HOTUBA FUPI YA
WAZIRI WA MAENDELEO YA MIFUGO NA UVUVI, MHE. DKT. TITUS MLENGEYA KAMANI (MB)
AKIWASILISHA BUNGENI MPANGO WA MAENDELEO NA MAKADIRIO YA MATUMIZI YA FEDHA KWA
MWAKA 2014/2015
1.0 UTANGULIZI
1.
Mheshimiwa Spika, kufuatia
taarifa iliyowasilishwa hapa Bungeni na Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge
ya Kilimo, Mifugo na Maji, iliyochambua bajeti ya Wizara ya Maendeleo ya Mifugo
na Uvuvi, naomba kutoa hoja kwamba Bunge lako Tukufu lipokee, lijadili na
kupitisha taarifa ya mapitio ya utekelezaji wa kazi za Wizara kwa mwaka
2013/2014 na mwelekeo wa kazi za Wizara kwa mwaka 2014/2015. Aidha, naliomba
Bunge lako Tukufu likubali kupitisha Mpango wa Maendeleo na Makadirio ya Mapato
na Matumizi ya Fedha ya Wizara ya Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha
2014/2015.
2.
Mheshimiwa
Spika, napenda
kumpongeza Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Mohamed Gharib Bilal, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania na Mheshimiwa Mizengo Kayanza Peter Pinda, Mbunge wa Katavi na Waziri Mkuu
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa jitihada zao za kuongoza, kusimamia na
kuendeleza amani, utulivu, mshikamano na uchumi wa nchi yetu. Pia, napenda
kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa uamuzi wake wa kuanzisha mchakato wa kupata katiba
mpya ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Vilevile, napenda kuwapongeza Wajumbe wa Bunge Maalum la Katiba kwa kuteuliwa na Mheshimiwa
Rais kushiriki
katika mchakato wa kupata katiba. Tuna imani kuwa mchakato huo utatuwezesha
kupata Katiba itakayofaa kwa kipindi kijacho. Aidha, naomba nichukue fursa hii
kumshukuru Mheshimiwa Rais kwa kuniteua mimi na Naibu Waziri, Mheshimiwa Kaika Saning’o Ole Telele Mbunge wa Ngorongoro kuongoza
Wizara ya Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi na tunaahidi kutumia uwezo wetu katika
kutekeleza majukumu tuliyopewa.
3.
Mheshimiwa
Spika, naomba
nichukue nafasi hii kuwapongeza Mawaziri na Naibu Mawaziri kwa kuteuliwa kwao
na Mheshimiwa Rais
katika nafasi zao mpya. Aidha, napenda kuwapongeza Waheshimiwa Wabunge wapya
waliojiunga na Bunge lako tukufu kufuatia chaguzi ndogo zilizofanyika katika
Jimbo la Chambani Mheshimiwa Yusuf Salim Hussein, Jimbo la Kalenga Mheshimiwa Godfrey William Mgimwa na Jimbo la Chalinze Mheshimiwa Ridhiwan Jakaya Kikwete.
4.
Mheshimiwa
Spika, Wizara ilipokea kwa masikitiko
makubwa taarifa za vifo vya Waheshimiwa Wabunge wenzetu; Hayati Mhe. Dkt. William Augustao Mgimwa aliyekuwa mbunge wa Kalenga na
Hayati Said Ramadhani Bwanamdogo aliyekuwa Mbunge wa Chalinze. Naungana na Waheshimiwa
Wabunge wenzangu, kutoa salaam za rambirambi kwa familia za marehemu, ndugu na
wananchi wa majimbo waliokuwa wanayawakilisha. Mwenyezi Mungu aziweke roho za
marehemu mahali pema peponi, Amina. Aidha, naomba nitumie fursa hii kuwakumbuka
wananchi wenzetu waliopoteza maisha kutokana na mafuriko, ajali na sababu
mbalimbali.
5.
Mheshimiwa
Spika, napenda kuchukua fursa hii
kumshukuru Mhe. Profesa Peter Mahamudu Msolla, Mbunge wa Kilolo na Mhe. Said Juma Nkumba, Mbunge wa Sikonge pamoja na
wajumbe wote wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kwa
ushauri, maoni, maelekezo na ushirikiano waliotupatia katika utekelezaji wa
majukumu ya Wizara na maandalizi ya bajeti hii. Napenda kulihakikishia Bunge
lako Tukufu kwamba Wizara yangu itaendelea kuzingatia ushauri, mapendekezo na
maoni ya Kamati na yale yatakayotolewa na Bunge lako Tukufu.
6.
Mheshimiwa
Spika, naomba kuchukua fursa hii kumpongeza
Waziri Mkuu, Mheshimiwa Mizengo Kayanza Peter Pinda, Mbunge wa Katavi kwa hotuba yake
nzuri yenye kutoa malengo ya Serikali na mwelekeo wa utendaji wa sekta
mbalimbali pamoja na kazi za Serikali kwa mwaka 2014/2015. Aidha, nachukua
nafasi hii kuwapongeza Mawaziri wote waliotoa hotuba zao ambazo zimeainisha
maeneo mbalimbali tunayoshirikiana katika kuendeleza sekta za mifugo na uvuvi nchini.
Vilevile, nawashukuru waheshimiwa Wabunge wote kwa michango yao kuhusu masuala
ya maendeleo ya sekta za mifugo na uvuvi kupitia hotuba hizo.
2.0 HALI YA SEKTA ZA MIFUGO NA UVUVI NA CHANGAMOTO ZILIZOPO
7.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka
2013, sekta ya mifugo ilikua kwa asilimia 3.8 ikilinganishwa na asilimia 3.1 mwaka 2012 na kuchangia asilimia 4.4 katika pato la Taifa ikilinganishwa na asilimia 4.6 mwaka 2012. Aidha, idadi ya
mifugo nchini inakadiriwa kuwa ng’ombe milioni 22.8, mbuzi milioni 15.6 na kondoo milioni 7.0. Pia, wapo kuku wa asili milioni 35.5, kuku wa kisasa milioni 24.5 na nguruwe milioni 2.01. Viwango vya
ulaji wa mazao ya mifugo kwa sasa ni wastani
wa kilo 12 za nyama, lita 45 za maziwa na mayai 75 kwa mtu kwa mwaka.
8.
Mheshimiwa Spika, Nchi
yetu ina ukanda wa pwani wa bahari wenye urefu wa kilometa 1,424 ambao
umegawanyika katika eneo la Maji ya Kitaifa (Territorial Sea) lenye ukubwa wa
kilometa za mraba 64,000 na eneo la Bahari Kuu kilometa za
mraba 223,000. Eneo la maji baridi linajumuisha maziwa makuu
matatu ambayo ni; Ziwa Victoria (kilometa za mraba 35,088),
Ziwa Tanganyika (kilometa za mraba 13,489) na Ziwa
Nyasa (kilometa za mraba 5,700), maziwa ya kati na madogo 29, mito na
maeneo oevu. Katika mwaka 2013,
sekta ya uvuvi ilikua kwa asilimia 2.2 ikilinganishwa na asilimia 2.9 mwaka 2012. Kupungua kwa kasi ya ukuaji kumechangiwa na
kupungua kwa mauzo ya samaki na mazao yake nje ya nchi. Aidha, mchango wa sekta
hii kwa pato la Taifa umeendelea kuwa asilimia 1.4 kwa mwaka 2013. Vilevile, idadi ya wavuvi wadogo
imeongezeka kutoka wavuvi 182,741 mwaka
2012/2013 hadi wavuvi 183,341 mwaka
2013/2014 na wananchi zaidi ya milioni 4.0
wameendelea kutegemea shughuli za uvuvi ikiwemo biashara ya samaki, uchakataji
wa mazao ya uvuvi, utengenezaji wa zana na vyombo vya uvuvi na biashara
nyingine.
9.
Mheshimiwa Spika, sekta
za mifugo na uvuvi kwa kipindi cha mwaka 2013/2014 zimeendelea kukabiliwa na
changamoto mbalimbali zilizoainishwa katika aya ya 10 ya
hotuba yangu.
3.0 MAPITIO YA UTEKELEZAJI WA MPANGO NA BAJETI YA MWAKA 2013/2014 NA MWELEKEO WA BAJETI YA MWAKA 2014/2015
UKUSANYAJI WA MAPATO
10. Mheshimiwa
Spika, mapitio ya utekelezaji wa mpango na bajeti ya mwaka
2013/2014 kwa upande wa ukusanyaji wa maduhuli na matumizi ya fedha
yamefafanuliwa kwa ufasaha kuanzia aya ya 12 hadi aya
ya 14 ya hotuba yangu.
UBUNIFU NA UTEKELEZAJI WA SERA NA SHERIA ZA SEKTA
11. Mheshimiwa
Spika, Wizara imeendelea kuratibu, kupitia na kusimamia
utekelezaji wa sera, sheria, mikakati na programu mbalimbali za kuendeleza
sekta za mifugo na uvuvi nchini. Katika mwaka 2013/2014, sera na sheria
za sekta za mifugo na uvuvi zimeendelea kupitiwa na Wizara kwa kushirikiana na
wadau mbalimbali ili kuboresha mazingira ya kibiashara kama ilivyoainishwa
katika aya ya 16.
UENDELEZAJI WA SEKTA YA MIFUGO
Uzalishaji na Biashara ya Mifugo na Mazao yake
Zao la Maziwa
12.
Mheshimiwa Spika uzalishaji wa maziwa umeongezeka kwa asilimia 3.5
kutoka lita bilioni 1.9 mwaka 2012/2013 hadi lita bilioni
2.0. Aidha, maziwa yanayosindikwa kwa siku yameongezeka kutoka
lita 135,300 mwaka 2012/2013 hadi lita 139,800 mwaka
2013/2014. Pia, Wizara imeendelea kuboresha Mashamba ya Uzalishaji Mifugo ili
kuongeza uzalishaji na ubora wa mifugo ya asili ambapo katika mwaka
2013/2014 jumla ya mitamba 681
ilizalishwa katika mashamba ya Wizara na kusambazwa kwa wafugaji mbalimbali
nchini.
13. Mheshimiwa
Spika, Wizara imeendelea kuhamasisha matumizi ya teknolojia ya
uhimilishaji kama njia yenye tija ya kuzalisha mifugo bora. Katika mwaka
2013/2014, Kituo cha Taifa cha Uhimilishaji – NAIC Usa River pamoja na vituo vya
Kanda vya Uhimilishaji vya Kibaha (Pwani), Dodoma, Lindi, ZVC Mwanza na Uyole
(Mbeya) vimeimarishwa. Jumla ya dozi 58,210 za
mbegu bora zimezalishwa na kusambazwa kwa wafugaji. Pia, ng’ombe 90,300 wamehimilishwa
katika mikoa mbalimbali.
14. Katika
mwaka 2014/2015, Wizara itaendelea kuimarisha uhimilishaji nchini kwa kuzalisha
dozi 190,000 za mbegu, kuendeleza ujenzi wa Kituo cha Taifa
cha Uhimilishaji cha Sao Hill, kuimarisha Kituo cha Uhimilishaji cha Taifa NAIC
– Usa River na Vituo sita (6) vya Kanda vya Uhimilishaji. Aidha,
Wizara itaendeleza teknolojia ya uhawilishaji kiinitete kwa kukamilisha ujenzi
wa maabara ya TALIRI-Mpwapwa na kuitumia teknolojia hiyo.
Nyama - Ng’ombe, Mbuzi, Kondoo, Nguruwe na Kuku
15. Mheshimiwa
Spika, katika mwaka 2013/2014, uzalishaji wa nyama umeongezeka
kutoka tani 553,455 mwaka
2012/2013 hadi tani 563,086 (nyama
ya ng’ombe tani 309,353, mbuzi na kondoo tani 120,199 nguruwe tani 79,174 na kuku tani 54,360) mwaka
2012/2013. Aidha, wadau wameendelea kuhamasishwa kutumia mfumo wa unenepeshaji
mifugo ambapo ng’ombe walionenepeshwa wameongezeka kwa asilimia 11 kutoka
ng’ombe 155,206 mwaka
2012/2013 hadi ng’ombe 175,000 mwaka
2013/2014. Katika mwaka 2014/2015, Wizara itaendelea kuhamasisha uzalishaji,
usindikaji wa nyama, kuweka mazingira mazuri ili sekta binafsi iwekeze zaidi. Pia,
Serikali itaendelea kuhamasisha unenepeshaji ili kufikia idadi ya ng’ombe 200,000
kwa mwaka.
16. Mheshimiwa Spika, katika
mwaka wa 2013/2014, Wizara imeimarisha minada ya Pugu (Dar es Salaam), Lumecha
(Songea), Meserani (Arusha) na Nyamatala (Misungwi). Aidha, mnada wa upili wa
Nyamatala umezinduliwa rasmi tarehe 8 Aprili, 2014. Minada ya Kirumi (Butiama)
na Longido inaendelea kujengwa. Vilevile, wafanyabiashara 340
walipatiwa mafunzo kuhusu biashara, matumizi ya mizani na umuhimu wa kulipa
mapato ya Serikali kwenye minada ya upili na ya mipakani. Katika mwaka
2014/2015, Wizara itaendelea na ujenzi wa minada ya Longido na
Kirumi na kukarabati minada ya Pugu, Weruweru, Sekenke, Kizota, Meserani na
Igunga. Aidha, Serikali itaendelea kuratibu uuzaji wa mifugo katika minada na
kuhamasisha matumizi ya mizani ya kupimia uzito wa mifugo.
17. Mheshimiwa
Spika, katika mwaka 2013/2014, jumla ya ng’ombe 1,215,541, mbuzi
960,199 na kondoo 209,292 wenye thamani
ya shilingi bilioni 989.3 waliuzwa
minadani. Katika mwaka 2014/2015, Wizara kwa kushirikiana na Wizara
ya Viwanda na Biashara itaendelea kuhamasisha wadau kuwekeza katika ujenzi wa
viwanda na biashara ya mifugo na
mazao yake ili kuongeza mauzo ya nyama ndani na nje ya nchi.
Uzalishaji wa Nyama katika Kampuni ya Ranchi za Taifa (National Ranching Company - NARCO)
18. Mheshimiwa
Spika, NARCO imeendelea kuzalisha, kunenepesha, kuuza mifugo
kwa ajili ya nyama na kuendesha machinjio ya Dodoma kwa ubia na Kampuni ya
NICOL. Aidha, Kampuni imeendelea kutoa huduma za ushauri kwa wafugaji
wanaozunguka ranchi 10 za mfano za Kagoma, Kalambo,
Kikulula, Kongwa, Mabale, Missenyi, Mkata, Mzeri, Ruvu na West Kilimanjaro. Katika mwaka 2014/2015, NARCO itaendelea
na ujenzi wa machinjio ya kisasa ya Ruvu na kununua ng’ombe wazazi 1,200 ili
kuongeza idadi ya ng’ombe katika ranchi zake. Aidha, jumla ya ndama 4,050
wanategemea kuzaliwa kutokana na ng’ombe wazazi 5,786. Pia,
Kampuni itaendelea na jitihada za kuongeza uzalishaji kwa kutafuta mitaji mipya
na kuvutia wawekezaji kwa ubia katika ranchi zake.
Kuku
19. Mheshimiwa
Spika, katika mwaka 2013/2014, jumla ya vifaranga milioni
61 vya kuku wa nyama na mayai vilizalishwa nchini
ikilinganishwa na vifaranga milioni 52 mwaka
2012/2013. Pia, mayai 348,000 ya kuku wazazi na mayai 6,240,000 ya
kutotolesha vifaranga yaliingizwa nchini. Vilevile, uzalishaji wa mayai
uliongezeka kutoka bilioni 3.7 mwaka 2012/2013 hadi mayai bilioni 3.9 mwaka
2013/2014. Katika mwaka 2014/2015, Wizara itaendelea
kuhamasisha wadau kuwekeza katika ufugaji wa kuku kibiashara na kushirikiana na
wadau kuandaa maonesho yatakayowezesha wadau kuzalisha mazao bora.
Nguruwe
20. Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2013/2014, uzalishaji wa nyama ya nguruwe umeongezeka kwa
asilimia 35 kutoka
tani 50,814 mwaka
2012/2013 hadi tani 79,174 mwaka
2013/2014. Ili kuimarisha ufugaji wa nguruwe nchini, Wizara imenunua nguruwe wa
mbegu 24 mbari
ya Large White na Duroc na kuwapeleka katika shamba la
Ngerengere ili kuwazalisha na kusambaza mbegu bora kwa wafugaji. Katika mwaka 2014/2015, Wizara itaendelea kuimarisha
uzalishaji wa nguruwe nchini kwa kuongeza nguruwe wazazi katika shamba la
Ngerengere. Aidha, Wizara itashirikiana na Halmashauri kuhamasisha sekta
binafsi kuwekeza katika ufugaji wa nguruwe wa kisasa.
Ngozi
21. Mheshimiwa
Spika, katika mwaka 2013/2014, ngozi zilizosindikwa na kuuzwa nje ya nchi ziliongezeka
kutoka vipande vya ngozi za ng’ombe 969,060 vyenye
thamani ya shilingi bilioni 32.3 na vipande
vya ngozi za mbuzi na kondoo 2,582,525
vyenye thamani ya shilingi bilioni 18.6
katika mwaka 2012/2013 hadi kufikia vipande vya ngozi za ng’ombe 1,060,777
vyenye thamani ya shilingi bilioni 39.4 na
vipande vya ngozi za mbuzi na kondoo
2,715,436 vyenye thamani ya shilingi bilioni 19.6
katika mwaka 2013/2014. Aidha, vipande vya ngozi za ng’ombe 250,000
vyenye thamani ya shilingi bilioni 12.5
vilisindikwa hadi hatua ya mwisho na kutumika kutengeneza bidhaa za ngozi hapa
nchini ikilinganishwa na vipande vya ngozi za ng’ombe 212,000
vyenye thamani ya shilingi bilioni 15.0 katika
mwaka 2012/2013.
22. Mheshimiwa
Spika, katika mwaka 2013/2014, Wizara
kwa kushirikiana na Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI, Wizara ya Viwanda na
Biashara, Halmashauri 75 na Chama cha Wadau wa Ngozi kupitia
Mfuko wa Maendeleo ya Mifugo imewajengea uwezo wataalam 40 wa
Halmashauri. Aidha, imewezesha uimarishaji wa Chama cha Wazalishaji wa Ngozi
cha Kitaifa na ukamilishaji wa taratibu za uanzishwaji wa Chama cha Wazalishaji
wa Ngozi nchini, ambacho kitasimamia maslahi ya wazalishaji wa ngozi wakiwemo
wafugaji, wachinjaji na wakusanyaji wa ngozi katika Halmashauri zote nchini. Katika
mwaka 2014/2015, Wizara itaendelea kutekeleza Mkakati wa Kufufua na Kuendeleza
Sekta na Viwanda vya Ngozi katika Halmashauri 75.
Matumizi ya Rasilimali za Ardhi, Maji na Malisho kwa Mifugo na Utatuzi wa Migogoro
23. Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2013/2014, Wizara
imeendelea kuhimiza Halmashauri kuandaa Mipango ya Matumizi bora ya Ardhi na
kutenga maeneo ya ufugaji kwa ajili ya kuendeleza malisho ya mifugo katika
Halmashauri zote nchini. Upatikanaji wa maeneo ya malisho utaepusha migogoro ya
mara kwa mara kati ya wafugaji na watumiaji wengine wa ardhi. Hadi sasa, vijiji
589 katika wilaya 80 ndani ya
mikoa 22 vimepimwa na kutenga maeneo kwa ajili ya ufugaji na kufanya
jumla ya eneo lililopimwa kufikia hekta milioni 1.51. Katika
mwaka 2014/2015, Wizara kwa kushirikiana na Halmashauri itaainisha na kutenga
maeneo ya malisho kwa ajili ya maendeleo endelevu ya rasilimali za mifugo
katika Wilaya za Busega, Kiteto, Kilosa, Ngorogoro, Mvomero, Kilindi, Igunga,
Iramba na Lindi.
24. Mheshimiwa Spika, Wizara
inakemea tabia inayozidi kujengeka ya kutesa mifugo kwa kuinyima chakula na
maji, kuipiga risasi au kuikata mapanga kwa kisingizio cha migogoro ya ardhi,
kwani huko ni kuvunja Sheria
ya Ustawi wa Wanyama Na. 19 ya Mwaka 2008 - The Animal Welfare Act. No.19
of 2008. Kosa haliwezi kurekebishwa kwa
kutenda kosa. Aidha, wafugaji
wanasisitizwa kuheshimu shughuli za watumiaji wengine wa ardhi kwani jamii zote
zinategemeana. Wizara itaendelea kuhamasisha jamii ya wafugaji kuanza kumiliki
ardhi na kuiendeleza, kufuga kibiashara na kuachana na ufugaji wa kuhamahama
kwani siyo endelevu. Katika mwaka
2014/15 Serikali itaangalia upya maeneo yaliyobinafsishwa na kushindwa
kuendelezwa ikiwa ni pamoja na maeneo ya ranchi za Taifa na maeneo ya hifadhi
yaliyopoteza sifa ili yatumike kwa shughuli za ufugaji.
25. Mheshimiwa Spika,
katika mwaka 2013/2014, Wizara imeendelea kuimarisha mashamba ya kuzalisha mbegu za malisho ya Vikuge
(Kibaha), Sao Hill (Mufindi), Langwira (Mbeya), Mabuki (Misungwi) na Kizota
(Dodoma). Mashamba
hayo yamezalisha mbegu za malisho tani 48.2 na marobota
ya hei 497,620. Pia, sekta binafsi imezalisha marobota 425,000 ya hei. Katika mwaka 2014/2015, Wizara
itaendelea kuimarisha mashamba ya uzalishaji wa mbegu bora za malisho na kuendelea
kuhamasisha sekta binafsi kuwekeza katika uzalishaji wa malisho na mbegu bora
za malisho. Pia, Serikali itawezesha uchimbaji wa kisima kirefu cha maji ya
mifugo katika Halmashauri ya Wilaya ya Same, kujenga malambo na majosho katika
Wilaya za Chemba, Handeni, Kiteto, Kilwa, Chunya, Kilindi na Ngorongoro .
Utoaji wa Kifuta Machozi kwa Wafugaji
26. Mheshimiwa Spika,
utekelezaji wa zoezi la kutoa kifuta machozi kwa wafugaji
waliopoteza mifugo yao yote katika wilaya za Longido (kaya 2,852),
Monduli (kaya 1,484) na Ngorongoro (kaya 1,791) kutokana
na ukame uliotokea mwaka 2008/2009 umeendelea kutekelezwa. Hadi
sasa ng’ombe 17,214
(mitamba 17,202 na madume bora 12) na mbuzi 6,190 wenye thamani
ya shilingi bilioni 7.4 waligawiwa kwa wafugaji sawa na
asilimia 70 ya malengo.
UDHIBITI WA MAGONJWA YA MIFUGO
Maeneo Huru ya Magonjwa ya Mifugo
27. Mheshimiwa
Spika, katika mwaka 2013/2014, Serikali imeendelea kuimarisha
miundombinu ya Kituo cha Uchunguzi wa Magonjwa ya Mifugo cha Kanda ya Kusini
Magharibi, mjini Sumbawanga kwa kukipatia vitendea kazi na wataalam. Katika
mwaka 2014/2015, Wizara itaendelea kuimarisha Eneo huru la Magonjwa ya Mifugo
kwa kukarabati jengo la ofisi la Kituo cha Uchunguzi wa Magonjwa ya Mifugo cha
Kanda ya Kusini Magharibi, kuwajengea uwezo wataalam na kukipatia vitendea kazi.
Magonjwa ya Mlipuko
28.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2013/2014, Wizara
iliendelea kuratibu na kusimamia kampeni za chanjo ya ugonjwa wa Sotoka ya
Mbuzi na Kondoo katika mikoa ya Arusha, Tanga, Morogoro na Kagera
ambapo jumla ya mbuzi na kondoo 1,163,451
walichanjwa dhidi ya ugonjwa huo.
Katika mwaka 2014/2015, Wizara itanunua dozi 1,000,000 za
chanjo ya Sotoka ya Mbuzi na Kondoo na kuzisambaza katika mikoa ya Arusha,
Tanga, Mara na Tabora iliyo katika hatari ya kuwa na mlipuko wa ugonjwa.
29. Mheshimiwa
Spika, katika mwaka 2013/2014, Wizara imeendelea kufuatilia
mwenendo wa Ugonjwa wa Mafua Makali ya Ndege hapa nchini na nje ya nchi.
Ufuatiliaji huu umebaini kuwa ugonjwa huo haujaingia hapa nchini. Aidha, Wizara kwa kushirikiana
na wadau wengine imeendelea kutoa tahadhari ili kuhakikisha kuwa virusi vya
ugonjwa huo haviingii hapa nchini. Katika mwaka 2014/2015, Wizara itaendelea
kuchukua tahadhari za kujikinga na ugonjwa huu. Aidha, Wizara itaendelea
kushirikisha wadau wengine ikiwa ni pamoja na AU-IBAR kufuatilia mwenendo wa
Ugonjwa ndani na nje ya nchi. Katika mwaka 2013/2014, Wizara imeendelea
kufuatilia Ugonjwa wa Homa ya
Mapafu ya Ng’ombe nchini kwa kuchanja ng’ombe 290,000
katika mikoa ya Pwani, Kagera, Manyara na Tanga. Katika mwaka
2014/2015, Wizara itanunua dozi 3,000,000 za chanjo kwa
ajili ya kuendeleza uchanjaji katika mikoa yenye matukio ya ugonjwa ikiwemo
mikoa ya Kagera, Geita na Shinyanga.
Magonjwa yanayoenezwa na Wadudu (Kupe na Mbung’o)
(i)
Udhibiti wa Kupe na Magonjwa yaenezwayo
30. Mheshimiwa
Spika, katika mwaka 2013/2014, Wizara imeendelea kushirikiana na wadau wengine kudhibiti
kupe na magonjwa yanayoenezwa na kupe.
Aidha, Wizara imeendelea kutekeleza mpango wa ruzuku ya asilimia 40 kwa
dawa za kuogesha mifugo ambapo lita 10,736 zenye
kiini cha pareto zilinunuliwa kwa thamani ya shilingi milioni 181.8 na
kusambazwa katika mikoa 24. Vilevile, Wizara kwa kushirikiana na
sekta binafsi imeendelea kuhamasisha matumizi ya chanjo dhidi ya ugonjwa hatari
wa Ndigana kali ambapo jumla ya ng’ombe 113,955 walichanjwa
dhidi ya ugonjwa huo katika mikoa ya Arusha, Manyara, Tanga, Kilimanjaro,
Dodoma, Tabora, Kagera na Pwani. Katika mwaka 2014/2015, Wizara itaendelea
kushirikiana na Halmashauri na wadau wengine kuhamasisha matumizi ya chanjo
hii, ujenzi na ukarabati wa majosho pamoja na matumizi sahihi ya dawa za kuogesha
mifugo.
31. Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2013/2014, Wizara
ilishirikiana na wadau mbalimbali kutekeleza Mkakati wa Kudhibiti Mbung’o na
Nagana. Katika mwaka 2014/2015, Wizara kupitia Program ya Pan African Tsetse
and Trypanosomiasis Eradication Campaign (PATTEC) itaendelea kudhibiti Mbung’o
na Nagana kwa kutekeleza miradi ya kuangamiza mbung’o kwa ajili ya mikoa ya
Mara - Ikolojia ya Serengeti, Kigoma, Tabora, Rukwa na Katavi.
Magonjwa ya Mifugo yanayoambukiza Binadamu
32.
Mheshimiwa
Spika, katika
mwaka 2013/2014, Wizara kupitia Mradi wa Kutokomeza Kichaa cha Mbwa
unaofadhiliwa na Taasisi ya Bill & Melinda Gates Foundation kwa uratibu wa
Shirika la Afya Ulimwenguni imeendelea kudhibiti Ugonjwa wa Kichaa cha Mbwa
katika mikoa ya Dar es Salaam, Lindi, Morogoro, Mtwara na Pwani kwa kushirikiana
na Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii na wadau mbalimbali. Jumla ya dozi 200,000 zimesambazwa katika Halmashauri 24 zinazotekeleza mradi huu. Udhibiti
wa magonjwa mengine ya mifugo yanayoambukiza binadamu ni pamoja na Homa ya
Bonde la Ufa, Ugonjwa wa Kutupa mimba na Kifua Kikuu kama ilivyoainishwa katika
Aya ya 43 na 44 ya Hotuba yangu.
Ukaguzi wa Mifugo na Mazao yake
33. Mheshimiwa
Spika, katika mwaka
2013/2014, jumla ya ng’ombe 987,172, mbuzi 885,061,
kondoo 275,197, nguruwe 440,000 na kuku 1,632,000
walikaguliwa na wataalam katika machinjio mbalimbali. Aidha, Wizara imeendesha
mafunzo rejea kwa Wakaguzi wa
Nyama 12 kutoka Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni na wadau 34
kutoka machinjio ya Vingunguti. Katika mwaka 2014/2015, Wizara itaendelea kufuatilia
usalama wa mazao yatokanayo na mifugo kwa kukagua mifugo na mazao yake ili
kukuza biashara ya mifugo na kulinda afya za walaji.
Utambuzi, Usajili na Ufuati liaji wa Mifugo
34. Mheshimiwa
Spika, Wizara imeendelea kuimarisha Mfumo wa Utambuzi na
Ufuatiliaji wa Mifugo kwa kutoa mafunzo kuhusu stadi za utambuzi wa mifugo na
ukusanyaji takwimu. Katika mwaka 2014/2015, Wizara itaendelea kuratibu
utekelezaji wa mfumo wa kielektroniki wa Utambuzi na Ufuatiliaji wa mifugo kwa
kutoa mafunzo kwa wataalam wa mifugo 75 kuhusu
mfumo huo na kuhamasisha umma ili kuwezesha utambuzi wa mifugo 45,000
katika makundi ya wafugaji wa ng’ombe wa asili na kisasa.
UENDELEZAJI WA SEKTA YA UVUVI
Uvunaji wa Samaki na Uuzaji wa Mazao ya Uvuvi
35. Mheshimiwa
Spika, katika mwaka 2013/2014, Wizara imetoa elimu ya usimamizi
wa rasilimali za uvuvi unaozingatia mfumo wa ikolojia na mazingira kwa wavuvi 641
kutoka Halmashauri za Bagamoyo, Kinondoni, Temeke na Mkuranga. Aidha, Maafisa Uvuvi 16 wa Wilaya,
Wavuvi 16 na Wawakilishi wa Vikundi vya Ulinzi wa
Rasilimali za Uvuvi (Beach Management Units – BMUs) 16
kutoka Halmashauri 16 za Ukanda wa Pwani walipatiwa mafunzo
kuhusu usimamizi endelevu wa rasilimali ya Jodari na samaki wanaopatikana
katika tabaka la juu la maji.
36. Mheshimiwa
Spika, nguvu ya
uvuvi nchini imeongezeka kutoka wavuvi 182,741 na vyombo vya uvuvi 56,985
mwaka 2012/2013 hadi wavuvi 183,431 wanaotumia vyombo vya uvuvi 57,385 mwaka 2013/2014. Kutokana na nguvu hiyo ya uvuvi, jumla ya tani 375,158
za samaki zenye thamani ya shilingi trilioni
1.4 zilivunwa ambapo kati ya hizo,
tani 52,846 ni kutoka ukanda wa
maji chumvi na tani 147,020 maji
baridi ikilinganishwa na tani 365,023.38 za
samaki zenye thamani ya shilingi trilioni 1.3
zilizovunwa mwaka 2012/2013. Katika mwaka
2014/2015, Wizara itaendelea kuratibu, kusimamia uvunaji na matumizi endelevu
ya rasilimali za uvuvi na kufanya sensa za uvuvi katika bahari, Ziwa Victoria,
Tanganyika, Nyasa, Rukwa, Bwawa la Nyumba ya Mungu na Mto Rufiji kwa lengo la
kuimarisha ukusanyaji, uchambuzi na uhifadhi wa takwimu za uvuvi na kuhamasisha
jamii za wavuvi kusimamia, kuendeleza na kulinda rasilimali za uvuvi kwa
kuzingatia mfumo wa ikolojia na mazingira.
Uwezeshaji Wavuvi Wadogo
37. Mheshimiwa
Spika, katika mwaka 2013/2014, Wizara kupitia
programu ya SmartFish na United Nations University Iceland imetoa mafunzo
kuhusu matumizi ya teknolojia sahihi kwa ajili ya uandaaji, uchakataji na usambazaji
wa mazao ya uvuvi kwa wavuvi 735 katika mikoa ya Kigoma,
Kagera, Mara, Mwanza na Pwani na kuwezesha ujenzi wa
vichanja vya kisasa 40 vya kukaushia samaki na majiko sanifu
manne katika Halmashauri ya
Uvinza.
38. Mheshimiwa
Spika, Wizara kwa kushirikiana na WWF, iliwawezesha
wavuvi kutoka Halmashauri za Kilwa, Lindi, Mtwara, Pangani na Mafia kuhudhuria
mafunzo ya uchakataji wa samaki
aina ya Jodari na utunzaji wa samaki wa mapambo; usimamizi shirikishi wa
rasilimali za uvuvi kupitia BMUs na uendeshaji wa miradi. Katika mwaka
2014/2015, Wizara itaendelea kutoa elimu kuhusu fursa za uwekezaji na matumizi
endelevu ya rasilimali za uvuvi na kuhamasisha sekta binafsi kuwekeza katika
ujenzi wa viwanda vya kutengeneza boti hasa za fibre na
zana za uvuvi zinazokubalika kisheria. Vilevile, itaendelea kuimarisha
miundombinu ya uvuvi kwa kukamilisha ujenzi wa mialo minne
katika ukanda wa Ziwa Tanganyika, ujenzi wa karakana ya kutengeneza boti katika
Ukanda wa Ziwa Nyasa (Mbamba Bay) na kuendeleza mchakato wa ujenzi wa Bandari ya Uvuvi.
Ukuzaji wa Viumbe kwenye Maji
39. Mheshimiwa
Spika, katika mwaka 2013/2014, jumla ya
vifaranga 2,295,032 vimezalishwa
na kusambazwa ambapo vifaranga 19,692
vimezalishwa katika vituo vya Serikali na 2,275,340 katika vituo
vya sekta binafsi. Aidha, wananchi 2,604 wamehamasishwa
kwa kupatiwa elimu ya ufugaji samaki na kutokana na uhamasishaji huo mabwawa ya
kufugia samaki yameongezeka kutoka 20,134 mwaka
2012/2013 hadi 20,493 mwaka 2013/2014 yenye uwezo wa
kuzalisha tani 3,546 za samaki. Pia, tani 320 za
kambamiti zenye thamani ya Shilingi bilioni 2.56
zimevunwa katika mabwawa ya kampuni ya Alphakrust katika Wilaya ya Mafia.
UTAFITI, MAFUNZO NA UGANI WA MIFUGO NA UVUVI
Taasisi ya Utafiti wa Mifugo Tanzania (TALIRI)
40. Mheshimiwa
Spika, katika mwaka 2013/2014, Wizara
imeendelea kuimarisha vituo vya
utafiti vya TALIRI vya Kongwa, Mabuki, Mpwapwa, Naliendele, Tanga,
Uyole na West Kilimanjaro kwa kuvipatia vitendea kazi na
kukarabati miundombinu. Aidha, Taasisi imeendelea kutekeleza
miradi ya utafiti wa mifugo ya kuboresha uzalishaji wa ng’ombe wa nyama na
maziwa; nguruwe; kuku, malisho na
masoko ya mazao ya mifugo.
41. Mheshimiwa
Spika, katika mwaka 2013/2014, TALIRI imetathmini na kusambaza
ng’ombe 143 aina ya Mpwapwa kwa wafugaji katika Manispaa za Dodoma
na Tanga na Halmashauri za Chamwino, Kilindi, Kisarawe na Bagamoyo. Aidha,
Taasisi imesambaza jumla ya madume 32 aina ya Friesian
katika Wilaya za Bagamoyo, Muheza, Mufindi na Njombe na Mbuzi aina ya Malya 65
katika maeneo ya mikoa ya Dodoma
na Pwani.
42. Mheshimiwa
Spika, kwa kutumia fedha za maendeleo chini ya COSTECH, TALIRI
imekamilisha ujenzi wa jengo la maabara ya nyama, nyumba tatu za watumishi
katika kituo cha Mabuki na ukarabati wa jengo la maabara ya viini tete Mpwapwa.
Pia, inaendelea na ukarabati wa
jengo la maabara ya maziwa Uyole, ofisi ya Tanga na mabanda ya mbuzi
West Kilimanjaro.
Utafiti wa
malisho ya Mifugo
43. Mheshimiwa
Spika, katika mwaka 2013/2014, jumla ya aina 39 za
malisho ya asili zimekusanywa kwa ajili ya kufanyiwa tathimini vituoni.
Vilevile, jumla ya marobota 44,347 ya malisho yalivunwa katika vituo vya Mpwapwa, Uyole na Kongwa. Katika
mwaka 2014/2015, TALIRI itaimarisha miundombinu ya utafiti kwa kununua vifaa vya
maabara, kemikali na samani katika maabara ya sayansi ya
nyama ya Mabuki, Uhawilishaji Viinitete (Mpwapwa), maabara ya teknolojia ya
maziwa (Uyole), maabara za lishe ya mifugo (Mpwapwa, Tanga, Naliendele na West
Kilimanjaro).
Taasisi ya Utafiti wa Uvuvi Tanzania (TAFIRI)
44. Mheshimiwa
Spika, katika mwaka 2013/2014, TAFIRI imekarabati
ofisi ya Utawala ya Kituo cha Kyela na kujenga uzio katika kituo cha Dar es
Salaam; matangi 9 katika kituo cha Dar es Salaam kwa
ajili ya utafiti wa majaribio ya vyakula vya samaki kutokana na malighafi asili.
Pia, imechimba mabwawa ya vifaranga bora vya samaki katika kituo cha Mwanza na
kuimarisha utafiti katika vituo vya Dar es Salaam, Mwanza, Kigoma, Kyela na kituo
kidogo cha Sota (Rorya). Aidha, TAFIRI imebaini kuwa wingi wa samaki aina ya
Sangara katika Ziwa Victoria umeshuka kutoka mavuno ya kilo 296 kwa
saa mwaka 2008 hadi kufikia kilo 185 kwa saa mwaka
2013. Katika mwaka 2014/2015, Wizara ikishirikiana na wadau wengine wa uvuvi
itaendelea kuiwezesha TAFIRI kuendelea na tafiti za uvuvi na mazingira katika
Bahari ya Hindi, maziwa, mito na mabwawa ili kubaini uwingi, mtawanyiko na
ikolojia ya rasilimali kwa ajili ya kuweka menejimenti ya uvuvi endelevu.
Wakala wa Elimu na Mafunzo ya Uvuvi (Fisheries Education and Training Agency - FETA)
45. Mheshimiwa
Spika, katika mwaka 2013/2014, FETA imekarabati Kituo cha
Kigoma na kupata usajili wa kudumu kutoka NACTE. Udahili wa wanafunzi
umeongezeka kutoka wanachuo 943 mwaka 2012/2013 hadi wanachuo 1,073
mwaka 2013/2014. Aidha, Wakala umeendesha mafunzo ya muda mfupi kwa wataalam
54 kutoka nchi za SADC. Katika mwaka 2014/2015, Wizara
itaendelea kuiwezesha Wakala kutekeleza majukumu yake na kuongeza udahili wa
wanafunzi kutoka 1,073 hadi 1,500.
Aidha, FETA itaendelea kujenga kituo cha Gabimori (Rorya) na kukarabati kituo
cha Mikindani Mtwara.
Wakala wa Vyuo vya Mafunzo ya Mifugo (Livestock Training Agency - LITA)
46. Mheshimiwa
Spika, katika mwaka 2013/2014, LITA imeongeza udahili wa
wanafunzi kutoka 949 mwaka 2012/2013 hadi 2,215 wakiwemo 655
wa Stashahada na 1,560 wa Astashahada
za Afya ya Mifugo na Uzalishaji. Vilevile, Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo na
vyuo binafsi vya Visele (Mpwapwa) na Kaole (Bagamoyo) vimedahili jumla ya
wanafunzi 492 wa Stashahada na Astashahada. Katika
mwaka 2014/2015, Wizara itaendelea kuiwezesha Wakala kutekeleza majukumu yake
na kuongeza udahili wa wanafunzi
kutoka 2,215 hadi 2,500; kuhamasisha
Sekta binafsi kuanzisha vyuo na kuongeza udahili kufikia lengo la wanafunzi 5,000 kwa
mwaka ili kupunguza pengo la maafisa ugani na kuwezesha mafunzo ya ufugaji
kibiashara kwa vijana (Emerging Young Commercial Farmers) ili waweze kujiajiri.
Huduma za Ugani
47. Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2013/2014, Wizara kwa kushirikiana na Halmashauri na wadau imeendelea kutoa elimu na kusambaza teknolojia za kisasa kuhusu uvuvi endelevu, ukuzaji bora wa viumbe kwenye maji na ufugaji bora wa mifugo. Aidha, Wizara imeendelea kuboresha utoaji huduma za ugani katika sekta ya uvuvi kwa kutoa mafunzo elekezi ya ufugaji wa samaki kwa wataalam 11 na wadau wa uvuvi 256 katika mikoa ya Tanga, Iringa na Morogoro.
Wakala wa Maabara ya Veterinari Tanzania (Tanzania Veterinary Laboratory Agency-TVLA)
48. Mheshimiwa
Spika, katika mwaka 2013/2014 Wizara kupitia
Wakala wa Maabara ya Veterinari Tanzania ilitekeleza kazi za utambuzi,
uchunguzi na utafiti wa magonjwa ya mifugo, uhakiki wa vyakula vya mifugo na
madawa ya kuogeshea mifugo katika maabara zake za Dar es Salaam, Arusha,
Mwanza, Tabora, Mpwapwa, Tanga, Kigoma, Iringa na Mtwara. Aidha, TVLA kwa
kushirikiana na Idara ya Wanyama Pori imetengeneza vitambaa 300 na
kuviweka katika maeneo ya Pori la
Akiba la Selous ili kudhibiti mbung’o. Katika mwaka 2014/2015, TVLA itaendelea
kutekeleza majukumu yake ikiwa ni pamoja na kuendelea kufanya utambuzi wa
magonjwa mbalimbali ya mifugo, kuendeleza tafiti za magonjwa ya mifugo,
kuzalisha dozi 100,000,000 za
chanjo ya Mdondo, dozi 500,000 za chanjo ya Chambavu, dozi 500,000 za
chanjo ya Kimeta na dozi 250,000 za chanjo ya Ugonjwa wa Kutupa
Mimba kwa Ng’ombe na Maabara Kuu ya Mifugo Temeke kukamilisha taratibu za
kupata ithibati ya Kimataifa.
USIMAMIZI WA UBORA WA MAZAO NA HUDUMA ZA MIFUGO NA UVUVI
Bodi ya Nyama Tanzania
49. Mheshimiwa
Spika, katika mwaka 2013/2014, Wizara
imeendelea kuimarisha Bodi ya Nyama Tanzania kwa kuipatia wataalam na vitendea
kazi. Aidha, Bodi imeandaa maelezo ya Sheria ya Nyama Sura 421 katika lugha ya
Kiswahili na kutoa elimu kwa wadau kupitia vipindi vya redio 14 na
kusambaza nakala 800 za vipeperushi. Vile vile, Bodi imehamasisha
wadau wa tasnia ya nyama katika mikoa ya Simiyu, Mwanza, Geita, Dar es Salaam,
Arusha, Iringa na Pwani kusajili, ambapo wadau 116 wamesajiliwa
na wadau wengine 50 wameunganishwa na soko la mifugo na
nyama. Katika mwaka 2014/2015, Bodi ya Nyama Tanzania itaendelea
kuimarisha Sekretarieti ya Bodi kwa kuajiri watumishi sita na kutambua
na kusajili wadau 200 wa tasnia ya nyama na vyama vyao.
Vilevile, Bodi itaendelea kuimarisha vyama vya wadau vya wafanyabiashara wa
Mifugo na Nyama Tanzania (TALIMETA), Wasindikaji wa Nyama Tanzania (TAMEPA) na
Wafugaji Tanzania (CCWT) kwa kushauri, kutoa mafunzo na kuratibu maendeleo ya
vyama hivyo.
Bodi ya Maziwa Tanzania
50. Mheshimiwa Spika, katika
mwaka 2013/2014, Wizara imeendelea kuimarisha Bodi ya Maziwa Tanzania iliyoundwa
kwa Sheria ya Maziwa Sura 262. Aidha, Bodi imeelimisha wadau 100 wa
maziwa kuhusu Sheria ya Maziwa katika Mkoa wa Njombe. Katika mwaka
2014/2015, Bodi itaendelea kuelimisha
wadau wa maziwa kuhusu Sheria ya Maziwa Sura 262 na kuisimamia, kuwajengea
uwezo wakaguzi 50 wa maziwa kutoka Halmashauri za mikoa
ya Iringa, Njombe na Mara na kuhamasisha Halmashauri kutekeleza Mpango wa Unywaji wa Maziwa Shuleni.
Baraza la Veterinari Tanzania
51. Mheshimiwa
Spika, katika mwaka 2013/2014, Baraza limeimarisha ukaguzi katika
ngazi za kanda, mikoa na Halmashauri ambapo Wakaguzi wapya 20 wameteuliwa.
Pia, imesajili madaktari wa mifugo 37, wataalam
wasaidizi wa afya ya mifugo 221 na vituo
106 vya kutolea huduma ya afya ya mifugo. Katika mwaka wa
2014/2015, Baraza
litasajili madaktari wa mifugo 40, vituo vya huduma za mifugo 200,
kuorodhesha na kuandikisha wataalamu wasaidizi 700, kutoa
leseni kwa wataalam wasaidizi 110 na kufanya ukaguzi wa maadili
kwa kushirikiana na Halmashauri 156 nchini.
Uthibiti wa Ubora na Usalama wa Mazao ya Uvuvi
52. Mheshimiwa
Spika, Wizara kupitia Kitengo cha Udhibiti wa
Ubora na Usalama wa Mazao ya Uvuvi na Maabara ya Taifa ya Udhibiti wa Ubora wa
Mazao ya Uvuvi-Nyegezi imeendelea kuratibu na kusimamia ubora, viwango na
usalama wa mazao ya uvuvi pamoja
na huduma za kitaalam
ikiwemo kufanya kaguzi mbalimbali za kuhakiki ubora wa mazao ya uvuvi katika
viwanda vya kuchakata mazao ya uvuvi, mialo, masoko na kwenye magari na boti
zinazosafirisha mazao ya uvuvi.
53. Mheshimiwa
Spika, Wizara imeendelea kuimarisha
vituo vya Udhibiti Ubora wa mazao ya Uvuvi vya Bukoba, Dar es
Salaam, Kigoma, Kilwa, Mafia, Musoma, Mwanza na Tanga, pamoja na Maabara
ya Taifa ya Udhibiti wa Ubora wa Mazao ya Uvuvi - Nyegezi kwa kuvipatia
watumishi na vitendea kazi. Katika mwaka 2013/2014, jumla ya
sampuli 1,318 za samaki, maji, vyakula vya samaki na udongo
zilifanyiwa uchunguzi. Kati ya hizo 966 zilichunguzwa
kubaini uwepo wa vimelea vya magonjwa na 352 kubaini
mabaki ya viuatilifu, madini tembo na kemikali. Matokeo ya uchunguzi wa sampuli
hizi ulionyesha kukidhi viwango. Katika mwaka 2014/2015, Wizara itaendelea
kuimarisha vituo vya Ubora na Udhibiti wa Mazao ya Uvuvi na Maabara za Uvuvi –
Nyegezi kwa kuvipatia vitendea kazi na mafunzo kwa watalaam.
USIMAMIZI WA RASILIMALI ZA UVUVI
54.
Mheshimiwa Spika, Wizara kwa kushirikiana na Ofisi ya
Makamu wa Rais – Mazingira, Ofisi ya Waziri Mkuu - TAMISEMI, Wizara ya Mambo ya
Ndani ya Nchi, Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Wizara ya Maliasili
na Utalii, Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) na Halmashauri imeendelea kusimamia
matumizi endelevu ya rasilimali za uvuvi kwa kudhibiti uvuvi haramu na
utoroshaji wa samaki na mazao ya uvuvi mipakani.
Udhibiti wa Uvuvi Haramu
55. Mheshimiwa
Spika, katika mwaka 2013/2014, Wizara imeanzisha kituo cha
doria cha Buhingu (Uvinza) na kufanya vituo vya doria kufikia 23. Pia, doria
zenye siku kazi 6,201 zimefanyika na kuwezesha kukamatwa nyavu
mbalimbali 33,861, vyandarua 123,
mabomu 73, tambi za kulipulia mabomu 15, mitungi
ya gesi 48, viatu vya kuzamia jozi 35, miwani ya
kuogelea jozi 11, mitumbwi 194, injini za
boti 10, magari 12 na pikipiki 2. Aidha,
samaki wachanga kilo 30,823 za sangara, 2,478 za
sato, 1,112 za samaki aina nyingine na kilo 187 za
samaki waliovuliwa kwa mabomu, kilo 682 za
dagaa, kilo 57 za
Pweza, kilo 5 za majongoo bahari na kilo 210 za
nyama ya Kasa zilikamatwa. Vilevile, watuhumiwa 319
walikamatwa kwa kujihusisha na uvuvi na biashara haramu ya mazao ya uvuvi
ambapo kesi 48 zilifunguliwa mahakamani. Katika mwaka
2014/2015, Wizara kwa kushirikiana na wadau mbalimbali itaendelea kuratibu na
kusimamia uvunaji endelevu wa rasilimali za uvuvi na kudhibiti biashara haramu
ya mazao ya uvuvi kwa kufanya doria zenye siku kazi 6,000
katika maeneo ya maji baridi, Bahari ya Kitaifa (territorial waters) na maeneo
ya mipakani. Aidha, itaendelea kuwezesha uanzishwaji wa Vikundi vya Usimamizi
Shirikishi wa Rasilimali za Uvuvi (BMUs) na
kuimarisha vikundi vilivyopo.
Mamlaka ya Kusimamia
Uvuvi Bahari Kuu
56. Mheshimiwa
Spika, Wizara kupitia Mamlaka ya Kusimamia Uvuvi Bahari Kuu (Deep Sea Fishing Authority)
kwa kushirikiana na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam inaendelea kufanya utafiti
kuhusu matumizi sahihi ya vifaa vya kuvutia samaki (Fish Aggregating Devises
– FADs). Pia, Mamlaka imeendelea kuandaa mazingira rafiki ambayo
yatawawezesha Watanzania kuingia ubia na wageni ili waweze kuwekeza kwenye
uvuvi katika Bahari Kuu. Aidha, Mamlaka kwa kushirikiana na nchi wanachama wa Indian Ocean Tuna
Commission (IOTC) za Comoro, Madagascar, Seychelles, Reuninon na
Mauritius, ilifanya doria za
pamoja za siku 8, kukagua meli 8
zinazovua katika Bahari Kuu ya Tanzania. Pia, ukaguzi ulifanyika kwa meli 25
za uvuvi wa purse seine na long
liner zenye
Bendera ya Hispania, Taiwan na China katika Bandari za Dar es Salaam na
Zanzibar, Mombasa, Mahe Victoria (Ushelisheli), Madagascar na Mauritius. Katika
ukaguzi huo meli husika zilionekana kukidhi masharti ya leseni. Vilevile,
leseni za uvuvi wa Bahari Kuu 68 zenye thamani ya Dola za
Kimarekani 1,472,153 sawa na shilingi bilioni 2.4 zilitolewa
kwa meli kutoka mataifa ya Hispania, Ufaransa, Ushelisheli, Taiwan, Japan, Oman
na China. Katika mwaka 2014/2015, Wizara itaiwezesha Mamlaka kukamilisha
marekebisho ya Sheria na Kanuni za Uvuvi wa Bahari Kuu, kuendesha doria na
kufanya tathimini ya utendaji wa FADs. Pia, kuendelea kuhamasisha wavuvi wa
Tanzania na wawekezaji wengine kuwekeza katika uvuvi wa Bahari Kuu na kusindika
mazao ya uvuvi. Vilevile, kuendelea kutoa mafunzo ya uvuvi wa Bahari Kuu kwa
wavuvi.
Hifadhi za Bahari na Maeneo Tengefu
57. Mheshimiwa
Spika, Wizara imeendelea kusimamia maendeleo ya
rasilimali za uvuvi katika maeneo yaliyohifadhiwa kupitia kitengo cha
Hifadhi za Bahari na Maeneo Tengefu ambapo doria zenye siku kazi 800 zilifanyika
iliyowezesha kukamatwa vifaa mbalimbali zikiwemo mabomu 21 na tambi zake, chupa za mbolea ya
Urea inayotumika kutengeneza mabomu na makokoro 5. Katika mwaka 2014/2015, Kitengo
kitafanya doria zenye siku kazi 416 katika eneo la
kilomita za mraba 2,000 kwa lengo la kudhibiti uvuvi haramu
kwenye Hifadhi za Bahari na Maeneo Tengefu na pia kuvutia uwekezaji wa utalii.
3.3 MASUALA MTAMBUKA
Uendelezaji wa Rasilimali Watu
58. Mheshimiwa
Spika, katika mwaka 2013/2014, Wizara imeajiri watumishi 124
wakiwemo 71 wa kada za mifugo, 43
kada za uvuvi na 10
kada mtambuka. Aidha, Maafisa Mifugo na Uvuvi 853 wameajiriwa
na kupelekwa katika Sekretarieti za Mikoa 17 na
Halmashauri 103 nchini kupitia Sekretarieti ya
Ajira katika Utumishi wa Umma. Vilevile, Watumishi 187 wamepandishwa
vyeo, 8 wamebadilishwa
kazi baada ya kupata sifa za Miundo ya Utumishi na 57 wamethibitishwa
kazini, 161 wamehudhuria mafunzo ya muda mfupi, 39
wanaendelea na mafunzo ya muda mrefu wakiwemo wa uzamivu sita (6),
uzamili 22 na Shahada ya Kwanza 11
na 55 walipatiwa mafunzo elekezi. Katika mwaka 2014/2015, Wizara inatarajia kuajiri
watumishi 214 (wakiwemo mifugo 62,
uvuvi 86 na mtambuka 66),
kupandisha vyeo watumishi 223, kuthibitisha kazini
watumishi 125 na watumishi 312
watahudhuria mafunzo ya muda mrefu na mfupi.
Mawasiliano na Elimu kwa Umma
59. Mheshimiwa Spika,
katika mwaka 2013/2014, vipindi vitano kuhusu mafanikio ya sekta za mifugo
na uvuvi na makala moja ya utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya 2010
vilitangazwa kupitia luninga na magazeti. Katika mwaka 2014/2015, Wizara itaendelea kuimarisha Dawati
la Malalamiko na Maktaba; na kutoa mafunzo kwa maafisa habari wawili. Aidha,
itatoa mafunzo kwa maafisa kutoka vituo vya nje kuhusu mawasiliano kwa umma na
kuchapisha na kusambaza kwa wadau nakala 1,000 za kalenda.
60. Mheshimiwa Spika,
katika mwaka 2013/2014, Wizara imeendelea kusimamia masuala mengine
mtambuka ya Utawala Bora,
Jinsia, UKIMWI,
TEHAMA na Hifadhi ya Mazingira na Mabadiliko ya Tabianchi kama yalivyoainishwa katika
Aya ya 110 hadi 115 ya
Hotuba yangu.
4.0 SHUKRANI
61.
Mheshimiwa Spika, Kabla ya
kuhitimisha hotuba yangu, napenda kutoa shukrani
zangu za dhati kwa Wafugaji, Wavuvi, Wasindikaji, Wafanyabiashara na wadau
wengine kwa kazi kubwa wanayoifanya ya kuendeleza sekta za mifugo na uvuvi
nchini. Wizara inaomba waendeleze juhudi hizo na inaahidi kuendelea
kushirikiana nao kuleta mapinduzi ya sekta za mifugo na uvuvi nchini. Aidha, napenda kuzitambua na kuzishukuru nchi za
Jumuiya ya Afrika Mashariki, Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika
(SADC), Umoja wa Nchi za Ulaya, Serikali za Australia, Austria, Brazil, Canada,
Jamhuri ya Czech, Hispania, Iceland, Ireland, Japan, Jamhuri ya Watu wa China,
Israel, Korea Kusini, Marekani, Misri, Norway, Poland, Sweden, Ubelgiji,
Ufaransa, Uholanzi, Uingereza, Ujerumani na Uswisi pamoja na mashirika ya Umoja
wa Mataifa ya FAO, IAEA, UNICEF, UNDP, UNIDO na WHO na mifuko ya kimataifa ya
GEF na IFAD kwa kuchangia katika maendeleo ya sekta za mifugo na uvuvi.
62. Mheshimiwa
Spika, vilevile, nazishukuru taasisi za
kimataifa ambazo ni pamoja na Benki ya Dunia, Benki ya Maendeleo ya Afrika;
Shirika la JICA, Shirika la KOICA, Shirika la Misaada la Ireland, USAID,
Shirika la Misaada la Australia (AUSAID), DfID, Taasisi ya Rasilimali za
Wanyama ya Umoja wa Afrika (AU-IBAR), Shirika la Afya ya Wanyama Duniani (OIE),
Shirika la Maendeleo la Uswisi (SDC), Shirika la Ushirikiano la Ujerumani
(GTZ), United Nations University (UNU), Shirika la Maendeleo la Denmark (DANIDA)
na Shirika la Maendeleo la Sweden
(SIDA) kwa michango yao katika kuendeleza sekta za mifugo na uvuvi. Pia,
nayashukuru Mashirika na Taasisi za hiari za Bill and Melinda Gates Foundation,
ASARECA, NEPAD, International Livestock Research Institute, World Wide Fund for
Nature, Indian Ocean Tuna Commission, South West Indian Ocean Fisheries
Commission (SWIOFC), Heifer Project Tanzania, Overseas Fisheries Co-operation
Foundation of Japan, Vetaid, Care International, OXFAM, Welcome Trust, World
Vision, FARM Africa, Land O’ Lakes, Building Resources Across Communities, World
Society for Protection of Animals,
Global Alliance for Livestock and Veterinary Medicine, Institute for Security
Studies, International Land Coalition, British Gas International, Sea Sense, International
Whaling Commission, SmartFish na Marine Stewardship Council.
63. Mheshimiwa
Spika, naomba nimalizie kuwashukuru kwa
dhati Mhe. Kaika Saning’o Ole Telele, Mbunge
wa Ngorongoro na Naibu Waziri wa Maendeleo ya Mifugo na Uvuvi kwa msaada wake wa
karibu katika kusimamia kazi za Wizara. Aidha, napenda pia nitoe shukurani
zangu kwa Katibu Mkuu Dkt. Charles Nyamrunda, Naibu
Katibu Mkuu Dkt. Yohana Budeba, Wakuu wa Idara na Vitengo,
Taasisi na watumishi wote wa Wizara kwa ushirikiano wao katika kutekeleza
majukumu tuliyopewa na Taifa na kufanikisha maandalizi ya bajeti hii. Vilevile,
napenda kuwashukuru wananchi wa Jimbo la Busega kwa ushirikiano wao
wanaoendelea kunipa na kuniwezesha kutekeleza majukumu yangu. Pia, naishukuru
familia yangu kwa kuendelea kunitia moyo ninapotekeleza majukumu ya kitaifa.
5.0 BAJETI KWA MWAKA WA FEDHA 2014/2015
64. Mheshimiwa
Spika, katika mwaka wa fedha wa
2014/2015, Wizara inaomba Bunge lako Tukufu
likubali kupitisha Makadirio ya Matumizi ya Wizara ya Maendeleo ya Mifugo na
Uvuvi ya jumla ya shilingi 66,142,627,000.00 kama ifuatavyo:-
(i)
Shilingi 40,952,022,00.00 ni kwa ajili ya Matumizi ya Kawaida. Kati ya hizo, shilingi 22,968,188,000.00 ni kwa ajili ya mishahara ya watumishi (PE); na
shilingi 17,984,834,000.00 ni kwa ajili ya Matumizi Mengine (OC); na
(ii)
Shilingi 25,190,605,000.00 ni kwa
ajili ya kutekeleza miradi ya maendeleo.
Kati ya hizo, shilingi 23,000,000,000.00 ni fedha za ndani na shilingi 2,190,605,000.00 ni fedha za nje.
6.5 Mheshimiwa
Spika, naomba tena nitoe shukurani zangu za
dhati kwako na kwa Waheshimiwa Wabunge kwa
kunisikiliza. Hotuba hii pia inapatikana katika Tovuti ya Wizara kwa
anuani: www.mifugouvuvi.go.tz.
66. Mheshimiwa
Spika, pamoja na hotuba hii
nimeambatanisha Randama ya Mpango na Bajeti ya Wizara kwa mwaka 2014/2015.
67.
Mheshimiwa Spika, naomba
kutoa hoja.
No comments:
Post a Comment