WATANO WAFARIKI DUNIA KWA KUSOMBWA NA MAJI

Wakazi hasa wa eneo la Tabata Matumbi Jijini Dar es Salaam na wapiti njia wakiangalia katika daraja la mto Msimbazi baada ya kuzagaa harufu ambayo inahisiwa kuwa ya binaadamu anayedaiwa kukwama eneo hilo baada kufa na kusombwa na maji na kukwama hapo.
Watu watano wamekufa katika matukio  matano tofauti baada ya kusombwa na maji katika maeneo tofauti ya jiji la Dar es Salaam.
Katika tukio la kwanza lililotokea Chanika, mtoto wa kike aliyefahamika kwa jina la Lainant Ramadhani (2) alikufa baada ya kutumbukia kwenye shimo la maji lililopo jirani na nyumba yao.
Akithibitisha kutokea kwa tukio hilo Kamanda wa Polisi Mkoa wa Ilala Marietha Minangi alisema mtoto huyo alitumbukia katika shimo hilo wakati alipokuwa akitoka kumfuata mama yake aliyekuwa nje anafua nje ya nyumba yao.
Alisema mama huyo hakumuona na hatimae alikunywa maji mengi na kufa papo hapo, maiti iliopolewa na baba mzazi akishirikiana na wananchi na maiti imehifadhiwa katika Hospitali ya Taifa Muhimbili.
Katika tukio jingine, maiti ya  Ibrahimu Ngangari (25-30) imekutwa huko Ubungo inasemekana alisombwa na maji ya mvua.
Akithibitisha kutokea kwa tukio hilo Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kinondoni, Camillius Wambura alisema mtu huyo alisombwa na mvua zilizonyesha mwishoni wa wiki, kwa maelezo ya watu wanaomfahamu walisema marehemu enzi za uhai wake alikuwa na tabia ya ulevi.
Mwili umehifadhiwa katika Hospitali ya Taifa Muhimbili kwa utambuzi na hifadhi.
Katika tukio la tatu lililotokea majira ya saa 2 huko Mbagala imekutwa maiti ya mtu mmoja mwanaume asiyefahamika anayekadiriwa kuwa na miaka 20-25, ikiwa imelala katika shamba la mihogo ambalo mmiliki wake hajajulikana.
Katika tukio la nne lililotokea huko Riverside imekutwa maiti ya mtu mmoja aliyefahamika kwa jina Damiani Damiani (40), fundi ujenzi Mimara ikielea kwenye maji.
Akithibitisha kutokea kwa tukio hilo Kamanda  Camillius Wambura alisema mtu huyo alikufa wakati akijaribu kuvuka katika kivuko cha gogo eneo la Makondeko na kusombwa na maji ya mvua.
Maiti iliopolewa na wananchi wa eneo hilo na imehifadhiwa katika Hospitali ya Mwananyamala.
Katika tukio la tano lililotokea huko Kisarawe mtu mmoja asiyefahamika (miaka 20-25) alizama kwenye tope wakati anaogelea kwenye bwawa lililopo maeneo hayo.
Akithibitisha kutokea kwa tukio hilo Kamanda wa polisi mkoa Temeke Engelbert Kiondo alisema juhudi za kumtafuta zilishindikana kutokana na giza kuingia, utaratibu wa kumtafuta unaendelea.

No comments: