Baba mzazi wa mtoto wa miaka minne,
aliyedhulumiwa haki yake ya utu na kuteswa kwa zaidi ya miaka mitatu kwa
kufungiwa ndani ya boksi tangu akiwa na
umri miezi tisa, Rashid Mvungi hatimaye amepatikana na kusema kuwa mtoto huyo
ni damu yake na kwamba yuko tayari kumlea
katika hali yoyote.
Mvungi alisema hayo jana, ambapo
alisema tukio la mtoto wake kuishi ndani ya boksi, limemtia simanzi kubwa.
Alisema alikuwa na tabia ya kwenda
kumuona mtoto wake kila mwezi na alikuwa akipeleka Sh 20,000 hadi 30,000 kwa
ajili ya matumizi ya mtoto, tangu alipochukuliwa na mama yake mlezi.
Alisema, katika kipindi cha mwanzo
alikuwa akipata fursa ya kumuona mtoto
na kwamba ana maendeleo mazuri.
Alisema katika kipindi cha karibuni,
hakuwa akipatiwa fursa hiyo, kutokana na
kuambiwa mtoto amelala.
Aidha, alisema hakutaka kuonesha hofu yake
juu ya majibu ya mama mlezi wa mtoto huyo, kwa kile alichodai ni kuogopa
kufikiriwa tofauti na mama huyo.
Hata hivyo, alidai anamlaumu mama mlezi
wa mtoto huyo kwa kumtesa mwanawe, ambapo alisema kama aliona amechoka kumlea,
angemwambia ili ajue cha kufanya.
"Kama alikuwa amechoka kumlea
angeniambia nami ningetengeneza mazingira ya kumchukua," alisisitiza na
kuongeza kuwa, mama mzazi wa mtoto huyo aliugua kwa muda mrefu na kusababisha
ashindwe kumnyonyesha, hali iliyochangia kudhoofika kwa afya ya mtoto kwa kuwa
hakunyonya maziwa ya mama.
Aidha, alisema baada ya mama wa mtoto
kufariki, mama yake mkubwa alimuomba
mtoto huyo ili akaishi naye, ambapo naye aliridhia, akiamini mama yake mkubwa
angeishi naye vizuri.
Akizungumzia suala la ulemavu wa mtoto,
alisema kuwa hakuwa mlemavu, isipokuwa afya yake ilikuwa dhaifu kutokana na
kukosa maziwa ya mama, ambapo alisema
alikuwa anaweza kusukuma gari la watoto.
Akizungumzia suala la kushindwa kuishi
na mwanawe, alisema kuwa alishindwa kutokana na kuwa hakuwahi kumwambia mkewe
kuwa ana mtoto mwingine nje, kutokana na uzito wa suala lenyewe.
"Mwanaume yeyote wa kitanzania
akizaa mtoto nje ya mkewe huwa anakuwa mzito kumpa taarifa mkewe kwa kuhofia
kupoteza ndoa," alidai Mvungi.
Uchunguzi wa awali aliofanyiwa mtoto
huyo, ulibaini alikuwa na nimonia na
ulegevu wa viungo, ikiwa ni pamoja na baadhi ya viungo katika mwili wake
kuvunjika.
Daktari Mshauri wa Watoto katika
Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Morogoro, Hores Msaky alipozungumza na mwandishi
juzi, alisema walimpokea mtoto huyo akiwa katika hali ya uchafu usio wa
kawaida.
Msaky alisema waliamua kumfanyia vipimo
vya awali pamoja na picha ya X-ray na kugundua mifupa yake si ya kawaida,
inaonekana imevunjika ingawa hawajajua ni nini hasa kimesababisha kuvunjika
kwake.
Akizungumza na mwandishi jana
alipotembelea hospitalini hapo ili kujua
maendeleo ya mtoto huyo,
daktari Msaky alisema bado
wanaendelea kumpatia matibabu na kwamba
hali ya mtoto huyo kwa sasa inatia matumaini.
Alisema kuwa tayari jopo la madaktari,
limekaa na kuamua kuwa wiki ijayo apelekwe katika Hospitali ya Taifa Muhimbili
(MNH) jijini Dar es Salaam kwa ajili ya uchunguzi zaidi.
Hatimaye juzi mateso ya mtoto huyo
ambaye alikuwa akiishi, kula na kujisaidia akiwa ndani boksi kama mnyama,
yalipungua baada ya msamaria kutoa
taarifa kuwa ndani ya nyumba, kuna kiumbe asiye na hatia na aliye katika mateso
makali. Msamaria huyo alitoa taarifa kwa Ofisa Mtendaji wa Kata ya Kiwanja cha
Ndege, Diana Zongo.
Zongo akiwa katika kazi zake za kawaida
katika Mtaa wa Azimio anaoishi mtoto huyo, alipata taarifa kwa majirani kuwa
kuna mtoto amefichwa ndani ya boksi na hamfanyii usafi wala kumtoa nje hali
iliyomfanya amtafute Mwenyekiti wa Mtaa, Tatu Mgagala na kuongozana naye mpaka
kwenye nyumba na kumkuta mtuhumiwa na kuanza kumhoji.
Kwa mujibu wa mtendaji huyo, wakati
mtuhumiwa akijibu maswali alikuwa akibabaika na kwamba ghafla mtoto huyo
alipiga chafya, hali iliyowapa wasiwasi na kuamua kuingia kwa nguvu chumbani
kwa Mariam Said, hatua iliyomuokoa mtoto huyo kutoka katika mateso aliyokuwa
nayo.
Mtoto huyo alikutwa akiwa ametapakaa
uchafu, uliotokana na kinyesi na mkojo kwa kuwa boksi hilo lilikuwa chumba
chake cha kulala, meza yake ya chakula na maji na choo kwa ajili ya haja ndogo
na kubwa.
Kwa upande wake, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro, Leonard Paul alisema
baba mzazi wa mtoto huyo, anashikiliwa kituoni hapo kwa ajili ya mahojiano.
Akizungumzia sakata la kupotea kwa kaka wa mtoto huyo, Kamanda Paul alisema
baada ya kupata taarifa hizo, walijaribu kupeleleza na kubaini kuwa marehemu
aliacha watoto wawili, ambao alizaa na wanaume wawili tofauti na kwamba taarifa za awali walizonazo ni kwamba kaka
yake mtoto huyo, alichukuliwa na baba yake mzazi.
No comments:
Post a Comment