HOTUBA YA WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA KIMATAIFA, MHESHIMIWA BERNARD KAMILLIUS MEMBE (MB.), AKIWASILISHA BUNGENI MAKADIRIO YA
MAPATO NA MATUMIZI YA
WIZARA YA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA KIMATAIFA KWA MWAKA WA FEDHA
2014/2015
1.
UTANGULIZI
Mheshimiwa
Spika, kufuatia taarifa iliyowasilishwa leo Bungeni na
Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa
Kimataifa, naomba kutoa hoja kwamba Bunge lako Tukufu likubali kujadili na
kupitisha Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Mambo ya Nje na
Ushirikiano wa Kimataifa kwa mwaka wa fedha 2014/2015.
Mheshimiwa Spika, awali ya yote naomba niungane
na wenzangu walionitangulia kutoa pole kwa familia, kwako binafsi na
kwa Bunge lako Tukufu kwa misiba iliyotokea katika mwaka huu wa fedha, ambapo
tuliondokewa na wabunge wenzetu wawili; Mheshimiwa William Augustao Mgimwa, aliyekuwa
Mbunge wa Kalenga na Mheshimiwa Saidi Ramadhani Bwanamdogo, aliyekuwa Mbunge wa
Chalinze. Taifa limepoteza watu waliokuwa na mchango mkubwa kwa maendeleo. Mwenyezi Mungu aziweke roho
za marehemu wote mahali pema peponi. Amina.
Mheshimiwa
Spika, kwa nafasi hii napenda nitoe shukrani kwa Viongozi
na Watanzania wote walioisaidia Wizara yangu wakati ilipopata msiba wa ghalfa
wa aliyekuwa Balozi wa Malawi hapa nchini Marehemu Flossie Gomile Chidyaonga
uliotokea tarehe 9 Mei, 2014. Napenda kutoa shukrani za pekee kwa Mheshimiwa
Jakaya Mrisho Kikwete, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kutoa
usafiri wa ndege wa kusafirisha mwili wa marehemu kwenda nyumbani kwao
Blantyre, Malawi.
Mheshimiwa
Spika, wakati kumbukumbu ya kifo cha Mzee Nelson
Rolihlahla Mandela bado ingalipo, napenda kuchukua nafasi hii kuwashukuru
Watanzania wote na Waheshimiwa Wabunge kwa maombolezo hayo. Pia, kumshukuru
tena Mheshimiwa Rais wetu kwa hotuba aliyoitoa kwenye mazishi yale kwa niaba ya
Watanzania wote, iliyogusa sana nyoyo za
ndugu zetu wa Afrika Kusini, hadi kupelekea Serikali yao kututumia salamu rasmi
za upendo na shukrani kwa yote ambayo Tanzania imeyafanya huko nyuma wakati wa
vuguvugu la ukombozi na wakati wa
kipindi cha msiba huo.
Mheshimiwa
Spika, napenda kutumia fursa hii pia kutoa pongezi kwa Mheshimiwa
Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa
uongozi wake mahiri wa Serikali ya Awamu ya Nne. Ni dhahiri kwamba chini ya
uongozi wake Taifa letu limeendeleza utamaduni wetu wa kudumisha amani, usalama
na mshikamano wa kitaifa pamoja na kuimarisha ushawishi wa Tanzania katika
nyanja za Kikanda na Kimataifa kupitia diplomasia thabiti na imara. Pamoja na utendaji
wake kuonekana kwetu, mtazamo wa watu wa nje ya Tanzania pia unadhihirisha
hivyo. Tarehe 9 Aprili 2014, Mheshimiwa Rais alitunukiwa tuzo ya kuwa kiongozi
mwenye mchango mkubwa zaidi katika maendeleo Barani Afrika kwa mwaka 2013, huko
jijini Washington DC. Tuzo hiyo ya
heshima kubwa niliyoipokea kwa niaba yake, ilitolewa na jarida maarufu la
kimataifa liitwalo African Leadership
Magazine Group.
Mheshimiwa
Spika,
ninawaomba Watanzania wenzangu, tuendelee
kushirikiana na wenzetu duniani kote katika kudumisha demokrasia, amani,
usalama, umoja na mshikamano bila kujali rangi, kabila, dini au itikadi zetu za
kisiasa. Napenda kuwakumbusha Waheshimiwa
Wabunge kwamba jumuiya ya kimataifa inatambua na kuthamini mchango wa Tanzania
katika maeneo hayo ya utawala bora na hivyo kuichukulia kama mfano wa kuigwa.
Mheshimiwa
Spika,
napenda vilevile kuwashukuru Mheshimiwa Mizengo Peter Pinda (Mb.), Waziri Mkuu
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mheshimiwa Stephen Masato Wassira (Mb.),
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mahusiano na Uratibu kwa hotuba zao nzuri.
Hotuba zao sio tu zimechambua kwa kina masuala ya kiuchumi, kijamii, kiusalama
na kisiasa na kutoa dira ya Taifa letu katika mwaka ujao wa fedha, bali zimegusia
pia mambo kadhaa ya msingi yanayohusu Wizara yangu. Aidha, nawashukuru Waheshimiwa
Mawaziri wote ambao wameshawasilisha hotuba zao, ambazo kwa namna moja au
nyingine ziligusa maeneo yanayohusu Wizara yangu. Kama mnavyofahamu, Wizara hii
inashughulikia masuala mtambuka ambayo yanagusa na kuguswa na Wizara, Idara na
Taasisi zote yanapokuja masuala ya nchi, kanda, kimataifa na mashirika
mbalimbali duniani. Wajibu wetu mkubwa ni kuratibu masuala hayo na utekelezaji
unabaki kwa Taasisi husika.
Mheshimiwa
Spika,
naomba nitumie fursa hii kutoa shukurani
zangu za dhati kwa wajumbe wote wa Kamati ya Bunge ya Mambo ya Nje na
Ushirikiano wa Kimataifa, chini ya uongozi wa Mheshimiwa Edward Ngoyai Lowassa
(Mb.), Mwenyekiti wa Kamati na Makamu wake Mheshimiwa Azan Zungu (Mb.) kwa kazi
nzuri waliyoifanya ya kuchambua na kushauri Wizara yangu kuhusu bajeti wakati
wa vikao vya Kamati. Uchambuzi na ushauri walioutoa utakuwa nguzo muhimu katika
utekelezaji wa bajeti hii na majukumu ya Wizara yangu na hivyo kusimamia
utekelezaji wa diplomasia ya uchumi kwa ukamilifu zaidi kwa manufaa ya nchi
yetu.
Mheshimiwa Spika, pongezi zangu pia kwa Wabunge
wapya watatu waliojiunga nasi mwaka huu, ambao ni Mheshimiwa Yusuf Salim
Hussein, Mbunge wa Chambani; Mheshimiwa Godfrey William Mgimwa, Mbunge wa
Kalenga; na Mheshimiwa Ridhiwan Jakaya Kikwete, Mbunge wa Chalinze. Nawapongeza
kwa kuchaguliwa kuwawakilisha wananchi katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania.
Mheshimiwa
Spika,
pia nawashukuru kwa dhati Mheshimiwa Dkt. Mahadhi Juma Maalim (Mb.), Naibu Waziri
wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa; Bwana John M. Haule, Katibu Mkuu;
Balozi Rajabu H. Gamaha, Naibu Katibu Mkuu; Wakurugenzi, Mabalozi na
Wafanyakazi wote wa Wizara yangu waliopo Makao Makuu, Ofisi yetu ya Zanzibar na
katika Balozi zetu mbalimbali duniani, kwa ushirikiano wanaonipa na kwa kazi nzuri
na ya kizalendo ya kutetea maslahi ya Taifa letu.
Mheshimiwa
Spika,
halikadhalika niwashukuru wananchi na viongozi wa Mkoa wa Lindi, hususan wa
Jimbo la Mtama kwa kuniunga mkono katika shughuli za maendeleo jimboni na
mkoani kwa ujumla. Shukurani za pekee ziwaendee mke wangu Mama Dorcas Membe na
watoto wetu kwa kunivumilia pale ninapolazimika kuwa mbali na familia kwa muda
mrefu na kunitia moyo katika kutimiza majukumu yangu ya kulitumikia Taifa.
2.
TATHMINI
YA HALI YA DUNIA
Mheshimiwa
Spika,
hali
ya dunia kwa sehemu kubwa ni shwari ingawaje bado kuna changamoto kubwa ya
vitendo vya kigaidi. Mbali na changamoto hiyo, viongozi duniani pamoja na
jumuiya za kimataifa wanaendelea kupambana na mabadiliko ya tabianchi ambayo
yanaathiri sana maisha ya walimwengu. Aidha, amani duniani ipo lakini usalama
wake umeathirika kwa kiwango kikubwa na migogoro ya vita vya wenyewe kwa
wenyewe kwenye baadhi ya nchi. Kwa upande wa maendeleo na kuboresha maisha ya
watu, nchi nyingi duniani zinajitahidi kufikia malengo ya milenia ambayo
yanakoma mwakani lakini Umoja wa Mataifa utaendeleza baadhi ya malengo hayo
baada ya 2015 ili dunia iwe na malengo endelevu ya maendeleo (SDGs). Napenda
kutoa tathmini ya maeneo machache ya dunia ambayo kwa namna moja au nyingine
yanatuhusu:-
2.1.
Mgogoro
wa Syria
Mheshimiwa
Spika, kama nilivyolieleza Bunge lako Tukufu
kwenye hotuba yangu ya bajeti ya mwaka 2013/2014 kuhusu mgogoro wa Syria, hali
imeendelea kuwa mbaya na hivyo kusababisha vifo vingi, wakimbizi wa ndani na
nje na uharibifu mkubwa wa mali. Hali hii inazidi kuwa mbaya zaidi baada ya
msuluhishi aliyechukua nafasi ya Kofi Annan, Mheshimiwa Lakhdar Brahimi naye
kuomba kujiuzulu nafasi hiyo mwezi huu. Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa kwa masikitiko
makubwa amekubali kujiuzulu kwake ifikapo tarehe 31 Mei 2014. Tanzania inaiomba
Jumuiya ya Kimataifa kuendelea na jitihada za makusudi kuhakikisha mgogoro huo
unapatiwa ufumbuzi, hususan kwa njia ya mazungumzo na hivyo kurejesha amani na
utulivu kwa nchi na wananchi wa Syria.
2.2
Mgogoro wa Ukraine
Mheshimiwa
Spika, kama mnavyofahamu, pamekuwepo na mgogoro nchini Ukraine
uliopelekea kujitenga kwa jimbo lake moja la Crimea na mengine kutaka kufanya
hivyo. Mgogoro huo umetishia kuigawa dunia pande mbili, zile zinazounga mkono
kujitenga zikiongozwa na Urusi na zile zinazopinga zikiongozwa na Mataifa ya
Ulaya na Marekani. Msimamo wa Tanzania ni kutofungamana na upande wowote ili
kuepuka kuingia kwenye mgogoro huo unaotishia amani na usalama wa dunia kwa
kuirudisha tena kwenye vita baridi. Tanzania inaendelea kuiomba Jumuiya ya
Kimataifa kushughulikia mgogoro huu kwa kutumia hekima na busara ambayo
itaiepusha dunia kuingia kwenye vita.
2.3
Hali ya Usalama Barani Afrika
Mheshimiwa Spika,
hali ya amani na usalama Barani Afrika kwa kipindi cha mwaka 2013/2014 imezidi
kuimarika. Baadhi ya migogoro kama vile wa Liberia, Cote d’Ivoire, Burundi,
Guinea, na Madagascar imepatiwa ufumbuzi wa kudumu. Jitihada zinaendelea ili
kutafuta suluhu kwenye migogoro ya kisiasa inayoendelea kwenye nchi kama Somalia, Sudan Kusini, Jamhuri
ya Afrika ya Kati, Misri na Libya.
2.3.1 Somalia
Mheshimiwa
Spika, katika kipindi cha mwaka 2013/2014, hali ya usalama
nchini Somalia imeendelea kuimarika ambapo mashambulizi ya kikundi cha Al
Shaabab dhidi ya vikosi vya Serikali na Umoja wa Afrika yamepungua kwa kiasi
kikubwa. Hali hiyo imefanya usalama wa raia kuimarika zaidi. Vilevile matukio
ya uharamia katika Pwani ya Afrika Mashariki yamepungua sana. Tanzania
inaipongeza Serikali ya Somalia kwa juhudi zake kubwa za kuimarisha hali ya
usalama nchini humo. Aidha, tunapongeza Umoja wa Afrika na Jeshi la Afrika la
kulinda amani nchini Somalia (AMISOM), na hasa majeshi ya Kenya ambayo
yaliingia hadi Kismayu na kuiteka kabisa ngome ya Maharamia. Tanzania
itaendelea kutumia ushiriki wake kwenye Baraza la Amani na Usalama la Umoja wa
Afrika kuhakikisha kuwa amani na usalama nchini Somalia vinazidi kuimarika.
2.3.2 Sudan Kusini
Mheshimiwa Spika,
dunia ilipatwa na mfadhaiko mkubwa mwezi Desemba 2013 baada ya taifa jipya na changa la Sudan Kusini
kuingia kwenye mapigano makali ya wenyewe kwa wenyewe. Mapigano hayo yaliyoanza
mwezi Julai 2013 yalisababishwa na kutoelewana kati ya Mheshimiwa Salva Kiir, Rais wa
Jamhuri ya Sudan Kusini na aliyekuwa Makamu wake, Bwana Riek Machar. Hali hii ilitokea
baada ya Rais Kiir kumfuta kazi Makamu wake huyo na baadhi ya viongozi wengine waandamizi.
Mheshimiwa Spika,
mgogoro kati ya viongozi hao ulichukua sura mpya tarehe 14 Desemba, 2013 baada
ya Serikali ya Sudan Kusini kutangaza kuwepo kwa jaribio la mapinduzi
lililofanywa na wafuasi wa Bw. Machar. Baada ya tangazo hilo, Bw. Machar
alikwenda mafichoni lakini wafuasi wake 11 walikamatwa na kufunguliwa mashtaka
ya uhaini. Hatua ya kuwakamata wafuasi wa Bw. Machar ilizusha mapigano makali
baina ya vikosi vya Serikali na wafuasi wa Bw. Machar, hususan kwenye majimbo
ya Jonglei, Unity na Upper Nile. Kadri muda ulivyokwenda, mapigano
yalichukua sura ya ukabila kati ya kabila la Ngok Dinka analotoka Rais Kiir na
Nuer la Bwana
Machar, ambapo idadi kubwa ya raia wasio na hatia waliuawa na wengine
kulazimika kukimbia makazi yao.
Mheshimiwa Spika,
kufuatia kuibuka kwa mapigano hayo, tarehe 24 Desemba, 2013, Baraza la Usalama
la Umoja wa Mataifa lilipitisha azimio la kuongeza askari kwenye kikosi chake
kilichopo Sudan Kusini (United Nations
Mission in South Sudan – UNMISS). Kufuatia
kazi nzuri iliyofanywa na Jeshi la Ulinzi la Wananchi Tanzania kule Darfur,
Lebanon na hasa DRC, Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa limeiomba Tanzania
kupeleka Kikosi cha Kulinda Amani Sudan ya Kusini na Serikali yetu tayari
imeridhia ombi hilo. Aidha, tarehe 27
Desemba 2013, Wakuu wa Nchi wa IGAD (the Inter-Governmental
Authority on Development) walifanya mkutano wa dharura mjini Nairobi,
Kenya, kujadili mgogoro huo. Tarehe 30 Desemba, 2013 Baraza la Amani na Usalama
la Umoja wa Afrika lilifanya kikao mjini Banjul, Gambia, na kuunga mkono
jitihada za IGAD kwa kuzitaka pande zinazohusika kuacha mapigano na kuanza
mazungumzo.
Mheshimiwa Spika,
pande zinazohusika na mgogoro nchini Sudan Kusini
zilianza mazungumzo mjini Addis Ababa, Ethiopia, tarehe 4 Januari, 2014.
Kufuatia majadiliano hayo tarehe 23 Januari, 2014 pande hizo mbili zilitia
saini Mkataba wa kusimamisha mapigano baada ya Serikali kukubali kuwaachia huru
wafuasi 7 kati 11 wa Bwana
Machar. Pande hizo mbili zilianza tena mazungumzo mwezi Februari 2014 ili
kutafuta suluhisho la kudumu la mgogoro huo. Hata hivyo, mazungumzo hayo
yalikwama na kusitishwa baada ya upande wa Bw. Machar kushinikiza kuachiwa huru
kwa wafuasi wanne waliobaki.
Mheshimiwa Spika,
tarehe 25 Aprili 2014,
Serikali ya Sudan Kusini iliwaachia huru wafuasi wanne wa Bwana Machar waliokuwa bado wakishikiliwa
na Serikali. Kufuatia uamuzi huo wa
Serikali, tarehe 9 Mei, 2014 Rais Kiir na Bwana
Machar walifanya mazungumzo
ya ana kwa ana, mjini Addis Ababa kwa mara ya kwanza tangu kuibuka kwa mgogoro
huo na kuweka saini makubaliano ya kusitisha mapigano.
Mheshimiwa Spika, makubaliano
yaliyofikiwa kati ya pande mbili zinazogombana katika kikao hicho cha Addis
Ababa ni; kwanza pande zote mbili kuacha mapigano; pili, pande zote ziruhusu
mashirika ya utoaji huduma za madawa, tiba na chakula kuwafikia waathirika ili
kuwapa misaada hiyo; tatu, kuchuja askari ili wale watiifu wasajiliwe na
kuingizwa kwenye jeshi la Taifa; nne kuunda Serikali ya Mseto na ya mpito na
tano kutengeneza Katiba mpya. Kutokana
na makubaliano hayo, uchaguzi ambao ulitakiwa kufanyika mwakani 2015, sasa
umeahirishwa. Tanzania inaunga mkono
makubaliano hayo.
2.3.3 Jamhuri ya Afrika ya Kati
Mheshimiwa Spika,
kama itakavyokumbukwa nchi ya Jamhuri ya Afrika ya Kati iliingia kwenye mgogoro
baada ya waasi wa Kikundi cha SELEKA kufanya mapinduzi yaliyomwondoa madarakani
aliyekuwa Rais wa nchi hiyo, Bwana
Francios Bozize mwezi Machi 2013. Kiongozi wa Kikundi cha SELEKA Bwana Michel Djotodia
alichukua madaraka lakini uongozi wake ulishindwa kurejesha utulivu nchini
humo. Hali ya usalama ilizidi kudorora zaidi mwezi Desemba 2013 baada ya kuanza
kwa mapigano makali yaliyochukua sura ya udini, baina ya wanamgambo wa Kundi la
SELEKA lenye wafuasi wengi wa Kiislamu na wanamgambo wa Kundi la ANTI-BALAKA
lenye wafuasi wengi wa Kikristo. Mapigano hayo yalisababisha madhara makubwa
nchini humo, ikiwemo idadi kubwa ya vifo vya raia na maelfu ya watu kukimbia
makazi yao.
Mheshimiwa Spika,
tangu kuibuka kwa mgogoro nchini Jamhuri ya Afrika ya Kati, Jumuiya ya Kimataifa ikiwemo Umoja wa
Afrika (AU),
Umoja wa Mataifa na Jumuiya ya Uchumi ya Nchi za Afrika ya Kati (Economic Community of the Central African
States – ECCAS) na wadau mbalimbali imekuwa ikifanya jitihada za kutatua
mgogoro nchini humo. Umoja wa Afrika uliisimamishia uanachama nchi hiyo kwa
kuwa Serikali yake iliingia madarakani kinyume cha sheria. Aidha, mwezi Julai 2013,
Baraza la Amani na Usalama la Umoja wa Afrika, ambalo Tanzania ni
mjumbe, lilipitisha uamuzi wa kupelekwa Kikosi cha Afrika cha Kulinda Amani
nchini Jamhuri ya Afrika ya Kati (Africa-led
International Support Mission in the Central African Republic –MISCA)
kuchukua nafasi ya vikosi vya nchi za ECCAS. Baraza la Usalama la Umoja wa
Mataifa liliridhia uamuzi wa kupelekwa kwa kikosi hicho chenye askari 6,000
tarehe 5 Desemba 2013,
kuungana na askari wengine 1,200 wa Ufaransa waliokuwemo nchini humo. Kikosi
hicho kwa sasa kinaundwa na askari kutoka Congo, Chad na Rwanda.
Mheshimiwa Spika,
kutokana na kuendelea kulegalega kwa uongozi wa Bwana Djotodia, Wakuu wa
Nchi wa ECCAS walifanya kikao nchini Chad tarehe 11 Januari, 2014. Wakati wa
kikao hicho, Bwana
Djotodia na Waziri wake Mkuu Bwana Nicolas Tiengaye
walitangaza kujiuzulu. Tarehe 20 Januari, 2014 Bunge la Mpito la Jamhuri ya
Afrika ya Kati lilimteua Bibi Catherine Samba-Panza, aliyekuwa Meya wa Mji wa
Bangui, kuwa Rais wa Mpito wa nchi hiyo hadi uchaguzi mkuu wa nchi hiyo utakapofanyika.
Tangu kuingia madarakani kwa Serikali mpya na kuwasili kwa vikosi vya MISCA,
hali ya usalama imeanza kuimarika.
Mheshimiwa Spika,
katika hatua nyingine, tarehe 10 Aprili 2014, Baraza la Usalama la Umoja wa
Mataifa lilipitisha Azimio la kuunda Kikosi cha Kulinda Amani nchini humo (UN Multilateral Integrated Stabilization
Mission in Central African Republic – MINUSCA) kwa kipindi cha mwaka mmoja
hadi 30 Aprili, 2015 kuchukua nafasi ya MISCA. MINUSCA ambayo itakuwa na idadi
ya walinda amani 12,000 inatarajiwa kuanza kazi rasmi mwezi Septemba 2014.
Mheshimiwa Spika,
Tanzania ikiwa mjumbe wa Baraza la Amani na Usalama la Umoja wa Afrika
itaendelea kuunga mkono jitihada zinazofanywa na Umoja wa Afrika, Umoja wa
Mataifa pamoja na wadau wengine ili kuhakikisha suluhu ya kudumu inapatikana
nchini Jamhuri ya Afrika ya Kati.
2.3.4 Misri
Mheshimiwa
Spika, mgogoro nchini Misri umeendelea hasa
baada ya Rais Mohamed Morsi kuondolewa madarakani mwezi Julai 2013 ambapo watu
wengi wamepoteza maisha kutokana na mgogoro huo. Kwa mujibu wa sheria za Umoja
wa Afrika, Serikali yoyote inayoingia madarakani kwa nguvu na kinyume na
Katiba, inapoteza uanachama wake AU na kuwekewa vikwazo. Ni matumaini yetu kuwa baada ya uchaguzi
kufanyika mwezi huu wa Mei, 2014 Misri itachukua tena nafasi yake kwenye Umoja
wa Afrika, na kwamba hali ya usalama na kisiasa nchini Misri itakuwa na unafuu.
Kama maoni ya magazeti na wanasiasa ni sahihi, basi Rais mpya wa Misri
anategemewa kuwa Mheshimiwa Mohamed Fatah El Sisi.
2.3.5 Libya
Mheshimiwa
Spika, hali ya usalama nchini Libya bado ni
tete. Baada ya kuuawa kwa kiongozi wa
Libya Kanali Muammar Gaddafi miaka mitatu iliyopita, na baada ya Balozi wa
Marekani nchini Libya kuuawa, miaka miwili iliyopita mapigano ya wenyewe kwa
wenyewe na mauaji ya wageni na raia yanazidi kushika kasi siku hadi siku. Hali imekuwa mbaya hadi kupelekea Waziri Mkuu
kutekwa nyara na baadae kuachiliwa na Bunge kuvamiwa na kuchomwa moto. Mapigano
na mauaji yanayoendelea, yanaifanya nchi ya Libya isitawalike na kusababisha
ofisi nyingi za Ubalozi mjini Tripoli na Benghazi kufungwa. Tunashauri
Watanzania wasiende Libya kwa sasa kutokana na hali iliyopo mpaka pale
watakaposhauriwa vinginevyo.
2.3.6 Burundi
Mheshimiwa
Spika, hivi karibuni kumekuwa na taarifa za hali ya
kisiasa na kiusalama nchini Burundi kuwa kuna mvutano wa Viongozi wa vyama vya
siasa. Hali hii inatokana na hofu kwamba Serikali iliyopo madarakani ya Rais
Pierre Nkurunziza inataka kubadilisha katiba ili kumpatia Rais Nkurunziza
nafasi nyingine ya kugombea Urais kwa mara ya tatu. Wanasiasa, hasa kutoka
kambi ya upinzani na Viongozi wastaafu wanasema kuwa kubadili katiba kutavunja
makubaliano ya Arusha ya Amani na Maelewano kwa Burundi (Arusha Peace and Reconcilliation Agreement for Burundi) na hivyo
kuhatarisha Amani na usalama wa nchi hiyo.
Mheshimiwa
Spika, sisi kama Tanzania tunalo jukumu la
kuhakikisha kuwa ndugu zetu wa Burundi hawatumbukii kwenye matatizo ya kisiasa
na usalama. Tunaamini kwamba, Mheshimiwa Pierre Nkurunziza hana nia wala sababu
ya kubadili katiba ili kumwezesha kuendelea kubaki madarakani. Hivi sasa,
mawasiliano ya kumaliza tatizo hili yanaendelea kati ya Serikali yetu, Umoja wa
Afrika na viongozi mbalimbali wa Burundi. Tunashawishika kuamini kuwa wale wote
wanaoitakia mema Burundi wataisaidia katika kulimaliza tatizo hili hasa nchi za
jirani zinazoizunguka.
2.3.7 Mapambano Dhidi ya Ugaidi
Mheshimiwa
Spika, vitendo vya kigaidi vinavyofanywa na
kikundi cha Boko Haram nchini Nigeria na pia kikundi cha Al-Shabaab nchini
Kenya ni vitendo vya kulaaniwa na kukomeshwa na wapenda amani wote duniani.
Mauaji ya hivi karibuni ya watu wasiopungua 400 na utekaji wa wanafunzi
wasichana zaidi ya 200 nchini Nigeria na vilevile mauaji ya jumla ya watu zaidi
ya 100 kwa jirani zetu Kenya ni ushaidi
tosha wa kuitaka dunia kushirikiana kwa pamoja kupambana na vitendo vya kigaidi
vya aina zote. Serikali yetu tayari imekwisha tuma salamu za pole tukilaani
vitendo hivi na kutumia fursa hiyo kuwahakikishia wenzetu utayari wetu katika
kushirikiana kwenye mapambano dhidi ya ugaidi.
Mheshimiwa
Spika,
Tanzania
ni nchi ya amani na yenye utulivu mkubwa. Pamoja na tofauti zetu, tusikubali
wala kushawishika kuzimaliza tofauti zetu kwa njia za kigaidi. Tuendelee na
tabia ya kukosoana na kumaliza tofauti zetu kwa mazungumzo na njia
zinazokubalika kisheria. Tuwe macho na watu wote wasioitakia mema nchi yetu.
3.
MSIMAMO
WA TANZANIA KATIKA MASUALA MUHIMU SADC NA UKANDA WA NCHI ZA MAZIWA MAKUU
3.1.
Jamhuri
ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC)
Mheshimiwa Spika,
Tanzania imeendelea kuwa mstari wa mbele katika kushiriki kulinda amani, usalama na demokrasia kwenye nchi za
Afrika. Kutokana na msimamo huo, Tanzania imechangia kikosi kimoja cha
askari wa Jeshi la Wananchi
wa Tanzania (JWTZ)
kwenye Force Intervention Brigade
(FIB) iliyoko chini ya kikosi cha Umoja wa Mataifa cha kulinda amani nchini DRC
(MONUSCO).
FIB inaongozwa na kamanda Mtanzania, Brig
Gen. James Alois Mwakibolwa, kwa ajili ya kupambana
na waasi ndani ya DRC. Ninafurahi kutamka kwamba askari wetu kwa kushirikiana
na majeshi ya DRC na MONUSCO walifanya kazi nzuri na kukisambaratisha kabisa
kikundi cha waasi wa M23 ambao wamekuwa wakivuruga amani kwa muda mrefu
mashariki mwa DRC na kupelekea kupatikana kwa amani ambayo ilikuwa imepotea kwa
muda mrefu.
Mheshimiwa Spika,
katika Mkutano wa dharura
wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa
Afrika (SADC) uliofanyika sanjari na Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali
wa Umoja wa Afrika jijini Addis Ababa, Ethiopia, tarehe 30 Januari, 2014,
Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) ilitoa taarifa kuhusu hali ya usalama
inavyoendelea nchini humo baada ya kusainiwa kwa makubaliano ya kusitisha
mapigano kati ya Serikali na kikundi cha M23.
Mheshimiwa Spika,
mwakilishi wa DRC
alieleza kuwa baada ya kutiwa saini makubaliano hayo, hivi sasa Serikali yake
imejielekeza katika kuvisambaratisha vikundi vya kijeshi vilivyosalia nchini
humo ikianza na ADF-Nalu na baadaye FDLR. Mwakilishi huyo pia alieleza kuwa
Bunge la nchi hiyo lilikuwa kwenye mchakato wa kutunga Sheria ya msamaha
(amnesty law) ambayo itafafanua ni waasi gani watanufaika nayo na wale ambao
hawataweza kunufaika na sheria hiyo.
Napenda kulifahamisha Bunge lako Tukufu kuwa, sheria hiyo imekwishapitishwa tangu tarehe 5
Februari 2014. Kwa mujibu wa sheria hiyo, walioshiriki
katika makosa ya kimbari, makosa ya kivita na jinai dhidi ya ubinadamu (genocide, war crimes and crimes against
humanity) hawatanufaika
nayo.
3.2.
Malawi
Mheshimiwa Spika, mazungumzo ya usuluhishi wa mgogoro wa mpaka kati yetu
na Malawi bado yanaendelea. Tarehe 20 na
21 Machi, 2014 tuliitwa Malawi kwenye jopo la usuluhishi lililopo chini ya
uenyekiti wa Rais Mstaafu wa Msumbiji Joachim Chissano. Wengine ni Rais Mstaafu wa Afrika Kusini
Thabo Mbeki na Rais Mstaafu wa Botswana Festus Mogae. Pamoja nao kulikuwa na kikosi cha wanasheria
sita waliobobea kwenye migogoro ya mipaka duniani.
Baada ya mjadala mkubwa
uliotoa fursa kwa kila upande kuwasilisha hoja zake za kisheria mbele ya Jopo,
Jopo lilishauri kuwa hoja za kisheria tuziweke pembeni kwa muda na badala yake
kila upande uainishe hoja zisizo za kisheria.
Tulitakiwa tujadili hoja zinazogusa maisha ya kila siku ya kijamii. Kwa mfano, Malawi wanatakiwa kueleza hasara
watakazozipata endapo itaamriwa kuwa mpaka utapita katikati. Na Tanzania tunatakiwa kueleza hasara
tutakazozipata endapo itaamriwa kuwa mpaka utapita kwenye ufukwe wa Ziwa.
Mheshimiwa Spika, timu ya Tanzania ambayo
inajumuisha Wizara ya Ardhi, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Wizara
yangu sasa inaandaa majibu. Napenda
kuchukua nafasi hii kuwapongeza Waheshimiwa Anna Tibaijuka (Mb.) na Mwanasheria
Mkuu Jaji Fredrick Werema kwa kazi nzuri sana wanayoifanya katika kujenga hoja
nzito na zenye ushawishi wa kuuweka mpaka katikati ya Ziwa na siyo ufukweni. Na
huo ndio msimamo wa Tanzania. Aidha, kwa
kuwa sasa Serikali mpya ya Malawi imechaguliwa na kuundwa, Jopo la usuluhishi
litaitisha kikao cha pili ili kuendelea na shughuli za usuluhishi. Niwashukuru
pia Mheshimiwa John Komba, Mbunge wa Mbinga na Mheshimiwa Deo Filikunjombe,
Mbunge wa Ludewa ambapo waliambatana nasi na kutoa mchango wa hoja nzito kwa
niaba ya wananchi wanaolizunguka Ziwa Nyasa.
3.3.
Zimbabwe
Mheshimiwa Spika, hali
ya kisiasa nchini Zimbabwe kwa sasa ni shwari. Zimbabwe ilifanya Uchaguzi wake
Mkuu wa Rais tarehe 31 Julai, 2013. Kabla
ya uchaguzi huo, Zimbabwe ilifanya mchakato wa kutengeneza Katiba mpya kwa
mafanikio makubwa. Tanzania ilishiriki katika
uangalizi wa shughuli zote mbili
kupitia timu ya uangalizi ya SADC ambayo niliiongoza mimi mwenyewe. Wananchi wa
Zimbabwe walitumia nafasi yao ya kidemokrasia katika kuchagua viongozi wao na
vyama walivyopenda kwa uhuru na haki. Katika uchaguzi huo, Mheshimiwa Robert G.
Mugabe aliibuka mshindi wa Urais kwa kipindi cha miaka mitano kwa kupata
asilimia 61.09 ya kura zote. Aidha, timu ya uangalizi ya SADC iliridhika na
maandalizi yaliyofanywa na Tume ya Uchaguzi katika mchakato mzima wa uchaguzi
nchini Zimbabwe kwa mwaka 2013 na kwamba ulikuwa huru na wa amani.
3.4.
Madagascar
Mheshimiwa Spika, baada ya jitihada za SADC za kuandaa mazingira ya
uchaguzi kufanyika Madagascar, na baada ya kufanikisha zoezi la kuwaomba
viongozi wa zamani; Ravanomanana, Rajoelina, Rasiraka na Mama Ravaromanana kutogombea
kwa sababu za kiusalama, wananchi wa Madagascar hatimaye walipiga kura tarehe
25 Oktoba, 2013 na kurudia Desemba 2013 ambapo Henry Martial Rakotoarimanana
Rajaonarimampianina alichaguliwa kuwa Rais mpya wa Madagascar. Hali ya kisiasa nchini Madagascar kwa ujumla
ni shwari ingawa kuna kutoelewana kati ya Rais aliyeondoka Rajoelina na Rais wa
sasa baada ya Rais mpya kukataa pendekezo la Rais Rajoelina la kutaka ateuliwe
kuwa Waziri Mkuu.
Mheshimiwa Spika, kufuatia ushindi huo, Wakuu
wa Nchi wanachama wa SADC walikubaliana kwa kauli moja kuiondolea vikwazo nchi ya
Madagascar na hivyo kuikaribisha rasmi kushiriki katika shughuli za SADC,
ikiwemo kuhudhuria vikao vyote kama mwanachama halali. Kufuatia hatua hiyo Rais Rajaonarimampianina pia alikaribishwa rasmi
kujumuika na kukalia kiti cha Madagascar katika mikutano
ya Umoja wa Afrika (AU). Tuendelee
kuwaombea amani ya kudumu wananchi wa Madagascar ili waweze kuijenga nchi yao.
4.
UTEKELEZAJI
WA DIPLOMASIA YA UCHUMI
Mheshimiwa
Spika,
Wizara kwa kushirikiana
na Wizara, Idara na Taasisi nyingine imeendelea kutekeleza Diplomasia ya Uchumi
kwa kuvutia wawekezaji wenye vigezo na sifa kuja kuwekeza katika sekta
mbalimbali hapa nchini. Mikakati inayotumika ni pamoja na kujenga mazingira wezeshi ya ndani ya
Kukuza Uchumi; Kuimarisha Ubia wa Kimataifa; Kuweka mbele Malengo ya Uchumi katika Ushirikiano Kati ya Nchi Mbili (Bilateral Cooperation); Kuimarisha Uhusiano wa Kimataifa (Multilateral Cooperation); kukuza ujirani mwema; na kukuza
Ushirikiano wa Kikanda. Masuala haya yanatekelezwa kupitia ushiriki
wetu kwenye Mikutano mbalimbali (Tume za Pamoja za Ushirikiano na mikutano mingine ya nchi na nchi na ile ya
Kikanda na Kimataifa); Ziara za Viongozi wa Kitaifa Nje ya Nchi; ziara za
Viongozi wa Mataifa ya Nje hapa nchini; na ofisi za uwakilishi nje ya nchi.
Mheshimiwa
Spika, kwa ufupi kabisa napenda kuelezea baadhi ya mafanikio tuliyoyapata
kwenye sekta mbalimbali ambayo yamechangiwa kwa kiasi kikubwa na utekelezaji wa
diplomasia ya uchumi:-
4.1.
Sekta
ya Kilimo
Mheshimiwa
Spika, mwaka jana nililiarifu
Bunge lako tukufu kuhusu mafanikio
tuliyoyapata katika kutafuta masoko ya bidhaa zetu za
kilimo kwenye soko kubwa la China. Mafanikio hayo ni pamoja na kuingia
Mikataba, Makubaliano na Itifaki mbalimbali na Mamlaka pekee ya China
inayoruhusu biashara za namna hiyo (Administration of Quality Supervision,
Inspection and Quarantine – AQSIQ) ambayo imeruhusu Tanzania kuingiza zao
la tumbaku nchini China. Nafurahi kuliarifu Bunge lako Tukufu kwamba, hivi sasa
Mamlaka hiyo imeruhusu pia mazao ya baharini kuingia nchini China. Makubaliano
hayo yaliwekwa saini mbele ya Mawaziri Wakuu Mhe. Li Keqiang na Mhe. Mizengo
Pinda wakati wa ziara ya Mhe. Waziri Mkuu nchini China mwezi Oktoba 2013. Hii ni fursa adhimu kwa wavuvi wetu kupata
soko la uhakika la bidhaa zao.
Mheshimiwa
Spika, mchakato wa kuliwezesha zao la pamba
kupata soko nchini China umefikia hatua nzuri, ambapo Mkoa wa Shinyanga na
kampuni ya Dahong ya Jimbo la Jiangsu zimeingia Mkataba wa kuendeleza zao la
pamba mkoani humo na kuuza katika viwanda vya Dahong, China. Mkataba huo
unajulikana kwa jina la “Agreement On China-Tanzania Modern
Agro-Industrial Zone” na ni mmoja kati ya mikataba mitano (5) iliyowekwa
saini Oktoba 17, 2013 mbele ya Mawaziri Wakuu Mizengo Pinda na Li Keqiang mjini
Beijing.
Mheshimiwa
Spika, hivi sasa Wizara kupitia Ubalozi wa
Tanzania Beijing, inafuatilia kwa karibu uingiaji wa Makubaliano na Serikali ya
China yatakayoiwezesha Tanzania kuingiza China zao la muhogo kwa ajili ya
matumizi ya viwandani ambako wanga wake unahitajika sana. Mchakato huo upo katika hatua nzuri baada ya AQSIQ kutoa taarifa kwamba imeridhika na
hoja za mapendekezo yetu na hivyo, Wizara inaendelea kufuatilia ujio wa timu ya
wataalam wa AQSIQ nchini kujiridhisha kuhusu utoshelevu na ubora wa viwango vya
zao hilo ili kukidhi mahitaji ya soko la China.
Mheshimiwa
Spika, Wizara imeziomba mamlaka za kilimo
nchini kuanzisha michakato kama hiyo kwa mazao ya korosho, kahawa, ufuta,
karanga, ngozi n.k, ili yaweze kuingia katika soko la China. Uzoefu unaonesha kwamba bila kuwa na mikataba
au makubaliano ya namna hiyo mazao yetu yatakumbana na vikwazo kuingia katika
soko hilo.
Mheshimiwa
Spika, katika Mkutano wa Tatu wa Ushirikiano
kati ya Nchi za Afrika na nchi za Kiarabu uliofanyika nchini Kuwait mwezi
Novemba 2013, Serikali ya Kuwait iliahidi kutoa kiasi cha Dola za Marekani bilioni
moja kila mwaka kwa kipindi cha miaka mitano
kwa ajili ya mikopo nafuu kwa nchi za Afrika, hususan katika sekta ya
kilimo. Wizara yangu kwa kushirikiana na
Wizara ya Fedha na Tume za Mipango za Tanzania Bara na Zanzibar imekwishawasilisha
miradi kadhaa ya umwagiliaji na maendeleo ya jamii.
Mheshimiwa Spika, katika Mkutano huo,
Serikali ya Saudi Arabia ilitenga kiasi cha dola za kimarekani bilioni nne kwa
lengo la kukuza uzalishaji na usalama wa chakula. Ili kuchangamkia fursa hiyo,
Wizara yangu imekamilisha majadiliano ya kuingia Mkataba wa Ushirikiano na
Saudi Arabia utakaowezesha nchi yetu kunufaika na fursa hiyo. Ninatarajia kusaini Mkataba huo wakati wowote
kabla ya mwisho wa Mwaka huu wa fedha.
Mheshimiwa
Spika, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa
Jakaya Mrisho Kikwete, ametoa mchango mkubwa kwenye sekta ya kilimo. Msisitizo
umekuwa katika masuala yanayohusu usalama wa chakula na majaribio ya kuongeza
matumizi ya teknolojia katika kilimo kwa lengo la kuwaongezea kipato wananchi
na kukuza uchumi wa nchi. Kwa kutambua mchango wa Mheshimiwa Rais, mwezi Septemba
2013, Chuo Kikuu cha Guelph cha nchini Canada, kilimtunukia Shahada ya Heshima
ya Uzamivu (Honorary Doctorate) ya
Sheria. Mheshimiwa Rais amekuwa
Mtanzania wa kwanza kutunukiwa shahada hiyo katika historia ya zaidi ya miaka
100 ya Chuo hicho maarufu kwa utafiti wa kilimo na magonjwa ya wanyama. Mchango huo wa Mheshimiwa Rais ambao
umetambuliwa na Chuo cha Guelph unatoa fursa kwa taasisi na vyuo vyetu
vinavyojihusisha na kilimo kuwa na ushirikiano wa karibu na chuo hicho katika
kufanya tafiti mbalimbali na kuendeleza sekta ya kilimo.
Mheshimiwa
Spika, kwa
kutambua ukweli kwamba asilimia kubwa ya watanzania wanategemea kilimo na
wanakabiliwa na changamoto ya umasikini wa kipato, serikali imefanya jitihada kuhakikisha
kuwa nchi yetu inakuwa ni moja ya nchi za majaribio ya mpango wa kuwawezesha
wananchi wengi zaidi kupata huduma za kifedha (Inclusive Financing for Development) hususan wasioweza kumudu
masharti ya kibenki.
Katika
kufanikisha juhudi hizo, Wizara yangu iliratibu kwa mafanikio makubwa ziara ya
Malkia Maxima wa Uholanzi aliyetembelea Tanzania kuanzia tarehe 11 hadi 13
Desemba 2013 akiwa Mwakilishi Maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa katika
masuala ya Inclusive Financing for
Development. Malkia Maxima
alifuatana na wakuu wa Mashirika Matatu ya Umoja wa Mataifa yanayoshughulikia
kilimo na chakula ambayo ni FAO, IFAD na WFP kuja kujionea maendeleo ya miradi
iliyo chini ya mpango huo hapa nchini. Mpango huu umekuwa msaada mkubwa kwa
wakulima wadogo katika kupunguza umasikini na kuongeza usalama wa chakula.
4.2.
Sekta
ya Nishati
Mheshimiwa
Spika, katika mwaka wa fedha uliopita Wizara
yangu ikitambua umuhimu wa nishati katika maendeleo ya Taifa letu, ilifanya
juhudi katika kutafuta uwekezaji katika sekta hiyo. Mwaka huu tumeendelea
kupata fursa mbalimbali ikiwa ni pamoja na mpango mpya wa ushirikiano na Serikali ya Marekani
kwenye uzalishaji umeme barani Afrika uitwao “Power Africa Initiative” uliozinduliwa hapa nchini tarehe 2 Julai
2013 na Rais Barack Obama wa Marekani pamoja na Rais Jakaya Mrisho Kikwete wa
Tanzania. Tanzania ni miongoni mwa nchi sita
barani Afrika zinazonufaika na Mpango huo. Nchi nyingine ni
Kenya, Ethiopia, Msumbiji, Ghana na Nigeria. Katika mpango huo, Serikali ya
Marekani imetenga kiasi cha Dola za Marekani bilioni saba wakati sekta binafsi
nchini humo imeahidi kuwekeza kiasi cha Dola za Marekani bilioni tisa za
kufanikisha utekelezaji wake.
Mheshimiwa
Spika, kwa kutambua umuhimu wa kuiandaa vyema
nchi yetu kunufaika na nishati ya gesi iliyogundulika kwa wingi hivi karibuni,
Wizara yangu kwa kushirikiana na Wizara ya Nishati na Madini imeanza kutafuta
fursa za kujifunza uzoefu wa wenzetu waliobahatika kuwa na nishati hiyo na
kupata mafanikio makubwa ili nasi tuweze kuingia katika uchumi wa gesi na
mafuta bila matatizo.
Mheshimiwa
Spika, Wizara yangu kupitia Balozi zake
imeratibu ziara za mafunzo nchini India, Japan, Malaysia, Canada, Algeria,
Oman, Australia na Qatar. Aidha,
tumeendelea kutafuta fursa mbalimbali za masomo kwa ajili ya wataalam katika
sekta ya mafuta na gesi. Napenda kuliarifu
Bunge lako Tukufu kuwa matunda ya juhudi hizo yameshaanza kupatikana. Tayari nchi
za Thailand, Australia, China na Canada zimetoa nafasi za masomo kwa wataalam
wetu. Tunaendelea kutafuta fursa zaidi katika nchi zingine.
Mheshimiwa
Spika, juhudi zetu za kutafuta fursa za
uwekezaji katika sekta ya Nishati zimewezesha nchi yetu kuingia makubaliano ya
ushirikiano wa kiuchumi na nchi ya Algeria ambapo miradi mbalimbali katika
masuala ya gesi na umeme itatekelezwa. Kwa kuanzia tumekubaliana kuanzisha kwa
pamoja migodi ya Phosphate kwa ajili ya uzalishaji wa mbolea kwa matumizi ya
ndani na kuuza nje. Pia tumekubaliana
kuanzisha Kampuni ya pamoja ya kusambaza umeme na kujenga kiwanda cha kusindika
gesi asilia kwa ajili ya matumizi ya nyumbani.
Kutekelezwa kwa miradi hiyo sio tu kutatoa ajira kwa wananchi wengi
katika sekta ya huduma, lakini pia kutalipatia taifa fedha za kigeni kwa ajili
ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo na kupunguza uharibifu wa mazingira.
Mheshimiwa
Spika, wakati wa ziara ya Mheshimiwa Rais wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, aliyoifanya nchini
Singapore mwezi Juni 2013, alikutana na viongozi wa Makampuni Makubwa ya
Biashara. Kufuatia mkutano huo, Kampuni ya Pavillion Energy ya nchini Singapore
imekubali kuwekeza katika sekta ya gesi nchini ambapo kwa kuanzia imenunua
asilimia 20 ya hisa za Kampuni ya Ophir Gas kwa kiasi cha Dola za Marekani
bilioni 1.3.
4.3.
Sekta
ya Biashara
Mheshimiwa
Spika, kwa upande wa sekta ya biashara, Wizara
yangu imeendelea kutafuta fursa mbalimbali za biashara kwa watanzania nje ya
nchi na pia masoko kwa bidhaa zetu nje ya nchi.
Balozi zetu zote duniani zimeendelea kuwezesha upatikanaji wa taarifa
juu ya maonesho ya biashara, masoko ya bidhaa na fursa za uwekezaji. Mwaka huu Kampuni ya Dragon Mart ya Dubai
imeonesha nia ya kuwekeza nchini kwa kushirikiana na TANTRADE. Lengo la ushirikiano huo ni kujenga eneo la
kisasa la maonesho ya kimataifa ya biashara nchini ambalo litakuwa linafanya
maonesho ya biashara kwa kipindi cha mwaka mzima. Kwa wale waliobahatika kufika katika jiji la
Dubai na kutembelea Dragon City, hivyo ndivyo itakavyokuwa hapa, pale mpango
huo wa kuanzisha eneo hilo hapa Tanzania utakapofanikiwa.
Mheshimiwa Spika, vilevile napenda
kulifahamisha Bunge lako Tukufu kuwa, Shirika la Emirates, limekubali kuanzisha
safari za ndege za Shirika lake lingine la FlyDubai kutoka Dubai kwenda
Kilimanjaro, Dar es Salaam na Zanzibar. FlyDubai ni shirika lenye bei nafuu kwa
wateja (budget airline), kwani mara
nyingi nauli zake zinakuwa nusu ya nauli ya ndege nyingine ikiwamo
Emirates. Huduma hii italeta unafuu mkubwa hasa kwa wafanyabiashara wetu
wanaofanya shughuli zao kati ya Tanzania na Dubai au maeneo mengine kupitia
Dubai.
4.4.
Sekta
ya Utalii
Mheshimiwa
Spika,
katika
jitihada za kukuza utalii Serikali kupitia Ubalozi wetu wa Washington Marekani
imefungua Ofisi tisa za Uwakilishi wa Heshima (Honorary Consulates) sehemu
mbalimbali nchini Marekani. Hatua hiyo inatarajiwa kuongeza idadi ya watalii
kutoka Taifa hilo.
Mheshimiwa
Spika, ni dhahiri kwamba soko kubwa la utalii
duniani lipo China. Wizara yangu kupitia
Ubalozi wake nchini China imeanza mazungumzo na mamlaka za Utalii za China
kuhusu utangazaji wa vivutio vya utalii vya Tanzania. Aidha, wakati wa Ziara ya Waziri Mkuu nchini
China mwezi Oktoba 2013, kampuni kubwa ya Usafirishaji wa Watalii ya Hong Kong
Travels iliahidi kusafirisha watalii wapatao 10,000 kila mwaka kutembelea
Tanzania. Kampuni hiyo imekubali ombi la Mheshimiwa Waziri Mkuu kuja kuwekeza
katika ujenzi wa hoteli zenye hadhi ya Nyota Tano katika maeneo ya karibu na
Mbuga za Wanyama kwa ajili ya kulaza watalii.
Mheshimiwa
Spika, katika kipindi cha mwaka wa Fedha
2013/2014, Wizara katika juhudi zake za kukuza utalii iliratibu kwa ushirikiano
na TANAPA kongamano la vijana wa Tanzania na Saudi Arabia kuhusu Bio-Anuai
lililofanyika mkoani Arusha mwezi Januari, 2014. Kongamano hilo lilisaidia sana
kukuza diplomasia ya uchumi hasa kwenye kuwavutia watalii kutoka Saudi Arabia
na wananchi wengine wa Nchi za Ghuba kuijua Tanzania. Tayari misafara zaidi ya mitatu
inayowahusisha wanafamilia za kifalme wa Nchi za Gulf Cooperation Council imefanya ziara nchini Tanzania ikifuata
mfano wa vijana hao wa Saudi Arabia.
Mheshimiwa
Spika, vilevile Mheshimiwa
Waziri Mkuu akiwa katika ziara nchini China alifanya mazungumzo na Watendaji
Wakuu wa Mashirika ya Ndege ya Hainan na South China Airlines ili kuwavutia
waanzishe safari za moja kwa moja kutoka China kuja nchini ili kurahisisha
usafiri wa watalii wanaotaka kuja nchini. Makampuni hayo yamekubali kutuma
wataalam wake kuja nchini kufanya upembuzi yakinifu.
Mheshimiwa
Spika, halikadhalika,
mnamo tarehe 25 Machi, 2014, Wizara iliratibu ziara ya kikazi ya Mhe.
Frank-Walter-Steinmeier,
Waziri wa Mambo ya Nje wa Ujerumani aliyewasili nchini na ujumbe wa watu 80
wakiwemo wafanyabiashara kutoka makampuni makubwa ya Ujerumani, Wabunge, watendaji
wa Serikali na Waandishi wa Habari. Lengo la ziara
yake
lilikuwa kuimarisha ushirikiano wa kihistoria uliopo kati ya Tanzania na
Ujerumani hususan katika nyanja za utalii,
biashara na uwekezaji. Kama sehemu
ya mafanikio ya ziara hiyo, Mhe Steinmeier alimkabidhi Waziri wa Maliasili
na Utalii, ndege ndogo
kwa ajili ya kukabiliana na uwindaji haramu wa wanyamapori.
4.5.
Sekta
ya Miundombinu na Uchukuzi
Mheshimiwa Spika, Ubalozi wetu Abu
Dhabi kupitia Ubalozi Mdogo wa Dubai kwa kushirikiana na Shirika la Taifa la
Nyumba (NHC) ulifanya vikao kadhaa na wamiliki wa mashirika makubwa ya ujenzi
wa majengo ya biashara na ya makazi ambapo walifanikiwa kuwapata wawekezaji
wakubwa kwenye sekta hiyo. Mashirika yaliyokubali kuja kuwekeza Tanzania ni:-
DAMAC, AL GHURAIR, SOBHA na NAKHIL. Mashirika hayo ndiyo yaliyojenga majengo
makubwa na mashuhuri yanayoonekana katika Jiji la Dubai. Kampuni ya DAMAC ipo
tayari kuwekeza kwenye eneo la ufukwe wa bahari, Kawe Dar es Salaam
lisilopungua ukubwa wa ekari 1000, kwa kujenga Hoteli za Nyota 5, nyumba za
kuishi (Villas) na uwanja wa kisasa wa Golf (golf course). Aidha, kwa kutambua
fursa hiyo Ubalozi umeandaa mkutano wa wawekezaji wa Dubai na Tanzania tarehe
11 Juni, 2014, katika Hoteli ya Jumeirah Emirates Tower, Jijini Dubai. Shirika la
NHC, ndio wanaoratibu ushiriki wa wawekezaji kutoka Tanzania. Tunawapongeza na
kuwaahidi ushirikiano wetu.
4.6.
Sekta
ya Ajira
Mheshimiwa Spika, baada ya mji wa
Dubai kushinda kinyang’anyiro cha kuwa mwenyeji wa Maonesho ya Biashara ya
Dunia ya 2020 (World Expo 2020), ni wazi fursa nyingi zitapatikana kupitia
maonesho hayo, hasa tukitilia maanani uhusiano mzuri wa kidiplomasia uliopo
kati yetu na Umoja wa Nchi za Falme za Kiarabu (U.A.E). Kati ya fursa
hizo, ni pamoja na nafasi za ajira milioni mbili na laki nane ambazo
serikali ya UAE itahitaji kuzijaza kwa ajili hiyo. Kwa kutambua fursa hiyo,
Wizara kwa kushirikiana na Ubalozi wetu wa U.A.E tumejipanga kikamilifu
ili kuchangamkia fursa hizo.
Mheshimiwa Spika, tayari Ubalozi
umekutana na Shirika la Emirates (Emirates
Group) ambalo ndio mmiliki wa Shirika la ndege la Emirates, Dnata, na
FlyDubai, na kuweka mikakati ya kuongeza ajira kwa watanzania katika mashirika
yote yaliyo chini ya Emirates. Shirika la Emirates limekubali kuajiri
wafanyakazi kutoka Tanzania katika kada za wahudumu wa ndege (cabin crews), mafundi (technicians), maafisa mipango (planning assistants), watoa huduma kwa
wateja na masuala ya tiketi (customer
care and ticketing). Napenda kuwasihi watanzania wote wenye sifa
zitakazotakiwa, waombe nafasi hizi kwa wingi mara zitakapotangazwa rasmi.
4.7.
Tume
za Pamoja za Kudumu za Ushirikiano (JPC)
Mheshimiwa
Spika, katika
kuratibu shughuli za Tume za Pamoja za Kudumu za Ushirikiano (JPC), Wizara
imeendelea kufanya vikao vya wadau wa ndani na nje ya nchi ili kutekeleza
shughuli hizo. Katika mwaka wa fedha
2013/2014, Wizara kwa kushirikiana na wadau kutoka Wizara nyingine, Taasisi za
Umma na Sekta Binafsi iliandaa awamu ya nane ya Mkutano wa
Tume ya Pamoja ya Ushirikiano kati ya Tanzania na India uliofanyika katika
Hoteli ya Kilimanjaro, Hyatt tarehe 8 hadi 9 Julai, 2013. Maazimio ya Mkutano
huo yalitiwa saini na mimi mwenyewe na Mhe. Prabeet Kaur, Waziri wa Nchi wa
Mambo ya Nje wa India. Maazimio ya Mkutano huo yanalenga katika kuweka maeneo
ya ushirikiano wa Tanzania na India kwa kipindi cha miaka mitatu. Aidha, Wizara imeendelea kuratibu
shughuli na utekelezaji wa makubaliano ya JPCs mbalimbali ambazo nchi yetu
imefikia makubaliano, hususan Algeria, Botswana, Kenya, Msumbiji, Rwanda na
Zambia.
Mheshimiwa
Spika, Wizara
imefanikiwa kutekeleza sehemu ya majukumu
yaliyotajwa hapo juu kwa ushirikiano na washirika wa maendeleo kutoka nchi na
asasi mbalimbali za kitaifa, kikanda, kimataifa pamoja na sekta binafsi. Naomba
nitumie fursa hii kuwashukuru washirika wetu wote wa maendeleo ikiwa ni pamoja
na Australia, Brazil, Canada, China, Cuba, Finland, India, Italia, Ireland, Japan,
Korea Kusini, Kuwait, Malaysia, Marekani, Norway, Oman, Sweden, Ubelgiji,
Ufaransa, Uhispania, Uholanzi, Uingereza, Ujerumani, Umoja wa Falme za Kiarabu,
Ureno, Urusi, Uswisi, Uturuki, Umoja wa Ulaya, FAO, IAEA, ILO, IMF, IOM, UNDP,
UNEP, UN-HABITAT, UNWTO, UNHCR, UNICEF, UNFPA,
UNESCO, UNIDO, WHO World Bank na WWF kwa mchango wao mkubwa katika
kufanikisha utekelezaji wa Diplomasia ya uchumi.
4.8.
Ziara
za Viongozi wa Kitaifa Nje ya Nchi
Mheshimiwa
Spika, Wizara
ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa ndiyo msimamizi mkuu wa masuala ya
Itifaki ya nchi. Katika kutekeleza jukumu hilo Wizara imeendelea kutoa huduma
ya Itifaki kwenye sherehe zote na maadhimisho ya Kitaifa; kuratibu safari za
Viongozi wa Kitaifa walipokwenda nje ya nchi; na kuratibu mapokezi ya Viongozi wa Nje waliotembelea
Tanzania. Wizara imeandaa
na kuratibu ziara za kikazi za Viongozi
wa Kitaifa katika nchi za:- Nigeria, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, Afrika
Kusini, Malawi, Namibia, Kenya, Uganda, Oman, Marekani,
Canada, Ethiopia, Uingereza,
Sri Lanka, Poland, Kuwait, Ufaransa, Falme za Kiarabu, India, Uholanzi na
China.
Mheshimiwa
Spika, ziara hizo
zimefungua milango mipya ya ushirikiano kati ya nchi yetu na nchi hizo, kati ya
wananchi wa nchi zetu na kati ya sekta binafsi kutoka pande zote. Aidha, ziara
hizo pia zimechochea na kukuza biashara na kuimarisha mahusiano. Nitapata muda
baadae mchana wa kutoa ufafanuzi zaidi kuhusu jambo hili ambalo kila mara
limekuwa linazua maswali.
4.9.
Ziara
za Viongozi wa Nchi na Mashirika ya Kikanda na Kimataifa Nchini
Mheshimiwa
Spika, kwa upande wa Viongozi wa Kimataifa kutoka nje ya
nchi, Wizara iliandaa na kuratibu ziara za kikazi za Wakuu wa Nchi na Serikali
kutoka nchi za; Marekani, Thailand, Burundi, Finland, Sweden, Uholanzi, Benin
na Comoro.
Mheshimiwa
Spika, pia
Wizara imehusika kikamilifu katika kuandaa na kuratibu ushiriki wa Viongozi
Wakuu wa Nchi na Serikali na Mashirika ya Kikanda na Kimataifa kutoka nchi
mbalimbali katika sherehe za maadhimisho ya miaka 52 ya Uhuru wa Tanganyika,
tarehe 09 Desemba, 2013, sherehe za maadhimisho miaka 50 ya Mapinduzi Matukufu
ya Zanzibar tarehe 12 Januari 2014 na maadhimisho ya Miaka 50 ya Muungano wa
Tanganyika na Zanzibar sherehe ambazo zilizofanyika tarehe 26 Aprili, 2014.
5.
KUSIMAMIA MIKATABA NA MAKUBALIANO YA KIMATAIFA
5.1
Mikataba ya Kimataifa
Mheshimiwa
Spika, katika
kutekeleza jukumu la kusimamia Mikataba na Makubaliano baina ya Tanzania, nchi
nyingine na Taasisi mbalimbali za Kimataifa, Wizara iliratibu na kusimamia uwekwaji saini wa
Mikataba kati ya Tanzania na Nchi Nyingine (Bilateral
Agreements) kama ifuatavyo:-
i.
Mkataba
kati ya Serikali ya Tanzania na Thailand
kuhusu kuanzisha mahusiano ya kibiashara na kiuchumi, 30 Julai 2013;
ii.
Mkataba
kati ya Serikali ya Tanzania na Thailand kuhusu Ushirikiano katika Utunzaji wa
Wanyamapori, 31 Julai, 2013;
iii.
Mkataba
kati ya Tanzania na Thailand kuhusu kubadilishana wafungwa, 30 Julai, 2013;
iv.
Mkataba
kati ya Tanzania na Thailand kuhusu kulinda Uwekezaji, 30 Julai 2013;
v.
Makubaliano
(MoU) ya kuongeza muda wa matumizi ya Hati ya Makubaliano kati ya Wizara ya
Nishati na Madini na Chuo cha Gem and Jewelery cha Thailand, 30 Julai 2013;
vi.
Hati
ya Makubaliano (MoU) kati ya Wizara ya Kilimo, Chakula na Ushirika ya Tanzania
na Taasisi ya Clinton Foundation kuhusu ushirikiano katika masuala ya Kilimo,
Agosti 2013;
vii.
Mkataba wa Kimataifa kati ya Serikali ya Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania na Serikali ya Nchi ya Kuwait kwa ajili ya Kukuza na
Kulinda Uwekezaji, 17 Novemba, 2013;
viii.
Mkataba kati ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na
Serikali ya Nchi ya Kuwait wa kushirikiana katika Sekta ya Utalii, 17 Novemba,
2013;
ix.
Mkataba wa Wenyeji wa Mahakama ya Kimataifa iliyorithi
shughuli za iliyokuwa Mahakama ya Kimataifa ya Mauaji ya Kimbari ya Rwanda kati
ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Umoja wa Mataifa, 26 Novemba,
2013;
x.
Hati za Makubaliano (Memoranda
of understanding) baina
ya Tanzania na Brazil,
Iceland, Yemen, Seychelles, Swaziland, Zimbabwe, Qatar na Saudi Arabia katika Sekta ya Usafiri wa Anga, Desemba 2013;
xi.
Mkataba wa Nyongeza kwenye Mkataba wa
Uenyeji baina ya Tanzania na Umoja wa Mataifa kuhusu ujenzi wa Makao Makuu ya
Mahakama ya Kimataifa (MICT), iliyorithi
shughuli za iliyokuwa Mahakama ya Mauaji ya Kimbari ya Rwanda (ICTR), Februari,
2014;
xii.
Mkataba kati ya Tanzania na Umoja wa
Ulaya kuhusu Mapambano dhidi ya Uharamia, Aprili 2014; na
xiii.
Mkataba kati ya Tanzania na Kosovo
kuhusu kuanzisha Mahusiano ya Kidiplomasia, Aprili 2014.
Mheshimiwa Spika, mikataba hii itasimamiwa na kutekelezwa na kila sekta
husika. Wizara yangu itaendelea na jukumu la kuratibu uwekaji saini na
kufuatilia utekelezaji wa mikataba na makubaliano mbalimbali baina ya nchi yetu
na nchi nyingine pamoja na mashirika ya kimataifa.
6.
USHIRIKI
WA TANZANIA KATIKA JUMUIYA ZA KIMATAIFA, BARA LA AFRIKA NA KIKANDA
6.1.
USHIRIKIANO
WA KIMATAIFA
Mheshimiwa
Spika, napenda kuliarifu Bunge lako Tukufu, japo
kwa ufupi, mafanikio yaliyopatikana kutokana na ushiriki wetu kwenye mikutano
ya kimataifa na katika jumuiya mbalimbali ambazo nchi yetu ni mwanachama.
6.1.1.
Baraza
Kuu la Umoja wa Mataifa (UNGA);
Mheshimiwa
Spika, Wizara iliratibu ushiriki wa nchi yetu kwenye
Mkutano wa 68 wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa (UNGA), uliofanyika New York,
Marekani kuanzia mwezi Septemba hadi Desemba 2013. Katika Mkutano huo masuala
mbalimbali yalijadiliwa ikiwa ni pamoja na suala la ajenda ya maendeleo baada
ya mwaka 2015 ambapo Malengo ya Maendeleo ya Milenia tunayoyatekeleza sasa
yatafikia ukomo. Katika kujadili ajenda hiyo, mjadala uligusa pia suala la
Malengo ya Maendeleo Endelevu (SDGs) ambayo kimkakati ndiyo yanaandaliwa
kuchukua nafasi ya Malengo ya Milenia ifikapo 2015.
Mheshimiwa
Spika, katika mkutano huo, Tanzania ilipata
fursa ya kuelezea ulimwengu jitihada zake kwenye maeneo mbalimbali ya kukuza
uchumi, kuendeleza kilimo, lishe na usalama wa chakula; utatuzi wa migogoro; na
ushiriki wa nchi kwenye ulinzi wa amani kupitia Umoja wa Mataifa. Vilevile,
Tanzania iliendeleza jitihada zake za kusimamia ukombozi duniani kuzitaka nchi
zote zinazotawaliwa ikiwemo Palestina na Saharawi kupatiwa uhuru wake.
Mheshimiwa
Spika, zaidi ya hayo, Mheshimiwa Rais alishiriki
kwenye Mikutano ya pembeni ya nchi na nchi na mingine ukiwemo Mkutano wa
Kupambana na Ujangili kwenye mbuga za wanyama unaotishia kutoweka kwa baadhi ya
wanyama kama vile tembo na faru. Mheshimiwa Rais alitumia mkutano huo kuelezea
ulimwengu jitihada zinazotumiwa na Serikali kupambana na ujangili, pia alitumia
fursa hiyo kuitaka Jumuiya ya Kimataifa kuweka nguvu za pamoja katika kupambana
na ujangili. Matokeo ya mkutano huo ni
kuanza kupatikana kwa misaada ya vifaa kwa ajili ya kupambana na ujangili
kutoka Marekani, Ujerumani na Uingereza.
6.1.2
Kikundi
Kazi cha kuandaa Malengo ya Maendeleo Endelevu (SDGs)
Mheshimiwa
Spika, Tanzania ni mjumbe wa kikundi kazi cha
nchi 30 kilichoanzishwa na Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa kwa ajili ya kufanya
majadiliano ya kuanzishwa kwa malengo ya maendeleo endelevu (SDGs) yanayotarajiwa
kurithi malengo ya maendeleo ya milenia baada ya muda wake kumalizika mwaka
2015. Kuanzia Machi 2013 hadi sasa imeshafanyika mikutano 11 ya majadiliano
hayo na Wizara imekuwa ikishiriki kikamilifu ili kuona kwamba taifa haliachwi
nje ya mchakato na maslahi ya nchi yanapata nafasi katika malengo ya maendeleo
endelevu.
Mheshimiwa
Spika, ili kuhakikisha wadau wote
wanashirikishwa kikamilifu kwenye mchakato huo zikiwemo taasisi za serikali na
zisizo za serikali, Wizara kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais, Tume ya Mipango
tayari imeshafanya makongamano manne; mawili Zanzibar na mawili Tanzania Bara.
Makongamano haya yameshirikisha Makatibu Wakuu na Naibu Makatibu Wakuu Zanzibar
na Tanzania Bara; Wakurugenzi wa Sera na Mipango, Zanzibar na Tanzania Bara; na
taasisi mbalimbali zisizo za serikali kwa pande zote mbili. Lengo la
makongamano hayo ni kuelezea kwa kina maendeleo ya mchakato huo na kupokea
maoni na ushauri wa taasisi hizo kuhusu majadiliano hayo
6.1.3
Mkutano
wa Mabadiliko ya Tabianchi (COP 19)
Mheshimiwa
Spika, Mkutano wa Mabadiliko ya Tabianchi (COP
19) ulifanyika Warsaw, Poland tarehe 11 - 22 Novemba 2013. Pamoja na ujumbe wa
Tanzania kushiriki kama nchi, Mheshimwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, Rais wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania aliwawakilisha Wakuu wa Nchi za Bara la Afrika
kwa nafasi yake ya Mwenyekiti wa Kamati
ya Wakuu wa Nchi na Serikali wa Afrika kuhusu Mabadiliko ya Tabianchi (CAHOSCC). Akiwa Warsaw, Mheshimiwa Rais alifanya
kikao na Mawaziri wa Mazingira na “negotiators” wa Afrika na kuweka msimamo wa
pamoja wa namna ya kuhakikisha maslahi ya Afrika yanalindwa kwenye mkutano huo
na mingine ya mabadiliko ya Tabianchi. Mheshimiwa Rais alisisitiza umuhimu wa
kutoa kipaumbele kwenye masuala ya upatikanaji wa fedha, teknolojia na kuijengea
Afrika uwezo wa kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.
Mheshimiwa
Spika, kwenye suala la upatikanaji wa fedha,
nchi tajiri na zenye viwanda duniani ziliahidi kuchangia kiasi cha Dola za
Marekani bilioni 100 kila mwaka hadi mwaka 2020. Kiasi hiki cha fedha
kitasaidia nchi maskini kwenye masuala ya adaptation
na mitigation.
6.1.4
Mkutano
wa Kimataifa kuhusu Biashara Haramu ya Wanyamapori
Mheshimiwa
Spika, Wizara iliratibu ushiriki wa nchi kwenye
Mkutano wa Kimataifa kuhusu Biashara Haramu ya Wanyamapori (London Conference on
illegal Wildlife Trade) uliofanyika London, Uingereza, tarehe 12 na 13 Februari
2014. Mkutano huu uliikutanisha Jumuiya ya Kimataifa kwa lengo la kujadili na
kutafuta mbinu za kupambana na hatimaye kutokomeza kabisa biashara haramu ya
pembe za Ndovu na Faru. Tanzania ni miongoni mwa nchi ambazo zimeathirika sana
na biashara hii na Serikali imeendelea kupambana vikali na vitendo vya
kijangili vinavyosabisha biashara hiyo haramu.
Mheshimiwa
Spika, katika mkutano huo, Mheshimiwa Dkt.
Jakaya Mrisho Kikwete, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania alipata fursa ya
kuifahamisha Jumuiya ya Kimataifa kuhusu juhudi na hatua ambazo Serikali ya
Tanzania inachukua kutokomeza tatizo hili. Aidha, Mheshimiwa Rais alitumia
jukwaa hilo kusisitiza umuhimu wa jumuiya ya kimataifa kuhakikisha kuwa soko la
bidhaa hizi linatokomezwa kabisa hasa kwenye nchi za Asia ambako ndiko kuna
soko kubwa.
Mheshimiwa
Spika, mkutano
ulikubaliana pamoja na masuala mengine, kuongeza ushirikiano kati ya mataifa
katika kudhibiti biashara hiyo; kupiga marufuku biashara hiyo bila kutoa ahueni
kama ilivyokuwa inafanyika awali; kuhakikisha kuwa nchi zinapitisha sheria kali
dhidi ya ujangili na kuhakikisha kuwa meno yaliyohifadhiwa sasa hivi yanakosa soko.
6.1.5
Mkutano
wa Jukwaa la Uchumi la Dunia (WEF)
Mheshimiwa Spika, Wizara
iliratibu ushiriki wa nchi kwenye Mkutano wa Jukwaa la Uchumi la Dunia (WEF)
uliofanyika Davos, Uswisi, kuanzia tarehe 22 hadi 25 Februari 2014. Kupitia
Jukwaa hili, Tanzania imeendelea kuvutia wawekezaji hasa katika sekta ya kilimo
kupitia mpango wa “Grow African
Partinership”. Aidha, katika mkutano huo, Serikali kupitia Wizara ya
Kilimo, Chakula na Ushirika, Bodi ya Chai na Tanzania Smallholder Tea Development Agency ilisaini makubaliano na
Kampuni ya Unilever. Makubaliano
hayo ni baada ya Kampuni hiyo kuonesha nia ya kuwekeza kwenye kilimo cha Chai
kupitia SAGCOT. Inatarajiwa kuwa uwekezaji huu utainua uzalishaji wa chai mara
tatu zaidi ya kiwango kinachozalishwa sasa na kuingiza wastani wa Euro Milioni
110. Hatua hii itasaidia kuongeza mapato kutokana na bidhaa zitakazosafirishwa
nje ya nchi.
Mheshimiwa Spika, vilevile,
Serikali imeingia makubaliano (MoU) na WEF katika maeneo ya uendelezaji wa
miundombinu na usimamizi wa Maji. Makubaliano hayo yamefanyika baina ya
Serikali kupitia Wizara ya Maji na “Water
Resources Group Partnership” ya WEF. Makubaliano hayo yatasaidia kuvutia
uwekezaji kwenye sekta ya Maji na hivyo kuhakikisha usimamizi endelevu wa maji
kwa maendeleo. Aidha, Makubaliano hayo yamejikita katika kuboresha huduma ya
maji katika maeneo matatu ambayo ni upatikanaji wa maji kwa ajili ya matumizi
yote ya viwanda na majumbani; usimamizi wa maji taka; na umwagiliaji.
Mheshimiwa Spika, eneo
lingine ambalo Serikali imenufaika kupitia Mkutano huo ni kwenye sekta ya
miundombinu. Serikali iliingia mkataba na WEF chini ya mpango wa “Africa Strategic Infrastructure Initiative”
wenye madhumuni ya kuvutia wawekezaji kwenye miundombinu na hivyo kuleta
manufaa kwa uchumi (Infrastructure with
larger multiplier effect). Mpango huu ambao pia unahusisha Benki ya
Maendeleo ya Afrika (AfDB) umeichagua Bandari ya Dar es salaam kuwa sehemu ya
miradi yake ya awali. Tayari AfDB ilituma timu yake nchini kufanya tathmini ya
awali ya mradi wa upanuzi wa Bandari hiyo.
6.1.6.
Jumuiya
ya Madola
Mheshimiwa Spika, Tanzania
ilichaguliwa tena na Wakuu wa nchi na Serikali wa Jumuiya ya Madola kuendelea
kuwa mjumbe wa Kikundi Kazi cha Mawaziri wa Jumuiya ya Madola (CMAG). Mawaziri
wanaounda CMAG walinipendekeza na kunichagua kwa nafasi yangu kama Waziri wa
Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa wa Tanzania kuwa Mwenyekiti wa CMAG
kwa mwaka 2013 - 2015. Kuchaguliwa kwangu ni mafanikio kwa Diplomasia ya nchi
na kumedhihirisha jinsi nchi inavyoheshimika kwenye Jumuiya ya Kimataifa,
ikizingatiwa kuwa CMAG ni chombo maalum na chenye hadhi ya kipekee kwenye
muundo wa Jumuiya ya Madola kinachosimamia kanuni na taratibu za Jumuiya hiyo
kwa nchi wanachama.
6.1.7
Diplomasia
ya Michezo
Mheshimiwa
Spika, Jumuiya ya Madola itakuwa na mashindano
ya Olimpiki huko Glasgow, Uingereza mwezi Julai mwaka huu. Katika mashindano hayo, vijana wanariadha wa
Tanzania watashiriki katika maeneo ya mbio fupi na ndefu, pamoja na michezo ya
mpira wa meza, ngumi, judo n.k vijana wasiopungua 50 wanatarajiwa kushiriki
katika mashindano hayo.
Kwa
kushirikiana na Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Wizara yangu,
kwa kutumia diplomasia ya mahusiano katika michezo, tumeweza kupeleka vijana 50
pamoja na walimu wao kwenye makambi ya mafunzo Ethiopia, Uturuki, New Zealand
na China. Vijana wapo huko na taarifa
tulizonazo ni kwamba mazoezi yanakwenda vizuri sana. Ni matumaini yetu kuwa huko Glasgow, vijana
wetu watafanya maajabu na kuijengea heshima nchi yetu.
6.2
USHIRIKIANO
WA KIKANDA
6.2.1
Jumuiya
ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC)
Mheshimiwa
Spika, Tanzania imeendelea kushiriki kikamilifu kwenye
Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika. Mwezi Agosti, 2013, Wizara
iliratibu na kushiriki Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa SADC uliofanyika
Lilongwe, Malawi. Mkutano huo ulijadili na kufanya maamuzi mbalimbali yakiwemo
yafuatayo:
a)
Kumteua Mheshimiwa Joyce Banda, Rais wa Malawi
kuwa Mwenyekiti wa SADC hadi Agosti, 2014; Mhe. Banda alichukua nafasi hiyo
kutoka kwa Mheshimiwa Emilio Armando Guebuza, Rais wa Msumbiji;
b)
Kumteua Mheshimiwa Hifikepunye Pohamba, Rais wa
Namibia kuwa Mwenyekiti wa Asasi ya SADC inayoshughulikia masuala ya Siasa,
Ulinzi na Usalama. Mheshimiwa Pohamba alichukua nafasi hiyo kutoka kwa Mheshimiwa
Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
c)
Kumteua Dkt. Stergomena L. Tax kutoka Tanzania
kuwa Katibu Mtendaji wa SADC kuchukua nafasi ya Dkt. Tomaz Agosto Salamao
ambaye kipindi chake kilimalizika. Dkt. Tax amekuwa mwanamke wa kwanza
kuteuliwa kuingoza Jumuiya hii katika miaka 33 ya uhai wake. Uteuzi huo ni
uthibitisho mwingine wa kuzidi kushamiri kwa diplomasia ya Tanzania na
umeendelea kuijengea heshima kubwa na kuitangaza nchi yetu katika medani
ya Kimataifa.; na
d)
Kuendelea kutoa ushauri juu ya utatuzi wa
migogoro mbalimbali ya kisiasa inayoendelea ukanda wa SADC.
6.2.2 Ukanda wa Nchi za Maziwa Makuu
(ICGLR)
Mheshimiwa
Spika, Tanzania imeendelea kushiriki kikamilifu katika Jumuiya ya
Nchi za Ukanda wa Maziwa Makuu (The International Conference on the Great Lakes
Region -ICGLR). Mkutano wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Nchi za ICGLR uliyofanyika
tarehe 15 Januari 2014 Luanda, Angola na uliiomba Jumuiya ya Kimataifa
kuendelea kutoa misaada ya kibinadamu Mashariki mwa DRC; na pia kuziomba
nchi zote za jirani na DRC zilizosaini Mpango wa Amani, Usalama na Ushirikiano
(The Peace, Security and Cooperation Framework for the DRC and the Region)
kuendelea kutekeleza makubaliano yaliyoazimiwa katika Mpango huo ikiwemo
kutohifadhi wala kusaidia makundi ya waasi.
Aidha, mkutano
huu uliiagiza Sekretarieti ya ICGLR kwa kushirikiana na Ofisi ya Mjumbe maalum
wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa katika nchi za Maziwa Makuu, Mhe. Mary
Robinson kuandaa mkutano wa kwanza wa aina yake katika eneo letu utaokojadili
suala la vijana na ukosefu wa ajira (ICGLR’s
Special Summit on Youth and Unemployment). Mkutano huu unatarajiwa
kufanyika mjini Nairobi, Kenya mwishoni mwa mwezi Juni 2014 na kuhudhuriwa na
Wakuu wa Nchi na Serikali wa ICGLR na pia wadau mbalimbali katika suala la
ajira za vijana.
Mheshimiwa
Spika, kwa kutambua umuhimu wa uwekezaji vitega uchumi na biashara
katika kuleta maendeleo ya haraka na endelevu, unaandaliwa mkutano mwingine maalum
wa uwekezaji (the Private Sector Special
Investment Forum) utakaofanyika baadaye mwaka huu. Lengo la mkutano huu ni
kuchochea uwekezaji katika nchi za Maziwa Makuu hususan zile ambazo zimekumbwa
na machafuko.
6.3
BARA
LA AFRIKA
6.3.1
Umoja
wa Afrika (AU)
Mheshimiwa
Spika, Wizara kwa kushirikiana na Balozi zetu imeendelea kuratibu ushirikiano wa Tanzania na nchi
nyingine Barani Afrika na kushiriki
kwenye shughuli za Umoja wa Afrika (AU).
Mwezi Julai 2013, Wizara iliratibu
ushiriki wa Tanzania kwenye Mkutano Maalum wa Wakuu wa Nchi wa Umoja wa Afrika
kuhusu UKIMWI, Kifua Kikuu na Malaria uliofanyika Abuja, Nigeria. Mhe. Dkt.
Mohamed Gharib Bilal, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
aliongoza ujumbe wa Tanzania kwenye mkutano huo. Mkutano huu, pamoja na masuala
mengine, ulipitisha Azimio linalozitaka nchi za Afrika kuchukua hatua za
makusudi kutokomeza
UKIMWI, Kifua Kikuu na Malaria Barani Afrika ifikapo mwaka 2030.
Mheshimiwa
Spika, Wizara
pia iliratibu ushiriki wa
Tanzania kwenye Mkutano Maalum wa Wakuu wa Nchi wa Umoja wa Afrika kuhusu
Mahakama ya Kimataifa ya Makosa ya Jinai (ICC)
uliofanyika Addis Ababa, Ethiopia, mwezi Oktoba 2013, ambapo Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho
Kikwete, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania aliongoza ujumbe wa Tanzania.
Mkutano huo, ulijadili suala la kesi inayowakabili Viongozi Wakuu wawili wa Serikali ya Kenya
kwenye ICC. Mkutano huo, ulipitisha Azimio
ambalo pamoja na masuala mengine, lilisisitiza umuhimu wa kuheshimu misingi ya
haki na kukabiliana na ukiukwaji wa sheria,
utawala bora, amani na usalama Barani Afrika pamoja
na kuheshimu utu na mamlaka ya nchi.
Mheshimiwa
Spika, Wizara vilevile iliratibu ushiriki wa Tanzania
kwenye Mkutano wa 22 wa Wakuu wa Nchi na
Serikali wa Umoja wa Afrika, ambapo nilimuwakilisha Mheshimiwa Rais kuongoza ujumbe
wa Tanzania. Mkutano huu ulijadili na kupitisha maamuzi mbalimbali yenye
maslahi kwa Taifa
letu, ikiwemo Msimamo wa pamoja wa Afrika kuhusu
Agenda ya Maendeleo baada
ya Mwaka 2015 (Common African Position on
Post – 2015 Development Agenda) na kuanzisha Chombo cha Mpito cha
Kukabiliana na Migogoro Barani Afrika (African
Capacity for Immediate Response to Crises – ACIRC). Tanzania ni miongoni mwa nchi waanzilishi wa chombo hicho. Aidha, wakati wa Mkutano
huo, Tanzania ilichaguliwa kwa muhula wa pili kuwa mjumbe wa Baraza la Amani na
Usalama la Umoja wa Afrika kwa kipindi cha miaka miwili hadi mwezi Aprili 2016.
Mheshimiwa
Spika, Tanzania imeendelea kutekeleza majukumu yake
ipasavyo kwenye Baraza hilo, ambapo mwezi Desemba 2013, Wizara iliratibu
ushiriki wa Tanzania kwenye Mkutano Maalum wa Wakuu wa Nchi wa Baraza hilo
uliofanyika mjini Banjul, Gambia, kwa ajili ya kujadili hali tete ya migogoro
nchini Jamhuri ya Afrika ya Kati na Sudan Kusini. Mkutano huo ndiyo uliotoa
pendekezo la kupelekwa kwa vikosi vya kulinda amani vya Umoja wa Afrika katika
nchi ya Jamhuri ya Afrika ya Kati.
7
WATANZANIA
WAISHIO UGHAIBUNI NA SWALA LA URAIA PACHA (DUAL CITIZENSHIP)
Mheshimiwa Spika, Wizara imeendelea kutekeleza jukumu lake la
kuwashirikisha Watanzania waishio ughaibuni (Diaspora)
katika maendeleo ya kiuchumi na ya kijamii ya nchi yetu. Wizara, kwa kutumia kurugenzi yake ya
Diaspora inaendelea na utafiti kwa kushirikiana na Balozi zetu duniani pamoja
na uongozi wa Jumuiya za Diaspora ili kubaini idadi kamili ya Watanzania
waishio nje, ikiwa ni pamoja na kubaini taaluma zao.
Changamoto na kilio
kikubwa cha wana-Diaspora cha kutaka Serikali yetu ikubali na kuipitisha sheria
ya kuruhusu uraia wa nchi mbili (dual
citizenship) inashughulikiwa kikamilifu na Wizara yangu. Wizara tayari imelifikisha suala la uraia
pacha kwa Tume ya Jaji Warioba na tayari suala hili limewekwa kwenye Rasimu ya
Katiba Mpya na tutajadili kwa nguvu za hoja na kwamba umefika wakati wa nchi
yetu kuwa na sheria ya kuruhusu uraia pacha kwa maslahi na maendeleo ya Taifa
letu. Ni matumaini yangu kuwa Bunge hili litaunga mkono pendekezo hilo.
8
ULINZI
NA UJENZI WA AMANI DUNIANI
Mheshimiwa
Spika, katika miaka ya hivi karibuni Jumuiya ya Kimataifa imeshuhudia
Tanzania ikichukua majukumu kwa kushiriki moja kwa moja katika harakati za ukombozi na utatuzi wa
migogoro Barani Afrika na duniani kote. Mpaka sasa, Tanzania imeendelea kushiriki katika utatuzi wa migogoro na
ulinzi wa amani ambapo imekuwa ikichangia
Vikosi vya kulinda amani katika nchi mbalimbali zinazokabiliwa na migogoro.
Mheshimiwa
Spika, hadi Machi 2014,
Tanzania ilikuwa na jumla ya wanajeshi 2,259 kwenye maeneo manne (4) ya kulinda
amani ya Umoja wa Mataifa. Maeneo hayo ni DRC (MONUSCO); Sudan (UNAMID); Lebanon
(UNFIL); na Ivory Coast (UNOCI). Hii inaonesha jitihada za Tanzania za kuifanya
dunia kuwa mahali salama pa kuishi.
Mheshimiwa Spika, ushiriki wa Tanzania kwenye misheni
za kulinda amani unazidi kuifanya nchi
yetu iaminike na kuheshimiwa na Jumuiya ya Kimataifa. Hii
imedhihirishwa na uteuzi wa Watanzania kwenye nafasi za juu kwenye misheni hizo
ikiwemo “Force Intervention Brigade – FIB” chini
ya MONUSCO nchini DRC na UNAMID ya Darfur,
Sudan. Aidha,
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa kwa niaba ya Baraza la Usalama la Umoja wa
Mataifa ameiomba Serikali yetu ipeleke jeshi lake Sudani ya Kusini. Tumekubali.
Mheshimiwa
Spika, ushiriki wetu kwenye maeneo hayo
umewawezesha wanajeshi wetu kuendelea kupata uzoefu. Pia, wanajeshi hao
wanaendelea kuongeza maarifa na mbinu za kijeshi na kujifunza matumizi ya vifaa
vya kisasa vya kijeshi. Ushiriki wetu pia huwa ni nafasi nzuri ya kuanzisha au
kuimarisha mahusiano ya kijeshi na nchi nyingine zinazoshiriki kwenye maeneo
hayo.
Watanzania
tunayo kila sababu ya kujivunia jeshi letu ambalo ni dogo lakini kali kweli
kweli. Mmeona wenyewe nguvu ya jeshi letu kwenye Maadhimisho ya miaka hamsini ya
Muungano kwenye Uwanja wa Taifa.
9
MAADHIMISHO
YA MIAKA HAMSINI YA MUUNGANO
Mheshimiwa
Spika, tarehe 26 Aprili, 1964 Jamhuri ya Tanganyika
iliungana na Jamhuri
ya Watu wa Zanzibar, kuunda Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Watanzania
tunajivuna kwamba tarehe 26 Aprili, 2014 Muungano umetimiza miaka 50 tangu kuundwa kwake. Hatua
tuliyoifikia ni ya kujivunia, kwani katika kipindi hicho
zipo nchi nyingi zilizojaribu kuungana bila mafanikio.
Mheshimiwa
Spika, katika
kipindi cha miaka 50,
Tanzania kupitia utekelezaji wa Sera yake madhubuti ya Mambo ya Nje tulikataa
kufungamana na upande wowote; tukatetea haki za wanyonge; tukadai usawa;
tukapambana dhidi ya ubaguzi wa rangi; tukapigania uhuru; na tukahimiza umoja na mshikamano wa Bara la Afrika. Msimamo wetu huu umetujengea heshima duniani na pengine tusingefanya
hayo nje ya muungano.
Mheshimiwa
Spika, napenda
kutoa wito kwa Bunge lako Tukufu na
na watanzania wote, tuendelee
kuunganisha nguvu katika kutekeleza Sera yetu ya Mambo ya Nje ambayo inahimiza diplomasia ya
uchumi. Tukumbuke kwamba nchi nyingi duniani sasa hivi zinaungana kwa malengo
ya kukuza uchumi wao. Hivyo nasi tudumishe muungano wetu ili tuendelee kunufaika
na kujenga uchumi wenye nguvu.
10
UTAWALA
NA MAENDELEO YA WATUMISHI WIZARANI NA BALOZINI
Mheshimwa
Spika,
Wizara
ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa ina jumla ya Watumishi 401 ambao kati yao 152 wapo kwenye Balozi zetu, 234
wapo Makao Makuu na Watumishi 15 waliopo Idara ya Mambo ya Nje Zanzibar. Aidha,
Watumishi wengine 12 wapo kwenye likizo bila malipo kwa kuwa wanafanya kazi
katika mashirika mbalimbali ya Kimataifa.
Mheshimwa
Spika,
ili
kuwezesha kuwajengea uwezo na kukidhi vigezo vya muundo kwa Watumishi, Wizara
imeandaa mpango wa mafunzo kwa kipindi cha miaka mitatu kuanzia mwaka 2013/2014
hadi 2015/2016.
Aidha, Wizara
yangu kwa kushirikiana na Wafadhili mbalimbali imeendelea kugharamia mafunzo ya
muda mrefu na mfupi ndani na nje ya nchi ambapo Watumishi 13 wamehudhuria
mafunzo ya muda mfupi na watumishi 14 wanahudhuria mafunzo ya muda mrefu katika
mwaka huu wa fedha.
Mheshimwa
Spika,
katika
kuendeleza uwakilishi wetu nje, Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, Rais wa Jamhuri
ya Muungano wa Tanzania alifanya uteuzi wa Mabalozi na Naibu Mabalozi
kuiwakilisha Tanzania katika nchi mbalimbali. Mabalozi walioteuliwa ni Mheshimiwa
Naimi Switie Aziz (Addis Ababa), Mheshimiwa Anthony Ngereza Cheche (Kinshasa),
Mheshimiwa Daniel Ole Njoolay (Abuja), Mheshimiwa Wilson Masilingi (The Hague),
Mheshimiwa Chabaka Kilumanga (Moroni), Mheshimiwa Lt. Gen. Abdulrahaman Amiri
Shimbo Rtd. (Beijing), Mheshimiwa Modest Mero (Geneva), Mheshimiwa Mbaruk
Nasoro Mbaruk (Abu Dhabi), Mheshimiwa Liberata Rutageruka Mulamula (Washington
D.C), Mheshimiwa Dkt. Azizi Ponaly Mlima (Kuala Lumpur), Mheshimiwa Dora Mmari
Msechu (Stockholm), Mheshimiwa Lt. Gen. Wynjones Mathew Kisamba (Moscow) na Mheshimiwa
Joseph Edward Sokoine (Idara ya Ulaya na Amerika). Aidha, Naibu Mabalozi ni; Bwana
Mohamed Hija Mohamed (New Delhi), Bwana Juma Othman Juma (Muscat) na Bwana
Omary Mjenga (Dubai).
Mheshimwa
Spika,
vilevile,
Wizara imewateua Wakurugenzi Wasaidizi 16 kuziba nafasi zilizokuwa wazi katika
Idara za; Diaspora (2), Itifaki (2), Ushirikiano wa Kimataifa (1), Ushirikiano
wa Kikanda (2), Asia na Australasia (2), Ulaya na Amerika (1), Mashariki ya
Kati (1), Afrika (1) Nje Zanzibar (1) na Sera na Mipango (3).
11
TAASISI
ZILIZO CHINI YA WIZARA
11.1
Chuo
Cha Diplomasia
Mheshimiwa
Spika, katika mwaka wa fedha 2013/2014, Chuo
cha Diplomasia kimeendelea kufanya maboresho ili kukidhi masharti ya Baraza la
Ithibati ya Elimu ya Ufundi (National Council for Technical Education – NACTE).
Chuo kimezidi kutambulika na kuimarika katika utoaji taaluma, ushauri na
kufanya tafiti katika masuala ya utatuzi wa migogoro, itifaki, diplomasia ya
uchumi, stratejia na menejimenti ya mahusiano ya kidiplomasia. Aidha, Chuo
kimeendelea kuishauri Wizara yangu katika masuala ya kidiplomasia na kutoa
mafunzo maalum kwa watumishi wa Wizara, Mabalozi na wenza wao.
Mheshimiwa
Spika, sambamba na kuongeza udahili kutoka wanafunzi 590
katika mwaka wa masomo wa 2012/2013 na kufikia wanafunzi 881 katika mwaka huu
wa masomo 2013/2014. Chuo kipo katika hatua za mwisho za mchakato wa kutoa shahada
na kufundisha lugha za kichina kwa watanzania na kiswahili kwa wageni kuanzia
mwaka ujao wa masomo.
Mheshimiwa
Spika, katika kujiimarisha zaidi, Chuo
kimejikita katika kutekeleza Mpango Mkakati wa Miaka Mitano 2012/2013 –
2016/2017 kwa kuboresha miundombinu kama ilivyoainishwa katika Master Plan ya Chuo, kuongeza ufanisi
katika utoaji taaluma, kuajiri wataalam wenye sifa ili kufanya Chuo kiwe kituo
bora cha kikanda kilichobobea katika taaluma, tafiti na utoaji ushauri wa
kitaaluma katika fani za mahusiano ya kimataifa, diplomasia ya uchumi na
stratejia. Mipango hii ina lengo la kukifanya Chuo kiwe na uwezo wa kujitegemea
katika utekelezaji wa majukumu yake.
11.2
Kituo
cha Kimataifa cha Mikutano cha Arusha (AICC)
Mheshimiwa
Spika, Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha
Arusha kimeendelea kutuwakilisha vyema katika diplomasia ya mikutano na kuvutia
utalii nchini kwa njia ya mikutano. Katika kipindi cha miaka mitatu iliyopita,
Kituo kimeweza kukaribisha wastani wa mikutano 61 kwa mwaka. Kati ya mikutano hii, asilimia 30 ya
mikutano ni ya kimataifa na asilimia 70 ni ya kitaifa. Idadi hiyo ya mikutano imeweza kuleta Arusha
wageni wanaokadiriwa kufikia 17,680 kila mwaka.
Kwa mwaka wa fedha ulioishia Juni 2013, Kituo kiliweza kuwa wenyeji wa
mikutano ya kimataifa 29 na ya kitaifa 33 iliyoingiza nchini wageni
wanaokadiriwa kufikia 15,040.
Mheshimiwa Spika, naomba
kuliarifu Bunge lako Tukufu
kuwa kwa mara nyingine tena, Kituo kimeendelea kupata hati safi ya hesabu zake
zilizoandaliwa na kukaguliwa kwa wakati kwa kipindi kilichoishia tarehe 30 Juni, 2013. Katika
kipindi hicho, kituo kilipata faida ghafi ya
shilingi milioni mia moja tisini na moja, mia tatu thelathini na moja elfu na mia
tatu themanini na tano (191,331,385.00) na kinaendelea kufanya
shughuli zake kwa ufanisi na bila kuwa tegemezi kwa Serikali Kuu.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka
2014/2015, Kituo kimepanga kuingiza mapato ya shilingi bilioni
kumi na tatu, mia nane themanini na tano milioni, mia saba na saba elfu, mia
nane thelathini na mbili (13,885,707,832.00)
kutokana na vyanzo vyake mbalimbali vya mapato ikiwemo ya Kituo kipya cha
Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC), ambacho kilikabidhiwa kwa AICC Agosti, 2013 na AICC
inategemea kukopa shilingi bilioni 5.4 kwa ajili ya miradi ya
maendeleo na mali za kudumu zenye
thamani ya shilingi bilioni tano, mia tisa sitini na tatu milioni, mia nne
thelathini na sita
elfu (5,963,436,000.00).
Mheshimiwa Spika, Wizara
yangu itaendelea kuhakikisha Kituo kinatimiza moja ya jukumu lake la kupangisha
asasi za kimataifa. Taasisi mbili za
Umoja wa Afrika (AU Advisory Board on
Corruption na African Institute of
International Law) zilizoanzishwa hivi karibuni, makao makuu yake ni katika
kituo cha AICC. Kwa kuzingatia
upatikanaji wa nafasi baada ya Mahakama ya Mauaji ya Kimbari ya Rwanda (UN-ICTR) kupunguza shughuli zake na
Jumuiya ya Afrika ya Mashariki (EAC)
kurudisha baadhi ya ofisi zake na kuhamia kwenye jengo lao jipya, Kituo
kitaendelea kupokea taasisi zingine za kitaifa na kimataifa zitakazopenda
kuweka makao yake jijini Arusha.
Mheshimiwa Spika, ili kuhakikisha
Mpango Mkakati wa Kituo unatekelezeka, Wizara yangu inaendelea kufuatilia ujenzi wa Kituo kipya cha
mikutano mjini Arusha kitakachoitwa Mount Kilimanjaro
International Convention Centre (MK-ICC). Mradi
huo ni moja ya miradi
itakayofadhiliwa na Serikali ya Watu wa China kupitia benki yao ya Exim.
Mheshimiwa
Spika, vilevile, Wizara yangu baada ya
kupata kibali cha Hazina iliidhinisha Kituo kukopa ili kiweze kujenga majengo matatu ya kisasa (condominium)
katika viwanja vyake vilivyoko Arusha kwa ajili
ya kupangisha. Aidha,
kituo kina mpango wa kujenga maduka ya kisasa (shopping malls) kwa ubia na Mfuko wa Hifadhi ya Jamii wa Serikali za Mitaa (LAPF) katika viwanja vyake
vilivyoko Kaloleni, Arusha na kina mpango wa kupanua Hospitali yake iliyoko
Arusha, kwa mkopo toka taasisi za fedha.
11.3
Mpango
wa Kujitathmini Kiutawala Bora Barani Afrika (APRM- Tanzania)
Mheshimiwa Spika, kulingana na Mpangokazi wa APRM kwa mwaka wa
fedha 2013/2014 baadhi ya shughuli zilizotekelezwa:
·
Kufanya
uchambuzi wa masuala yaliyojitokeza katika Ripoti ya APRM na kuoanisha masuala
hayo na Mipango ya Maendeleo ya Taifa ambayo ni pamoja na Mpango wa
Maendeleo wa Miaka Mitano (2011/12 – 2015/16),
MKUKUTA II, MKUZA II na mipango mingine;
·
Kutafsiri
Ripoti ya Nchi ya Utawala Bora katika lugha ya Kiswahili kwa lengo la kuifanya
Ripoti hiyo ieleweke kwa watu wengi zaidi ukizingitia kuwa lugha ya Kiingereza
ambayo Ripoti hii imeandikwa inafahamika na Watanzania wachache;
·
Kuwasilisha Taarifa ya Utekelezaji wa Mpango
wa APRM Tanzania toka mwaka 2007 (ulipoanza) hadi Aprili 2014 kwenye kikao cha
Makatibu Wakuu kwa lengo la kuwafahamisha hatua zilizofikiwa. Pia kuwaomba
Makatibu Wakuu waingize changamoto zilizobainishwa katika Ripoti ya Nchi ya
Utawala Bora kwenye Mipango yao ya Wizara ya Muda Mfupi na wa Kati. Hatua hii
ni mwanzo wa utekelezaji wa Mpango Kazi wa Taifa wa Kuondoa Changamoto za
Utawala Bora zilizobainishwa na Ripoti ya APRM na kuzitolea Taarifa
itakayowasilishwa kwenye vikao vya AU kila mwaka;
·
Kutayarisha
mfumo wa tathmini na ufuatiliaji wa utekelezaji wa Mpango Kazi wa Taifa wa
Kuondoa Mapungufu yaliyojitokeza ya Utawala Bora;
·
Kutayarisha
makala zitakazotumika wakati wa uwasilishaji wa matokeo ya Ripoti ya Nchi ya
Tathmini ya Utawala Bora kwa wadau mbalimbali ikiwa ni pamoja na Makatibu Wakuu
Tanzania Bara na Zanzibar, Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Baraza la
Wawakilishi Zanzibar, taasisi za kiraia na sekta binafsi.
Mheshimiwa Spika, mipango
ya baadae ya APRM ni kufanya uzinduzi wa Ripoti ya Nchi ya Utawala Bora ambao
utafanywa na Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; kuendelea
kuwafahamisha wananchi kuhusu matokeo ya Ripoti ya Nchi ya Utawala Bora (CRR); kufuatilia
utekelezaji wa Mpango kazi wa Taifa wa kuondoa changamoto za utawala bora
zilizobainishwa na kutayarisha Ripoti za utekelezaji za kila mwaka; na kuendelea
kushirikiana na taasisi zinazoshughulikia masuala mbalimbali ya Utawala Bora
ambazo APRM Tanzania imeanzisha ushirikiano kama vile CHRAGG na PDB kwa lengo
la kubadilishana uzoefu kwa manufaa ya nchi yetu.
12
MAPATO
NA MATUMIZI YA WIZARA KWA MWAKA WA FEDHA 2013/2014
Mheshimwa Spika, Katika mwaka wa fedha 2013/2014, Wizara yangu iliidhinishiwa
kutumia kiasi cha Shilingi
bilioni mia moja na thelathini na nane, mia tatu hamsini na tisa milioni, mia
tisa arobaini na nne elfu na mia mbili ishirini na moja (138,359,944,221.00). Kati ya fedha hizo, Shilingi bilioni mia moja
na kumi, mia tatu hamsini na tisa milioni, mia tisa arobaini na nne elfu na mia
mbili ishirini na moja (110,359,944,221.00)
ni kwa ajili ya Matumizi ya Kawaida na Shilingi bilioni ishirini na nane (28,000,000,000.00) ni kwa ajili ya
bajeti ya maendeleo. Katika fedha zilizotengwa kwa Matumizi ya Kawaida
(Recurrent Budget), Shilingi bilioni mia moja na nne, mia tisa na sita milioni,
mia mbili themanini na nne elfu na mia saba kumi na tisa (104,906,284,719.00) ni kwa
ajili ya Matumizi Mengineyo (OC) na
Shilingi bilioni tano, mia nne
hamsini na tatu milioni, mia sita hamsini na tisa elfu na mia tano na
mbili (5,453,659,502.00) ni
kwa ajili ya Mishahara.
Mheshimwa
Spika,
Wizara kupitia Balozi zake
ilitarajia kukusanya kiasi
cha Shilingi bilioni kumi na sita, milioni mia tisa sitini na sita, mia saba
ishirini na tisa elfu na mia tatu (16,966,729,300.00)
kama maduhuli ya Serikali. Hadi
kufikia tarehe 31 Machi 2014, Wizara imefanikiwa kukusanya kiasi cha Shilingi
12,909,470,376.00 ikiwa ni makusanyo ya maduhuli Balozini. Kiasi hicho cha
makusanyo ya maduhuli ni sawa na asilimia
76 ya makisio ya makusanyo yote ya maduhuli kwa mwaka wa fedha 2013/2014.
Mheshimwa Spika, hadi kufikia tarehe 31 Machi 2014, Wizara ilikuwa imepokea kiasi
cha Shilingi bilioni mia moja kumi na saba, milioni mia tatu ishirini
na saba na mia tisa sitini na mbili (117,327,353,962.00). Kati ya kiasi hicho, Shilingi bilioni mia moja na sita,
milioni mia nne tisini na mbili, mia nane arobaini na nane na arobaini na mbili
(106,492,848,042.00) ni kwa ajili ya
Matumizi Mengineyo, Shilingi bilioni nne, milioni mia tatu sitini na nane, mia
saba na tano elfu na mia tisa ishirini (4,368,705,920.00)
ni kwa ajili ya Mishahara na Shilingi
bilioni sita, mia nne sitini na tano milioni na mia nane elfu (6,465,800,000.00) ni kwa ajili ya Bajeti ya Maendeleo.
13
CHANGAMOTO
ZILIZOJITOKEZA KATIKA UTEKELEZAJI WA MAJUKUMU YA WIZARA KWA MWAKA WA FEDHA
2013/2014
Mheshimiwa Spika, katika
kipindi cha mwaka wa fedha 2013/2014, Wizara yangu imekabiliwa na changamoto
mbalimbali za kiutawala na kibajeti katika utekelezaji wa majukumu yake. Baadhi
ya changamoto hizo ni upungufu wa Watumishi Makao Makuu ya Wizara na Balozini; upungufu
wa vitendea kazi; uchakavu wa majengo ya ofisi na makazi Balozini; na uchakavu
wa magari ya uwakilishi na huduma Balozini.
Mheshimiwa
Spika, Katika
kukabiliana na changamoto hizo, Wizara imechukua hatua mbalimbali ikiwa ni
pamoja na kuomba kibali Ofisi ya Rais -
Menejimenti ya Utumishi wa Umma cha kuajiri Watumishi wapya. Vilevile, Wizara
imeendelea kununua vitendea kazi vya Watumishi kwa awamu kulingana na
upatikanaji wa fedha. Aidha, Wizara itaendelea kutumia fedha za bajeti ya
Maendeleo zinazopangwa katika bajeti kwa ajili ya kutekeleza miradi ya
maendeleo kwa kuzingatia vipaumbele na kuishirikisha mifuko ya Hifadhi ya Jamii
katika kuingia ubia wa kutekeleza miradi ya maendeleo iliyopo Balozini.
Halikadhalika, Wizara imepanga kutumia utaratibu wa higher purchase katika
kufanikisha ununuzi wa magari Balozini. Utaratibu huu ni mzuri kwa kuwa
utapunguza gharama za ununuzi wa magari hayo.
14
MALENGO YA WIZARA KWA MWAKA WA FEDHA 2014/2015
Mheshimiwa
Spika,
katika mwaka wa fedha wa
2014/2015, pamoja na mambo mengine, Wizara yangu imepanga kutekeleza malengo
makuu muhimu kulingana na majukumu yake kama ifuatavyo:-
i.
Kuitangaza
nchi yetu kama moja ya nchi duniani yenye mazingira mazuri kwa ajili ya
uwekezaji;
ii.
Kuendelea
kufuatilia utekelezaji wa ahadi zilizotolewa kwa nchi yetu na nchi mbalimbali
wahisani na mashirika ya kikanda na ya kimataifa katika kusaidia utekelezaji wa
mipango yetu ya maendeleo;
iii.
Kuendelea
kuratibu Wizara, Idara na Taasisi nyingine za Serikali kikanda na kimataifa kwa
lengo la kuvutia wawekezaji na watalii; kutafuta nafasi za masomo, ajira na
nafasi za kubadilishana uzoefu; na kutafuta masoko;
iv.
Kusimamia,
kufuatilia na kuratibu utekelezaji wa mikataba mbalimbali iliyosainiwa kati ya
nchi yetu na nchi nyingine na ile ya mashirika ya kikanda na kimataifa;
v.
Kuendelea
kufuatilia kwa karibu mageuzi kwenye taasisi za Umoja wa Mataifa kama vile
Baraza la Kiuchumi na Kijamii (ECOSOC); Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa (UNGA);
kuanzishwa kwa Malengo Endelevu ya Maendeleo – Sustainable Development Goals –
SDGs na agenda ya maendeleo baada ya kumalizika kwa kipindi cha Malengo ya
Milenia 2015. Tutaendelea kufuatilia kwa karibu masuala yote yanayogusa maslahi
yetu;
vi.
Kuendelea
kusimamia na kupigania maslahi ya nchi maskini kwenye mikutano yote mikubwa na
hasa ile ya Umoja wa Mataifa na taasisi zake. Vilevile, tutaendelea kufanya mazungumzo na nchi tajiri
duniani ili kuhakikisha zinatekeleza ahadi mbalimbali zilizozitoa ili
kuharakisha maendeleo ya nchi maskini;
vii.
Kuongeza
uwakilishi wetu nje kwa kufungua Balozi mpya na Balozi ndogo na kuongeza
umiliki wa nyumba za makazi na ofisi za Ubalozi katika Balozi zetu nje kwa
kadri hali ya fedha itakavyoruhusu;
viii.
Kutekeleza
maelekezo ya Viongozi wa kitaifa pamoja na kuzingatia ushauri wa Kamati ya
Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa na Bunge la Jamhuri
ya Muungano wa Tanzania;
ix.
Kujenga
mahusiano ya kirafiki na ushirikiano wa kiuchumi kati ya vyombo vya Kikanda na
Kimataifa, unaozingatia maslahi muhimu ya Taifa letu;
x.
Kuendelea
kusimamia na kuzihimiza Balozi zetu nje kutafuta wawekezaji, fursa za ajira,
nafasi za masomo na masoko kwa bidhaa zetu;
xi.
Kuendelea
kuitambua Jumuiya ya Watanzania wanaoishi ughaibuni na kuweka utaratibu
utakaowawezesha kuchangia maendeleo ya Taifa lao; na
xii.
Kuendeleza
Ujirani Mwema.
15
MAKADIRIO
YA MAPATO NA MATUMIZI KWA MWAKA WA FEDHA 2014/2015
Mheshimiwa Spika, ili kuweza kutekeleza kikamilifu majukumu yaliyotajwa
hapo juu, kwa mwaka wa fedha 2014/2015 Wizara yangu imepangiwa bajeti ya kiasi
cha Shilingi bilioni mia
moja tisini na moja, mia tisa kumi na tisa milioni na mia saba arobaini na nane
elfu (191,919,748,000.00). Kati ya fedha hizo Shilingi bilioni mia moja sitini na
moja, mia tisa kumi na
tisa milioni na mia saba arobaini na nane elfu (161,919,748,000.00)
ni kwa ajili ya Matumizi ya Kawaida na Shilingi bilioni thelathini (30,000,000,000.00) ni kwa ajili ya
bajeti ya Maendeleo. Aidha, katika bajeti ya Matumizi ya Kawaida ya Wizara,
Shilingi bilioni mia moja hamsini na sita, mia moja hamsini na nane milioni na
sabini na nane elfu (156,158,078,000.00) ni kwa ajili ya Matumizi Mengineyo na Shilingi
bilioni tano, mia saba sitini na moja milioni na mia sita sabini elfu (5,761,670,000.00)
ni kwa ajili ya Mishahara.
Mheshimiwa Spika, katika bajeti ya Matumizi Mengineyo ya Wizara kwa mwaka
wa fedha 2014/2015, Shilingi bilioni moja, mia saba sitini na nne milioni (1,764,000,000.00) ni kwa ajili ya Mpango wa Kujitathmini Kiutawala Bora
Tanzania (APRM), Shilingi bilioni moja, mia tano na nne milioni, mia tano
sabini na nne elfu, mia nne sabini na nane (1,504,574,478.00)
ni kwa ajili ya Mahakama ya Afrika ya Haki za Binadamu na Watu na Shilingi
bilioni nne, tisini na nne milioni na mia tisa na mbili elfu (4,094,902,000.00) ni kwa ajili ya
fedha za Mishahara na Matumizi Mengineyo ya Chuo cha Diplomasia.
Mheshimiwa
Spika,
katika fedha za bajeti ya
maendeleo za kiasi cha Shillingi bilioni thelathini (30,000,000,000.00)
zilizopangwa kwa mwaka wa fedha 2014/2015, kiasi cha Shilingi bilioni kumi na
nne, mia moja sitini na saba milioni, mia tano na nne elfu (14,167,504,000.00) ni kwa ajili ya kukamilisha ununuzi wa jengo la ofisi na
makazi ya balozi jijini Paris, kiasi cha Shilingi bilioni saba,
mia nne ishirini na tano milioni (7,425,000,000.00) ni
kwa ajili ya ujenzi wa makazi ya Balozi Mount
Vernon-New York, kiasi cha
Shilingi bilioni moja, mia tatu na tisa milioni, mia sita sitini na saba elfu
na tisini na sita (1,309,667,096.00) ni kwa ajili ya ukarabati wa majengo
ya Serikali yaliyopo jijini Khartoum, Sudan, kiasi cha Shilingi bilioni nne,
mia tisa hamsini milioni (4,950,000,000.00)
ni kwa ajili ya ukarabati wa Ofisi
ya Ubalozi jijini New York, kiasi cha shilingi milioni mia moja arobaini na
mbili, mia mbili ishirini na saba elfu (142,227,000.00)
ni kwa ajili ya ukarabati
wa makazi ya Balozi jijini
Geneva na kiasi cha shilingi bilioni mbili na milioni tano, mia sita na mbili
elfu (2,005,602,000.00) ni kwa ajili
ya ukarabati wa jengo la Makao Makuu ya Wizara.
Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha wa 2014/2015, Wizara yangu kupitia Balozi zake, inatarajia kukusanya
kiasi cha Shilingi bilioni kumi na nane, mia tano sitini na nane milioni,
ishirini na mbili elfu, mia nne sabini na nane (18,568,022,478.00) kama maduhuli ya Serikali. Kwa maana ya
utekelezaji wa Bajeti, kiasi hiki cha maduhuli tayari kimejumuishwa kama sehemu
ya bajeti ya Matumizi Mengineyo ya Wizara.
16
HITIMISHO
Mheshimiwa
Spika, ili kuweza
kutekeleza kikamilifu majukumu yaliyotajwa hapo juu, kwa mwaka wa fedha
2014/2015, naomba Bunge lako Tukufu liidhinishe jumla ya Shilingi bilioni mia moja tisini na moja, mia tisa kumi na tisa milioni
na mia saba arobaini na nane elfu (191,919,748,000.00). Kati ya fedha hizo Shilingi bilioni mia moja sitini na
moja, mia tisa kumi na
tisa milioni na mia saba arobaini na nane elfu (161,919,748,000.00)
ni kwa ajili ya Matumizi ya Kawaida na Shilingi bilioni thelathini (30,000,000,000.00) ni kwa ajili ya
bajeti ya Maendeleo.
Mheshimiwa
Spika, naomba kutoa hoja.
1 comment:
I would like to thank you for the efforts you've put in writing this blog.
I'm hoping to view the same high-grade blog posts from
you later on as well. In truth, your creative writing abilities has
inspired me to get my very own website now ;)
Post a Comment