AWAUA WAZAZI WAKE KWA SHOKA NA KUTEKETEZA NYUMBA YAO



Simanzi kubwa imetanda katika Kijiji cha Roo, Kata ya Masama Mashariki wilayani Hai, Kilimanjaro, baada ya kijana mwenye umri wa miaka 32 kuwaua wazazi wake wawili kwa  kutumia panga na shoka, kisha kuchoma moto nyumba yao.
Kijana huyo aliyetambulika kwa jina la Yusuph Njau aliwaua wazazi wake, Shahidu Njau (60) na Minae Swai (57) baada ya kuwafungia ndani na kuwakata kata kwa kutumia shoka na panga.
Akizungumza na mwandishi, Diwani wa Kata ya Masama Mashariki, Ally Mwanga alisema mauaji hayo yalitokea juzi majira ya saa 12: 30 jioni, katika nyumba waliyokuwa wanaishi wanafamilia hao.
Mwanga alisema baada ya kijana huyo kufanya mauaji hayo, alichukua uamuzi wa kuchoma nyumba huku miili ya wazazi wake ikiwa ndani, ambapo majirani walitoa msaada wa kudhibiti moto huo baada ya kuona moshi ukifuka ndani.
Alisema wakati wananchi wakiendelea kuudhibiti moto huo, ndipo waliona miili ya marehemu ikiwa inavuja damu, hali iliyosababisha kutoa taarifa Polisi.
Alisema mtuhumiwa alitoroka baada ya matukio hayo na kwamba maziko ya wazazi wake yalitarajiwa kufanyika jana jioni kijijini kwao Roo.
Mwanga alisema taarifa za awali zilizopatikana kuhusiana na tukio hilo kuwa chanzo ni matumizi ya dawa za kulevya na bangi ambazo amekuwa akitumia kwa muda mrefu kijana huyo.
“Hili tukio ni la kutisha sana, linahuzunisha sana, kijana huyu amekuwa akitumia dawa za kulevya kwa muda mrefu, hivyo kichwa kimeathiriwa kwa matumizi hayo,” alisema Mwanga.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Kijiji cha Roo, Khalfan Swai, alilieleza gazeti hili kuwa kijana huyo amekuwa na matukio ya kutishia watu hapo kijijini, na amewahi kufungwa kwa muda baada ya kuwapiga baba mdogo na shangazi yake.
Swai alisema kijana huyo amekuwa akitembea na shoka na panga kwa kuwatishia watu, lakini wazazi wake walikuwa wakimtetea kuwa mwana wao hahusiki na vurugu zozote za kutishia watu.
Pia alisema kijana huyo awali alikuwa anaishi Dar es Salaam akiwa anajifunza ngumi za kulipwa, lakini baada ya kuathirika na matumizi ya dawa za kulevya ndipo aliporejea kijijini.
Kamanda wa Polisi mkoani Kilimanjaro, Robert Boaz akitoa taarifa za tukio hilo, alisema  Jeshi la Polisi linaendelea na msako wa kumtafuta mtuhumiwa, ili hatua za kisheria ziweze kuchukuliwa.

No comments: