ASKARI WANYAMAPORI WAUA NG'OMBE 150 BIHARAMULO



Ng’ombe 150 wameuawa na askari wa Wanyama Pori katika Hifadhi ya Biharamulo, kutokana na mgogoro uliokuwepo wa kuwaondoa baadhi ya wafugaji, waliovamia eneo la hifadhi.
Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Profesa Anna Tibaijuka, amekiri kuuawa kwa ng'ombe hao wakati akizungumza na gazeti hili kwa njia ya simu jana.
Alisema Waziri Mkuu, Mizengo Pinda amewaagiza baadhi ya mawaziri kwenda wilayani humo, kusuluhisha mgogoro huo, na kwamba kwa sasa wamefikia mahali pazuri.
"Tuko huku baadhi ya mawaziri, tumeagizwa na Serikali Kuu kuja kushughulikia mgogoro huu, kulikuwa na mgogoro ambapo watu waliokuwa wakiondolewa hifadhini, sasa mchakato huo ukasababisha ng'ombe hao uliowataja kufa," alisema Waziri Tibaijuka.
Alisema wachungaji wa ng’ombe hao, walikamatwa ndani ya hifadhi  pamoja na mifugo yao,  na utaratibu ulipaswa  kuwapiga faini au kufikishwa mahakamani kwa wale watakaogoma kulipa faini, lakini katika mazingira hayo kuliibuka mgogoro huo.
"Tuko huku na sasa hivi ndiyo tumetoka kwenye kikao cha kushughulikia mgogoro huu, lakini mpaka sasa tumeshafikia pazuri," alisema Waziri Tibaijuka.

No comments: