Wakati
mchakato wa mabadiliko ya Katiba ukitarajiwa kuendelea katika ngazi ya Bunge
Maalumu la Katiba Agosti mwaka huu, Askofu Mkuu mpya wa Jimbo Kuu Katoliki la
Songea, Damian Dallu, amesifu Katiba iliyopo kwa kuunganisha Watanzania kwa
miaka 50.
Askofu
Dallu aliyesimikwa jana kushika wadhifa huo katika Kanisa Kuu la Mtakatifu
Mathias Mulumba, mjini Songea, alisema Katiba iliyopo imefanikiwa kuwaunganisha
Watanzania kiroho na sio katika makaratasi, ambayo yanaweza kuchakachuliwa wakati
wowote.
Akizungumza
katika Ibada hiyo maalumu, Askofu Dallu alifikia hatua akasema, Katiba iliyopo
ingeweza kuendelea kutumika kwa kuwa ina mambo mengi ya msingi na kwa mtazamo
wake, upungufu upo lakini ni kidogo na unaweza kurekebishwa.
‘’Ndugu
zangu, Tume ya Warioba ilifanya kazi nzuri ya kukusanya maoni kutoka kwa
Watanzania, lakini tungeweza kutumia Katiba iliyopo sasa ambayo ina mambo mengi
ya msingi na upungufu kidogo ambao unaweza kurekebishika,” alisema.
Askofu
Dallu ambaye amesimikwa baada ya kuteuliwa na Baba Mtakatifu Francis, alisema
kuna watu wanaodhani kuwa Katiba mpya ikipatikana matatizo yao yote yatakuwa
yamekwisha na kuhadharisha kwamba mawazo hayo si sahihi.
Badala
yake aliwataka Watanzania wamuombe Mungu awasaidie kupata viongozi
watakaoongoza Taifa kuanzia ngazi ya chini mpaka juu, kwa kufuata maadili ili
nchi isije ikaingia kwenye machafuko.
Askofu
Dallu amesema hayo wakati hoja kubwa katika mchakato unaoendelea wa kupata
Katiba mpya, ikiwa muundo wa Muungano, uliogawa wajumbe wa Bunge Maalumu la
Katiba katika makundi mawili ya watetezi wa Muungano wa serikali tatu na
watetezi wa Muungano wa serikali mbili.
Watetezi
wa Muungano wa serikali mbili, msingi wa hoja yao ni umoja, mshikamano na amani
ya Watanzania, ambayo ndiyo msingi wa maendeleo ya Mtanzania mmoja mmoja na
Taifa kwa ujumla.
Watetezi
hao ambao ndani ya Bunge Maalumu la Katiba wameunda umoja wao wa Tanzania
Kwanza, wamekuwa wakiungwa mkono na wasomi na wakisisitiza kuwa Muungano wa
serikali tatu, si tu utavunja Muungano uliodumu kwa mika 50 sasa, lakini pia
utavuruga umoja na mshikamano wa Watanzania.
Mmoja
wa wasomi wanaounga mkono Muungano wa serikali mbili, Profesa Bonaventura
Rutinwa wa Shule Kuu ya Sheria ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), amekuwa
akionya kuwa muundo wa serikali tatu, unaotaka kurejeshwa kwa Serikali ya
Tanganyika, utaibua ubaguzi kati ya Wazanzibari na watakaokuwa Watanganyika.
“Sasa
kwa kuwa Zanzibar tayari ina Katiba yake, inayotoa na kulinda haki za kisiasa,
kijamii na kiuchumi kwa Wazanzibari, huhitaji nguvu za kinabii kubashiri kuwa
Katiba ya Tanganyika ikija, itatoa na kulinda haki za kiuchumi, kisiasa na
kijamii kwa Watanganyika.
“Hii
ikitokea, itasababisha wananchi kutoka Tanganyika wanaoishi Zanzibar na
Wazanzibari wanaoishi Tanganyika kushindwa kudai haki zao za uraia kisheria,”
alionya Profesa Rutinwa.
Katika
mazingira hayo, mfumo unaopendekezwa wa serikali tatu, utafifisha mshikamano wa
Watanzania na serikali za nchi washirika, na katika hali mbaya zaidi utazalisha
kero mpya za Muungano zitakazokuwa na nguvu ya kuvunja Muungano.
“Kunahitajika
umakini katika hili, la sivyo historia imeshaonesha kuwa ni rahisi kuvunja
Taifa kuliko kulikusanya na kulijenga upya,” ameonya Profesa Rutinwa.
Katika
sehemu ya ushauri wake, Profesa Rutinwa alipendekeza pamoja na mambo mengine,
utatuzi wa kero za Muungano, ufanyike pamoja na kulitazama wazo la kuwa na
serikali moja, ambayo kwa mujibu wa ushauri huo, serikali hiyo ndiyo lengo la
siku nyingi la Muungano kati ya Tanzania Bara na Zanzibar.
Watetezi
wa Muungano wa serikali tatu, wamekuwa na hoja tofauti ambazo zimekuwa
zikitolewa na kubadilishwa kulingana na mazingira, lakini kila mara wakidai
wanatetea mapendekezo ya rasimu ya Katiba mpya, inayopendekeza serikali tatu.
Kwanza
watetezi hao ambao ndani ya Bunge Maalumu la Katiba wamejiundia kundi la Umoja
wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), walidai kuwa Muungano uliopo ni batili kwa madai
kuwa hakukuwa na Hati ya Muungano na Sheria ya Kuridhia Muungano, sahihi zake
zimechakachuliwa.
Serikali
ilipotoa Hati halisi ya Muungano, Ukawa ilibadilisha hoja na kudai kuwa
watahitaji ikaguliwe na wataalamu wa kimataifa na baadaye kurudi katika hoja ya
kutetea maoni ya rasimu ya Katiba mpya, iliyotengenezwa na Tume ya Mabadiliko
ya Katiba.
Baada
ya kupoteza hoja kulikosababishwa na kutolewa hadharani kwa Hati ya Muungano,
wajumbe hao walianza kujenga hoja kutaka Bunge Maalumu la Katiba, lisibadilishe
maoni ya rasimu ya Katiba yanayotaka Muungano wa serikali tatu.
Kupungua
nguvu kwa hoja ya Muungano wa serikali tatu, kulisababisha wajumbe hao mwishoni
mwa Bunge Maalumu la Katiba, kutoka nje ya Bunge na ambapo sasa wameazimia
kutembea nchi nzima kunadi walichoita utetezi wa rasimu ya Katiba mpya.
Akitoa
salamu za Mkoa wa Ruvuma, Mkuu wa Mkoa Said Mwambungu, alisema Serikali itatoa
ushirikiano kwa Askofu huyo kwa kuwa inaunga mkono juhudi za Kanisa Katoliki
katika kutoa huduma katika sekta ya afya, elimu, kilimo na maji.
Alisema
mafanikio katika sekta hizo katika Mkoa wa Ruvuma, yamechangiwa na viongozi wa
dini ambao walikuwa wakijituma kwa bidii kusaidia wananchi bila kujali
madhehebu wanayotoka, na kuipa Serikali faraja na inaomba ushirikiano huo
uendelee.
Kwa
upande wake Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania,
Anne Makinda akitoa salamu kwa niaba ya Serikali, amewataka Watanzania kufanya
kazi kwa bidii badala ya kuitegemea Serikali au Kanisa kuwaletea maendeleo
jambo ambalo linaweza kusababisha waendelee kuwa masikini.
No comments:
Post a Comment