USAJILI MABASI YA DART WASOGEZWA MBELE

Wakala wa Mradi wa Mabasi Yaendayo Haraka Dar es Salaam (DART) umesogeza hadi kesho mchakato wa usajili wa mabasi ya abiria (Daladala) yanayopita katika barabara ya Morogoro au kukatiza katika njia hiyo.
Awali mchakato huo ulioanza Machi 3, mwaka huu, ulipangwa kumalizika Aprili 21, lakini umesogezwa hadi kesho kufidia siku za Sikukuu ya Pasaka. 
Akitangaza kuongezwa kwa siku za usajili huo, Mhandisi wa Wakala huo, John Shauri alisema jana jijini Dar es Salaam: “Tumeona ni vyema kusogeza siku hadi Ijumaa ili kutoa nafasi kwa wamiliki kumalizia vyema usajili huu.”
Akitoa ufafanuzi zaidi alisema wamiliki wa daladala ambao hawajajisajili watumie muda huo ulioongezwa ili kufanikisha zoezi hilo kwa kiwango cha juu.
Hatua hiyo ya kuandikisha mabasi hayo ya abiria ni moja ya matayarisho ya kupisha mradi huo wa mabasi yaendayo haraka.
Kwa sasa wakala huo uko kwenye mchakato wa kuwezesha upatikanaji wa watoa huduma kwenye mfumo mpya wa mabasi yaendayo haraka awamu ya kwanza ambayo inajumuisha Barabara ya Morogoro, Kawawa na Mtaa wa Msimbazi kwa njia kuu na nyingine za kiungo.
Kulingana na mpango wa uendeshaji wa mfumo wa DART, barabara zinazohusika zitapaswa kutumiwa na mabasi ya mfumo huo pekee.
Kwa mujibu wa Shauri, jumla ya njia 64 zitakoma kutumika kutokana na kuanza kwa mradi huo.
Alitaja baadhi ya njia zitakazoguswa na mpango huo kuwa ni pamoja na Mbagala Rangi 3 kwenda Masaki, Vingunguti kwenda Makumbusho, Kunduchi Kwenda Mwenge, na Msata kwenda Ubungo.
Njia nyingine ni Kariakoo kwenda Makumbusho, Buguruni kwenda Kawe, Kivukoni kwenda Mburahati, Mbagala Kuu kwenda Mwenge, na Mkata kwenda Ubungo.
Njia nyingine ni Mburahati kwenda Muhimbili, Segerea kwenda Mwenge, Vingunguti kwenda Kawe, Vingunguti kwenda Mbezi, Kunduchi kwenda Posta, na Kunduchi kwenda Makumbusho.
Alizitaja njia nyingine kuwa ni Temeke kwenda Masaki, Kivukoni kwenda Mabibo, Muhimbili kwenda Mabibo, Posta kwenda Ubungo, Posta kwenda Mabibo, Kawe kwenda Kimara, Kivukoni kwenda Mbezi, Mwenge kwenda Mbezi, Posta kwenda Mbezi, Mbezi kwenda Tegeta na Bunju kwenda Makumbusho.
Katika mpango huo wamiliki hao wa daladala wanatakiwa kwenda ofisi za DART wakiwa na nakala ya leseni ya SUMATRA, nakala ya usajili wa gari, na nakala za rangi za leseni za madereva wao.

No comments: