Mtuhumiwa
wa mauaji ya kutisha aliyekuwa akisakwa na
Polisi pamoja na wananchi, kwa tuhuma za kuua wazazi wake wawili, amekamatwa baada ya kujitokeza mwenyewe
kuomba chakula, kutokana na njaa aliyokuwa nayo.
Mtuhumiwa
huyo, Yusuph Njau (32), mkazi wa Kijiji cha Masama Roo Wilaya ya Hai mkoani
Kilimanjaro, alikamatwa jana saa 2:15 asubuhi na wananchi wenye hasira kali,
akiwa katika moja ya nyumba ya ndugu yake, akisubiri kupewa chai.
Akizungumza
na mwandishi, Mwenyekiti wa Kijiji cha Roo, Khalfani Swai, alisema mtuhumiwa
alitokea porini alikokuwa amejificha, baada ya kuua wazazi wake wawili, Shahidu
Njau (60), Minei Swai (57) na kuchoma
moto nyumba ya familia hiyo.
Kwa
mujibu wa Swai, wakati mtuhumiwa akiwa kwa ndugu yake aliyetambulika kwa jina
la Halifa, jirani na Shule ya Sekondari ya Roo akisubiri kupatiwa chai,
walijitokeza wananchi wenye hasira kali na kumkamata, baada ya ndugu yake huyo kupiga
simu kwenye ofisi ya kijiji, kutoa taarifa za kuonekana kwa mtuhumiwa huyo.
"Tumefanikiwa
kumkamata Yusuph aliyefanya mauaji ya kikatili, baada ya kutoka maporini akiwa anahitaji msaada wa chakula…ambapo
alifika kwa kaka yake kuomba chai, wakati akisubiri kupatiwa huduma hiyo ndugu
yake akatupa taarifa ambapo tulifanikiwa kumtia mbaroni,” alisema Swai.
Aidha,
Swai alisema mtuhumiwa huyo alinusurika kuuawa na wananchi wenye hasira
kali, ambao walidhamiria kumcharanga
mapanga kabla ya ndugu zake kufika
haraka katika eneo la tukio, ambapo walimtorosha kwa gari na kumfikisha Kituo
cha Polisi cha Boma Ng’ombe.
Kamanda
wa Polisi mkoani Kilimanjaro, Robert Boaz alisema Polisi kwa sasa wanaendelea
na uchunguzi, ili kubaini sababu za mtuhumiwa kuchukua hatua ya kuua wazazi
wake kikatili.
Kukamatwa
kwa Yusuph, kumekuja siku chache tangu
alipoua wazazi wake wawili kwa kuwacharanga mapanga na shoka Mei 9 mwaka huu
kisha kuteketeza nyumba kwa moto, kwa
lengo la kufuta ushahidi.
No comments:
Post a Comment