Uganda na
Kenya. Hadi Aprili 2014, uwekaji wa alama za mpaka wa eneo la kilomita 51 za nchi kavu kati ya
Tanzania na Msumbiji umekamilika. Mpaka kati ya Tanzania na Malawi katika ziwa
Nyasa mazungumzo yanaendelea. Vilevile, uwekaji wa alama 78 za mpaka kati ya
Tanzania na Zambia umefanyika katika eneo la Tunduma/Nakonde lenye urefu wa
kilomita 46.
Uwekaji wa alama 70
za mpaka kati ya Tanzania na Kenya umefanyika katika eneo la Sirari lenye urefu
wa kilomita 14.8.
Uwekaji wa alama za mpaka kati ya Tanzania na Burundi umeanza katika Wilaya ya
Ngara. Hadi Aprili 2014 alama 143 zimesimikwa na kupimwa. Mazungumzo ya upimaji
wa mpaka kati ya Tanzania na Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo yamefanyika kwa
nia ya kuanza upimaji.
43.
Mheshimiwa
Spika,
katika mwaka wa fedha 2014/15 Wizara yangu itaendelea na kazi ya upimaji wa
mipaka kati ya Tanzania na nchi za Kenya, Burundi, Zambia, Msumbiji na Jamhuri
ya Kidemokrasi ya Kongo pamoja na kuandaa kanzi ya mipaka hiyo. Aidha, kuhusu
mpaka kati ya Tanzania na Uganda, Wizara inaendelea kuwasiliana na Serikali ya
Uganda ili kuanzisha mazungumzo kwa ajili ya kukamilisha kazi zilizoanza
kufanyika katika mwaka wa fedha 2001/02.
Upimaji wa Mipaka ya
Vijiji
44.
Mheshimiwa
Spika,
Wizara yangu imekuwa ikiendelea na upimaji wa vijiji vinavyoendelea kuzaliwa
katika Halmashauri mbalimbali nchini. Katika mwaka wa
fedha 2013/14
Wizara iliahidi kupima mipaka ya vijiji 100 katika wilaya za Songea, Tunduru,
Nyasa, Namtumbo na Mbinga. Hadi Aprili 2014, Wizara imekamilisha upimaji wa
vijiji 145
katika Wilaya za Nyasa (29), Mbinga (68), Wanging’ombe (22) na Bagamoyo (26).
Upimaji wa Viwanja
na Mashamba
45.
Mheshimiwa
Spika, katika mwaka wa fedha 2013/14
Wizara yangu iliweka lengo la kuidhinisha ramani zenye viwanja 60,000 na mashamba 1,000. Hadi Aprili 2014, Wizara imeratibu na kuidhinisha ramani za upimaji zenye
viwanja 67,237 na mashamba 325 (Jedwali Na. 7A). Katika mwaka wa fedha 2014/15 Wizara imepanga
kuratibu na kuidhinisha ramani za upimaji
zenye viwanja 70,000 na mashamba 500.
46.
Mheshimiwa Spika, ili kurahisisha upimaji wa ardhi na kupunguza
gharama za upimaji kwa wananchi, Wizara katika mwaka wa fedha 2013/14 iliahidi kusimika na kupima alama za msingi za upimaji (control points) 300 katika miji 50. Hadi Aprili, 2014 Wizara imeweza kusimika na
kupima alama 104
katika miji saba (7)
ya Sikonge (15),
Kigoma Ujiji (20),
Mbogwe (10),
Karumwa (10)
Katoro (5),
Uvinza (20)
na Bagamoyo (24).
Katika mwaka wa fedha 2014/15 Wizara itaendelea kukamilisha usimikaji wa alama 240 zilizosalia katika
miji hiyo (Jedwali Na. 7B).
47.
Mheshimiwa
Spika,
ili kuhakikisha kuwa huduma ya upimaji ardhi inasogezwa karibu zaidi na wananchi,
Wizara yangu iliahidi kugatua Mamlaka ya kusimamia kazi za upimaji ardhi katika
Kanda. Hadi Aprili, 2014 Wizara imefanya maandalizi ya kuhamishia huduma za
upimaji na ramani katika ofisi za kanda sita zilizopo Tabora, Mwanza, Dodoma,
Moshi, Mbeya na Mtwara. Katika mwaka wa fedha 2014/15, Wizara itaanza
kutoa huduma za Upimaji Ardhi katika Kanda hizo.
48.
Mheshimiwa
Spika,
katika mkakati wa kuboresha utunzaji wa kumbukumbu za Upimaji Ardhi, Wizara
inaendelea na kazi ya kuzibadili kumbukumbu zilizopo kwenda katika mfumo wa
kanzi ya kie-lektroniki (Digital Cadastral Database) ili ziweze
kuunganishwa na mfumo unganishi wa kutunza kumbukumbu za ardhi (Integrated
Land Management Information System – ILMIS). Ili kurahisisha upatikanaji wa taarifa za upimaji ardhi
na kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi, Wizara imebadilisha kumbukumbu za
ramani 5,000
za Jiji la Dar Es Salaam na kuziweka katika ramani unganishi (Cadastral
Index Map).
Katika mwaka wa fedha 2014/15, Wizara itaandaa kanzi ya viwanja katika miji
mbalimbali nchini na kutayarisha vipengele (Modules) vitatu vya Mfumo wa
Utunzaji Kumbukumbu za Upimaji Ardhi (Survey Registration System – SRS) ili kuboresha utoaji
wa huduma za Upimaji Ardhi nchini.
Upimaji wa Ardhi
Chini ya Maji
49.
Mheshimiwa
Spika,
jukumu mojawapo la Wizara ni upimaji wa ardhi chini ya maji na kutayarisha
ramani zinazoonesha umbile la ardhi chini ya maji hususan milima, mabonde,
miinuko na kina cha maji. Katika mwaka wa fedha 2013/14 Wizara ilipanga
kununua kifaa cha upimaji ardhi chini ya maji kijulikanacho kama echo
sounder
ili kuwezesha kazi ya upimaji vina vifupi iweze kufanyika. Kifaa hicho
kimenunuliwa.
Mfuko wa Kupima
Viwanja
50.
Mheshimiwa Spika, Wizara inaendelea
kusimamia Mfuko wa Mzunguko
wa Kupima Viwanja (Plot Development Revolving Fund – PDRF) ambao huzipatia
mikopo Halmashauri mbalimbali nchini kwa ajili ya kulipa fidia, kupima viwanja
na kuvimilikisha kwa wananchi na taasisi mbalimbali. Katika mwaka wa fedha 2013/14
Wizara iliahidi kuongeza juhudi za ufuatiliaji wa urejeshaji wa mikopo pamoja
na Halmashauri sugu kukatwa madeni ya mikopo hiyo kutoka katika marejesho ya
asilimia 30 ya fedha ambazo Halmashauri hurejeshewa baada ya makusanyo yake.
Hadi Aprili, 2014 madeni kwa Halmashuri mbalimbali yamepungua kutoka Shilingi milioni
633.6
hadi kufikia Shilingi milioni 325.5 (Jedwali Na. 7C). Nahimiza
Halmashauri zinazodaiwa kulipa madeni haya ili fedha hizi zikopeshwe katika
Halmashauri zingine.
51.
Mheshimiwa
Spika,
Wizara imeendelea kuhimiza Halmashauri kurejesha fedha zilizokopeshwa kutoka
kwenye mradi wa viwanja 20,000. Hadi Aprili 2014, Halmashauri nne (4)
zilizokopa fedha kutoka kwenye mradi huo zilirejesha sehemu ya mikopo yao na
kufanya deni hilo kupungua kutoka shilingi bilioni 1.87 hadi kufikia Shilingi milioni 780.39 (Jedwali Na. 7D). Wizara itaendelea
kufuatilia Halmashauri ambazo zinadaiwa ili ziweze kurejesha fedha hizo.
MIPANGOMIJI NA
VIJIJI
52.
Mheshimiwa
Spika,
mojawapo ya majukumu ya msingi ya Wizara yangu ni usimamizi wa uendelezaji na
udhibiti wa ukuaji wa miji na vijiji nchini. Jukumu ambalo hutekelezwa kwa
mujibu wa Sera, Sheria, Kanuni, Taratibu na Miongozo mbalimbali inayotolewa
kuhusiana na masuala ya uendelezaji miji na vijiji nchini.
53.
Mheshimiwa
Spika,
katika kipindi cha muongo mmoja tumeshuhudia ongezeko la watu na kasi ya ukuaji
wa miji na vijiji hapa nchini. Ongezeko hili linajidhihirisha katika takwimu za
sensa ya Taifa ya Watu na Makazi ya mwaka 2012. Wakazi wa mijini waliongezeka
kutoka milioni 7.9
sawa na asilimia 23.1 mwaka 2002 hadi kufikia watu milioni 12.7 sawa na asilimia 29.1 mwaka 2012. Ongezeko
hili limekuwa changamoto kubwa kwa Mamlaka za Upangaji miji kushindwa kutoa
huduma za kiuchumi na kijamii kwa kiwango stahiki na kufanya miji yetu kukua
kiholela. Suala la ukuaji wa miji endelevu ni kichocheo cha maendeleo hivyo
tunahitaji kuwekeza katika ustawi wa miji kwa kizazi cha sasa na kijacho kwa
kupanga na kusimamia uendelezaji wa miji hapa nchini.
Uandaaji na
utekelezaji wa Mipango ya Jumla ya Uendelezaji Miji
54.
Mheshimiwa
Spika,
katika kupanga miji, Wizara kwa kushirikiana na Halmashauri za miji nchini
huandaa Mipango ya Jumla kwa ajili ya kusimamia uendelezaji na udhibiti wa
ukuaji wa miji hiyo. Mipango hiyo iko ya aina mbili: Mipango Kabambe ambayo hutoa mwongozo wa uendelezaji miji
kwa muda mrefu wa miaka ishirini na Mipango ya Muda wa Kati ya Matumizi ya
Ardhi ambayo hutoa mwongozo wa uendelezaji miji kwa muda wa miaka kumi. Kazi ya
uaandaaji wa Mipango hiyo hufanyika kwa kutumia dhana shirikishi ambapo Mamlaka
zote za Upangaji zinazohusika na mchakato huo hujengewa uwezo.
55.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2013/14
Wizara kwa kushirikiana na Halmashauri za Jiji la Dar es Salaam ziliendelea
kukamilisha maandalizi ya Mpango Kabambe wa jiji la Dar es Salaam ambapo rasimu
ya mwisho iliwasilishwa kwa wadau na Mtaalam Mwelekezi anaendelea kuiboresha
kwa kutumia maoni na mapendekezo yaliyotolewa na wadau. Aidha, Wizara kwa kushirikiana na
Halmashauri ya Mji Mdogo wa Bagamoyo imekamilisha maandalizi ya Rasimu ya awali
ya Mpango Kabambe wa mji huo. Pia, Wizara kwa kushirikiana na Halmashauri ya
Wilaya ya Mafia ilikamilisha maandalizi ya Rasimu ya Mpango wa Muda wa Kati wa
Matumizi ya Ardhi wa Mji wa Kilindoni. Rasimu za mipango hiyo ziliwasilishwa
kwa wadau wa Halmashauri husika kwa ajili ya kuzitolea maoni. Wizara inaendelea
kushirikiana na Halmashauri za Manispaa ya Sumbawanga na Mji wa Bariadi kuandaa
Mipango Kabambe ya miji hiyo.
56.
Mheshimiwa
Spika,
katika mwaka wa fedha 2014/15 Wizara kwa kushirikiana na Halmashauri za Manispaa
ya Sumbawanga, Wilaya ya Mafia, Mji Mdogo wa Bagamoyo na Bariadi itakamilisha
kuandaa Mipango ya Jumla ya miji hiyo. Aidha, Wizara kwa kushirikiana na
Halmashauri ya Jiji la Arusha na Halmashauri za Arusha na Meru itaanza
maandalizi ya Mipango Kabambe ya Jiji hilo na viunga vyake kwa kutumia Mtaalam
Mwelekezi. Aidha, Wizara kwa kushirikiana na Halmashauri za Manispaa za Lindi
na Mtwara zitaanza maandalizi ya Mipango Kabambe ya Miji hiyo. Natoa wito
kwa Halmashauri zote nchini ambazo hazina Mipango ya Jumla kutenga fedha za
kuandaa mipango hiyo.
Uandaaji na
Utekelezaji wa Mipango ya Kina ya Uendelezaji Miji
57.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha
mwaka wa fedha 2013/14 Wizara kwa kushirikiana na Halmashauri ya Manispaa
ya Kinondoni imeendelea na utekelezaji wa hatua ya awali ya uandaaji wa Mpango
wa Uendelezaji upya eneo la Manzese. Uhamasishaji wa wadau katika ngazi ya
Mkoa, Wilaya, Kata na Mtaa pamoja na ukusanyaji wa taarifa na takwimu za hali
halisi ya eneo hilo umefanyika. Aidha, Wizara kwa kushirikiana na Halmashauri
ya Mji wa Njombe imekamilisha maandalizi ya Rasimu ya Mpango wa Uendelezaji
Upya Eneo la Kati la Mji huo. Pia, Wizara kwa kushirikiana na Manispaa ya
Kinondoni imeanza zoezi la kuhuisha Mpango wa Kina wa Makongo kwa kutumia dhana
ya kuendeleza eneo na kudai tozo ya maboresho (betterment fee). Awamu ya kwanza ya
utekelezaji wa zoezi hili itahusisha upimaji wa barabara kuu.
58.
Mheshimiwa
Spika,
katika mwaka wa fedha 2014/15 Wizara kwa kushirikiana na Manispaa ya Kinondoni
itaendelea na kazi ya kuchambua takwimu na kuandaa rasimu ya awali ya Mpango wa
Uendelezaji Upya Eneo la Manzese. Wizara itaendelea na utekelezaji wa kuboresha
Mpango wa Kina wa Makongo; zoezi ambalo litahusisha upimaji wa barabara za
ndani (access roads)
pamoja na kupima viwanja ndani ya eneo la Mpango. Wizara kwa kushirikiana na
Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni itawezesha uboreshaji wa eneo la Mbweni
JKT kwa kuweka miundombinu stahiki. Aidha, Wizara itaendelea na utekelezaji wa
jukumu lake la kukagua, kuidhinisha na kuhifadhi michoro ya Mipangomiji 500 ya maeneo yaliyopangwa.
Vilevile, Wizara itaandaa miongozo ya namna ya kupanga matumizi ya ardhi katika
miji midogo nchini.
Uendelezaji wa Mji
Mpya wa Kigamboni
59.
Mheshimiwa
Spika,
katika mwaka wa fedha 2013/14 Wizara yangu iliahidi kuendeleza Mji wa Kigamboni;
kuingia mkataba na makampuni mawili ya kujenga nyumba, kufanya uthamini wa mali
na kulipa fidia kwa wananchi ili kupisha utekelezaji wa mradi na kujenga uwezo
wa Wakala wa Uendelezaji wa Mji Mpya Kigamboni ili iweze kutekeleza majukumu
yake ipasavyo. Naomba kuliarifu Bunge lako Tukufu kwamba Wizara yangu haikuweza
kutekeleza kazi hizo kama ilivyoahidi kutokana na ukosefu wa fedha. Hata hivyo,
Wizara yangu imekamilisha uandaaji wa rasimu ya muundo wa Wakala wa Uendelezaji
wa Mji Mpya wa Kigamboni na kuanzisha ofisi yake katika eneo la mradi.
Kulitokea ucheleweshwaji katika kumteua Mtaalamu wa Fedha (Transaction
Adviser and Fund Raiser) kwa sababu ya kukidhi matakwa ya sheria ya manunuzi.
Hatimaye mwezi Machi, 2014 mtaalam aliteuliwa na sasa ameanza kazi yake. Jambo
hili linatarajiwa kuongeza kasi katika kupata fedha za kutosha kwa ajili ya
utekelezaji wa mradi.
60.
Mheshimiwa
Spika,
katika mwaka wa fedha 2014/15 Wizara yangu itakamilisha Mpango wa Mji Mpya wa
Kigamboni kwa kufanya mkutano wa wadau (public hearing) ili uweze
kuidhinishwa; Kuandaa mipango ya kina ya maeneo yaliyopo ndani ya Mpango
Kabambe wa Mji Mpya wa Kigamboni; Kuainisha, kulipa fidia na kupima maeneo ya
miundombinu na umma katika eneo la mradi na kusimamia utekelezaji wa Mpango
Kabambe kupitia Wakala wa Uendelezaji wa Mji Mpya Kigamboni kwa kushirikiana na
wananchi.
61.
Mheshimiwa
Spika,
ninatoa rai tena kwa wananchi wa Kigamboni kuwa na imani na mradi huu.
Ninawashukuru kwa uvumilivu na ushirikiano wao na kutambua azma ya Serikali
kujenga Mji Mpya wenye viwango. Jambo hili ni gumu na linachukua mda lakini
hatua iliyofikiwa si haba kwa zoezi lenyewe. Niondoe wasiwasi kwa wale ambao
wanadhani kwamba kazi hii imeshindikana kwa hiyo tuondokane nayo. Mradi huu umetajwa kwa jina katika
Ibara ya 60(b)(iv) ya Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi ya Mwaka 2010
ambayo inaahidi “Kuanzisha Mji Mpya wa Kisasa wa Kigamboni (Kigamboni New City)”. Hii pekee ni ishara
tosha kuonesha wajibu wa Serikali katika kutoa kipaumbele kutekeleza kazi hii.
62.
Mheshimiwa
Spika,
kazi ya kuanzisha mji ilianza kwa Serikali kuunda chombo cha Kigamboni
Development Agency - (KDA) ambao ni Wakala wa Kuendeleza Mji Mpya wa Kigamboni.
Tayari Makao Makuu ya Wakala huo yamefunguliwa huko Kigamboni ambayo ni hatua
kubwa na muhimu katika utekelezaji wa mradi huu. Miaka 50 baada ya Uhuru, KDA
ni Wakala wa pili kuundwa baada ya CDA ambayo inajenga Makao Makuu yetu hapa
Dodoma. Nirudie tena kwamba ili kulinda maslahi ya wananchi, viwango vya fidia
vilivyopangwa ni endelevu na wakati ukifika umahiri na umuhimu wake utaonekana.
Ninahimiza wananchi wa Kigamboni kuendelea kuwa wavumilivu na kutokubali
kurubuniwa kwa kuuza maeneo yao kwa wajanja ambao, baada ya viwango vya fidia
kutajwa, wamejitokeza wakitaka
kununua ardhi za wananchi kwa bei poa ili wao baadaye wafidiwe na KDA.
Itambuliwe kuwa viwango vya fidia katika Awamu ya Kwanza ya Mradi ni shilingi
35,000 kwa mita mraba sawa na shilingi 141,645,000 kwa ekari moja. Hiki ni
kiwango kwa mujibu wa sheria kulingana na soko na thamani ya ardhi itakavyokuwa
katika mji mpya.
63.
Mheshimiwa
Spika, wananchi wa Kigamboni
watambue Mamlaka ya Upangaji Mji wao ni KDA na wasikubali na kuyumbishwa na
wanaotaka kupima maeneo ya wananchi kabla ya fidia stahiki kulipwa. Pia
nifafanue kwamba wananchi wa Kigamboni wataendelea kubaki Kigamboni katika
makazi yatakayojengwa huko Uvumba- kata ya Kibada (Resettlement City). Wananchi
watawezeshwa kutumia sehemu isiyopungua asilimia kumi ya fidia yao kununua hisa
za KDA hivyo kuendelea kufaidi matunda ya mji mpya wa Kigamboni kwa sasa na
vizazi vijavyo. Hii ndiyo njia ya kisasa kwa mwananchi kubaki kwenye ardhi yake
katika soko huria wakati mji mpya wenye viwango unajengwa.
64.
Mheshimwa
Spika,
katika fani yoyote na kazi yoyote, hakuna viwango bila weledi na nidhamu kwa
hiyo hali hii inataka pia uzalendo. Ninafurahi kuwatangazia kuwa Serikali
imeomba msaada wa wataalam kutoka Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China. Jopo la
wataalam wa Mipango Miji kutoka China litawasili Juni, 2014 ili kushirikiana na
wataalam wetu katika Upangaji wa Mji Mpya wa Kigamboni, Miji ya Lindi na
Mtwara. Wizara ina imani kuwa utaratibu wa kupata fedha za kuendeleza Mji Mpya
wa Kigamboni ukikamilika mambo mengi ya mwanzo (teething problems) yatapungua na kasi
utekelezaji wa mji huo itaongezeka.
Urasimishaji
Makazi Holela
65.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2013/14
Wizara ilishirikiana na Halmashauri ya jiji la Mwanza kurasimisha makazi
holela. Hadi Aprili 2014, jumla ya makazi 3,008 yalirasimishwa na
jumla ya viwanja 2,308 vimepimwa na Hati miliki za muda mrefu 911 zimetolewa katika Jiji
la Mwanza. Aidha, elimu ya urasimishaji na mikakati ya kuzuia makazi holela
mijini imetolewa kwa wataalam wa Halmashauri 25 katika mikoa ya Kanda
ya Nyanda za Juu Kusini ambayo ni Iringa, Mbeya na Rukwa. Katika mwaka wa fedha 2014/15,
Wizara itaendelea kuratibu na kusimamia Programme ya Taifa ya kurasimisha na
Kuzuia Makazi Holela kwa kutoa elimu ya urasimishaji na mikakati ya kuzuia
makazi holela mijini kwa wataalam wa Halmashauri katika mikoa ya Kanda ya
Kaskazini ambayo ni Tanga, Kilimanjaro, Arusha na Manyara.
Usimamizi na
Udhibiti wa Uendelezaji wa Miji
66.
Mheshimiwa Spika, Wizara imeendelea
kutoa elimu na kusambaza nakala za Sheria ya Mipangomiji Na.8 ya mwaka 2007 kwa
wadau mbalimbali. Elimu ya Sheria hiyo imetolewa kwa wataalamu wa sekta ya
ardhi katika mikoa ya Tabora, Shinyanga, Kigoma, Katavi, Singida na Dodoma.
Lengo ni kuwajengea uwezo wataalamu wa Mipangomiji katika kutekeleza majukumu
yao. Katika mwaka wa fedha 2014/15, Wizara itaendelea kutoa elimu ya Sheria hiyo na
marekebisho yake kwa wataalam katika mikoa ya Tanga, Kilimanjaro, Arusha,
Manyara, Iringa, Mbeya, Njombe na Ruvuma.
Usimamizi na
Udhibiti wa Uendelezaji wa Vijiji
67.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2013/14
Wizara ilitoa elimu ya Mwongozo wa kupanga makazi ya vijiji kwa wataalam na
wadau katika mikoa iliyopo Kanda ya Nyanda za Juu Kusini (Iringa, Njombe, Rukwa
na Mbeya) ili kwenda sambamba na Programu ya Southern Agricultural Growth
Corridor of Tanzania
(SAGCOT). Vilevile, Halmashauri ya Wilaya ya Bagamoyo na Mvomero zilijengewa
uwezo wa kuandaa Mipango ya Makazi ya Vijiji vinne (4) vya Fukayosi na Kidomole
Wilayani Bagamoyo; Lukenge na Hembeti Wilayani Mvomero.
68.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2014/15
Wizara itaendelea kuzijengea uwezo Mamlaka za Upangaji zikiwemo Halmashauri za
Wilaya na Vijiji ili kuziwezesha kuandaa Mipango ya Kina ya Makazi ya Vijiji
kwa ajili ya vitovu vya huduma vya vijiji 10 vinavyokua kwa kasi. Vilevile,
Wizara itaandaa na kutunza Mfumo wa Kitaifa wa kumbukumbu za vijiji; itaendelea
kufuatilia na kutathmini utekelezaji wa mipango ya uendelezaji makazi vijijini
katika wilaya zenye Mipango hiyo zikiwemo wilaya za Urambo, Manyoni, Bariadi na
Babati. Aidha, elimu ya mwongozo wa uandaaji wa mipango ya makazi ya vijiji
itatolewa na miongozo hiyo kusambazwa katika mikoa iliyopo katika Kanda ya Ziwa
ambayo ni Kagera, Mwanza, Shinyanga, Mara, Geita na Simiyu. Natoa rai kwa
Halmashauri za Wilaya zote nchini, hasa katika maeneo ambapo elimu hii imetolewa;
wasimamie na kuwezesha upangaji wa makazi ya vijiji vyao, ili kuwezesha vijiji
hivyo kuwa na makazi yaliyopangwa na kuwa na maeneo ya huduma za jamii.
MIPANGO YA MATUMIZI YA ARDHI
Mpango wa Taifa wa Matumizi ya ardhi
69.
Mheshimiwa Spika, umuhimu wa ardhi ni wa
kipekee. Nikimnukuu R. S. Simpson kwenye kitabu chake cha Land Law and
Registration, 1976 alisema:-
“ardhi ni chanzo cha utajiri wote. Kutokana na ardhi tunapata kila
kitu tutumiacho chenye thamani iwe chakula, mavazi, nishati, makazi, vyuma au vito.
Matumizi yote ya thamani yanatokana na ardhi yawe chakula, nguo, mafuta ya
kuendeshea mitambo, hifadhi, chuma au mawe ya thamani (vito). Tunaishi juu ya
ardhi na kutokana na ardhi na maiti au majivu yetu hurudi ardhini tunapokufa.
Uwepo wa ardhi ni ufunguo wa uhai wa binadamu na mgawanyo na matumizi yake ni
muhimu sana”.
70.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2013/14, Serikali ilipitisha Mpango wa Taifa wa Matumizi ya Ardhi.
Madhumuni ya Mpango huo ni kuweka utaratibu wa kuongoza matumizi ya rasilimali
za ardhi yenye usawa kwa ajili ya kuboresha maisha ya jamii, maendeleo ya
kiuchumi na kijamii na uendelevu wa rasilimali za kimazingira nchini; na hivyo,
kuchangia katika jitihada za serikali katika utekelezaji wa MKUKUTA. Hivi sasa
marekebisho ya mwisho pamoja na kuhuisha takwimu vipo katika hatua za mwisho
ili uchapishwe na kusambazwa kwa wadau. Utekelezaji wa programu za kipaumbele
(Kilimo, Mifugo, Maji, Makazi, Mipango ya Matumizi ya Ardhi) utaanza katika
mwaka wa fedha 2014/15 kwa
ushirikiano na wadau.
71.
Mheshimiwa
Spika,
katika mwaka wa fedha 2013/14 Wizara iliahidi kutoa mafunzo kwa viongozi na watendaji wa
Wilaya kuhusu sheria za ardhi na mbinu shirikishi za uandaaji wa mipango ya
matumizi ya ardhi na kushirikiana na Halmashauri za Wilaya za Newala, Tarime,
Rorya na Maswa kuandaa Mipango ya Matumizi ya Ardhi ya Wilaya. Hadi Aprili,
2014 Viongozi na watendaji wa Wilaya za Tarime, Rorya, Newala na Geita wamepewa
mafunzo juu ya maudhui ya sheria za ardhi na sheria ya upangaji matumizi ya
ardhi. Aidha, kazi ya kuandaa Mipango ya Matumizi ya Ardhi ya Wilaya hizo
inaendelea. Katika mwaka wa fedha 2014/15 Wizara itakamilisha kazi ya kuandaa Mipango ya Matumizi ya Ardhi
ya Wilaya za Tarime, Rorya, Newala na Geita pamoja na kutoa mafunzo kwa viongozi na watendaji wa Wilaya nne kuhusu sheria za ardhi na mbinu
shirikishi za uandaaji wa mipango ya matumizi ya ardhi pamoja na kuwezesha
uandaaji wa mipango ya matumizi ya ardhi ya wilaya kwa kushirikiana na Halmashauri
za Wilaya husika.
72.
Mheshimiwa Spika,
katika mwaka wa fedha 2013/14 Wizara iliahidi kukamilisha uandaaji na uchapaji wa Kanuni za
Sheria ya Mipango ya Matumizi ya Ardhi ya Mwaka 2007 na kuchapisha na kusambaza toleo la pili
la Mwongozo wa Upangaji na Usimamizi Shirikishi wa Matumizi ya Ardhi ya Vijiji.
Wizara imekamilisha uandaaji wa Kanuni za Sheria ya Mipango ya Matumizi ya
Ardhi ya mwaka 2007. Pia, Mwongozo wa Upangaji na Usimamizi Shirikishi wa
Matumizi ya Ardhi umechapishwa na kusambazwa kwa wadau. Katika mwaka wa fedha 2014/15 Wizara itachapisha kanuni hizo na kuzisambaza
kwa wadau na itatafsiri Mwongozo wa Upangaji na Usimamizi Shirikishi wa
Matumizi ya Ardhi ya Vijiji katika lugha ya Kiswahili.
Mipango ya Matumizi ya Ardhi ya Wilaya na Vijiji
73.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2013/14,
Tume ya Taifa ya Mipango ya Matumizi ya Ardhi iliahidi kushirikiana na wadau
kuwezesha uandaaji wa mipango ya matumizi ya ardhi ya vijiji 150 katika wilaya mbalimbali hususan za mipakani mwa nchi na zile zenye
migogoro sugu ya ardhi. Aidha,
Wizara ilipanga kutekeleza mradi wa SAGCOT kwa kuandaa mipango ya matumizi ya
ardhi ya vijiji ili kutenga maeneo yanayotosheleza mahitaji ya matumizi ya
ardhi ya wananchi, kutenga maeneo ya vyanzo vya maji na ardhi inayofaa kwa
uwekezaji. Hadi Aprili, 2014 jumla ya vijiji 94 vimeandaliwa
mipango ya matumizi ya ardhi katika Wilaya mbalimbali (Jedwali Na. 8). Pia, kazi ya kutekeleza mradi wa SAGCOT imeanza kwa Mkandarasi kupitia
Mpango wa Matumizi ya Ardhi katika ukanda wa Reli ya Uhuru. Katika mwaka wa fedha 2014/15 Wizara kwa kushirikiana na wadau mbalimbali
itawezesha uandaaji wa Mipango ya Matumizi ya Ardhi ya Vijiji 200 pamoja na kuendelea na uandaaji wa mipango ya matumizi ya Ardhi ya
vijiji na wilaya katika ukanda wa SAGCOT na kutenga maeneo ya uwekezaji.
MAENDELEO YA NYUMBA
74.
Mheshimiwa
Spika,
Wizara yangu imeendelea kusimamia Sekta ya Nyumba ili kuwezesha upatikanaji wa
nyumba na kuona kuwa sekta hii inachangia kikamilifu katika maendeleo ya
kiuchumi na kijamii. Katika kutekeleza jukumu hilo, Wizara itaendelea kuweka
sera na mikakati ya utekelezaji itakayowezesha wananchi kumiliki au kuwa na
nyumba bora za gharama nafuu.
75.
Mheshimiwa
Spika,
katika mwaka wa fedha 2013/14, Wizara yangu iliahidi kuendelea kushirikiana na
Wizara ya Fedha na Benki Kuu katika kuweka mifumo ya kifedha itakayowezesha
upatikanaji wa mikopo yenye masharti nafuu. Napenda kuliarifu Bunge lako tukufu
kuwa mkataba wa mkopo wa Tanzania Housing Finance umerejewa upya ili
kuipata kampuni ya Tanzania Mortgage Refinancing Company iliyowezeshwa kutoa
mikopo ya nyumba au mtaji kwa benki za biashara ili nazo zitoe huduma ya mikopo
ya nyumba kwa wananchi hata kama benki hizo hazijaanza kutoa mikopo kwa
wananchi wanaonunua nyumba (Pre-financing). Hadi Aprili, 2014 jumla ya benki 19 zilikuwa zinatoa mikopo
ya nyumba kwa miaka 15-20, tofauti na benki 10 zilizokuwa zinatoa mikopo ya nyumba kwa
kipindi kisichozidi miaka 15.
76.
Mheshimiwa
Spika, Katika mwaka wa fedha 2014/15,
Wizara yangu itatoa elimu kwa umma kuhusu utaratibu wa mikopo ya nyumba, ikiwa
ni pamoja na haki na wajibu wa mkopaji na mkopeshaji kwa mujibu wa sheria.
Aidha, Wizara itaendelea kushirikiana na Benki Kuu ya Tanzania kuweka utaratibu
utakaowezesha mikopo ya nyumba kutolewa kwa masharti nafuu kuliko mikopo ya
kibiashara. Wizara itashirikiana na vyombo vya fedha kuweka mazingira ya
kuvutia uwekezaji katika sekta ya nyumba ikiwa ni pamoja na kuvutia
waendelezaji milki binafsi ili wajenge nyumba za gharama nafuu za kuuza na
kupangisha.
77.
Mheshimiwa
Spika,
katika mwaka wa fedha 2013/14 Wizara yangu iliendelea kushirikiana na Wizara ya
Fedha pamoja na Benki Kuu ya Tanzania kukamilisha uundwaji wa Mfuko wa Mikopo
Midogomidogo ya Nyumba. Mfuko huo umeanza kwa mtaji wa Dola za Marekani milioni
3
ambazo ni sehemu ya mkopo uliotolewa na Benki ya Dunia kupitia mradi wa
kuendeleza sekta ya nyumba hapa nchini (Tanzania Housing Finance Project). Aidha, Serikali
iliendeleza mazungumzo na Benki ya Dunia kwa lengo la kupata fedha zaidi kwa
ajili ya Mfuko huo. Katika mwaka wa fedha 2014/15, Wizara yangu
kwa kushirikiana na wadau mbalimbali itatoa elimu kwa umma kuhusu mfuko huo na
kuwahamasisha kutumia huduma zake.
78.
Mheshimiwa
Spika,
katika mwaka wa fedha 2013/14, Wizara iliahidi kuandaa Sheria ya kusimamia Sekta
ya Nyumba ikiwa ni pamoja na kuweka masharti ya uendelezaji nyumba, kuelekeza
haki na wajibu wa waendelezaji nyumba, wanunuzi, wamiliki na wapangaji wa
nyumba. Kazi hiyo itaendelea katika mwaka wa fedha 2014/15.
79.
Mheshimiwa
Spika,
katika mwaka wa fedha 2013/14, Wizara iliahidi kuwa mpango wa nyumba kwa
watumishi wa umma ungeanza kutekelezwa. Katika kuwezesha utekelezaji wa mpango
huo Wizara ilizielekeza Halmashauri zote kutenga ardhi kwa ajili ya ujenzi wa
nyumba kwa watumishi wa umma. Aidha, Watumishi Housing Company (WHC) iliyoundwa na
Mifuko ya Hifadhi ya Jamii na Shirika la Nyumba la Taifa itasimamia utekelezaji
wa mpango huo. Katika mwaka wa fedha 2014/15, Wizara
itaendelea kuwezesha utekelezaji wa mpango huo ikiwa ni pamoja na kuunda Mfuko
wa Dhamana ya Mikopo ya Nyumba kwa Watumishi wa Umma.
Wakala wa Taifa wa
Utafiti wa Nyumba na Vifaa vya Ujenzi
80.
Mheshimiwa Spika, Wakala wa Taifa wa
Utafiti wa Nyumba na Vifaa vya
Ujenzi (NHBRA) una majukumu ya kutafiti, kukuza, kuhamasisha na kusambaza
matokeo ya utafiti na utaalamu wa ujenzi wa nyumba za gharama nafuu nchini.
81.
Mheshimiwa
Spika,
katika mwaka wa fedha 2013/14 Wizara kupitia Wakala imeendesha Semina na mafunzo
kwa vitendo ambapo jumla ya washiriki 974 kutoka katika Wilaya za Sikonge (100), Biharamulo (56), Halmashauri ya
Arusha (160)
na Muleba (550).
Aidha, mafunzo kwa vitendo yalitolewa kwa wakufunzi na wahitimu wa VETA (47), Tarime (42), Korogwe (15) na Mafundi sanifu (4) kutoka Manispaa ya
Tabora. Vilevile, jumla ya mashine 250 za kufyatulia tofali zilizalishwa.
Katika mwaka wa fedha 2014/15 Wakala utaendelea kuhamasisha na kueneza
teknolojia ya ujenzi wa nyumba za gharama nafuu katika Wilaya za Nkasi,
Kishapu, Chunya na Tandahimba.
82.
Mheshimiwa
Spika,
katika mwaka wa fedha 2013/14, Wizara iliahidi kushirikiana na Halmashauri za
Miji na Wilaya kuimarisha vikundi vya ujenzi wa nyumba vilivyoanzishwa na
kutangaza huduma zinazotolewa kupitia vyombo vya habari. Napenda kuliarifu
Bunge lako tukufu kuwa Wakala umeendelea kujitangaza kupitia vyombo vya habari.
Katika mwaka wa fedha 2014/15 Wakala utaendelea kujitangaza kupitia vyombo vya
habari na kushiriki maonesho mbalimbali ya kitaifa ili kusambaza huduma kwa
wananchi wengi zaidi.
SHIRIKA LA NYUMBA LA
TAIFA
Kuimarisha
Utendaji Kazi wa Shirika
83.
Mheshimiwa
Spika,
katika
mwaka wa fedha 2013/14 Wizara iliendelea kusimamia Shirika la Nyumba la
Taifa (NHC) katika utekelezaji wa malengo ya Mpango Mkakati wake wa kipindi
cha mwaka 2010/11-2014/15 ikiwa ni
pamoja na kuimarisha utendaji kazi. Shirika limeendelea kuboresha utendaji kazi
wake kwa kuajiri wataalamu wa fani mbalimbali wapatao 31 kwa ajili ya kuongeza
ufanisi na tija. Ajira hizi zimepandisha uwiano wa wafanyakazi wenye taaluma na
wasiokuwa na taaluma kufikia asilimia 51 kwa 49 dhidi ya lengo la
asilimia 70
kwa 30
ifikapo Juni, 2015. Pia, watumishi
wa ngazi zote walipatiwa mafunzo ya utambuzi na ulezi wa vipaji pamoja na
ushirikiano kati ya sekta za umma na sekta binafsi (public – private
partnership).
84.
Mheshimiwa
Spika, Wizara
iko kwenye mchakato wa kurekebisha Sheria Na. 2 ya Shirika la Nyumba la Taifa
ya mwaka 1990 iliyoliunda upya shirika hilo. Lengo la marekebisho haya ni
kuliwezesha shirika kufanya yafuatayo:- kupanua wigo wa shughuli za Shirika ili
liweze kuwa mwendelezaji milki
mkuu; kuliwezesha Shirika kuendesha shughuli zake katika mazingira shindani;
na, kuoanisha sheria ya Shirika na sheria zingine.
Upatikanaji
wa Ardhi kwa Ajili ya Ujenzi wa Nyumba
85.
Mheshimiwa
Spika,
katika
mwaka wa fedha 2013/14, Shirika liliweka lengo la kuendelea na mchakato
wa ununuzi wa ardhi katika Wilaya mbalimbali nchini. Lengo la ununuzi huu ni
kuliwezesha Shirika kuwa na hazina ya ardhi (land bank) ya kutosha
itakayoliwezesha kutekeleza jukumu lake jipya la kuwa mwendelezaji mkuu wa
miliki. Hadi Aprili, 2014, Shirika lilifanikiwa kununua ardhi yenye ukubwa wa
ekari 3,686.9 na
viwanja 464 (Jedwali Na 9A). Pia, Shirika
limeendelea na mchakato wa ununuzi wa ardhi yenye ukubwa wa ekari 2,627.5 iliyoko kwenye maeneo
mbalimbali nchini. Katika mwaka wa fedha 2014/15, Shirika
litaendelea na ununuzi wa ardhi ambao kwa sasa umefikia hatua mbalimbali.
Ujenzi
wa Nyumba za Makazi na Majengo ya Biashara
86.
Mheshimiwa
Spika,
katika mwaka wa fedha 2013/14, Shirika liliweka lengo la kuendelea kukamilisha
miradi iliyokuwa ikiendelea na kuanza miradi mingine mipya. Aidha, Shirika
liliweka kipaumbele kwenye ujenzi wa nyumba za gharama nafuu zisizopungua 20
kwa
kila mkoa. Hadi Aprili, 2014, Shirika liliendea na utekelezaji wa miradi 26 ya ujenzi wa nyumba za makazi
yenye jumla ya nyumba 1,947. Miradi hii, ililiwezesha Shirika kuifikia
mikoa 14
kwa kujenga nyumba za gharama nafuu 921 na nyumba za gharama ya kati na juu 978 katika Mikoa ya
Arusha, Dar es Salaam na Dodoma. Kati ya nyumba hizo, nyumba 697 zilikamilika ambapo 193 ni za gharama nafuu na
504
ni za gharama ya kati na juu (Jedwali Na. 9B). Shirika pia
linaendelea na maandalizi ya kuanza ujenzi wa miradi 31 yenye jumla ya nyumba
za gharama nafuu 1,717 na miradi 18 yenye nyumba 3,493 za gharama ya juu na
kati zitakazojengwa katika mikoa 17.
Katika mwaka wa fedha 2014/15, Shirika
litaendea kukamilisha miradi inayoendea; kuanza miradi mingine mipya ya nyumba
za gharama ya juu, kati na nafuu na hivyo kuifikia mikoa yote ya Tanzania Bara
kwa kujenga nyumba zisizopungua 50 kwa kila mkoa.
87.
Mheshimiwa
Spika, kwa mujibu wa Mpango Mkakati
wa kipindi cha 2010/11 – 2014/15, Shirika linauza asilimia 70 ya nyumba za makazi
zinazojengwa na kupangisha asilimia 30. Hadi Aprili, 2014, Shirika
limefanikiwa kuuza nyumba 456 katika miradi yake na kupata kiasi cha
shilingi bilioni 43.95 kati ya Shilingi bilioni 67.05 zinazotarajiwa wakati
miradi hii itakapokamilika.
88.
Mheshimiwa
Spika,
katika
mwaka wa fedha 2013/14, Shirika lilipanga kuendelea na utekelezaji wa
miradi tisa (9)
ya majengo makubwa ya biashara na majengo mengine 20 yanayojengwa kwa ubia
kwa kushirikiana na sekta binafsi.
Hadi Aprili, 2014 Shirika liliweza kukamilisha mradi wa jengo moja la
ghorofa 10
lililojengwa kwenye Kiwanja Na. 1 Barabara za Ufukoni na Ali Hassan Mwinyi,
Upanga - Dar es Salaam ambalo ni makao makuu mapya ya Shirika. Vilevile,
Shirika lilianza ujenzi wa majengo manne (4) ya biashara ambayo ni
jengo la ghorofa tano (5) lililoko Kiwanja Na. 2 Barabara ya Old Dar es Salaam mkoani Morogoro; jengo
la ghorofa moja (1)
katika Mtaa wa Kitope Manispaa ya Morogoro; jengo la ghrofa tano (5) lililoko Mtaa wa Lupa
Way, Manispaa ya Mbeya; na, jengo la ghorofa tatu (3) lililoko Mitaa ya
Mkendo na Kusaga mjini Musoma. Aidha, Shirika kwa kushirikiana na wabia wake
liliweza kukamilisha miradi ya majengo 57 na miradi mingine 27 ya biashara ilikuwa katika hatua mbalimbali
za matayarisho ya kuanza ujenzi. Vilevile, Shirika lilikamilisha miradi 16 ya ubia iliyotekelezwa
kwa kushirikiana na sekta binafsi na kuendelea na ujenzi wa miradi mingine
minne (4).
89.
Mheshimiwa
Spika, katika
mwaka wa fedha 2014/15, Shirika litaendelea na utekelezaji wa jumla ya
miradi ya majengo ya biashara 30 ikiwemo inayoendea na ile ambayo kwa sasa iko
katika hatua za maandalizi pamoja na kukamilisha miradi minne (4) ya ubia.
Undelezaji
wa Vituo vya Miji Midogo (Satellite Cities)
90.
Mheshimiwa
Spika,
katika
mwaka wa fedha 2013/14 Shirika limeendelea na matayarisho ya kuanza
jukumu lake jipya la kuendeleza vituo vya miji midogo kama mwendelezaji miliki
mkuu (master developer). Wizara ilikabidhi rasmi Shirika eneo la Luguruni lenye
ekari 156.53
na eneo la Kawe lenye ekari 267.71 kwa ajili ya kuyaendeleza. Aidha, Shirika kwa
niaba ya Serikali liliingia Mkataba wa makubaliano (memorandum of
understanding)
na kampuni ya Surbana International Consultants ya Singapore kwa ajili
ya kulipanga upya eneo la Luguruni. Pamoja na juhudi hizo, Shirika pia
lilikamilisha matayarisho ya mipango ya kina (detailed plans) ya kuendeleza maeneo
linaloyamiki ikiwa ni pamoja na eneo la Burka/Matevesi – Arusha lenye ekari
579.2
na eneo la Usa River - Arusha lenye ekari 296 na pia kuendelea na
matayarisho ya mipango hiyo kwa maeneo ya Uvumba, Kigamboni (ekari 202) na Kawe.
91.
Mheshimiwa
Spika,
Shirika
litaanza uendelezaji wa eneo la Burka/Matevesi kwa kujenga miundombinu pamoja
na nyumba za gharama nafuu 200 kabla ya Juni, 2014. Uendelezaji wa miradi hii
ambao utakuwa na nyumba za makazi zisizopungua 15,000 pamoja na majengo ya
biashara, utaishirikisha sekta binafsi kulingana na sera ya sasa ya Serikali ya
ushirika wa sekta ya umma na sekta ya binafsi (PPP). Katika mwaka wa fedha 2014/15,
Shirika litaendelea na ukamilishaji wa mpango wa kina wa eneo la Luguruni, Kawe
na Uvumba na kuendelea na
uendelezaji wa maeneo ya Usa River na Burka/Matevesi.
Utafutaji
wa Mitaji kwa Ajili ya Miradi na Mikopo ya Ununuzi wa Nyumba
92.
Mheshimiwa
Spika,
katika
mwaka wa fedha 2013/14, Shirika limeendelea kutafuta mitaji kwa ajili
utekelezaji wa miradi ya ujenzi. Hadi Aprili, 2014 Shirika limefanikiwa kuingia
mikataba ya mikopo ya kiasi cha Shilingi bilioni 210 na kuweza kutumia
kiasi cha Shilingi bilioni 124. Aidha, Shirika limeendelea na juhudi za kuwahamasisha
wanunuzi wa nyumba zake kutumia fursa za mikopo inayotolewa na benki za Azania
Bank, Bank of Africa, CRDB - Bank, Exim Bank, KCB, NBC, Commercial Bank of Africa,
NMB na Stanbic zilizoingia makubaliano ya kutoa mikopo ya ununuzi wa nyumba.
Hadi Aprili, 2014, wanunuzi wapatao 89 waliweza kupata mikopo ya nyumba yenye
jumla ya kiasi cha Shilingi bilioni 12.2 na wengine wanaendelea na mchakato wa
kupata mikopo hiyo. Katika mwaka wa fedha 2014/15, Wizara kupitia
Shirika itaendelea na juhudi za kupata mikopo kwa ajili ya utekelezaji wa
miradi ya ujenzi wa nyumba za makazi na majengo ya biashara pamoja na kuwahamasisha wananchi kuchukua mikopo
kwa ajili ya ununuzi wa nyumba zinazojengwa na Shirika au wanazoweza kujenga
wenyewe.
Mapato
ya Shirika
93.
Mheshimiwa
Spika,
katika
mwaka wa fedha 2013/14 Shirika lilitarajia kukusanya jumla ya Shilingi
bilioni 68.2 kutokana
na kodi za pango la nyumba zake na hivyo kuendelea kuchangia mapato ya Serikali
kwa kulipa kodi mbalimbali. Hadi Aprili, 2014, mapato ya shirika yalifikia Shilingi
bilioni 55.63 sawa
na asilimia 98 ya
lengo la kipindi cha Julai 2013 hadi Aprili 2014 (Jedwali Na. 9C). Mafanikio haya
yalitokana na juhudi za ukusanyaji wa kodi za pango pamoja na malimbikizo ya
madeni. Mapato hayo yaliliwezesha Shirika kuchangia mapato ya Serikali kwa
kiasi cha Shilingi bilioni 10.02 kupitia kodi mbalimbali kama vile kodi ya
pango la ardhi, kodi ya ongezeko la thamani, kodi ya majengo, kodi ya mapato,
ushuru wa huduma za Halmashauri za Miji na Manispaa, kodi za mapato ya
wafanyakazi, ushuru wa maendeleo ya taaluma na mchango wa pato ghafi kwa
Serikali Jedwali Na.9D. Kwa mwaka 2014/15
Shirika linategemea kuingiza kiasi cha Shilingi bilioni 70.1 kutokana na kodi za
pango la nyumba na hivyo kuendelea kuchangia mapato ya Serikali.
Matengenezo
ya Nyumba na Majengo
94.
Mheshimiwa
Spika,
katika
mwaka wa fedha 2013/14 Shirika lilipanga kutumia jumla ya Shilingi
bilioni 9.0 kwa
ajili ya matengenezo makubwa ya nyumba na majengo yake. Hadi Aprili, 2014
Shirika lilitumia kiasi cha Shilingi bilioni 4.2 kwa ajili ya
matengenezo ya nyumba zipatazo 3,500. Katika mwaka wa
fedha 2014/15,
Shirika litatenga kiasi cha Shilingi bilioni 6.1 kwa ajili ya matengenezo
na ukarabati wa nyumba na majengo ya yake.
HUDUMA ZA KISHERIA
95.
Mheshimiwa Spika, kwa kushirikiana na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali huduma
mbalimbali za kisheria zimeendelea kutolewa na wizara. Huduma hizo zinajumuisha
kutunga sheria mpya, kuhuisha sheria na kusimamia mashauri yanayohusu Wizara.
96.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2013/14
Wizara yangu iliahidi kuhuisha Sheria ya Ardhi, Sura 113; Sheria ya Ardhi ya
Vijiji, Sura 114; Sheria ya Mahakama za Ardhi, Sura 216 na Sheria ya Wapima
Ardhi, Sura 324. Napenda kuliarifu bunge lako tukufu kuwa kazi ya kukusanya maoni ya wadau ili kuhuisha Sheria ya Ardhi,
Sheria ya Ardhi ya Vijiji na Sheria ya Mahakama za Ardhi imekamilika na
mapendekezo yatawasilishwa katika Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa
hatua stahiki. Aidha, mchakato wa kuhuisha Sheria ya Wapima Ardhi utaendelea
katika mwaka wa fedha 2014/15.
97.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2013/14 Wizara ilipanga kuanza mchakato wa kutunga
upya Sheria ya Utwaaji Ardhi. Kazi hii inaendelea na inatarajiwa kukamilika
katika mwaka wa fedha 2014/15. Baada ya mchakato wa kutunga sheria hizo kukamilika, miswaada husika itawasilishwa
katika Bunge lako tukufu. Aidha, Wizara yangu itaendelea na utaratibu wa
kuzihuisha sheria mbalimbali za utawala wa ardhi kila mara inapolazimu ili
kuzifanya ziendane na wakati na kukidhi makusudio ya kutungwa kwake.
MAWASILIANO SERIKALINI
98.
Mheshimiwa Spika, Wizara yangu inatoa elimu kwa umma kuhusu sera, sheria, kanuni na
taratibu zinazo simamia Sekta ya Ardhi nchini. Katika mwaka wa fedha 2013/14 niliahidi kuongeza kasi ya kutoa elimu kwa
umma kwa kuanzisha mtandao rasmi wa kijamii (official ardhi blog); kuhuisha mkakati wa mawasiliano; na kuimarisha kitengo cha
Mawasiliano cha Wizara. Napenda kuliarifu Bunge lako Tukufu kuwa Wizara
ilianzisha mtandao rasmi wa kijamii unaopatikana kupitia anuani: www.ardhi.go.tz/blog; pia, kitengo cha Mawasiliano kilipatiwa vitendeakazi pamoja na
kuongezewa rasilimali watu. Vilevile, Wizara imekamilisha mchakato wa kumpata
mtaalam mwelekezi atakayehuisha Mkakati wa Mawasiliano wa Wizara.
99.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2013/14,
Wizara iliendelea kutoa elimu iliyolenga kuelimisha umma kuhusu sekta ya ardhi
kupitia vyombo mbalimbali vya habari. Wizara kwa kutambua umuhimu huo,
iliendesha semina elekezi kwa wahariri wa vyombo vya habari nchini. Pia, wizara
ilishiriki kwenye vipindi vinne (4) vya moja kwa moja (live programmes) vilivyorushwa kupitia runinga na redio. Pia, Wizara inakamilisha
uandaaji wa vitabu
vya sheria za Ardhi vitakavyosomeka kwa maandishi nundu, hii ni moja ya jitihada za
kuhakikisha wadau
wote muhimu wa sekta ya ardhi (wakiwemo wenye ulemavu wa macho) wanapata elimu
kuhusu Sekta ya Ardhi.
100.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2014/15
Wizara itakamilisha kuhuisha mkakati wa mawasiliano wa wizara; kuratibu mawasiliano kati ya Wizara na
wadau wake; kuandaa na kurusha vipindi vya televisheni na redio; na, kuboresha
mawasiliano.
HUDUMA ZA UTAWALA NA RASILIMALI WATU
101.
Mheshimiwa
Spika,
Wizara yangu inaendelea kuboresha mifumo ya usimamizi wa rasilimali watu na uendeshaji wa ofisi ili kuleta tija
na ufanisi wa kazi. Hatua hii inajidhihirisha kutokana na hatua mbalimbali
zinazoendelea kuchukuliwa za kuboresha mifumo ya utendaji kazi na usimamizi wa
rasilimali watu. Katika mwaka wa fedha 2013/14 Wizara
imeendelea kutoa mafunzo, kuboresha mazingira ya ofisi, kutoa stahili kwa
watumishi zinazoendana na masharti ya ajira zao, pamoja na kudumisha utawala
bora. Msisitizo umelenga katika kutumia dhana shirikishi ya kupanga, kujenga
uwezo, kutekeleza, kusimamia na kutathmini utekelezaji wa majukumu ili
kuboresha utendaji kazi na kusimamia nidhamu na watumishi. Vile vile Wizara inaendeleza mapambano
dhidi ya UKIMWI kwa kuhamasisha watumishi kujikinga na kupima afya zao.
102.
Mheshimiwa
Spika,
katika hotuba yangu ya mwaka jana, nililifahamisha Bunge lako tukufu kuwa,
wizara yangu ilikuwa inaendelea kujenga kituo cha kuhudumia wateja (customer
service centre).
Napenda kutoa taarifa kuwa Wizara imekamilisha ujenzi wa kituo hicho, na kwamba
kituo hiki kitaanza kutoa huduma katika mwaka wa
fedha 2014/15.
Kituo hiki kitasaidia kuboresha utoaji wa huduma zinazotolewa na Wizara na
kuleta ufanisi zaidi katika utendaji kazi wa pamoja na kuepusha mianya ya
rushwa. Katika mwaka wa fedha 2014/15 Wizara
itaendelea kuboresha utaoji wa huduma kwa kusimamia mifumo ya utendaji kazi,
kuboresha mazingira ya ofisi, na kutoa stahili kwa watumishi zinazoendana na
masharti ya ajira zao.
103.
Mheshimiwa
Spika,
kwa kutambua umuhimu wa maendeleo ya rasilimali watu katika kufanikisha malengo
yaliyopangwa, Wizara imeendelea kuwawezesha watumishi kuhudhuria mafunzo
mbalimbali ndani na nje ya nchi kwa ajili ya kuwajengea uwezo zaidi. Katika
mwaka wa fedha 2013/14 jumla ya Watumishi 166 walihudhuria mafunzo
mbalimbali ya muda mrefu na mfupi nje na ndani ya nchi. Kati ya hao 36 walipatiwa mafunzo ya
muda mrefu na mfupi ndani na nje ya nchi; 40 walipatiwa mafunzo
yaliyohusu maadili katika utumishi wa umma; na, waajiriwa wapya 90 walipatiwa mafunzo ya
awali (induction course). Katika kipindi hicho watumishi 88 wa taaluma mbalimbali
waliajiriwa, watumishi 13 walibadilishwa kazi baada ya kupata sifa na watumishi 8 walithibitishwa katika
vyeo vyao.
104.
Mheshimiwa
Spika, katika
mwaka wa fedha 2014/15 Wizara inatarajia kuwapatia mafunzo ya aina
mbalimbali watumishi 250 wa kada mbalimbali. Aidha, kwa kutambua umuhimu wa michezo kwa
afya za watumishi, Wizara katika mwaka wa fedha 2013/14 ilishiriki
katika mashindano ya SHIMIWI na kufanikiwa kupata tuzo mbalimbali na pia
iliandaa bonanza la michezo kwa watumishi wote. Vilevile viongozi wa michezo
waliwezeshwa kuhudhuria mikutano na semina mbalimbali za michezo.
105.
Mheshimiwa
Spika,
ili kupambana na janga la UKIMWI katika sehemu ya kazi, Wizara imeendelea
kuhamasisha watumishi kupima kwa hiari afya zao kwa kutumia utaratibu wa
kuwaleta Wizarani wataalam wa huduma ya ushauri nasaha. Katika mwaka wa fedha 2013/14,
watumishi 720 wa makao makuu walifanyiwa semina ya uhamasishaji, na watumishi 416 walipima na kufahamu
hali za afya zao. Wizara imeendelea kuwapatia watumishi wanaoishi na virusi vya
UKIMWI msaada wa dawa na lishe. Katika mwaka wa
fedha 2014/15
Wizara itaendelea kuhamasisha upimaji wa afya za watumishi kwa hiari na kutoa
huduma stahiki.
Vyuo vya Ardhi
106.
Mheshimiwa
Spika, Wizara ina vyuo viwili
vya Ardhi vilivyopo Tabora na Morogoro. Vyuo hivi vinatoa mafunzo ya stashahada
katika fani za Urasimu Ramani na Upimaji Ardhi; na, Cheti katika fani za
Upimaji Ardhi, Umiliki Ardhi, Uthamini, Usajili na Uchapaji Ramani. Katika
mwaka wa fedha 2013/14 idadi ya wahitimu ilikuwa 250 kati yao 178 walitoka Chuo cha
Ardhi Morogoro na 72 walitoka Chuo cha Ardhi Tabora (Jedwali Na. 10). Katika mwaka wa
fedha 2014/15
Chuo cha Ardhi Tabora kitaanzisha mafunzo ya stashahada katika fani ya Umiliki,
Uthamini na Usajili wa ardhi ambayo itawapa wanafunzi sifa ya kujiunga na vyuo
vikuu. Fani hizi ni muhimu kwa ajili ya kukidhi mahitaji ya soko la wataalam wa
sekta ya ardhi. Aidha, Wizara itaendelea kuviimarisha vyuo hivi ili viweze
kutekeleza majukumu yake ipasavyo. Natoa wito kwa Halmashauri kuajiri
wataalamu wanaohitimu katika vyuo hivi pamoja na kuwaendeleza watumishi wao
kitaaluma kupitia vyuo hivi.
CHANGAMOTO MAALUM
Utatuzi wa Migogoro
ya Ardhi
107.
Mheshimiwa
Spika, takriban katika kazi
zote tunazotekeleza changamoto na kero kubwa imeendelea kuwa ni ongezeko la
migogoro ya ardhi inayoibuka sehemu mbalimbali nchini. Ninachukua nafasi hii kuwaeleza
kwamba kimsingi hakuna migogoro ya ardhi bali ni “migogoro ya watumiaji wa
ardhi”. Ili kuondokana na migogoro hii ni muhimu kwa watumiaji wote wa ardhi
kutambua ukweli huu na kujitathmini wenyewe pindi mgogoro unapoibuka.
Kuna aina kuu sita za migogoro ya watumiaji wa
ardhi vijijini ambazo ni:-
i. Migogoro Kati ya
Wakulima na Wafugaji;
ii. Migogoro Kati ya
Wafugaji na Hifadhi;
iii. Migogoro kati ya
Wanavijiji na Wamiliki wa Migodi;
iv. Migogoro kati ya
Wanavijiji na Wamiliki wa Mashamba Makubwa (Wawekezaji);
v. Migogoro ya Mipaka
kati ya Vijiji na Wilaya; na
vi. Migogoro ya Wanavijiji
na Miji Inayopanuka.
Ufafanuzi wa kina wa
migogoro hiyo na namna wizara inavyoishughulikia upo kwenye Kiambatisho Na.
1.
SHUKRANI
108.
Mheshimiwa
Spika, Wizara yangu inashughulikia
majukumu mbalimbali ambayo ni mtambuka. Ni mategemeo yangu kwamba, Bunge
litaendelea kuwa na mtazamo chanya na kuipa kipaumbele sekta ya ardhi kwa
ujumla ili kuiwezesha kutoa mchango mkubwa katika maendeleo ya kiuchumi na
kijamii.
109.
Mheshimiwa Spika, mafanikio ya Wizara
yangu yametokana na kuwepo kwa ushirikiano kati ya Serikali na Wadau wa
Maendeleo zikiwemo taasisi za
fedha za kimataifa, nchi wahisani, taasisi zisizokuwa za kiserikali na
mashirika ya kidini. Wadau hao ni
pamoja na Benki ya Dunia, Shirika la Makazi la Umoja wa Mataifa (UN-HABITAT),
Shirika la Maendeleo la Ujerumani; na Serikali za Denmark, Sweden, Uholanzi na
Uingereza kupitia Mradi wa Kuboresha Mazingira ya Biashara.
110.
Mheshimiwa Spika, kwa mara nyingine napenda kumshukuru Naibu Waziri wa Wizara ya Ardhi,
Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mheshimiwa George Simbachawene (Mb), kwa
kunisaidia katika kutekeleza majukumu yangu. Pia napenda kumshukuru Katibu Mkuu
Bw. Alphayo Japani Kidata, na Naibu Katibu Mkuu Dkt. Selassie David Mayunga kwa
ushirikiano mkubwa wanaonipa. Nawashukuru Wakuu wa Idara na Vitengo, Makamishna
Wasaidizi na Wasajili Wasaidizi wa kanda, viongozi wa taasisi zilizo chini ya
Wizara, watumishi na wataalamu wote wa sekta ya ardhi kwa kunisaidia katika
kutimiza majukumu yangu kwa ufanisi. Naomba kila mmoja wetu aendelee kutekeleza
majukumu yake kwa kujielekeza katika kuiwezesha ardhi kuwaondolea wananchi
umaskini. Natambua kuwa Wizara yangu haina nyenzo na rasilimali za kutosha
kutimiza matarajio ya Watanzania,
lakini hata kwa kutumia rasilimali chache zilizopo kwa uangalifu tutatoa mchango mkubwa kwa Taifa.
HITIMISHO
111.
Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2014/15 Wizara imeazimia kutekeleza Mpango Mkakati wa Utekelezaji wa
Sheria za Ardhi uliohuishwa mwaka 2013 (SPILL 2013); na Mpango Mkakati wa
Wizara wa miaka mitano (2012/13 - 2016/17) ili kufikia malengo yaliyoainishwa
kwenye Mpango wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka Mitano (2011/12 – 2015/16) na
MKUKUTA II ambayo kwa pamoja yanalenga kufikia malengo makuu ya Dira ya
Maendeleo ya Taifa ya 2025.
112.
Mheshimiwa Spika, kwa hali hiyo Wizara imejipanga kutayarisha mipango ya kuendeleza miji
na vijiji na kuisimamia, kupanga
matumizi ya ardhi, kupima ardhi, kuhakiki milki, kusajili na kutoa hati ili
kuwezesha kuwepo kwa usalama wa milki. Natoa rai kwa mamlaka na asasi
mbalimbali kutoa ushirikiano unaotakiwa kuhakikisha kuwa ardhi inaziwezesha
sekta zote ili kufikia malengo ya maisha bora kwa kila Mtanzania.
MAOMBI YA FEDHA KWA MWAKA 2014/15
113.
Mheshimiwa Spika, ili Wizara yangu iweze kutekeleza kazi zilizopangwa kwa mwaka wa fedha
2014/15, naomba kutoa hoja kwamba Bunge lako Tukufu liidhinishe makadirio ya
mapato na matumizi ya Wizara kama ifuatavyo:-
Mapato
ya Serikali
|
Shilingi
|
61,320,005,000
|
|
|
|
|
|
°
|
Matumizi
ya Mishahara
|
Shilingi
|
11,536,899,480
|
°
|
Matumizi
Mengineyo (OC)
|
Shilingi
|
42,933,854,000
|
Jumla
Matumizi ya
Kawaida
(A)
|
Shilingi
|
54,470,753,480
|
|
|
|
|
|
°
|
Fedha
za Ndani
|
Shilingi
|
21,000,000,000
|
°
|
Fedha
za Nje
|
Shilingi
|
13,379,977,000
|
Jumla
Matumizi ya Miradi ya Maendeleo
(B)
|
Shilingi
|
34,379,977,000
|
114.
Mheshimiwa Spika, napenda kukushukuru tena wewe na Waheshimiwa Wabunge wote
kwa kunisikiliza. Hotuba hii inapatikana
kwenye tovuti ya Wizara www.ardhi.go.tz.
No comments:
Post a Comment