Simanzi
kubwa imetanda katika Kijiji cha Roo, Kata ya Masama Mashariki wilayani Hai,
Kilimanjaro, baada ya kijana mwenye umri wa miaka 32 kuwaua wazazi wake wawili
kwa kutumia panga na shoka, kisha kuchoma moto nyumba yao.
Kijana
huyo aliyetambulika kwa jina la Yusuph Njau aliwaua wazazi wake, Shahidu Njau
(60) na Minae Swai (57) baada ya kuwafungia ndani na kuwakata kata kwa kutumia
shoka na panga.
Akizungumza
na mwandishi, Diwani wa Kata ya Masama Mashariki, Ally Mwanga alisema mauaji
hayo yalitokea juzi majira ya saa 12: 30 jioni, katika nyumba waliyokuwa
wanaishi wanafamilia hao.
Mwanga
alisema baada ya kijana huyo kufanya mauaji hayo, alichukua uamuzi wa kuchoma
nyumba huku miili ya wazazi wake ikiwa ndani, ambapo majirani walitoa msaada wa
kudhibiti moto huo baada ya kuona moshi ukifuka ndani.
Alisema
wakati wananchi wakiendelea kuudhibiti moto huo, ndipo waliona miili ya
marehemu ikiwa inavuja damu, hali iliyosababisha kutoa taarifa Polisi.
Alisema
mtuhumiwa alitoroka baada ya matukio hayo na kwamba maziko ya wazazi wake
yalitarajiwa kufanyika jana jioni kijijini kwao Roo.
Mwanga
alisema taarifa za awali zilizopatikana kuhusiana na tukio hilo kuwa chanzo ni
matumizi ya dawa za kulevya na bangi ambazo amekuwa akitumia kwa muda mrefu
kijana huyo.
“Hili
tukio ni la kutisha sana, linahuzunisha sana, kijana huyu amekuwa akitumia dawa
za kulevya kwa muda mrefu, hivyo kichwa kimeathiriwa kwa matumizi hayo,”
alisema Mwanga.
Kwa
upande wake Mwenyekiti wa Kijiji cha Roo, Khalfan Swai, alilieleza gazeti hili
kuwa kijana huyo amekuwa na matukio ya kutishia watu hapo kijijini, na amewahi
kufungwa kwa muda baada ya kuwapiga baba mdogo na shangazi yake.
Swai
alisema kijana huyo amekuwa akitembea na shoka na panga kwa kuwatishia watu,
lakini wazazi wake walikuwa wakimtetea kuwa mwana wao hahusiki na vurugu zozote
za kutishia watu.
Pia
alisema kijana huyo awali alikuwa anaishi Dar es Salaam akiwa anajifunza ngumi
za kulipwa, lakini baada ya kuathirika na matumizi ya dawa za kulevya ndipo
aliporejea kijijini.
Kamanda
wa Polisi mkoani Kilimanjaro, Robert Boaz akitoa taarifa za tukio hilo,
alisema Jeshi la Polisi linaendelea na msako wa kumtafuta mtuhumiwa, ili
hatua za kisheria ziweze kuchukuliwa.
No comments:
Post a Comment