ACT-TANZANIA KUMSHAWISHI ZITTO KUJIUNGA NAO



Mwanachama wa chama kipya cha siasa cha Alliance for Change and Transparency (ACT-Tanzania), Dk Kitila Mkumbo, amesema atahakikisha anazungumza na viongozi wa chama hicho, ili wamshawishi mbunge wa Kigoma Kaskazini, Kabwe Zitto, ajiunge na chama hicho.
Mkumbo, aliyasema hayo, Dar es Salaam jana wakati alipohojiwa na gazeti hili kuhusu kuhusika kwake na chama hicho kipya kilichopata usajili wake wa kudumu juzi, ambapo alikiri kuwa mwanachama wa chama hicho.
“Ni kweli mimi ni mwanachama wa ACT, lakini sina nafasi yeyote ya uongozi kutokana na kazi yangu, ila nitakuwa natoa ushauri wa namna ya kukiendeleza chama chetu, likiwemo suala hili la Zitto,” alisema.
Alisema yeye ni rafiki mkubwa wa Zitto na wamekuwa wakishirikiana pamoja kwenye masuala ya siasa kwa miaka mingi na anatambua uwezo wake hivyo endapo atashindwa na Chadema, atahakikisha mwanasiasa huyo anajiunga na chama hicho cha ACT.
“Zitto ni mwanasiasa mashuhuri na ni mtu muhimu katika siasa za nchi yetu, si vizuri aendelee kutangatanga, kwa sasa uhusiano wake na Chadema si mzuri kwani ni mbunge kwa kupitia mahakama, endapo hali itazidi kuwa mbaya, nitawashauri viongozi wangu, tumshawishi ajiunge huku tuendeleze siasa ya kweli,” alisisitiza.
Mkumbo aliwahi kuwa mjumbe wa Kamati Kuu ya Chadema lakini yeye, Zitto pamoja na aliyekuwa Mwenyekiti wa chama hicho, mkoani Arusha Samson Mwigamba, walivuliwa nyadhifa zao na Chadema kwa madai ya uhaini na hujuma dhidi ya chama hicho kutokana na waraka unaojulikana kama mkakati wa uchaguzi 2013.

No comments: